Kwa Sababu Gani Tusali Kuomba Ufalme wa Mungu?
“BABA yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.
Kwa karibu miaka 2,000, Wakristo waaminifu wameyatumia maneno hayo kama kielelezo cha sala zao wenyewe ambazo wanampelekea Mungu. Hiyo ni sala iliyosemwa kwanza na Yesu Kristo, nayo inajulikana kuwa Sala ya Bwana au ya Baba Yetu.
Lakini, leo watu wengi hawaisali tena Sala ya Bwana. Badala ya kuutegemea Ufalme wa Mungu, wanategemea serikali za kibinadamu, mifumo ya kiuchumi, njia za kisayansi, au Umoja wa Mataifa uwatolee tumaini kwa wakati ujao. Je! wewe unafanya hivyo? Ikiwa ndivyo, je, kwa kufanya hivyo unafanya jambo linalofaa?
Matatizo Yaliyopo
Watu wengine wanauona ustaarabu wa leo kuwa ndio wenye ufanisi mwingi zaidi katika historia yote. Lakini umo mashakani. Kuna kani nyingi zinazoelekea kufanya kusiwe na wakati ujao katika mambo ya ustaarabu, hata wakati ujao wa uhai wenyewe hapa duniani. Fikiria chache tu kati ya kani hizo zenye kuleta tisho.
Silaha za Nyukilia:
Jumla ya nguvu za silaha za namna hiyo zinazopatikana kwa sasa zinalingana na zaidi ya tani tatu za TNT kwa kila mwanamume, mwanamke, na mtoto aliye duniani. Katika makala yenye kichwa “Lile Kombora—Je! Limekuwa Lisiloweza Kuzuiwa?” Mwandikaji Mkanada wa habari za majarida, David Lanchasire, alisema kwamba “kwa sababu ya silaha kuendelea kutengenezwa zikiwa za hali ya juu zaidi, uwezekano umeongezeka wa kuweza kutokea kwa vita ya aksidenti kutokana na kosa la kompyuta.” Tena aliutaja uchunguzi uliofanywa na Umoja wa Mataifa kuwa ukisema hivi: “Historia inaonyesha kwamba namna fulani ya silaha ikiisha kufanyiwa maendeleo mpaka iache kuwa silaha ya matumizi ya kujaribia tu, kwa kawaida silaha hiyo itatumiwa. Hata hivyo sivyo imekuwa kwa silaha za nyukilia, isipokuwa zilipotumiwa katika visa viwili [kule Hiroshima na Nagasaki], lakini hakuwezi kuwa na uhakikisho wa kwamba zitabaki bila kutumiwa.”
Umaskini wa Ulimwenguni Pote:
Ingawa leo mataifa fulani yana kiwango cha juu kabisa cha maisha, mengine ni maskini wa mwisho. Mwandikaji katika gazeti New Scientist aliona kwamba ukosefu wa usawa ukiendelea kuwapo kati ya watu, “yataelekeza kwenye namna fulani ya pigano lisiloepukika.” Lakini hata usipoongoza kwenye pigano, ukosefu huo wa usawa unaweza kuleta maafa. Jinsi gani?
Nchi zilizo maskini zaidi zina madeni makubwa sana. Mwaka 1981 mchangaji wa habari za magazeti, John Madeley, alieleza hivi: “Jambo hilo limeuweka mfumo wa ulimwengu wa benki na mambo ya kifedha karibu na anguko kubwa kuliko lile ambalo benki zenyewe zimetaka kukiri wakati uliopita. Yasipofanywa bila kukawia mabadiliko makubwa sana katika mfumo wa kiuchumi wa ulimwengu ili kuzipa nchi zinazositawi nafasi ya kuchuma pesa nyingi zaidi, [kungeweza kuwako] upungufu mwingi zaidi na marekebisho mapya katika mipango, kisha kuwe daima na mwelekeo wa kupatwa na mfululizo wa anguko.” (World Press Review) Katika nchi mbalimbali, mfumo wa kifedha unabaki katika hali yenye mashaka.
Anga Lililochafuliwa:
Kwa muda mrefu, wanadamu wameendelea kuingiza-ingiza vichafuaji katika anga, wasitake kukomesha jambo hilo. Sasa, kulingana na Chicago Tribune, “hesabu inayoongezeka ya wanasayansi wanaogopa kwamba tabaka ya hewa ya Dunia imesukumwa ikafikia kadiri ambayo huenda mabadiliko yenye uharibifu yakatokea, kama tufe lililofura likakaribia kupasuka. . . . Mengine ya maafa hayo yamekwisha kutujilia na mengine yatakuja karibuni kuliko inavyotazamiwa.”
Maji Yaliyochafuliwa:
Wanadamu wamechafua maji ya dunia katika sehemu mbalimbali. Kwa mfano, katika United States inaripotiwa hivi: “Katika Biscayne Bay, samaki wanageuka kuwa madude yenye ugonjwa. Katika New Orleans, ambako kemikali tofauti-tofauti 112 zimepatikana katika maji ya kunywa, hesabu ya watu wanaouawa na kansa inapanda sana. Kutoka pwani mpaka pwani, watu na wanyama pia wanapata hasara yenye kuogopesha kwa sababu uchafu unaendelea kutiwa katika maji safi yetu, maji yetu ya baharini, na maji yetu yaliyo katika mabomba.”—New Times.
