Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 12/15 kur. 10-15
  • Tangaza Ufalme wa Mungu Kote Kote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tangaza Ufalme wa Mungu Kote Kote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova Awa Mfalme Juu ya Israeli
  • Mfalme-Mchungaji Aliyetabiriwa Atokea
  • “Uwe Mfuasi Wangu”​—Wewe Unaitikiaje?
  • Maagizo ya Kuuhubiri Ufalme
  • Je, Unaitegemeza Enzi Kuu ya Yehova?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • “Nifuateni, Nami Nitawafanya Kuwa Wavuvi Watu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • “Habari Njema Lazima Zihubiriwe Kwanza”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • “Uwe Mfuasi Wangu”—Yesu Alimaanisha Nini Aliposema Maneno Hayo?
    ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 12/15 kur. 10-15

Tangaza Ufalme wa Mungu Kote Kote

“Waache wafu wawazike wafu wao, lakini wewe nenda ukatangaze Ufalme wa Mungu kote kote.”​—LUKA 9:60, Biblia ya New World Translation.

1. Ni maulizo gani ya maana yanayotokezwa na maneno ya Yesu katika Luka 9:60?

UFALME wa Mungu​—hilo ndilo lililokuwa pendezi la maana zaidi maishani mwa Yesu! Ndivyo ilivyo leo kwetu sote tulio wafuasi wa kweli wa hatua zake. Sisi Wakristo tunajitahidi kufuata kwa ukaribu hatua za Yesu kwa kuishi kulingana na Biblia. (1 Petro 2:21) Lakini sasa, tunapouingia mwaka 1986, je, ingeweza kuwa kwamba tunahitaji kuchunguza tena tuone ni mambo gani tunayotanguliza maishani? Kwa mfano, wewe ungeelezaje maana ya Yesu kuambia mtu “waache wafu wawazike wafu wao”? Unafikiri ni kwa sababu gani Yesu alikazia wakati huo umaana wa kutangaza ujumbe wa Ufalme, badala ya mambo ya kijamaa ambayo ndiyo yangeelekea kuwa yalifaa kuhangaikiwa?

2. Ni wakati gani ilipoanza enzi kuu ya Yehova, nayo itaendelea mpaka wakati gani?

2 Muda mrefu kabla Yesu hajayatumia maneno “ufalme wa Mungu,” Daudi mtunga zaburi aliandika hivi kwa uongozi wa Mungu: “[Yehova] ameweka kiti chake cha enzi mbinguni, na ufalme wake unavitawala vitu vyote.” (Zaburi 103:19) Enzi kuu ya Yehova ilianza alipoanzisha uumbaji wake. Msingi wa kiti cha enzi chake hauwezi kuondoshwa kamwe! Hawezi kamwe kupokonywa haki yake ya kuwa na enzi kuu ya ulimwengu! Si ajabu kwamba mtunga zaburi mmoja anahimiza hivi: “Wahubirini mataifa habari za utukufu wake, . . . kwa kuwa [Yehova] ni mkuu mwenye kusifiwa sana.”​—Zaburi 96:3, 4; 109:21; Danieli 4:34, 35.

3. (a) Ni matukio gani yaliyofanya ubishi utokezwe juu ya utawala wa Yehova? (b) Mungu anakusudiaje kuliamua suala la enzi kuu ya ulimwengu wote?

3 Lakini, si watu wote wameendelea kumsifu Yehova. Shetani, yule mwasi-imani wa kwanza, alitokeza ubishi juu ya jinsi Yehova alivyoonyesha na kutumia enzi kuu Yake kuelekea viumbe wake duniani. (Mwanzo 3:1-5; Ayubu 1:6-12; 2:1-5) Matokeo ni kwamba, viumbe fulani waliambukiwa na mwelekeo wa uasi wa Shetani, duniani na baadaye mbinguni. Pia Shetani alifanya mavutano yake juu ya wanadamu ili waanzishe mfululizo wa falme za kibinadamu. Yeye amezitumia ili apinge ufaaji wa utawala wa Mungu. (Ufunuo 13:1-6) Ili aamue suala hilo la enzi kuu ya ulimwengu wote, Yehova alikusudia jambo fulani lisilo la kawaida, kama lilivyotabiriwa kwenye Danieli 2:44: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele . . . utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”

