Sura 65
Kisafari cha Siri cha Kwenda Yerusalemu
NI KATIKA vuli ya 32 W.K., na Sikukuu ya Mahema (Vibanda) iko karibu. Yesu amewekea mipaka utendaji wake uwe sana-sana wa Galilaya, tangu Sikukuu ya Kupitwa ya 31 W.K., wakati Wayahudi walipojaribu kumuua. Inaelekea kwamba, tangu hapo Yesu amezuru Yerusalemu ili tu ahudhurie zile sikukuu tatu za Wayahudi za kila mwaka.
Sasa ndugu za Yesu wamhimiza hivi: “Pita usonge mbele kutoka hapa ukaingie Yudea.” Yerusalemu ndio mji mkuu wa Yudea na ndicho kitovu cha kidini cha nchi nzima. Ndugu zake wanawaza hivi: “Hakuna mtu ambaye hufanya jambo lolote katika siri huku yeye mwenyewe anatafuta kujulikana peupe.”
Ingawa Yakobo, Simoni, Yusufu, na Yuda hawaamini kwamba Yesu, ndugu yao mkubwa, ndiye Mesiya kweli kweli, wao wanataka yeye aonyeshe nguvu zake za kimuujiza kwa wote wale waliokusanyika kwenye sikukuu ile. Hata hivyo, Yesu anajua hatari ya kufanya hivyo. “Ulimwengu hauna sababu ya kuchukia nyinyi,” yeye anasema, “lakini unachukia mimi, kwa sababu mimi natoa ushahidi kuuhusu kwamba kazi zao ni mbovu.” Kwa hiyo Yesu anaambia ndugu zake: “Nyinyi pandeni mwende kwenye sikukuu; mimi bado sipandi kwenda kwenye sikukuu hii.”
Sikukuu ya Mahema ni mwadhimisho wa siku saba. Katika siku ya nane unamaliziwa kwa utendaji mbalimbali wenye kufanywa kwa fikira nzito. Sikukuu hiyo inatia alama mwisho wa mwaka wa kilimo na ni wakati wa kufanya shangwe na utoaji-shukrani. Siku kadhaa baada ya ndugu za Yesu kuondoka wakahudhurie pamoja na ule msafara mkuu, yeye na wanafunzi wake wanaenda kwa siri, wakikaa mbali ili watu wasiwaone. Wao wanafuata ile njia ya kupitia Samaria, badala ya ile ambayo watu walio wengi wanafuata karibu na Mto Yordani.
Kwa kuwa Yesu na waandamani wake watahitaji mahali pa kulala katika kijiji cha Wasamaria, yeye anapeleka wajumbe mbele yake wakafanye matayarisho. Hata hivyo, watu wa huko wanakataa kufanyia Yesu jambo lolote baada ya kujua kwamba yeye anaelekea Yerusalemu. Kwa kughadhibika, Yakobo na Yohana wanauliza: “Bwana, je! wewe unataka tuambie moto uje chini kutoka mbinguni na kuwaangamiza?” Yesu anawakemea kwa kudokeza jambo kama hilo, nao wanasafiri kwenda kijiji kingine.
Wanapokuwa wakitembea njiani, mwandishi mmoja amwambia Yesu: “Mwalimu, mimi nitakufuata wewe kokote wewe uendako.”
“Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota,” Yesu anajibu, “lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” Yesu anaeleza kwamba mwandishi huyo atapatwa na magumu ikiwa atakuwa mfuasi Wake. Na maana inayogusiwa inaonekana kwamba mwandishi huyo ni mwenye kiburi mno asiweze kukubali maisha ya namna ile.
Yesu anasema kwa mwanamume mwingine: “Uwe mfuasi wangu.”
“Niruhusu kwanza niondoke na kuzika baba yangu,” mwanamume huyo anajibu.
“Acha wafu wazike wafu wao,” Yesu ajibu, “lakini wewe nenda zako na kutangaza kotekote ufalme wa Mungu.” Ni dhahiri kwamba baba ya mwanamume huyo hajafa bado, kwa maana kama angalikuwa amekufa, haingalielekea kwamba mwanaye angekuwa hapo akimsikiliza Yesu. Inaonekana mwana huyo anaomba wakati wa kungojea kifo cha baba yake. Yeye hayuko tayari kuweka Ufalme wa Mungu kwanza katika maisha yake.
Wanaposonga mbele njiani kuelekea Yerusalemu, mwanamume mwingine anaambia Yesu: “Mimi nitakufuata wewe, Bwana; lakini kwanza niruhusu mimi kusema kwaheri kwa wale walio katika nyumba yangu.”
Katika kujibu Yesu anasema: “Hakuna mtu ambaye ametia mkono wake kwenye plau na kutazama vitu vilivyo nyuma anafaa vizuri kwa ufalme wa Mungu.” Wale ambao watakuwa wanafunzi wa Yesu lazima wakaze macho yao juu ya utumishi wa Ufalme. Sawa na vile mfuo wa kulimwa utakavyoelekea kupotoka-potoka ikiwa mshika-plau haendelei kutazama mbele kabisa, ndivyo mtu yeyote anayetazama nyuma kwenye huu mfumo wa kale wa mambo anavyoweza kujikwaa atoke katika ile njia inayoongoza kwenye uhai wa milele. Yohana 7:2-10; Luka 9:51-62; Mathayo 8:19-22, NW.
▪ Ni nani ndugu za Yesu, nao wanahisije juu yake?
▪ Kwa nini Wasamaria ni wakali kadiri hiyo, na Yakobo na Yohana wanataka kufanya nini?
▪ Ni mazungumzo gani matatu Yesu anakuwa nayo njiani, naye anakaziaje uhitaji wa utumishi wa kujidhabihu?