Hayo ni machache tu kati ya matatizo yanayofanya wakati ujao wetu uwe wenye hatari. Mengine ni kutia kumalizika kwa vyanzo vya nishati, ongezeko kubwa mno la watu, kuharibiwa kwa misitu, kuenea kwa majangwa, na upungufu unaoongezeka wa maji safi. Huenda ikawa kwamba mengine ya matisho yametiliwa chumvi kuliko jinsi yalivyo hasa. Lakini je, kwa kusema kweli wewe unaamini kwamba yote yametiliwa chumvi? Na unapoyafikiria matatizo yote hayo kwa ujumla, je, unafikiri kwamba mwanadamu ana uwezekano wo wote wa kuyatatua? Na hali yasipotatuliwa, jamii ya kibinadamu itakuwapo wakati ujao? Tena ni kwa sababu gani tumekumbwa na matatizo mengi sana yanayoelekea kuwa yasiyotatulika?
Matatizo Yameletwa na Nini?
Matatizo hayo yanaonyesha ukweli mmoja wa msingi: Mwanadamu hawezi kujisimamia mwenyewe kwa matokeo mazuri. Hakuna mtawala ye yote wa kibinadamu ambaye amepata kuwa na hekima, hali ya kufikiria wengine bila uchoyo, au uwezo wa kusimamia watu kwa njia yenye kumfaidi kabisa kila mtu. Biblia inatuambia hivi: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Mwanadamu hakufanyizwa ili ajitawale mwenyewe.
Pia kuna jambo jingine, ambalo watu wengi wanaona ni vigumu kulikubali katika kizazi hiki cha utafutaji wa vitu vya kimwili. Utawala wa wanadamu hauhusu wanadamu peke yao. Wakati Yesu alipokuwa duniani, mtu fulani mwenye nguvu zinazozidi zile za kibinadamu, yaani, Shetani, alimtolea utawala wa falme zote za ulimwengu. Na baadaye, Paulo mfuasi wa Yesu alimwita Shetani “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (Mathayo 4:8, 9; 2 Wakorintho 4:4, NW) Shetani anaweza kuwaje ndiye mtawala wa ulimwengu huu, hali watu wengi sana hawana tena imani naye? Ni kwa sababu watu walio wengi—hata bila kujua—hawaukubali utawala wa Mungu na kwa hiyo wanaendeleza hila za Shetani.—Mathayo 12:30.
Hali ya Shetani imekuwa mbaya zaidi tangu siku za Yesu. Biblia inafunua kwamba leo Shetani ana “ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:12) Kama Hitler mwishoni mwa ile vita ya ulimwengu ya mwisho, Shetani sasa ameazimia sana “kutawala au kuharibu.” Kwa kuwa utawala wake wa muda mrefu umekosa sana mafanikio, ni wazi sasa Shetani Ibilisi amekaza nia sana aharibu jamii ya kibinadamu. Je! si jambo linalopasa kufikiriwa kwa uzito kujua kwamba kuna kani yenye nia ya uadui na nguvu nyingi namna hiyo? Ndivyo ilivyo hasa tunapokumbuka kwamba zile silaha zote za nyukilia ambazo zimerundikwa zinaelekea kuwa ‘zisizoweza kuzuiliwa na mwanadamu’! Lakini yote hayo yanahusianaje na Ufalme wa Mungu?
Tunauhitaji Ufalme
Kwa kuwa matatizo yetu yanaletwa na kutokuweza kwa mwanadamu kujitawala mwenyewe, pia na mavutano yenye kudhuru ya nguvu fulani yenye nguvu zinazozidi zile za mwanadamu, ni wazi kwamba utatuzi wayo unapatikana nje ya jamii ya kibinadamu. Hiyo ndiyo sababu tunauhitaji sana Ufalme wa Mungu. Ufalme huo ni serikali halisi. Lakini ina nguvu nyingi kuliko ile ya kibinadamu, ni ya kimbingu, na ina uwezo wa kumshinda Shetani. Kwa kuwa serikali hiyo ni Ufalme wa Mungu, ina hekima, fadhili, na mamlaka ya kufanya maamuzi yanayofaa na kutawala kwa mafanikio.
Kwa hiyo, tunaweza kufurahi kwamba Biblia inatuambia: “Katika siku za wafalme hao [watawala wa kisasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Danieli 2:44) Mfalme wa Ufalme huo ni Yesu Kristo, ambaye amesemwa hivi kwa unabii: “Katika siku zake mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo. Naye atakuwa na raia kutoka bahari mpaka bahari na kutoka Mto mpaka miisho ya dunia.”—Zaburi 72:7, 8, NW.
Ndiyo, Ufalme wa Mungu utatatua matatizo ya wanadamu. Sababu gani basi usiipekue Biblia uone Ufalme huo ni nini na jinsi wewe unavyoweza hata sasa kuwa raia wake. Wewe, na wanadamu wengine wote, unauhitaji kweli kweli Ufalme huo. Mashahidi wa Yehova wako tayari kukusaidia ujue habari zinazouhusu.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]
U.S. National Archives
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]
WHO photo