Sura 17
Kumfundisha Nikodemo
ANAPOKUWA akihudhuria Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka 30 W.K., Yesu afanya ishara za kustaajabisha, au miujiza. Matokeo ni kwamba, watu wengi wamwamini. Nikodemo, mshiriki mmoja wa Sanhedrini, ambayo ni mahakama kuu ya Kiyahudi, avutiwa na mambo hayo na kutaka kujua mengi zaidi. Kwa hiyo amtembelea Yesu wakati wa giza la usiku, labda kwa kuhofu kwamba akionwa sifa yake itaharibika mbele ya viongozi wale wengine Wayahudi.
“Rabi,” asema, “twajua ya kuwa u mwalimu, umetoka kwa Mungu; kwa maana hakuna mtu awezaye kuzifanya ishara hizi uzifanyazo wewe, isipokuwa Mungu yu pamoja naye.” Kwa kujibu, Yesu amwambia Nikodemo kwamba ili mtu auingie Ufalme wa Mungu, ni lazima ‘azaliwe mara ya pili.’
Hata hivyo, mtu aweza kuzaliwaje mara ya pili? “Aweza kuingia tumboni mwa mamaye mara ya pili akazaliwa?” Nikodemo auliza.
Hapana, hiyo siyo maana ya kuzaliwa mara ya pili. “Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho,” Yesu aeleza, “hawezi kuuingia ufalme wa Mungu.” Wakati Yesu alipobatizwa na roho takatifu ikashuka juu yake, kwa njia hiyo alizaliwa ‘kwa maji na roho.’ Kwa kuandamanisha jambo hilo na tangazo lililotoka mbinguni kusema, ‘Huyu ni Mwanangu ninayependezwa naye,’ Mungu alitangaza kwamba alikuwa amezaa mwana wa kiroho mwenye taraja la kuuingia Ufalme wa kimbingu. Baadaye, wakati wa Pentekoste ya mwaka 33 W.K., wengine waliobatizwa watapokea roho takatifu na hivyo wao pia wazaliwe mara ya pili wakiwa wana wa kiroho wa Mungu.
Lakini ni la maana sana fungu lile linalotimizwa na Mwana wa kibinadamu wa Mungu aliye maalumu kwake. “Kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani,” Yesu amwambia Nikodemo, “vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele.” Ndiyo, kama vile Waisraeli wale walioumwa na nyoka wenye sumu walivyopaswa kumtazama nyoka wa shaba ili waokolewe, ndivyo wanadamu wote wanavyohitaji kujizoeza imani katika Mwana wa Mungu ili waokolewe kutoka hali yao ya kufa.
Akikazia fungu lenye upendo analotimiza Yehova katika jambo hilo, Yesu amwambia Nikodemo: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Hivyo, miezi sita tu baada ya Yesu kuanza huduma yake, ajulisha waziwazi hapa Yerusalemu kwamba yeye ndiye njia ya Yehova ya kuokolea aina ya kibinadamu.
Yesu aendelea kumweleza zaidi Nikodemo: “Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu,” yaani, si auhukumu vibaya, au kuushutumu, akiihukumia uharibifu jamii ya kibinadamu. Bali, kama Yesu asemavyo, alitumwa ili “ulimwengu uokolewe katika yeye.”
Nikodemo kwa hofu amemjia Yesu wakati wa giza la usiku. Kwa hiyo inapendeza kwamba Yesu amalizia mazungumzo yake pamoja naye kwa kusema: “[Hii] ndiyo hukumu; ya kuwa nuru [ambayo Yesu aliipa utu katika maisha na mafundisho yake] imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa. Bali yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu.” Yohana 2:23-3:21; Mathayo 3:16, 17; Matendo 2:1-4; Hesabu 21:9.
▪ Ni jambo gani lililomsukuma Nikodemo amtembelee Yesu, na kwa nini akaja usiku?
▪ Maana yake nini ‘kuzaliwa mara ya pili’?
▪ Yesu aonyeshaje fungu atimizalo ili sisi tupate wokovu?
▪ Inamaanisha nini kwamba Yesu hakuja kuhukumu ulimwengu?