Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 254-256
  • Kitabu cha Biblia Namba 61—2 Petro

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu cha Biblia Namba 61—2 Petro
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA PETRO WA PILI
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • Acheni Tuishike Sana Imani Yetu Yenye Thamani!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Mtume Petro Anasema na Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Weka Siku ya Yehova Karibu Akilini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Kitabu cha Biblia Namba 60—1 Petro
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 254-256

Kitabu cha Biblia Namba 61—2 Petro

Mwandikaji: Petro

Mahali Kilipoandikiwa: Babuloni (?)

Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 64 W.K.

1. Ni mambo gani ya hakika ambayo yathibitisha kwamba Petro ndiye mwandikaji wa Petro wa Pili?

PETRO alipoandika barua yake ya pili, alitambua kwamba muda si muda angekabili kifo. Kwa hamu nyingi alitamani kukumbusha Wakristo wenzake umaana wa maarifa sahihi ili kuwasaidia kudumisha uthabiti katika huduma yao. Je! kungekuwa na sababu yoyote ya kutia shaka kwamba mtume Petro ndiye aliyekuwa mwandikaji wa barua ya pili yenye jina lake? Barua yenyewe hufuta shaka zozote ambazo zingaliweza kuwa zimezuka juu ya uandikaji. Mwandikaji asema yeye ni “Simoni Petro, mtumwa na mtume wa Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:1) Yeye huirejezea hii kuwa ‘waraka wa pili niwaandikiao ninyi.’ (3:1) Ajisema kuwa shahidi aliyejionea kugeuka sura kwa Yesu Kristo, likiwa ni pendeleo ambalo Petro alilishiriki pamoja na Yakobo na Yohana, naye aandika juu yalo kwa hisia zote za shahidi aliyejionea. (1:16-21) Ataja kwamba Yesu alikuwa ametabiri kifo chake.—2 Pet. 1:14; Yn. 21:18, 19.

2. Ni nini hutoa hoja ya kutetea kukubalika kwa Petro wa Pili?

2 Hata hivyo, wachambuzi fulani wameonyesha tofauti katika mtindo wa barua mbili hizo kuwa sababu ya kutoihesabu barua ya pili kuwa kazi ya Petro. Lakini hilo halipasi kuwa tatizo halisi, kwa maana habari na kusudi la kuandika lilikuwa tofauti. Kwa kuongezea, Petro aliandika barua yake ya kwanza “kwa mkono wa Silwano, ndugu mwaminifu,” na ikiwa Silwano alipewa kadiri fulani ya uhuru katika kufanyiza zile sentensi, hiyo ingeweza kueleza ni kwa nini kuna tofauti ya mtindo katika barua mbili hizo, kwa kuwa yaonekana Silwano hakushiriki katika kuiandika barua ya pili. (1 Pet. 5:12) Kukubalika kwayo kumefanyiwa ubishi pia kwa msingi wa kwamba barua hiyo “haina ushuhuda wa kutosha katika Mababa.” Hata hivyo, kama vile iwezavyo kuonwa kutokana na ile chati “Orodha za Mapema Zenye Kutokeza za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo,” Petro wa Pili ilichukuliwa kuwa sehemu ya orodha ya Biblia na wajuzi kadhaa kabla ya Baraza la Tatu la Carthage.a

3. Yaonekana ni lini na wapi Petro wa Pili iliandikwa, nayo ilielekezwa kwa nani?

3 Barua ya pili ya Petro iliandikwa lini? Yawezekana sana kwamba iliandikwa karibu 64 W.K. kutoka Babuloni au ujirani wayo, muda mfupi baada ya barua ya kwanza, lakini hakuna uthibitisho wa moja kwa moja, ulio wazi juu ya mahali penyewe. Wakati wa kuandikwa, nyingi za barua za Paulo zilikuwa zikizunguka miongoni mwa makundi na zilijulikana na Petro, aliyezichukua kuwa zenye pumzi ya Mungu na kuzipanga kuwa aina moja na “maandiko mengine.” Barua ya pili ya Petro yaelekezwa “kwa wale waliopata imani moja na sisi,” nayo yawahusisha ndani wale ambao barua ya kwanza ilielekezwa kwao na wengine ambao Petro aliwahubiri. Kama vile barua ya kwanza ilivyokuwa imezunguka katika maeneo mengi, ndivyo barua ya pili pia ilivyopata kuwa yenye kuenea mahali pengi.—2 Pet. 3:15, 16; 1:1; 3:1; 1 Pet. 1:1.

YALIYOMO KATIKA PETRO WA PILI

4. (a) Akina ndugu wapaswa kujitahidije kuzaa matunda kwa habari ya maarifa sahihi, nao waahidiwa nini? (b) Neno la kiunabii lahakikishwaje zaidi, na kwa nini lapasa kutiiwa?

