Maisha na Huduma ya Yesu
Kujifunza Kutokana na Vishawishi vya Yesu
MARA tu baada ya ubatizo wake, Yesu anaongozwa na roho ya Mungu kuingia katika jangwa la Yudea. Ana mengi ya kufikiria, kwa maana kwenye ubatizo wake “mbingu zilifunguliwa” ili aweze kufahamu mambo ya kimbingu. Hivyo sasa Yesu anayakumbuka kwa ukamili maisha aliyokuwa nayo akiwa mwana wa kiroho wa Mungu, kutia na mambo yote ambayo Mungu alikuwa amemwambia. Kwa kweli, ana mambo mengi ya kutafakari!
Yesu anatumia michana 40 na masiku 40 katika jangwa, naye hali cho chote wakati huo. Halafu, anapoona sana njaa, Ibilisi anamfikia amshawishi, akisema: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, ambia mawe haya yawe madonge ya mkate.” Lakini Yesu anajua ni kosa kutumia nguvu za miujiza alizo nazo ili atosheleze tamaa zake binafsi. Kwa hiyo anakataa kushawishwa.
Lakini Ibilisi haachi. Anajaribu njia nyingine. Anamtolea Yesu mwito wa ushindani kwamba aruke kutoka ukuta wa hekalu ili malaika za Mungu wamwokoe. Lakini Yesu hashawishiki ajionyeshe kwa njia hiyo ya kutazamisha. Akitumia maneno ya Maandiko, anaonyesha kwamba ni kosa kumjaribu Mungu kwa njia hiyo.
Katika kishawishi cha tatu, Ibilisi anamwonyesha Yesu falme zote za ulimwengu kwa njia fulani ya muujiza na kusema: “Vitu vyote hivi nitakupa wewe ikiwa utaanguka na kufanya tendo moja la kuniabudu mimi.” Lakini Yesu anakataa tena kujiachilia ashindwe na kishawishi cha kufanya kosa, akichagua kubaki mwaminifu kwa Mungu.
Tunaweza kujifunza mambo fulani kutokana na vishawishi hivyo vya Yesu. Kwa mfano, vinaonyesha kwamba Ibilisi si sifa tu ya uovu, kama wanavyodai watu wengine, bali kwamba yeye ni mtu halisi, asiyeonekana. Kushawishwa kwa Yesu kunaonyesha pia kwamba serikali zote za ulimwengu ni mali ya Ibilisi. Kwa maana toleo la Ibilisi kwa Yesu la serikali hizo lingaliwezaje kuwa halisi kama si zake kikweli?
Tena fikiria jambo hili: Ibilisi alisema alikuwa na nia ya kumthawabisha Yesu kwa kitendo kimoja cha ibada, hata kumpa falme zote za ulimwengu. Huenda Ibilisi akajaribu kutushawishi sisi kwa njia inayofanana na hiyo, labda aweke mbele yetu nafasi zenye kuamsha sana tamaa yetu ya kujipatia utajiri wa kilimwengu, mamlaka, au cheo. Lakini tungekuwa wenye hekima sana tukifuata mfano wa Yesu kwa kubaki waaminifu kwa Mungu hata iwe tutapatwa na kishawishi gani! Mathayo 3:16; 4:1-11; Marko 1:12, 13; Luka 4:1-13, NW.
◆ Maana yake nini kwamba Yesu alifunguliwa mbingu?
◆ Ibilisi alijaribuje kumshawishi Yesu?
◆ Tunaweza kujifunza nini kutokana na vishawishi vya Yesu?
[Picha ya ukurasa nzima katika ukurasa wa 7]