Maswali kutoka kwa Wasomaji
◼ Yesu alikuwa na maana gani aliposema hivi juu ya shetani mmoja: “Namna hii haiwezi kutoka kwa neno lo lote, isipokuwa kwa kuomba”?
Mtu mmoja ambaye mwana wake alikamatwa na “pepo bubu” alimwomba Yesu afukuze roho huyo mwovu, kwa maana wanafunzi hawakuweza. Kwa msaada hodari wa Mungu, Yesu alimfukuza shetani huyo. Baadaye wanafunzi wakamwuliza: ‘‘Mbona sisi hatukuweza kumtoa?” Kulingana na masimulizi ya Marko, Kristo alijibu hivi: “Namna hii haiwezi kutoka kwa neno lo lote, isipokuwa kwa kuomba.” (Marko 9:14-29) Katika masimulizi yake yanayolingana na hayo, Mathayo anamtaja Yesu kuwa alijibu hivi: “Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu.”—Mathayo 17:14-20.
Kwa sababu gani alikazia imani na sala? Matukio ya maisha yanaonyesha kwamba si lazima mashetani wote wawe wana mapendezi yale mamoja wala uwezo ule ule mmoja. Kwa mfano, wengine wanaonekana kuwa wanashikilia sana kazi ya kufanya makao yao katika nyumba za watu, na huku roho wengine waovu wanakaza fikira zao juu ya kunyanyasa wanadamu au kuwapagaa (kuishi ndani yao). Nasi tunaweza kukata shauri kutokana na jibu la Yesu kwamba mashetani fulani wana uwezo mwingi kuliko wengine.—Waefeso 6:12.
Yesu alipokuwa duniani, Mungu aliwezesha wengine wa watumishi wake watupe roho waovu nje ya watu maskini waliowapagaa. Wale mitume kumi na wawili na wanafunzi 70 waliwezeshwa kufanya hivyo. (Mathayo 10:8; Luka 10:17) Lakini mitume waliohusika katika kisa kinachosimuliwa katika Mathayo 17:14-20 na Marko 9:14-29 walishindwa kumfukuza shetani huyo. Kwa sababu gani? Kulikosekana nini? Ni wazi kwamba kilichokosekana ni matayarisho yaliyohitajiwa ili kuweza kukabiliana na namna ya shetani aliyehusika katika kisa hicho. Imani yenye nguvu ilihitajiwa, pamoja na sala ya mapema ya kuomba msaada wa Mungu wenye kuwapa uwezo. Ingawa masimulizi yenyewe hayataji kwamba katika kisa hicho Yesu alitoa sala ya kutaja jambo hilo waziwazi, huenda ikawa kwamba aliitoa. Ndipo alipofaulu kumtupa nje shetani huyo mwenye uwezo mwingi.