Yehova Awa Mfalme Juu ya Israeli

4. Ni katika maana gani Daudi angeweza kusema “[Yehova] ametamalaki,” na tukio hilo lilihitaji jambo gani lifanywe?

4 Basi sasa inakuwa wazi kwamba, ingawa enzi kuu ya Yehova ilianza wakati alipoanzisha uumbaji, yeye alikusudia kufanya wonyesho wa waziwazi wa utawala wake ili aamue milele suala la ufaaji wa enzi kuu yake. Wonyesho huo ulikuwa Ufalme wa Kimasihi wa mbinguni. Ufalme wa kidunia ambao Yehova alisimamisha utawale taifa la Israeli ulikuwa kiwakilishi kidogo cha Ufalme huo “ambao hautaangamizwa milele.” Kwa hiyo, Mfalme Daudi alipopandisha sanduku la agano kuliingiza mjini Yerusalemu, aliweza kuimba hivi kwa shangwe: “Mbingu na zifurahi, nchi na ishangilie; na waseme katika mataifa, [Yehova] ametamalaki!” (1 Mambo ya Nyakati 16:31) Ndiyo, katika maana ya pekee Yehova alikuwa “ametamalaki” (amekuwa mfalme) kwa Israeli wote. Ulikuwa wakati wa furaha kuu, naye Daudi alitaka kulitangaza kote kote tukio hilo la kufurahisha sana!

5, 6. (a) Ni kwa njia gani Daudi hakuwa na kifani kati ya wafalme? (b) Daudi alitangulia kufananisha nani, na kwa njia gani?

5 Maisha yake pale mwanzoni akiwa mchungaji ndiyo yaliyomwekea Mfalme Daudi msingi wa kuwa mfalme asiye na kifani kati ya wafalme. Yeye alikuwa mfalme-mchungaji. Mtunga zaburi anaeleza habari za jinsi Daudi alivyochaguliwa na Mungu achukue cheo hicho wakati anaposema hivi: “[Yehova] akamchagua Daudi, mtumishi wake, akamwondoa katika mazizi ya kondoo . . . awachunge Yakobo watu wake, na Israeli urithi wake. Akawalisha kwa ukamilifu wa moyo wake, na kuwaongoza kwa busara ya mikono yake.”​—Zaburi 78:70-72.

6 Uchungaji ambao Daudi aliwafanyia watu wake, ukamilifu wake wa moyo kuelekea Mungu wake, na ustadi wake akiwa kiongozi ulimstahilisha sana awe mfananishi wa Masihi, ambaye angetumiwa kwa njia ya pekee aonyeshe umaliki wa enzi kuu ya Yehova na pia atende akiwa Mfalme-Mchungaji mwenye upendo. Tukio hilo la kufurahisha sana katika makusudi ya Yehova lilitabiriwa baadaye na nabii Ezekieli: “Nitaweka mchungaji mmoja juu [ya Israeli], naye atawalisha, naam, mtumishi wangu, Daudi . . . Na mimi, [Yehova], nitakuwa Mungu wao, na mtumishi wangu, Daudi, atakuwa mkuu kati yao; mimi, [Yehova], nimesema haya.”​—Ezekieli 34:22-24.

Mfalme-Mchungaji Aliyetabiriwa Atokea

7, 8. (a) Mfalme-Mchungaji aliyetabiriwa alitambulishwaje, na kutokea kwake kulistahili nini? (b) Ni kwa kusudi gani Yesu ‘alikubaliwa’ na Yehova?

7 Yule aliyetabiriwa na Yehova alikuwa Mwanaye mwenyewe, Yesu. Kwa habari yake malaika Gabrieli alimwambia hivi Mariamu bikira: “Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na [ Yehova] Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.” (Luka 1:31-33) Huo ungekuwa wonyesho mzuri kama nini wa umaliki wa Yehova! Hakika tukio hilo lenye kuja lingestahili kufanyiwa tangazo lililo kubwa zaidi ulimwenguni pote: “[Yehova] ametamalaki,” [“Yehova amekuwa mfalme!”]

8 Baada ya Yesu kuzaliwa kimuujiza na kuwa mwanamume aliyekomaa, alijitoa abatizwe katika maji ya mto Yordani. Wakati huo Mungu alimtambua Yesu kuwa Mwanaye kwa kumimina roho juu yake na kusema: “Wewe ni Mwana wangu, yule mpendwa; mimi nimekukubali wewe.” (Luka 3:22, NW) Yesu ‘alikubaliwa’ kwa jambo gani? Masimulizi ya Luka yanaeleza: “Yesu mwenyewe, wakati alipoanza kazi yake, alikuwa na umri wa karibu miaka thelathini.” (Luka 3:23; maelezo ya chini ya Ref. Bi.: “Au, alipoanza [kufundisha].’”) Biblia za Revised Standard Version na New International Version zinasema, “Alipoanza huduma yake.” “Kazi,” au “huduma” ya Yesu ilikuwa nini? Yeye ‘alifundisha’ nini? Mwandikaji Mathayo anatoa jibu: “[Yesu] alikuwa akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao, na kuihubiri Habari Njema ya ufalme, na kuponya ugonjwa na udhaifu wa kila namna katika watu.”​—Mathayo 4:23.

9. Ni kwa njia zipi Yesu alikuwa kama Daudi babu yake wa zamani?

9 Yesu aliyatumia maisha yake ‘kutangaza ufalme wa Mungu kote kote.’ Kama Daudi babu yake wa zamani, yeye alionyesha ukamilifu wake wa moyo kwa kutouacha kamwe msimamo wake wa kuutii kwa dhati Ufalme wa Yehova. (Luka 9:60, 7NW; 4:3-13; Yohana 16:33, UV) Yesu alijithibitisha kuwa ndiye yule “mchungaji mmoja” ambaye Yehova alikuwa ameahidi kumwinua. Alifurahia kuwalisha kiroho watu ambao viongozi wa kidini walikuwa ‘wamewachuna na kuwatupa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36, NW) Kwa habari ya kazi yake stadi ya kuchunga watu na jinsi ingepanuka pole kwa pole katika miaka ya baadaye, Yesu alisema: “Mimi ndimi mchungaji mwema; nao [kondoo] walio wangu nawajua; nao [kondoo] walio wangu wanijua mimi . . . Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.”​—Yohana 10:14, 16.

10. Tunaweza kupataje masomo kutokana na jinsi Wayahudi walivyouitikia kwa njia mbalimbali ukaribishaji wa Yesu kwamba wamfuate?

10 Wayahudi waliuitikiaje ukaribishaji wa Yesu kwamba wawe wafuasi wake walio mfano wa kondoo? Waliitikia kwa njia mbalimbali. Tunapochunguza baadhi ya maitikio hayo, fikiria itikio lako limekuwa nini tangu ulipoupata ujumbe wa Ufalme wa Mungu.

“Uwe Mfuasi Wangu”​—Wewe Unaitikiaje?

11. Eleza lilivyokuwa itikio la Simoni, Andrea, Yakobo, Yohana, na Mathayo kwa ukaribishaji wa Yesu, “Njoni mnifuate.”

11 Yesu alipokuwa akitembea karibu na Bahari ya Galilaya, alimwona Simoni na Andrea ndugu yake wakivua samaki. “Yesu akawaambia, Njoni mnifuate, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu. Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata. Akaendelea mbele kidogo, akamwona Yakobo wa Zebedayo, na Yohana nduguye . . . akawaita, wakamwacha baba yao Zebedayo ndani ya chombo pamoja na watu wa mshahara, wakaenda, wakamfuata.” (Marko 1:16-20) Mkusanya kodi Lawi, au Mathayo, aliitikia vizuri pia. “[Yesu] akamwambia: ‘Uwe mfuasi wangu.’ Naye akiacha kila kitu nyuma akainuka na kwenda akimfuata yeye.”​—Luka 5:27, 28, NW.

12. Tatizo lilikuwa nini kwa mwanamume aliyemwambia Yesu, “Nitakufuata ko kote utakakokwenda”?

12 Lakini, si watu wote waliotikia vizuri ukaribishaji wa Yesu aliposema, “Uwe mfuasi wangu.” Fikiria mwanamume yule anayeelezwa katika Luka sura ya 9, ambaye Yesu alikutana naye alipokuwa akisafiri kutoka kijiji kimoja kwenda kingine. Alimwambia Yesu: “Nitakufuata ko kote utakakokwenda.” Masimulizi ya Mathayo yanaonyesha kwamba mwanamume huyo alikuwa mwandishi. Waandishi waliheshimiwa sana na watu na waliitwa “Rabi.” Sasa angalia jibu la Yesu: “Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana vioto, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake.” (Luka 9:57, 58) Yesu alikuwa akimwambia mwanamume huyo kwamba angelazimika kuona magumu akiwa mfuasi wa Kristo. Wazo linalotolewa hapo ni kwamba mwanamume huyo alikuwa mwenye kiburi mno asiweze kukubali maisha ya namna hiyo. Yeye hangeweza kuyakubali mambo hayo ya kukaa bila kujua angelala wapi wakati wa usiku.

13. Ni kwa sababu gani Yesu alijibu kama alivyofanya akisema na mtu mwingine ambaye angaliweza kuwa mfuasi?

13 Yesu aliambia hivi mtu mwingine aliyesimama karibu: “Uwe mfuasi wangu.” Lakini yeye akamjibu Yesu: “Niruhusu kwanza niondoke nikazike baba yangu.” Angalia jibu la Yesu: “Waache wafu wawazike wafu wao, lakini wewe nenda ukatangaze kote kote ufalme wa Mungu.” (Luka 9:59, 60, NW) Udhuru uliotolewa na mtu huyo haukutoa wazo la kwamba baba yake alikuwa amekwisha kufa. Kama angalikuwa amekufa, ingalikuwa vigumu sana mwana huyo kuwapo pale njiani akimsikiliza Yesu. Hapana, inaonekana kutokana na maneno ya mwanamume huyo kwamba alikuwa akitaka aendelee kuwa na wakati wa kungoja kifo cha babaye. Hakuwa tayari kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwake bila kukawia.​—Mathayo 6:33.

14, 15. (a) Ni jambo gani linaloonyeshwa katika ombi ambalo mtu yule wa tatu alimtolea Yesu? (b) Ni somo gani leo tunaloweza kujifunza kutokana na jibu ambalo Yesu alimpa mtu huyo?

14 Maandishi yanatuambia habari za mwanamume wa tatu, aliyejitolea akisema, “Nitakufuata, Bwana; lakini kwanza niruhusu niseme kwaheri kwa wale walio katika jamaa yangu.” Inaonekana mwanamume huyo alikuwa akiomba kwamba aruhusiwe kuweka masharti ya kuwa mfuasi wa Yesu. Alikuwa ni kama anamwambia Yesu hivi: ‘Tazama! mimi nitakuwa mmoja wa wafuasi wako, ikiwa . . . ’ Yesu alijibuje? “Hakuna mtu ambaye ameshika plau na kutazama vitu vilivyo nyuma anayeufaa vizuri ufalme wa Mungu.” (Luka 9:61, 62, NW) Wakati mtu anayetumia plau ya kulimia anapotaka kulima mstari wa matuta ulionyooka katika shamba, ni lazima aendelee kutazama mbele kabisa. Akigeuza kichwa kutazama nyuma, inaelekea kwamba mstari huo wa matuta utapotokapotoka. Huenda hata akajikwaa! Ndivyo ilivyo kwa wafuasi wa hatua za Yesu; wakitazama nyuma kwenye huu mfumo wa kale wa mambo, hata kwa muda mchache tu, wanajitafutia matata, wanafanya miguu yao ijikwae na kupepesuka iiache ile ‘njia nyembamba ya uzima.’​—Mathayo 7:14; ona Luka 17:31-35.