4 Kuhakikisha wito kwenye Ufalme wa kimbingu (1:1-21). Petro ni mwepesi kuonyesha hangaiko lenye upendo kwa “wale waliopata imani.” Atamani kwamba neema na amani ziongezwe kwao “katika kumjua Mungu na Yesu Bwana wetu.” Mungu amewapa kwa wingi “ahadi kubwa mno, za thamani,” ambazo kwazo wao waweza kuwa washiriki katika hali ya kimungu. Kwa hiyo, kwa jitihada yenye bidii ya moyoni acheni watie kwenye imani yao nguvu za wema, maarifa, kujiweza, uvumilivu, ujitoaji kimungu, shauku ya kidugu, na upendo. Sifa hizo zikifurika ndani yao, hawatakuwa kamwe wasiotenda wala wasiozaa matunda kuhusiana na maarifa sahihi. Akina ndugu wapaswa kufanya yote wawezayo wahakikishe wito na uchaguliwa wao, na pia mwingio wao ndani ya Ufalme wa milele wa Bwana wao. Akijua kwamba ‘kule kuwekewa mbali maskani yake kwaja upesi,’ Petro ana nia ya kuwakumbusha mambo ili wayataje baada ya kuondoka kwake. Petro alikuwa shahidi aliyejionea kwa macho utukufu mkuu wa Kristo katika ule mlima mtakatifu ambapo maneno haya ‘yaliletwa kwake katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.’ Hivyo, neno la kiunabii lahakikishwa zaidi, na lapasa kutiiwa, kwa maana hilo si kwa mapenzi ya binadamu, ‘bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na roho takatifu.’—1:1, 2, 4, 14, 17, 21.

5. Petro atoa onyo gani juu ya walimu bandia, naye atumia vielezi gani vyenye nguvu juu ya uhakika wa hukumu za Mungu juu ya watu hao?

5 Onyo kali juu ya walimu bandia (2:1-22). Manabii na walimu bandia wataingiza mafarakano (madhehebu) yenye uharibifu, waendeleze mwenendo mlegevu, na kuleta suto juu ya ile kweli. Lakini uharibifu wao hausinzii. Mungu hakusita kuadhibu malaika waliotenda dhambi, asilete gharika katika siku ya Nuhu, wala asiteketeze Sodoma na Gomora ziwe majivu. Lakini alimkomboa mhubiri Nuhu na Lutu mwadilifu, kwa hiyo “Bwana [Yehova, NW] ajua kuwaokoa watauwa na majaribu, na kuwaweka wasio haki katika hali ya adhabu hata siku ya hukumu.” Kwa maana watu hao ni wenye kuthubutu sana kufanya mambo, wenye kufuata kauli yao wenyewe, kama wanyama wasiofikiri, wasiojua mambo, waongeaji wenye kutukana, wenye kupendezwa na mafundisho ya udanganyifu, wazinzi, wenye tamaa ya kichoyo, nao ni kama Balaamu katika kuipenda thawabu ya kutenda kosa. Waahidi uhuru lakini wao wenyewe ni watumwa wa upotovu. Ingalikuwa bora zaidi kama wasingalikijua kijia cha uadilifu, kwa maana ule usemi umetukia kwao: “Mbwa ameyarudia matapiko yake mwenyewe, na nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaa-gaa matopeni.”—2:9, 22.

6. (a) Kwa nini Petro aandika, naye asema nini kuhusu ahadi ya Mungu? (b) Tofauti na wadhihaki, ni lazima Wakristo wajionyesheje kuwa macho?

6 Kuiweka karibu akilini siku ya Yehova (3:1-18). Petro anaandika ili aamshe uwezo wa kufikiri wazi wa Wakristo, ili kwamba wapate kukumbuka semi zilizotajwa hapo kwanza. Wadhihaki watakuja katika siku za mwisho, wakisema: “Ku wapi huku kuwapo kwake [Kristo] kulikoahidiwa?” Watu hawa waponyokwa na ufahamu wa kwamba Mungu aliharibu ulimwengu wa nyakati za kale kwa maji na kwamba “kwa neno lile lile zile mbingu na dunia zilizopo sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto” nazo “zimewekewa ile siku ya hukumu na ya kuharibiwa watu wasioogopa Mungu.” Kwa Yehova miaka elfu moja ni kama siku moja, kwa hiyo “Yehova si mtu wa polepole kwa habari ya ahadi yake,” bali ni mwenye saburi, asitake mtu yeyote aharibiwe. Kwa sababu hiyo, Wakristo wapaswa waangalie mwenendo wao na wapaswa kuzoea matendo ya ujitoaji kimungu wangojeapo na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova, ambayo kupitia hiyo mbingu zitayeyushwa na moto na viasili vitayeyuka kwa joto kali sana. Lakini kutakuwa na “mbingu mpya na dunia mpya” kulingana na ahadi ya Mungu.—3:4, 7, 9, 13, NW.

7. Wakiwa na maarifa haya ya mapema, Wakristo wapaswa kujitahidije?

7 Kwa sababu hiyo, yawapasa wafanye yote wawezayo ‘wakutwe naye wakiwa hawana madoa na kasoro na katika amani.’ Yawapasa waifikirie saburi ya Bwana wao kuwa wokovu, kama vile Paulo alivyowaandikia. Wakiwa na maarifa hayo, acheni waangalie wasianguke kutoka kwenye uthabiti wao. “Sivyo,” amalizia Petro, “bali endeleeni kukua katika fadhili zisizostahilika na maarifa ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo. Kwake na kuwe utukufu sasa na hadi siku ya umilele.”—3:14, 18, NW.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

8. (a) Petro ashuhudiaje kupuliziwa na Mungu kwa Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki pia? (b) Sisi tutafaidikaje kwa kushikamana na maarifa sahihi?

8 Lo! maarifa sahihi ni ya maana kama nini! Petro mwenyewe ahusisha katika hoja zake maarifa sahihi ambayo amejipatia kutokana na Maandiko ya Kiebrania. Ashuhudia kwamba yalipuliziwa na roho takatifu: “Kwa maana unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema kutoka kwa Mungu wakati walichukuliwa na roho takatifu.” Pia, yeye ataja kwamba Paulo alikuwa ‘amepewa’ hekima yake. (1:21; 3:15, NW) Sisi hufaidika sana kwa kufikiria Maandiko yote haya yaliyopuliziwa na Mungu na kushikamana sana na maarifa sahihi. Hapo hatutakuwa kamwe na ukinaifu, kama wale ambao Petro asimulia juu yao kuwa wakisema: “Vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.” (3:4) Wala hatutatumbukia katika mitego ya walimu bandia kama wale ambao Petro asimulia juu yao katika sura ya 2 ya barua yake. Bali, yatupasa tufikirie daima vikumbusho vilivyotolewa na Petro na waandikaji wengine wa Biblia. Hivyo vyatusaidia kubaki tukiwa ‘tumekaa imara katika ukweli’ na kwa saburi na uthabiti ‘tuendelee kukua katika fadhili zisizostahiliwa na maarifa ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.”—1:12; 3:18, NW.

9. Sisi twatiwa moyo tufanye jitihada gani ya moyo wa bidii, na kwa nini?

9 Kama msaada wa kuongezeka katika “maarifa sahihi ya Mungu na ya Yesu Bwana wetu,” Petro apendekeza jitihada ya bidii ya moyoni ili kujenga sifa zile za Kikristo zilizoorodheshwa katika sura ya 1, mistari 5 mpaka 7, NW. Halafu, katika mstari wa 8, aongezea hivi: “Kwa kuwa ikiwa mambo hayo yanakaa ndani yenu na kufurika, yatawazuieni msiwe ama wasiotenda ama wasiozaa matunda kwa habari ya maarifa sahihi ya Bwana yetu Yesu Kristo.” Kwa kweli hiki ni kitia-moyo bora cha kuwa na utendaji tukiwa wahudumu wa Mungu katika hizi siku zenye hatari!—1:2.

10. (a) Petro akazia ahadi gani, naye ahimiza nini kuhusiana nazo? (b) Petro atoa uhakikisho gani kuhusu unabii mbalimbali wa Ufalme?

10 Ni jambo la maana kama nini mtu kujitahidi kwa kadiri yote awezayo ili ahakikishiwe kushiriki katika “ahadi kubwa mno” za Yehova Mungu! Hivyo ndivyo Petro awahimiza Wakristo wapakwa-mafuta waendelee kukaza macho juu ya mradi wa Ufalme, akisema: “Jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe. Maana hivi mtaruzukiwa kwa ukarimu kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo.” Halafu Petro avuta uangalifu kwenye adhama ya utukufu wa Ufalme wa Yesu, ambao yeye ni shahidi aliyekuwa ameuona kupitia ile njozi ya kugeuka sura, naye aongezea hivi: “Nasi tuna lile neno la unabii lililo imara zaidi.” Ni kweli kwamba kila unabii kuhusu Ufalme wa adhama wa Yehova litatimizwa kwa uhakika. Hivyo, ni kwa kuwa na uhakika kwamba sisi twavumisha mwangwi wa maneno ya Petro yaliyonukuliwa kutokana na unabii wa Isaya: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Pet. 1:4, 10, 11, 19, UV; 3:13, NW; Isa. 65:17, 18, UV.

[Maelezo ya Chini]

a Ona chati katika ukurasa 303.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki