Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 6/1 kur. 22-24
  • Mtume Petro Anasema na Wewe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mtume Petro Anasema na Wewe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mchungaji Mwenye Sifa za Kustahili
  • Ithamini Imani
  • Kufurahi Sana Yajapokuwako Matatizo
  • Kukabiliana na Tisho Baya
  • Acheni Tuishike Sana Imani Yetu Yenye Thamani!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Alijifunza Kusamehe Kutoka kwa Bwana Wake
    Igeni Imani Yao
  • Alijifunza Kusamehe Kutoka kwa Bwana Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Mtume Petro—Kwa Sababu Gani Anapendwa Sana na Wengi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 6/1 kur. 22-24

Mtume Petro Anasema na Wewe

LEO si jambo jepesi kuwa Mkristo. Kuna mikazo mingi. Katika nchi fulani-fulani Serikali inajaribu kutulazimisha tufanye mambo yanayopingana na dhamiri ya Kikristo. Wake wengi wa Kikristo wana waume wasio waamini. Vijana wanavutiwa na kumetameta kwa ulimwengu na “hekima” yake. Na, baada ya makumi kadha ya miaka ya kungojea, huenda hata wengine wakawa wanajiuliza hivi: ‘Kweli Har–Magedoni itakuja?’

Ikiwa wewe unaelekeana na matatizo kama hayo​—na hata hivyo ni Mkristo gani asiyeelekeana nayo?​—zile barua mbili zilizo katika Biblia ambazo ziliandikwa na mtume Petro zinasema na wewe moja kwa moja. Petro aliandikia makundi ya siku zake labda muda unaozidi kidogo miaka 30 baada ya kifo cha Yesu. Lakini matatizo ambayo Wakristo wanaelekeana nayo hayajabadilika kwa muda wa karne nyingi. Mashauri ambayo Petro alitoa yangali yanafaa hata sasa, sawasawa na wakati alipoyatoa. Naye alikuwa na sifa za kumstahilisha sana kutoa mashauri ya namna hiyo.

Mchungaji Mwenye Sifa za Kustahili

Kwa kusoma masimulizi mbalimbali ya Injili na kitabu cha Matendo, tunajifunza mengi juu ya mwanamume mvuaji wa samaki wa Galilaya ambaye alikuja kuwa mtume Petro. Anaonekana kuwa mwanadamu mwenye kuchangamsha moyo, Hakukuwa kamwe na shaka lo lote katika jambo la kwamba alimwonyesha Yesu ushikamanifu, lakini alikuwa mwepesi wa kuchukuliwa na fikira na nyakati nyingine alifanya makosa. Labda sisi tunaweza kutambua kosa fulani upande wetu wenyewe kutokana na mambo fulani ambayo Petro alikosea.

Kwa mfano kumbuka namna Petro alivyotenda alipomwona Yesu akitembea juu ya maji. Yeye alipatwa na msisimuko akataka hata naye atembee juu ya maji. Lakini alipopatambua mahali alipokuwa, aliona wasiwasi na ikawa lazima aokolewe. Kumbuka, pia, wakati Petro alipojipiga moyo konde akasisitiza kwamba yeye hangekwazika kamwe. Lakini saa chache baadaye alimkana Yesu mara tatu.​—Mathayo 14:23-34; 26:33, 34, 69-75.

Lakini, mwandikaji wa barua mbili hizo ambazo zinakubalika kuwa zenye ustahili alikuwa amebadilika tangu alipopokea maneno haya makali ya Yesu: “Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu.” (Mathayo 16:23) Mtume huyo ndiye yule aliyepewa na Yesu agizo hili: “Lisha kondoo zangu.” (Yohana 21:17) Katika barua za Petro tunakuta yeye akiwa mwanamume ambaye amegeuzwa tabia na ujuzi wa miaka zaidi ya 30 aliopata kwa ‘kulisha kondoo.’

Hivyo wakati sisi tunaposoma onyo lake la upole linalosema, “Jitahidini kupendana kwa moyo,” huenda tukakumbuka kwamba huyo ndiye yule mtume aliyemwuliza Yesu hivi: ‘Ni lazima nimsamehe ndugu yangu mara ngapi? Ni mpaka mara saba?’ Kufikia sasa, Petro anajua kwamba hakuna kikomo katika upendo ambao Wakristo wanaonyeshana. (1 Petro 1:22; Mathayo 18:21) Na wakati alipohimiza Wakristo wenzake waendelee ‘kukesha katika sala,’ tunaona kwamba yeye amejifunza somo zito tangu usiku ule mbaya sana katika Gethsemane wakati Yesu alipowaacha mitume wakisali kisha akarudi akawakuta wamelala.​—1 Petro 4:7; Luka 22:39-46.

Ndiyo, huyo mvuaji wa samaki wa Galilaya alikuwa amekuwa mchungaji mwenye sifa za kumstahilisha vya kutosha. Na kwa kuwa aliongozwa na roho takatifu, uchungaji wake unathaminika siku zetu kama ulivyothaminika siku zake. Angalia mengine ya mawazo aliyotoa.

Ithamini Imani

Katika karne ya kwanza ulimwengu wa Wayahudi na Waroma ulikuwa wenye kumetameta kwa kuvutia watu na ulikuwa wenye mamlaka. Lilikuwa jambo la maana Wakristo wasishawishwe na fahari ya ulimwengu au wasisongwe na mikazo yake mpaka waache mwendo. Kwa hiyo Petro anaanza kwa kuwatia moyo wasomaji wake ‘wakaze akili zao kwa ajili ya utendaji, watunze akili zao kabisa.’ (1 Petro 1:13, NW) Kwa njia gani? Kwa uthamini wenye uchangamshi wa mapendeleo waliyofurahia.

Petro aliwakumbusha kwamba manabii wa kale na hata malaika walipendezwa sana na kujua mambo ambayo Mungu alikuwa amefunulia Wakristo. Alionyesha namna walivyokuwa wamebarikiwa sana: wakawa wamenunuliwa kwa damu ya Yesu Kristo, wakawa wamezaliwa kwa mbegu isiyoharibika kupitia Neno la umilele la Mungu kisha wakafanywa kuwa “mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu.” (1 Petro 2:9) Walipaswa kukumbuka walikuwa akina nani: wakaaji wa kigeni katika ulimwengu usiomcha Mungu​—watu wenye kufurahia rehema kuu ya Yehova Mungu.

Leo, ulimwengu huo wa kale umekwisha kupita. Lakini tungali tunaishi katika ulimwengu usiomcha Mungu ambao unatuvuta kwa werevu kwa kutumia vishawishi vyake au unapotosha fikira zetu kwa kutumia mikazo yake. Mashauri ya Petro yangali yanafaa. Haitupasi kamwe kuacha kuona faida tulizo nazo. Ili kuepuka kulemewa na maoni ya kudharau mambo na ufuatiaji wa mambo ya kimwili ya ulimwengu wa leo, ni lazima ‘tufanyize nia ya kutamani sana maziwa yasiyochanganywa kitu ambayo ni ya lile neno, ili kupitia kwalo tupate kukua kwenye wokovu.’​—1 Petro 2:2, NW.

Kufurahi Sana Yajapokuwako Matatizo

Mara nyingi kuishi kwetu katika ulimwengu usiomcha Mungu kunatokeza matatizo, kama kulivyofanya siku za Petro. Hali tatu anazotaja ni (1) daraka la Mkristo kuelekea Serikali, (2) uhusiano wa mtumishi wa kinyumbani aliye Mkristo pamoja na bwana wake wa kazi na (3) tendo la mke Mkristo kusaidia mume asiyeamini kwa kunyenyekea.

Huko nyuma, masuala ya namna hiyo yalihusu uzima au kifo. Mara nyingi watawala walikuwa na mamlaka ya kutesa vibaya au kuua raia wasio Waroma. Watumwa wa kinyumbani hawakuruhusiwa sana nafasi ya kuweza kwenda kushtaki wenyeji wao ikiwa waliwatenda kwa ukatili. Wake walikuwa mali za waume wao, nao hawakuwa na haki nyingi za kujitetea kisheria.

Leo, Wakristo wangali wana magumu katika kushughulika na “Kaisari” au wenye kuwaajiri kazi, ingawa hali yenyewe hailingani kabisa na ule uhusiano wa bwana wa kazi na mtumwa wake. Na wanawake wengi wa Kikristo walio na waume wasioamini wanaelekeana na matatizo makubwa. Hivyo mashauri ya mtume Petro yanathaminika sana. Yeye anasema nini?

Kwa ufupi, anatukumbusha mambo matatu. Kwanza, tunahitaji kuwa na maoni yanayofaa juu ya utii​—wote wanapaswa kutii serikali, wafanya kazi wanapaswa kutii mabwana wa kazi na wake wanapaswa kuheshimu na kutii waume zao. Halafu, njia yetu ya kujiendesha inapasa ionyeshe wasioamini kwamba Ukristo ndio njia bora zaidi ya maisha. (1 Petro 3:1; 4:15) Mwishowe, inatupasa tuendeleze dhamiri njema mbele za Yehova Mungu, sikuzote tukiwa tayari kueleza kwa upole sababu ya matendo yetu.​—1 Petro 3:15, 16.

Je! kufanya hivyo kutatatua matatizo yetu yote? Petro alijua hakungefanya hivyo. Nyakati zinafika ambapo ulimwengu unatokeza madai ambayo Mkristo hawezi kukubali. Kwa hiyo, huenda tukalazimika kuteseka kwa ajili ya uadilifu. Lakini, Petro alisema, “ikiwa kwa sababu ya dhamiri kwa Mungu mtu anavumilia mambo ya kusikitisha na kuteswa isivyo haki, hilo ni jambo linalokubalika.”​—1 Petro 2:19, NW.

Kwa kweli, wakati kuteseka kwa ajili ya uadilifu kunapoonwa kwa maoni yanayofaa, kunakuwa sababu ya kufurahi sana. Petro alijua hivyo kutokana na aliyojionea yeye mwenyewe. Miaka mingi mapema alikuwa amepigwa mijeledi kwa sababu ya imani yake. Baadaye, yeye na wenzake wenye kuteseka ‘walitoka wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo.’ (Matendo 5:41) Kwa hiyo, sasa yeye anawaandikia hivi Wakristo wanaopata mateso: “Kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini.”​—1 Petro 4:12, 13.

Petro aliwaambia akina ndugu kwamba, kwa kweli, wao walikuwa wakizoezwa na Yehova. Alisema hivi: “Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari.” Aliwaambia wapendane, na kwamba wazee wanapaswa kuyachunga makundi wakiwa na makusudi yanayofaa. Kisha akaahidi kwamba baada ya muda mfupi “Mungu wa neema yote . . . yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu.”​—1 Petro 5:1-3, 6, 10.

Je! shauri hilo haliufai wakati huu sawasawa na vile lilivyoufaa wakati huo? Je! halitolewi kama kwamba Petro anasema na wewe moja kwa moja? Wazia namna lilivyowatia moyo Wakristo huko nyuma katka siku za Petro. Lakini baada ya muda mfupi mtume aliyekuwa akiendelea kuzeeka alilazimika kuandika barua ya pili ili kutoa onyo juu ya tisho baya kwa ndugu zake.

Kukabiliana na Tisho Baya

Katika barua hii ya pili Petro anasema kwamba uhitaji wake wa kuonya Wakristo wenzake ni wa haraka zaidi kwa sababu yeye hana wakati mwingi zaidi wa kuishi. Anatoa orodha ya sifa ambazo ni lazima Wakristo wakuze ili waendelee kuwa wenye nguvu, kisha anataja nguvu fulani-fulani ambazo zitatokea ndani ya kundi ili kulidhoofisha.​—2 Petro 1:5-8, 14, 16.

‘Watakuwako pia walimu wa uongo miongoni mwenu ninyi,’ anaonya. (2 Petro 2:1, 2 NW) Walimu wa uongo hao wangeendeleza kati ya watu mwenendo mpotovu na kuwa mafundi katika kutumia “maneno ya bandia.” Lakini wangesahau jambo moja la maana kabisa: “Yehova ajua jinsi ya kuokoa watu wenye utawa katika jaribu, bali kuwaweka akiba watu wasio haki kwa siku ya hukumu wakatiliwe mbali.” (2 Petro 2:3, 9, NW): Huenda ikawa wangesitawi kwa muda, lakini hukumu yao ilikuwa hakika.

Wengine wangesema hivi kwa dhihaka: “Ku wapi huku kuwapo kwake kulikoahidiwa? Kwani, tangu ile siku mababu zetu walipolala usingizi wa kifo, mambo yote yaendelea sawasawa kama yalivyokuwa tangu mwanzo wa kuumba.” Hao, pia, wangesahau upesi kwamba wakati wa Yehova si sawa na wakati wetu. Naye ni mwenye subira. Lakini sawasawa na vile mwisho ulivyokuja kwa uhakika siku za Noa, ndivyo mwisho wa mfumo huu utakavyokuja.​—2 Petro 3:4-10, NW.

Mwishowe, hata katika siku za Petro wengine ndani ya kundi walikuwa ‘wakiyapotoa maandiko.’ Lakini kufanya hivyo kungewaletea wao wenyewe uharibifu.​—2 Petro 3:16.

Kwa sababu ya matisho hayo, Petro alitaka ‘kuamsha uwezo wa kufikiri waziwazi’ wa akina ndugu. (2 Petro 3:1, NW) Hawakupaswa kuyasahau mambo ya kihistoria yaliyohakikisha kwamba Yehova anaweza kuwaharibu waovu na kuwaokoa waadilifu, na iliwapasa “kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” (2 Petro 3:12, NW) Siku hiyo ni halisi. Inakuja. Uhakika huo unapasa kuongoza kila jambo wanalotenda au kupanga kutenda.​—2 Petro 1:19-21.

Kwa kuwa tunaishi karibu sana na siku hiyo himizo la Petro linapata nguvu zaidi: “Fanyeni bidii sana ili mwishowe mkutwe naye mkiwa hamna madoa na kasoro na katika amani.” (2 Petro 3:14, NW) Kwa kweli, maneno hayo yanatuhusu sisi. Mtume Petro anasema na kila mtu ambaye tumaini lake linategemea “mbingu mpya na nchi mpya” iliyoahidiwa na Yehova. Kwa hiyo, kitia-moyo chake cha mwisho kinasikika muda wa karne zote kikiwa na nguvu zote za mamlaka yake ya kimtume kikisema: “Jilindeni nafsi zenu, msije mkachukuliwa na kosa la hao wahalifu, mkaanguka na kuuacha uthibitifu wenu. Lakini, kueni katika neema, na katika kumjua Bwana wetu na Mwokozi Yesu Kristo.”​—2 Petro 3:13, 17, 18.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki