Kitabu cha Biblia Namba 62—1 Yohana
Mwandikaji: Mtume Yohana
Mahali Kilipoandikiwa: Efeso, au karibu
Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 98 W.K.
1. (a) Ni sifa gani yaenea katika miandiko yote ya Yohana, hata hivyo ni nini chaonyesha kwamba yeye hakuwa mtu wa kusisimuka bure tu? (b) Kwa nini barua zake tatu zilikuwa za wakati ufaao?
YOHANA, mtume mpendwa wa Yesu Kristo, alikuwa na upendo wenye nguvu kwa uadilifu. Hiyo ilisaidia kumpa muono-ndani wa kufahamu sana mambo yaliyokuwa ndani ya akili ya Yesu. Kwa hiyo hatushangai kwamba kichwa cha upendo ndilo jambo kuu la miandiko yake. Hata hivyo, yeye hakuwa mtu wa kusisimuka bure tu kwa maana Yesu alimrejezea kuwa mmoja wa “wana wa ngurumo [Boanerge].” (Mk. 3:17) Kwa uhakika, yeye aliandika barua zake tatu kwa kutetea kweli na uadilifu, kwa maana uasi-imani uliotabiriwa na mtume Paulo ulikuwa umeonekana wazi. Kwa kweli barua tatu za Yohana zilikuwa za wakati ufaao, kwa maana zilikuwa za kusaidia kuimarisha Wakristo wa mapema katika pigano lao na minyemeleo ya kujipenyeza kwa “yule mwovu.”—2 The. 2:3, 4; 1 Yn. 2:13, 14; 5:18, 19.
2. (a) Ni nini chaonyesha kwamba barua za Yohana ziliandikwa baada sana ya Mathayo, Marko, na zile barua za kimisionari? (b) Yaonekana barua hizo ziliandikwa lini na wapi?
2 Kwa kuamua kutokana na yaliyomo, barua hizi ni za kipindi cha baadaye sana kuliko Gospeli za Mathayo na Marko—za baadaye, pia, kuliko barua za kimisionari za Petro na Paulo. Nyakati zilikuwa zimebadilika. Hakuna mrejezo wowote kuhusu Dini ya Kiyahudi, ambayo ilikuwa ndilo tisho kubwa kwa makundi katika siku za uchanga wao; na haionekani kuwa kuna nukuu hata moja la moja kwa moja kutokana na Maandiko ya Kiebrania. Kwa upande mwingine, Yohana aongea juu ya “wakati wa mwisho” na kutokea kwa “wapinga Kristo wengi.” (1 Yn. 2:18) Arejezea wasomaji wake kwa semi kama “watoto wangu wadogo” na kujirejezea mwenyewe kuwa “mzee.” (1 Yn. 2:1, 12, 13, 18, 28; 3:7, 18; 4:4; 5:21; 2 Yn. 1; 3 Yn. 1) Yote hayo yaonyesha kwamba barua zake tatu ziliandikwa katika tarehe ya baadaye. Pia, 1 Yohana 1:3, 4 yaonekena ni kama yaonyesha kwamba Gospeli ya Yohana iliandikwa karibu wakati ule ule. Huaminiwa kwa ujumla kwamba barua tatu za Yohana zilimalizwa karibu 98 W.K., muda mfupi kabla ya kifo cha mtume, na kwamba ziliandikwa katika ujirani wa Efeso.
3. (a) Ni nini kithibitishacho uandikaji na uasilia wa Yohana wa Kwanza? (b) Ni habari gani zilizoongezwa baadaye, lakini ni nini chaonyesha si za kweli?
3 Jambo la kwamba Yohana wa Kwanza iliandikwa kwa kweli na Yohana mtume laonyeshwa na jinsi ilivyo na ufanani mwingi na Gospeli ya nne, ambayo pasipo shaka yeye ndiye aliyeiandika. Kwa kielelezo, yeye afanya utangulizi wa barua hiyo kwa kujieleza kuwa shahidi aliyeona “Neno la uzima . . . , uzima wa milele, uliokuwa kwa Baba, ukadhihirika kwetu,” hizo zikiwa ni semi zenye ufanani wa ajabu na zile ambazo Gospeli ya Yohana yafunguka kwazo. Kudumishwa kwa uasilia wayo kwathibitishwa na Muratorian Fragment na waandikaji wa mapema kama Irenaeus, Polycarp, na Papias, wote wakiwa wa karne ya pili W.K.a Kulingana na Eusebio (c. 260-342 W.K.), uasilia wa Yohana wa Kwanza hakukutiliwa shaka kamwe.b Hata hivyo, yapasa kuangaliwa kwamba tafsiri fulani za zamani zaidi zimeongezea sura ya 5 maneno yanayofuata mwishoni mwa mstari wa 7 na mwanzoni mwa mstari wa 8: “Mbinguni, Baba, na Neno, na Roho Mtakatifu, na watatu hawa ni umoja. Kisha wako watatu washuhudiao duniani.” (Union Version) Lakini andiko hili halipatikani katika yoyote ya hati-mkono za mapema za Kigiriki na kwa wazi limeongezewa ili kuimarisha fundisho la Utatu. Tafsiri zilizo nyingi za ki-siku-hizi, za Kikatoliki na Kiprotestanti, hazihusishi maneno haya katika wazo kuu la andiko.—1 Yn. 1:1, 2.c
4. Yohana anatafuta kulinda Wakristo wenzake na nani, naye akanusha mafundisho gani bandia?
4 Yohana aandika ili kulinda “wapendwa” wake, “watoto wachanga” wake, na mafundisho mabaya ya “wapinga Kristo wengi” ambao wametoka miongoni mwao na wanaojaribu kuwatongoza kutoka kwenye ukweli. (2:7, 18, NW) Hawa wapinga Kristo wenye kuasi imani wamevutwa na falsafa ya Kigiriki, kutia na Ugnosti wa mapema, ambao wafuasi wao hudai kuwa na maarifa maalumu juu ya namna ya mafumbo kutoka kwa Mungu.d Akichukua msimamo imara juu ya uasi-imani, Yohana ashughulika kirefu na vichwa vitatu: dhambi, upendo, na mpinga Kristo. Taarifa zake juu ya dhambi, na kwa utegemezo wa dhabihu ya Yesu kwa ajili ya dhambi, zaonyesha kwamba kwa kujihesabia uadilifu wao wenyewe wapinga Kristo hawa walikuwa wakidai hawana dhambi na hawana uhitaji wa dhabihu ya ukombozi ya Yesu. “Maarifa” yao ya kujifikiria wenyewe tu yamewafanya wawe wabinafsi na wasio na upendo, hali ambayo Yohana aifunua wazi akaziapo upendo wa kweli wa Kikristo kwa uendelevu. Zaidi ya hilo, yaonekana kwamba Yohana anapambana na fundisho lao bandia wakati afafanuapo kwamba Yesu ndiye Kristo, kwamba alikuwako kabla hajawa mwanadamu, na kwamba alikuja katika mwili akiwa Mwana wa Mungu ili atolee wanadamu wanaoamini wokovu. (1:7-10; 2:1, 2; 4:16-21; 2:22; 1:1, 2; 4:2, 3, 14, 15) Yohana huwabandika hawa walimu bandia jina la “wapinga Kristo,” naye atoa njia kadhaa ambazo katika hizo watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi waweza kutambuliwa.—2:18, 22; 4:3.
5. Ni nini chaonyesha kwamba Yohana wa Kwanza ilikusudiwa kwa kundi zima la Kikristo?
5 Kwa kuwa hakuna kundi lenye kurejezewa waziwazi, bila shaka barua hii ilikusudiwa kwa ajili ya ushirika mzima wa Kikristo. Ukosefu wa salamu mwanzoni na salamu mwishoni ungeonyesha hivyo pia. Watu fulani wameeleza mwandiko huu kuwa maelezo yenye kuelekezwa kwa watu fulani hasa wala si barua. Utumizi wa ‘nyinyi’ sehemu zote waonyesha kwamba mwandikaji alielekeza maneno yake kwa kikundi fulani wala si kwa mtu mmoja.
YALIYOMO KATIKA YOHANA WA KWANZA
6. Yohana afanya tofauti gani kati ya wale watembeao katika nuru na wale walio katika giza?
6 Kutembea katika nuru, si katika giza (1:1–2:29). “Haya twayaandika,” asema Yohana, “ili furaha yetu itimizwe.” Kwa kuwa “Mungu ni nuru,” wale tu ‘wanaoenenda nuruni’ ndio ‘wanaoshirikiana naye’ na pamoja na mtu na mwenzake. Hao wamesafishwa dhambi kwa “damu yake Yesu, Mwana wake.” Kwa upande mwingine, wale ambao ‘wanaenenda gizani’ na kudai hivi, “Hatuna dhambi,” wanajidanganya wenyewe, na kweli haimo ndani yao. Wakiziungama dhambi zao, Mungu atakuwa mwaminifu na kuwasamehe.—1:4-8.
7. (a) Mtu huonyeshaje kwamba amjua na kumpenda Mungu? (b) Mpinga Kristo atambulishwaje?
7 Yesu Kristo atambulishwa kuwa “dhabihu ya upatanisho” kwa ajili ya dhambi, akiwa “msaidiaji pamoja na Baba.” Yeye adaiye kumjua Mungu lakini hashiki amri Zake ni mwongo. Yeye apendaye ndugu yake hubaki katika nuru, lakini yeye achukiaye ndugu yake anatembea katika giza. Yohana ashauri kwa imara kutopenda ulimwengu wala mambo yaliyo katika ulimwengu, kwa maana, yeye asema, “Ikiwa mtu yeyote apenda ulimwengu, upendo wa Baba haumo ndani yake.” Wapinga Kristo wengi wamekuja, ‘nao walienda wakatoka kwetu,’ aeleza Yohana, kwa maana “hawakuwa wa namna yetu.” Mpinga Kristo ndiye hukana kwamba Yesu si Kristo. Yeye hukana Baba na Mwana pia. Acheni “watoto wadogo” wakae na yale ambayo wamejifunza kuanzia mwanzo ili ‘wakae katika mwungano pamoja na Mwana na katika mwungano pamoja na Baba,’ kulingana na upakwa-mafuta waliopokea kutoka kwake, ambao ni wa kweli.—2:1, 2, 15, 18, 19, 24, NW.
8. (a) Ni nini hupambanua watoto wa Mungu kutoka kwa wale wa Ibilisi? (b) “Watoto wadogo” wamekujaje kuujua upendo, na ni lazima waendelee kufanya uchunguzi gani juu ya mioyo yao?
8 Watoto wa Mungu hawazoei dhambi (3:1-24). Kwa sababu ya upendo wa Baba, wao huitwa “wana wa Mungu,” na kwenye udhihirisho wa Mungu watafanana naye na ‘kumwona kama alivyo.’ Dhambi ni kutotii sheria, na wale wanaobaki katika mwungano pamoja na Kristo hawazoei dhambi. Yule ambaye aendeleza dhambi hutokana na Ibilisi, ambaye Mwana wa Mungu atavunja-vunja kazi zake. Watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi huonekana wazi hivyo: Wale wanaotokana na Mungu wana upendo kwa mtu na mwenzake, lakini wale wanaotokana na yule mwovu ni kama Kaini, aliyechukia na kuchinja ndugu yake. Yohana awaambia “watoto wadogo” kwamba wao wamekuja kujua upendo kwa sababu “yeye aliutoa uhai wake kwa ajili’ yao, naye awaonya ‘wasizuie huruma zao’ kwa ndugu zao. Acheni wao ‘wapende, si katika neno wala kwa ulimi, bali katika tendo na kweli.’ Ili kupambanua kama wao ‘ni wa kweli,’ ni lazima wachunguze yaliyo katika mioyo yao na kuona kama ‘wanayatenda yapendezayo machoni pake’ Mungu. Ni lazima washike amri yake ‘kuliamini jina la Mwana wake Yesu Kristo, na kupendana wao kwa wao.’ Hivyo watajua kwamba wao wanabaki katika mwungano pamoja naye, na yeye pamoja nao kwa roho.—3:1, 2, 16-19, 22, 23.
9. (a) Ni mtihani gani upasao kufanywa juu ya semi zilizopuliziwa? (b) Ni nini hukazia wajibu wa kupendana?
9 Kupendana katika mwungano pamoja na Mungu (4:1–5:21). Semi zilizopuliziwa zapasa kupitishwa kwenye mtihani. Semi zile ambazo hukana kwamba Kristo alikuja katika mwili ‘hazitokani na Mungu’ bali ni za mpinga Kristo. Zatokana na ulimwengu na zimo katika mwungano pamoja nao, lakini usemi uliopuliziwa na Mungu wa ukweli ni kutoka kwa Mungu. Yohana asema hivi: “Mungu ni upendo,” na “hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.” Basi, jinsi ulivyo mkubwa wajibu wa kupendana! Wale wapendao wengine huwa na Mungu akibaki katika mwungano pamoja nao, na hivyo upendo umekamilishwa ili kwamba ‘wawe na ujasiri,’ unaotupa hofu nje. Yohana asema, “Sisi twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza.” “Yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake.”—4:3, 8, 10, 17, 19, 21.
10. (a) Ni jinsi gani watoto wa Mungu wawezavyo kuushinda ulimwengu, nao wana uhakika gani? (b) Ni lazima wawe na maoni gani kuelekea dhambi na ibada ya sanamu?
10 Kuonyesha upendo kama watoto wa Mungu kwamaanisha kushika amri zake, na tokeo la hilo huwa kushinda ulimwengu, kupitia imani. Kwa habari ya wale wanaotia imani katika Mwana wa Mungu, Mungu atoa ushahidi kwamba Yeye aliwapa “uzima wa milele; na uzima huu umo katika Mwanawe.” Hivyo, wao waweza kuwa na uhakika kwamba yeye atawasikia katika lolote waombalo kulingana na mapenzi yake. Ukosefu wote wa uadilifu ni dhambi, hata hivyo kuna dhambi isiyoleta kifo. Kila mtu aliyezaliwa kutoka kwa Mungu hafanyi zoea la dhambi. Ingawa “dunia yote pia hukaa katika yule mwovu . . . , Mwana wa Mungu amekwisha kuja,” naye amewapa wanafunzi wake “akili” ya kupata maarifa ya Mungu wa kweli, ambao sasa wao wana umoja naye kwa njia ya “Mwana wake Yesu Kristo.” Ni lazima pia wajilinde na sanamu!—5:11, 19, 20.
KWA NINI NI CHENYE MAFAA
11. Ni jinsi gani Wakristo leo waweza kupambana na wapinga Kristo na tamaa za kilimwengu?
11 Kama vile katika miaka ya kumalizia ya karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida, ndivyo leo kulivyo na “wapinga Kristo wengi” ambao ni lazima Wakristo waonywe juu yao. Ni lazima hawa Wakristo wa kweli washike sana ‘ujumbe waliousikia kutoka mwanzo, wapendane,’ na kubaki katika mwungano pamoja na Mungu na fundisho la kweli, wakizoea uadilifu kwa uhuru wa usemi. (2:18; 3:11; 2:27-29) Lililo la maana kabisa pia ni onyo juu ya “tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima,” yale maovu ya kilimwengu ya kufuatia vitu vya kimwili ambayo yamegharikisha walio wengi wa wenye kujidai kuwa Wakristo. Wakristo wa kweli wataepuka ulimwengu na tamaa yao, wakijua kwamba “yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.” Katika muda huu wa tamaa ya kilimwengu, ufarakano wa kidini, na chuki, kuna mafaa kweli kweli kujifunza mapenzi ya Mungu kupitia Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu na kufanya mapenzi hayo!—2:15-17.
12. Ni tofauti gani ambazo Yohana wa Kwanza yafanya kwa mafaa yetu, nasi twaweza kuushindaje ulimwengu?
12 Ni kwa mafaa yetu kwamba Yohana wa Kwanza yatofautisha wazi kati ya nuru itokanayo na Baba na giza lenye kuharibu kweli litokalo kwa yule mwovu, kati ya mafundisho yenye kupa uhai ya Mungu na uwongo mdanganyifu mbalimbali wa mpinga Kristo, kati ya upendo ulieneao kundi zima la wale walio katika mwungano na Baba pamoja na Mwana na ile chuki ya uuaji kama ya Kaini iliyo katika wale ambao “walitoka kwetu . . . ili wafunuliwe kwamba si wote walio wa kwetu.” (2:19; 1:5-7; 2:8-11, 22-25; 3:23, 24, 11, 12) Tukiwa na uthamini huo, yapasa kuwa tamaa yetu yenye bidii nyingi ‘kuushinda ulimwengu.’ Nasi twawezaje kufanya hivyo? Kwa kuwa na imani yenye nguvu na kwa “kumpenda Mungu,” ambako kwamaanisha kushika amri zake.—5:3, 4.
13. (a) Upendo wa Mungu wakaziwaje kuwa wenye nguvu inayotumika? (b) Upendo wa Mkristo wapasa kuwa wa aina gani, ukitokeza mwungano gani?
13 “Kumpenda Mungu”—lo! nguvu hii yenye kuchochea yakaziwa vizuri kama nini mwotemwote katika barua hii! Katika sura ya 2 twapata tofauti ya wazi sana ikifanywa kati ya kuupenda ulimwengu na kumpenda Baba. Baadaye uangalifu wetu wavutwa kwenye jambo la kwamba “Mungu ni upendo.” (4:8, 16) Nao ni upendo wenye kufanya kazi kama nini! Wapatikana katika wonyesho wao mtukufu katika kutuma kwa Baba “Mwana [wake] kuwa Mwokozi wa ulimwengu.” (4:14) Hilo lapasa kuchochea katika mioyo yetu upendo usio na hofu, wenye uthamini kupatana na maneno ya mtume: “Sisi twapenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza.” (4:19) Upendo wetu wapasa kuwa wa aina ile ile kama ule wa Baba na Mwana—upendo wa kudhabihu, wenye kufanya kazi. Kama vile Yesu alivyotoa nafsi yake kwa ajili yetu, “imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu,” ndiyo, kutozuia huruma zetu nyororo ili tuwapende ndugu zetu, si kwa maneno tu, bali “kwa tendo na kweli.” (3:16-18) Kama vile barua ya Yohana ionyeshavyo wazi sana, ni upendo huu, kwa kuunganishwa na maarifa ya kweli juu ya Mungu, ambao huwafunga pamoja wale wanaoendelea kutembea pamoja na Mungu katika mwungano usiovunjika pamoja na Baba na Mwana. (2:5, 6) Warithi wa Ufalme walio katika kifungo hiki chenye kubarikiwa ndio ambao Yohana asema kwao hivi: “Nasi tumo ndani yake yeye aliye wa kweli, yaani, ndani ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli, na uzima wa milele.”—5:20.
[Maelezo ya Chini]
a The International Standard Bible Encyclopedia, Buku 2, 1982, iliyohaririwa na G. W. Bromiley, kurasa 1095-6.
b The Ecclesiastical History, III, XXIV, 17.
c Insight on the Scriptures, Buku 2, ukurasa 1019.
d New Bible Dictionary, hariri la pili, 1986, kilichohaririwa na J. D. Douglas, kurasa 426, 604.