Sura 13
Kujifunza Kutokana na Vishawishi vya Yesu
MARA tu baada ya ubatizo wake, Yesu aongozwa na roho ya Mungu kuingia katika jangwa la Yudea. Ana mengi ya kufikiria, kwa maana kwenye ubatizo wake ‘mbingu zilimfunukia’ ili aweze kufahamu mambo ya kimbingu. Kwa kweli, ana mambo mengi ya kutafakari!
Yesu atumia michana 40 na masiku 40 katika jangwa, naye hali chochote wakati huo. Halafu, anapoona njaa sana, Ibilisi amwendea amshawishi, akisema: “Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, amuru kwamba mawe haya yawe mikate.” Lakini Yesu ajua kwamba ni kosa kutumia nguvu zake za kimuujiza kutosheleza tamaa za kibinafsi. Kwa hiyo akataa kushawishwa.
Lakini Ibilisi haachi. Ajaribu njia nyingine. Amtolea Yesu mwito kwamba aruke kutoka ukuta wa hekalu ili malaika za Mungu wamwokoe. Lakini Yesu hashawishwi ajionyeshe kwa njia hiyo ya kutazamisha. Akitumia maneno ya Maandiko, aonyesha kwamba ni kosa kumjaribu Mungu kwa njia hiyo.
Katika kishawishi cha tatu, Ibilisi amwonyesha Yesu milki zote za ulimwengu kwa njia fulani ya kimuujiza na kusema: “Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia.” Lakini Yesu akataa tena kujiachilia ashindwe na kishawishi cha kufanya kosa, akichagua kuendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu.
Tunaweza kujifunza mambo fulani kutokana na vishawishi hivyo vya Yesu. Kwa kielelezo, vinaonyesha kwamba Ibilisi si sifa tu ya uovu, kama wanavyodai watu wengine, bali kwamba yeye ni mtu halisi, asiyeonekana. Kushawishwa kwa Yesu kunaonyesha pia kwamba serikali zote za ulimwengu ni mali ya Ibilisi. Kwa maana toleo la Ibilisi kwa Yesu la serikali hizo lingaliwezaje kuwa la kweli kama hasingekuwa zake kikweli?
Tena fikiria jambo hili: Ibilisi alisema alikuwa na nia ya kumthawabisha Yesu kwa kitendo kimoja cha ibada, hata kumpa milki zote za ulimwengu. Huenda Ibilisi akajaribu kutushawishi sisi kwa njia inayofanana na hiyo, labda kwa kuweka mbele yetu nafasi yenye kuamsha sana tamaa yetu ya kujipatia utajiri wa kilimwengu, mamlaka, au cheo. Lakini tungekuwa wenye hekima sana tukifuata kielelezo cha Yesu kwa kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu hata tupatwe na kishawishi gani! Mathayo 3:16; 4:1-11; Marko 1:12, 13; Luka 4:1-13.
▪ Yaonekana ni mambo gani Yesu atafakari wakati wa siku zake 40 za kuwa jangwani?
▪ Ibilisi ajaribuje kumshawishi Yesu?
▪ Tunaweza kujifunza nini kutokana na vishawishi vya Yesu?