Sura 72
Yesu Awatuma Nje Wale 70
NI VULI ya 32 W.K., miaka mitatu kamili tangu ubatizo wa Yesu. Yeye na wanafunzi wake wamehudhuria majuzi Sikukuu ya Mahema katika Yerusalemu, na inaonekana wazi wangali wako karibu na huko. Kwa kweli, Yesu anatumia sehemu kubwa ya miezi sita inayobaki ya huduma yake ama akiwa katika Yudea ama pale ng’ambo tu ya Mto Yordani katika wilaya ya Perea. Eneo hili linahitaji kufanyiwa kazi pia.
Ni kweli, baada ya Sikukuu ya Kupitwa ya 30 W.K., Yesu alitumia karibu miezi minane akihubiri katika Yudea. Lakini baada ya Wayahudi kujaribu kumuua huko katika Sikukuu ya Kupitwa ya 31 W.K., yeye alitumia mwaka mmoja na nusu uliofuata akifundisha karibu Galilaya peke yake. Wakati huo, yeye alipanga kitengenezo kundi kubwa la wahubiri waliozoezwa vizuri, hicho kikiwa kitu ambacho hakupata kuwa nacho hapo mapema. Kwa hiyo sasa anaanzisha kampeni ya mwisho ya kutoa ushahidi mwingi kweli kweli katika Yudea.
Yesu anaanzisha kampeni yake kwa kuchagua wanafunzi 70 na kuwatuma nje wawili-wawili. Hivyo, kwa ujumla, kuna vikoa 35 vya wahubiri wa Ufalme wa kufanya kazi katika eneo. Hawa wanamtangulia kuingia katika kila jiji na mahali ambako Yesu anapanga kwenda, kwa wazi mitume wake wakiwa wanaandamana naye.
Badala ya kuelekeza hao 70 waende kwenye masinagogi, Yesu anawaambia waingie nyumba za faragha, akieleza hivi: “Mahali kokote ambako nyinyi mtaingia ndani ya nyumba semeni kwanza, ‘Nyumba hii na iwe na amani.’ Na ikiwa rafiki ya amani yumo, amani yenu itakaa juu yake.” Ujumbe wao utakuwa nini? “Endeleeni kuwaambia,” Yesu anasema, “ufalme wa Mungu umekuja karibu na nyinyi.” Kuhusu utendaji wa wale 70, kitabu Matthew Henry’s Commentary kinaripoti hivi: “Kama Bwana wao, mahali kokote ambako wao walizuru, walihubiri nyumba kwa nyumba.”
Maagizo ya Yesu kwa wale 70 yanafanana na yale waliyopewa wale 12 wakati alipowatuma nje katika kampeni ya kuhubiri katika Galilaya karibu mwaka mmoja mapema. Si kwamba tu yeye anawaonya wale 70 juu ya upinzani watakaoelekeana nao, akiwatayarisha wakawatolee wenye nyumba ujumbe, bali anawapa nguvu pia za kuponya wagonjwa. Hivyo, wakati Yesu anapowasili muda mfupi baadaye, wengi watakuwa na hamu ya kukutana na Bwana-mkubwa ambaye wanafunzi wake wanaweza kufanya mambo hayo ya kustaajabisha.
Kuhubiri kwa wale 70 na kazi ya Yesu ya kufuatia kuhubiri kwao, kunachukua wakati mfupi kwa kulinganishwa. Upesi vile vikoa 35 vya wahubiri wa Ufalme vinaanza kurudi kwa Yesu. “Bwana,” wao wanasema kwa shangwe, “hata roho waovu wanafanywa watutii kwa kutumia jina lako.” Hakika ripoti nzuri kama hiyo ya utumishi inasisimua Yesu, kwa maana yeye anaitikia hivi: “Mimi nalianza kuona Shetani tayari amekwisha kuanguka kama umeme kutoka mbinguni. Tazama! Mimi nimewapa nyinyi mamlaka ya kuwakanyaga-kanyaga nyoka na nge chini ya nyayo.”
Yesu anajua kwamba baada ya kuzaliwa kwa Ufalme wa Mungu wakati wa mwisho, Shetani na roho waovu wake watatupwa nje watoke katika mbingu. Lakini sasa kutupwa nje huku kwa roho waovu wasioonekana kunakofanywa na wanadamu wa kawaida tu kunatumika kama uhakikisho wa ziada wa tukio hilo linalokuja. Kwa hiyo, Yesu ananena juu ya anguko la Shetani la wakati ujao kutoka katika mbingu kuwa ni jambo hakika kabisa. Kwa sababu hiyo, ni katika maana ya mfano kwamba wale 70 wanapewa mamlaka ya kukanyaga-kanyaga nyoka na nge. Hata hivyo, Yesu anasema: “Msishangilie jambo hili, kwamba wale roho wamefanywa wawatii nyinyi, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa katika mbingu.”
Yesu anafurikwa na shangwe sana, naye amsifu Baba yake peupe kwa kutumia hawa watumishi wake wanyenyekevu katika njia hii yenye nguvu. Akigeukia wanafunzi wake, yeye anasema: “Yenye furaha ni macho ambayo yanaona mambo ambayo nyinyi mnaona. Kwa maana mimi nasema kwenu nyinyi, Manabii wengi na wafalme walitamani kuona mambo ambayo nyinyi mnaona lakini hawakuyaona, na kusikia mambo ambayo nyinyi mnasikia lakini hawakuyasikia.” Luka 10:1-24; Mathayo 10:1-42; Ufunuo 12:7-12, NW.
▪ Yesu alihubiri wapi wakati wa miaka mitatu ya kwanza ya huduma yake, na ni eneo gani ambalo yeye anafanyia kazi katika miezi yake sita ya mwisho?
▪ Yesu anaelekeza wale 70 wapi wakapate watu?
▪ Kwa nini Yesu anasema alimwona Shetani akiwa tayari ameanguka kutoka mbinguni?
▪ Wale 70 wanaweza kukanyaga-kanyaga nyoka na nge kwa maana gani?