Sura 50
Matayarisho Ya Kukabiliana Na Mnyanyaso
BAADA ya kuwaagiza mitume wake katika njia za kuendesha kazi ya kuhubiri, Yesu anawaonya juu ya wapinzani. Yeye anaseme: “Tazameni! Mimi nawatuma nyinyi kama kondoo kati ya mbwa-mwitu . . . Jilindeni dhidi ya watu; kwa kuwa watawatoa nyinyi kwenye mahakama za kwenu, nao watawapiga mijeledi katika masinagogi yao. Naam, nyinyi mtaitwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu.”
Ujapokuwa mnyanyaso mkali watakaokabili wafuasi wake, Yesu anawatia moyo kwa kuwaahidi hivi: “Wakati wanapowatoa nyinyi, msiwe wenye wasiwasi juu ya jinsi au yale ambayo nyinyi mtasema; kwa kuwa yale ambayo nyinyi mtasema mtapewa nyinyi saa hiyo; kwa kuwa wale wanaosema si nyinyi tu, bali ni ile roho ya Baba ambayo inasema kupitia nyinyi.”
“Tena,” Yesu aendelea, “ndugu atamtoa ndugu kwenye kifo, na baba mtoto wake, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na watawafanya wauawe.” Anaongezea hivi: “Nyinyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu; lakini yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye ambaye ataokolewa.”
Kuhubiri ndilo jambo lenye maana ya kwanza. Kwa sababu hiyo Yesu anakazia uhitaji wa busara ili kubaki huru kuendesha kazi. “Wakati wanapowanyanyasa katika jiji moja, kimbilieni jingine,” yeye asema, “kwa kuwa kweli mimi nasema kwenu nyinyi, Nyinyi hamtamaliza kamwe mzunguko wa majiji ya Israeli mpaka Mwana wa binadamu awasilipo.”
Ni kweli kwamba Yesu alitoa agizo hili, onyo, na kitia moyo kwa mitume wake 12, lakini hayo pia yalikusudiwa kwa ajili ya wale ambao wangeshiriki kuhubiri ulimwenguni pote baada ya kifo na ufufuo wake. Yeye anaonyeshwa hivyo kwa kusema kwamba wanafunzi wake ‘wangechukiwa na watu wote,’ si na Waisraeli pekee ambao kwao mitume walitumwa kuhubiri. Zaidi ya hilo, kwa wazi mitume hawakuitwa mbele ya magavana na wafalme wakati Yesu alipowatuma nje katika kampeni yao ya muda mfupi ya kuhubiri. Isitoshe, wakati huo waamini hawakutolewa kwenye kifo na washiriki wa jamaa zao.
Hivyo alipokuwa akisema kwamba wanafunzi wake hawangemaliza mzunguko wa kuhubiri kwao, “mpaka Mwana wa binadamu awasilipo,” Yesu alikuwa akituambia sisi kwa njia ya kiunabii kwamba wanafunzi wake hawangemaliza mzunguko wa dunia yote inayokaliwa na watu kwa kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa kabla ya Mfalme Yesu Kristo aliyetukuzwa kuwasili akiwa ofisa mfishaji wa Yehova kwenye Har–Magedoni.
Akiendelea kutoa maagizo yake ya kuhubiri, Yesu anasema: “Mwanafunzi hawi juu ya mwalimu wake, wala mtumwa juu ya bwana wake.” Hivyo wafuasi wa Yesu lazima watazamie kutendwa vibaya na kunyanyaswa kama alivyotendewa kwa kuhubiri Ufalme wa Mungu. Hata hivyo yeye anaonya kwa upole hivi: “Msiwe wenye kuogopa wale ambao huua mwili lakini hawawezi kuua nafsi; afadhali mwe wenye kuogopa yeye ambaye anaweza kuharibu nafsi na mwili pia katika Gehena.”
Yesu angeweka kielelezo katika jambo hili. Bila woga yeye angevumilia kifo badala ya kukana ushikamanifu wake kwa Yule aliye na uwezo wote, Yehova Mungu. Ndiyo, ni Yehova ambaye anaweza kuharibu “nafsi” (kumaanisha katika habari hii mataraja ya wakati ujao ya mmoja akiwa nafsi inayoishi) ya mtu au badala ya hivyo aweza kufufua mtu afurahie uhai wa milele. Lo! Yehova ni Baba wa kimbingu mwenye upendo, na huruma kama nini!
Halafu Yesu anawatia moyo wanafunzi wake kwa kielezi ambacho chakazia utunzaji wenye upendo wa Yehova kwao. “Je! si mashore wawili huuzwa kwa sarafu moja yenye thamani ndogo?” yeye auliza. “Na bado hata mmoja wao hataanguka chini bila ya Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiwe na woga: nyinyi ni wenye thamani zaidi ya mashore wengi.”
Ujumbe wa Ufalme ambao Yesu anawatuma wanafunzi wake wakapigie mbiu utawagawanya washiriki wa jamaa, kwa kuwa washiriki fulani wa jamaa wanaukubali na wengine wanaukataa. “Msifikiri mimi nilikuja kuweka amani juu ya dunia,” yeye akaeleza, “mimi nilikuja kuweka, si amani, bali upanga.” Hivyo, ili mshiriki wa jamaa aukubali ukweli wa Biblia uhodari unahitajiwa. “Yeye ambaye ana shauku kubwa zaidi kwa baba au mama kuliko mimi hanistahili mimi,” Yesu akasema, “na yeye ambaye ana shauku kubwa zaidi kwa mwana au binti kuliko kwangu mimi hanistahili.”
Akimalizia maagizo yake, Yesu anaeleza kwamba wale wanaopokea wanafunzi wake wanampokea yeye pia. “Na yeyote ambaye anampa mmoja wa hawa walio wadogo kikombe kimoja tu cha maji baridi anywe kwa sababu yeye ni mwanafunzi, mimi nawaambia nyinyi kweli kweli, yeye hatapoteza kamwe thawabu yake.” Mathayo 10:16-42, NW.
▪ Yesu anaandalia wanafunzi wake maonyo gani?
▪ Yesu awapa kitia-moyo na faraja gani?
▪ Kwa nini maagizo ya Yesu yanatumika pia kwa Wakristo wa ki-siku-hizi?
▪ Ni kwa njia gani mwanafunzi wa Yesu hawi juu ya mwalimu wake?