15 Je, wewe umeusikia ukaribishaji wa Yesu, “Uwe mfuasi wangu”? Itikio lako limekuwa nini? Je, umeonyesha itikio zuri sawa na wanafunzi Simoni, Andrea, Yakobo, Yohana, na Mathayo? Kama wanaume hao, je, wewe uko tayari kujinyima kwa njia yo yote inayohitajiwa ili ufuate hatua za Mkubwa? Ikiwa unajibu ndivyo, basi utafurahia pia pendeleo lisilo na kifani la kushiriki kuzitangaza kote kote habari njema za Ufalme wa Mungu.

16. Yesu aliwatayarishaje wanafunzi wake washiriki pamoja naye kuzihubiri habari njema?

16 Kabla Yesu hajatuma wanafunzi wake wakautangaze Ufalme, kwa mfano wake binafsi aliwafundisha kwa ustadi jinsi ya kufanya hivyo. Baada ya hapo, Yesu aliwaagiza kwa urefu jinsi ya kutafuta wenye mfano wa kondoo katika eneo lo lote. Maagizo ya Yesu yangali yanafaa kutumiwa katika karne hii ya 20. Na tuchunguze baadhi ya hayo kama yalivyoandikwa katika sura ya 10 ya masimulizi ya Mathayo.

Maagizo ya Kuuhubiri Ufalme

17. Linganisha mambo yaliyokuwa katika ujumbe wa Ufalme uliohubiriwa katika Karne ya Kwanza na yale yaliyomo leo.

17 Kichwa cha ujumbe wa wanafunzi kilipasa kuwa kile kile ambacho Yesu alikuwa akitangaza: “Katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mathayo 10:7) Lakini, sasa Ufalme huo umesimamishwa mbinguni. Mfalme-Mchungaji aliyewekwa na Yehova, Kristo Yesu, sasa anatawala! Kwa hiyo, maneno ya Daudi sasa yana maana kubwa zaidi: “Mbingu na zifurahi, nchi na ishangilie; na waseme katika mataifa, [Yehova] ametamalaki,” [“Yehova amekuwa mfalme!”] (1 Mambo ya Nyakati 16:31) Leo, tunalo, si pendeleo tu la kuunga mkono wonyesho huo wa pekee wa umaliki wa enzi kuu ya Yehova, bali pia tunayo furaha ya kuishi katika wakati ambao suala la enzi kuu ya Yehova litaamuliwa kwa umilele wote.

18. Yesu alikazia nini kwa wafuasi wake katika Mathayo 10:8-10, na ni nani hasa wanaoweza kuthamini jambo hilo leo?

18 Andiko la Mathayo 10:8-10 linaeleza ni mwelekeo gani wa kiroho walio nao wale wanaoishiriki kazi ya kuhubiri. Ni lazima Ufalme wa Mungu upewe nafasi ya kwanza maishani mwetu, na nafasi ya pili iwe ni ya mahitaji ya kimwili. Kwa sababu gani? Yesu alisema: “Maana mtenda kazi astahili posho lake.” Baba yetu wa kimbingu atawatunza sikuzote wale wanaomtumaini yeye. Na mamia kwa maelfu ya wahudumu wa wakati wa Mashahidi wa Yehova leo wanaweza kushuhudia kwamba ndivyo ilivyo.​—Hesabu 18:30, 31; Kumbukumbu la Torati 25:4.

