Sura 61
Mvulana Mwenye Kupagawa na Roho Mwovu Aponywa
HUKU Yesu, Petro, Yakobo na Yohana wakiwa wamekwisha kwenda zao, yaelekea juu ya kilima cha Mlima Hermoni, wale wanafunzi wengine wanapatwa na tatizo fulani. Anaporudi, mara hiyo Yesu anaona kwamba jambo fulani si sawa. Pana umati wa watu ambao wamekusanyika kuzunguka wanafunzi wake, na waandishi wanahojiana pamoja nao. Wanapoona Yesu, wale watu wanashtuka sana na kukimbia kumsalimu. “Mnabishania nini nao?” yeye anauliza.
Akija mbele kutoka ule umati, mwanamume mmoja anapiga magoti mbele ya Yesu na kueleza: “Mwalimu, mimi nilileta mwana wangu kwako kwa sababu yeye ana roho asiyesema; na mahali popote anapomshika, anamwangusha chini, naye hutoa povu na kusaga meno yake na kupoteza nguvu zake. Nami niliambia wanafunzi wako wamtoe, lakini wao hawakuweza kufanya hivyo.”
Inaonekana waandishi wanajaribu kwa kadiri wawezavyo kutumia vibaya kule kushindwa kwa wanafunzi kuponya mvulana yule, labda wakidhihaki jitihada zao. Katika wakati uo huo wa kutatizika sana, Yesu anafika. “O kizazi chenye imani pungufu,” yeye anasema, “ni muda mrefu kadiri gani nitalazimika kuendelea kuwa pamoja na nyinyi? Ni muda mrefu kadiri gani nitalazimika kuchukuliana nanyi?”
Yesu anaonekana ni kama anaelekeza maelezo yake kwa kila mmoja aliyepo, lakini bila shaka yanaelekezwa moja kwa moja kwa waandishi hasa, ambao wamekuwa wakifanyia wanafunzi wake matata. Ndipo, Yesu anaposema juu ya mvulana yule: “Mleteni kwangu.” Lakini wakati mvulana yule anapokuwa akija kwa Yesu, yule roho mwovu ambaye humpagaa anampigisha chini na kumfanya atukutike-tukutike kwa jeuri. Mvulana yule anagaa-gaa chini na kutoa povu kinywani.
“Ni muda mrefu kadiri gani jambo hili limekuwa likitukia kwake?” Yesu anauliza.
“Kutoka utoto na kuendelea,” baba yule anajibu. “Tena na tena [yule roho mwovu] angemtupa ndani ya moto na ndani ya maji pia kumwangamiza.” Ndipo baba yule anaposihi sana: “Ikiwa wewe unaweza kufanya jambo lolote, utusikitikie na kutusaidia.”
Labda kwa muda wa miaka kadhaa, baba yule amekuwa akitafuta msaada. Na sasa, wakati wanafunzi wa Yesu wanaposhindwa, mtamauko wake ni mkubwa. Akianza na maneno ya ombi lile la kusihi la mwanamume huyo mwenye kutaka sana msaada, Yesu anasema hivi kwa kutia moyo: “Huo usemi, ‘Ikiwa wewe unaweza’! Kwani, mambo yote yanawezekana kwa mmoja ikiwa mmoja ana imani.”
“Mimi nina imani!” baba yule analia kwa kupaaza sauti mara hiyo, lakini anasihi sana, “Nisaidie mimi mahali ambapo ninahitaji imani!”
Akiona kwamba umati ule unakimbia kwa kusongamana pamoja kuwazunguka, Yesu anakemea yule roho mwovu: “Wewe roho asiyesema na aliye kiziwi, mimi nakuamuru wewe, toka ndani yake na usiingie tena ndani yake.” Wakati yule roho mwovu anapokuwa akiondoka, anasababisha tena mvulana yule kulia akipaaza sauti na kumfanya atukutike-tukutike sana. Ndipo mvulana yule anapolala chini bila kujisogeza-sogeza, hivi kwamba walio wengi wa watu wale wanaanza kusema: “Yeye amekufa!” Lakini Yesu anachukua mvulana yule kwa kumshika mkono, naye anainuka.
Mapema kabla ya hapo, wakati wale wanafunzi walipokuwa wametumwa waende wakahubiri, walikuwa wamefukuza roho waovu. Kwa hiyo, sasa, wakati wanapoingia nyumba fulani, wanauliza Yesu kwa faragha: “Kwa nini sisi hatukuweza kumfukuza?”
Akionyesha kwamba sababu ilikuwa ukosefu wao wa imani, Yesu ajibu: “Aina hii haiwezi kutoka kwa kitu chochote isipokuwa kwa sala.” Kwa wazi kujitayarisha kulihitajiwa ili kufukuza yule roho mwovu mwenye nguvu nyingi sana ambaye alihusika katika kisa hiki. Imani yenye nguvu pamoja na sala yenye kuomba msaada wa Mungu unaotia nguvu vilihitajiwa.
Ndipo Yesu anapoongezea: “Kwa kweli mimi nasema kwenu nyinyi, Ikiwa nyinyi mna imani kiasi cha punje ya haradali, mtauambia mlima huu, ‘Hama kutoka hapa uende pale,’ nao utahama, na hakuna kitu kitakachokuwa hakiwezekani kwenu.” Imani yaweza kuwa yenye nguvu kama nini!
Vipingamizi na magumu ambayo yanazuia maendeleo katika utumishi wa Yehova huenda yakaonekana kuwa yasiyoshindika na yasiyoondoleka kama vile mlima halisi ulio mkubwa. Hata hivyo, Yesu anaonyesha kwamba ikiwa sisi tunasitawisha imani katika mioyo yetu, tukiitia maji na kuitia moyo ikue, itapanuka ifikie ukomavu na kutuwezesha kushinda vipingamizi na magumu kama hayo yaliyo mfano wa mlima. Marko 9:14-29; Mathayo 17:19, 20; Luka 9:37-43, NW.
▪ Yesu anakuta hali gani anaporudi kutoka Mlima Hermoni?
▪ Yesu anampa yule baba wa mvulana mwenye kupagawa na roho mwovu kitia-moyo gani?
▪ Kwa nini wale wanafunzi hawakuweza kufukuza yule roho mwovu?
▪ Yesu anaonyesha kwamba imani inaweza kuwa yenye nguvu kadiri gani?