Sura 36
Imani Kubwa ya Ofisa Wa Jeshi
WAKATI Yesu anapotoa Mahubiri yake ya Mlimani, amefika karibu nusu ya huduma yake ya peupe. Hii yamaanisha kwamba ana mwaka mmoja na miezi tisa tu hivi inayobaki amalize kazi yake duniani.
Sasa Yesu aingia jiji la Kapernaumu, ambapo ni kama makao ya kuendeshea utendaji wake. Akiwa huko wanaume wazee Wayahudi wamfikia wakiwa na ombi fulani. Wao wametumwa na ofisa mmoja katika jeshi la Roma ambaye ni Mtaifa, mwanamume wa jamii tofauti na Wayahudi.
Mtumishi mpendwa wa ofisa huyo wa jeshi yuko karibu kufa kutokana na ugonjwa mkali, naye ataka Yesu aponye mtumishi wake. Wayahudi wanamsihi kwa bidii kwa ajili ya ofisa yule: “Astahili huyo umtendee neno hili,” wao wanasema, “maana, analipenda taifa letu, naye alitujengea sinagogi.”
Bila kusita, Yesu aondoka pamoja na wanaume hao. Lakini, wanapofika karibu, yule ofisa wa jeshi anatuma rafiki wakaseme: “Bwana, usijisumbue, maana mimi sistahili wewe uingie chini ya dari yangu; kwa hiyo nilijiona sistahili mwenyewe kuja kwako.”
Hayo ni maneno ya unyenyekevu kama nini kwa ofisa ambaye amekuwa na desturi ya kutolea wengine maagizo! Lakini labda yeye afikiria Yesu pia, akitambua kwamba desturi inamkataza Myahudi kuwa na uhusiano wa kirafiki pamoja na watu wasio Wayahudi. Hata Petro alisema: “Ninyi mnajua ya kuwa si halali mtu aliye Myahudi ashikamane na mtu aliye wa taifa lile lingine wala kumwendea.”
Labda kwa sababu hataki Yesu apatwe na matokeo mabaya ya kuvunja desturi hiyo, ofisa yule anawaagiza rafiki zake wakamwombe hivi: “Sema neno tu, na mtumwa wangu atapona. Kwa maana mimi nami ni mtu niliyewekwa chini ya mamlaka, mwenye askari chini yangu; nikimwambia huyu, Nenda, huenda; na huyu, Njoo, huja; na mtumwa wangu, Fanya hivyo, hufanya.”
Basi, Yesu anaposikia hilo anastaajabu. “Nawaambia,” yeye asema, “hata katika Israeli sijaona imani kubwa namna hii.” Baada ya kuponya mtumishi wa ofisa huyo, Yesu atumia pindi hiyo kusimulia jinsi watu wenye imani wasio Wayahudi watapendelewa kupewa baraka zinazokataliwa na Wayahudi wasio na imani.
“Wengi,” Yesu asema, “watakuja kutoka mashariki na magharibi, nao wataketi pamoja na Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo katika ufalme wa mbinguni; bali wana wa ufalme watatupwa katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.”
“Wana wa ufalme . . . [wanaotupwa] katika giza la nje,” ni Wayahudi wa asili wasioikubali fursa iliyotolewa kwao kwanza ya kuwa watawala pamoja na Kristo. Ibrahimu, Isaka, na Yakobo wafananisha mpango wa Mungu wa Ufalme. Hivyo Yesu asimulia jinsi watu wa Mataifa watakavyokaribishwa waegemee kana kwamba ni penye meza ya kimbingu, “katika ufalme wa mbinguni.” Luka 7:1-10; Mathayo 8:5-13; Matendo 10:28.
▪ Kwa nini Wayahudi wasihi kwa ajili ya ofisa wa kijeshi Mtaifa?
▪ Ni jambo gani linaloweza kueleza sababu kwa nini ofisa hakualika Yesu aingie nyumba yake?
▪ Yesu amaanisha nini kwa maneno yake ya kumalizia?