Maisha na Huduma ya Yesu
Kumfundisha Nikodemo
ANAPOKUWA akihudhuria Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka 30 W.K., Yesu anafanya ishara za kustaajabisha, au miujiza. Matokeo ni kwamba watu wengi wanamwamini. Nikodemo, mshiriki mmoja wa Sanhedrini, ambayo ni mahakama kuu ya Kiyahudi, anavutiwa na mambo hayo na kutaka ajue mengi zaidi. Kwa hiyo anamtembelea Yesu wakati wa giza la usiku, labda kwa kuogopa kwamba akionwa sifa yake itaharibika mbele ya viongozi wale wengine Wayahudi.
“Rabi,” anasema, “twajua ya kuwa u mwalimu, umetoka kwa Mungu; kwa maana hakuna mtu awezaye kuzifanya ishara hizi uzifanyazo wewe, isipokuwa Mungu yu pamoja naye.” Kwa kujibu, Yesu anaambia Nikodemo kwamba ili mtu auingie Ufalme wa Mungu ni lazima ‘azaliwe mara ya pili.’
Hata hivyo mtu anaweza kuzaliwaje mara ya pili? “Aweza kuingia tumboni mwa mamaye mara ya pili akazaliwa?” Nikodemo anauliza.
Hapana, hiyo siyo maana ya kuzaliwa mara ya pili. “Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa [roho],” Yesu anaeleza, “hawezi kuuingia ufalme wa Mungu.” Wakati Yesu alipobatizwa kisha roho takatifu ikashuka juu yake, kwa njia hiyo alizaliwa ‘kwa maji na roho.’ Kwa kufuatanisha jambo hilo na tangazo lililotoka mbinguni kusema, ‘Huyu ni Mwanangu ninayependezwa naye,’ Mungu alitangaza kwamba alikuwa amezaa mwana wa kiroho mwenye taraja la kuuingia Ufalme wa kimbingu. Baadaye, wakati wa Pentekoste ya mwaka 33 W.K., wabatizwa wengine walipokea roho takatifu na hivyo wao pia ‘wakazaliwa mara ya pili’ wakiwa wana wa kiroho wa Mungu.
Lakini ni ya maana sana sehemu ile inayotimizwa na Mwana wa kibinadamu wa Mungu aliye maalum kwake. “Kama vile Musa alivyomwinua yule nyoka jangwani,” Yesu anamwambia Nikodemo, “vivyo hivyo Mwana wa Adamu hana budi kuinuliwa; ili kila mtu aaminiye awe na uzima wa milele.” Ndiyo, kama vile Waisraeli wale walioumwa na nyoka wenye sumu walivyopaswa kumtazama nyoka wa shaba ili waokolewe, ndivyo wanadamu wote wanavyohitaji kujizoeza imani katika Mwana wa Mungu ili waokolewe kutoka hali yao ya kufa.
Akikazia sehemu yenye upendo anayotimiza Yehova katika jambo hilo, Yesu anamwambia Nikodemo: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Hivyo, miezi sita tu baada ya Yesu kuanza huduma yake, anajulisha waziwazi hapa Yerusalemu kwamba yeye ndiye njia ya Yehova ya kuokolea wanadamu. Yohana 2:23–3:21; Mathayo3:16, 17; Matendo 2:1-4; Hesabu 21:9.
◆ Ni jambo gani lililofanya Nikodemo afanye ziara, na kwa sababu gani akaja usiku?
◆ Maana yake nini ‘kuzaliwa mara ya pili’?
◆ Yesu alionyeshaje sehemu anayotimiza ili sisi tupate wokovu?