Ni Nani Wanaozaliwa Mara ya Pili?
JE! WATU wote wazuri wanaenda mbinguni? Watu wengi hufikiri hivyo, lakini Yesu Kristo hakukubaliana na hilo. Akisema na mtawala Myahudi Nikodemo, aliyekuja kwake usiku, Yesu alisema: “Hakuna mtu aliyepaa mbinguni.”—Yohana 3:13.
Hata hivyo, Yesu alimwonyesha Nikodemo kwamba wakati ungekuja ambapo watu fulani wangekuwa na fursa ya kuingia Ufalme wa mbinguni. Yesu alisema hivi juu yao: “Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu. Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho. Usistaajabu kwa kuwa nilikuambia, Hamna budi kuzaliwa mara ya pili.” Lakini Nikodemo alitaka kujua jinsi mtu yeyote angeweza kuzaliwa mara ya pili.—Yohana 3:1-9.
Labda wewe pia hutaka kujua lile ambalo Yesu alimaanisha. Je! maneno yake yangeweza kuhusu maono ya wongofu wa ghafula ambayo wengi wanaohisi kwamba wamejazwa na roho takatifu, hudai kuwa nayo?
Hisiamoyo na Akili
Wengine husema kwamba katika kuamua kama mtu amezaliwa mara ya pili, jambo la maana ni kuhisi nguvu ya roho. Hata hivyo moyo na akili yetu inaweza kutuongoza vibaya, hasa ikivutiwa na hisiamoyo yenye nguvu.—Yeremia 17:9.
William Sargant mtafiti wa matokeo ya hisiamoyo juu ya akili, ataja uhitaji wa “kujilinda wenyewe dhidi ya imani zinazopatikana katika hali za kuchochewa kihisiamoyo wakati ambapo mabongo yetu huenda yakawa yanatudanganya.” Kulingana na Sargant, mfano mmoja ni matokeo ya kule kuhubiri kunakovutia hisiamoyo na matisho kuhusu adhabu ya moto wa helo. Ni nani hangetaka kuzaliwa mara ya pili ili kwenda mbinguni ikiwa jambo badala peke yake lilikuwa kupatwa na mateso ya milele? Sargant asema kwamba chini ya mkazo wa kihisiamoyo, “kusababu huwekwa kando, na kompyuta-bongo ya kawaida huacha kutenda kwa muda fulani, na mawazo na imani mpya zinakubaliwa bila maswali.”—The Mind Possessed.
Kwa hiyo, basi, mtu aweza kujuaje ikiwa imani juu ya jambo la kuzaliwa mara ya pili ‘imekubaliwa bila maswali’? Mwendo wa hekima ya kweli ni kuongozwa na kila jambo ambalo roho takatifu ya Mungu iliwasababisha waandishi wa Biblia warekodi. Wakristo wanatiwa moyo wamwabudu Mungu ‘kwa nguvu zao za kufikiri’ na wanahitaji kuhakikisha kwamba lile wanaloamini ni kweli.—Warumi 12:1, 2, New World Translation; 1 Wathesalonike 5:21.
Kuzaliwa mara ya pili humfungulia mtu moja la mapendeleo makubwa zaidi sana yaliyotolewa kwa wanadamu. Kunalinganishwa na tukio lenye kutokeza kwelikweli katika utimizo wa kusudi la Mungu. Ingawa yote hayo ni kweli, maswali kama haya yanatokea: Ni nani wanaozaliwa mara ya pili? Hilo hutukiaje? Ni matarajio gani yanayowekwa mbele ya watu hao? Na ni wao tu watakaookolewa?
[Picha katika ukurasa wa 3]
Nikodemo alitaka kujua jinsi mtu yeyote angeweza kuzaliwa mara ya pili