19. Utafutaji wa wenye kustahili unafanywaje leo na chini ya mwelekezo wa nani?

19 Ndipo Yesu anapoagiza hivi: “Ndani ya mji wo wote au kijiji mnachoingia, mtafute-tafute ni nani humo anayestahili, nanyi mkae humo mpaka mtakapoondoka.” (Mathayo 10:11, NW) Mwenye kustahili nini? Mwenye kustahili pendeleo la kumpokea mtumishi huyo wa Yehova na kuusikiliza ujumbe wa Ufalme wa Mungu. Bila shaka, huko nyuma labda wanafunzi walikaa katika nyumba ya mtu huyo mwenye kustahili na kutumia mahali hapo kama kituo chao walipokuwa wakichambua eneo ili kutafuta wengine wenye kustahili. Leo, Mashahidi wa Yehova wanafuata utaratibu unaofanana na huo. Wanatumia mamilioni ya saa na kujitahidi sana wakitafuta wenye kustahili katika maeneo mbalimbali. Halafu, hao wanapopatikana, Mashahidi wanafurahi sana kuwatembelea tena wenye nyumba hao na kuwaeleza Neno la Mungu. Hivyo, leo, Yesu anawachunga kwa ustadi wengine ‘wenye mfano wa kondoo’ ili waje kwenye mkono wake wa kuume wenye upendeleo.​—Mathayo 25:31-33.

20. ‘Nyumba inayostahili’ inapataje amani anayoitakia mhubiri Ufalme?

20 Mnapoingia ndani ya nyumba, salimuni watu wa nyumba hiyo; na ikiwa nyumba ile inastahili, acheni amani mnayoitakia ije juu yayo.” (Mathayo 10:12, 13, NW) Kusema “Nyumba hii na iwe na amani” kulikuwa salamu ya kawaida sana siku za Yesu. (Luka 10:5, NW) Malaika waliimba hivi wakati wa kuzaliwa kwa Yesu: “Utukufu kwa Mungu juu mbinguni, na amani duniani kwa watu aliopendezwa nao.” (Luka 2:14, HNWW) ‘Nyumba yenye kustahili’ ilipata amani hiyo iliyotabiriwa kwa kuukubali ujumbe wa Ufalme ilioletewa na wanafunzi. Leo, habari njema za Ufalme zina matokeo yale yale. Zinaingiza watu katika uhusiano wenye amani pamoja na Mungu kupitia Yesu Kristo, na pia zinaleta amani kati ya waamini wenzetu.​—2 Wakorintho 5:20, 21; Wafilipi 4:7; Waefeso 4:3.

21. Kwa sababu gani andiko la mwaka 1986 linafaa sana?

21 Mwaka 1986 Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova duniani pote yatakuwa na kichwa cha mwaka kilichotolewa katika Luka 9:60, NW: ‘Tangaza Ufalme wa Mungu Kote Kote.’ Hicho kitakuwa kikumbusho na kichocheo kizuri kama nini kwa wote walio wahudumu wa kweli wa Mungu ili washiriki kwa ukawaida kuuhubiri Ufalme wa Mungu! Ndiyo, Ufalme huo umekuwapo tangu mwaka 1914! Ukiwa mikononi mwa Mfalme wa Kimasihi aliyemweka, hicho ndicho chombo kitakachotumiwa na Mungu kuponda-ponda falme zote za kilimwengu za Shetani. Basi, si ajabu kwamba Ufalme wa Mungu ndio unaopasa kuwa wa maana zaidi katika maisha ya kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Tunajua kwamba kufanya hivyo kutatupa sisi wokovu wa kupata uzima!—1 Timotheo 4:16.

Wewe Ungejibuje?

◻ Umaliki wa Yehova unaendelea na kudumu mpaka wakati gani?

◻ Sasa ni suala gani la ulimwengu wote linalohitaji kuamuliwa?

◻ Ni lazima wafuasi wote wa Yesu wawe tayari kufanya nini?

◻ Kwa sababu gani maneno “[Yehova] ametamalaki” ni ya maana zaidi leo?

◻ Ni kusudi gani litakalotimizwa na andiko la mwaka 1986?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mathayo aliacha nyuma kila kitu akamfuata Yesu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki