Sura 91
Wakati Lazaro Anapofufuliwa
YESU, pamoja na wale wanaoandamana naye, sasa anawasili kwenye ziara la ukumbusho la Lazaro. Kwa kweli, hilo ni pango lililowekelewa jiwe kwenye mwingilio. “Liondoeni jiwe,” Yesu anasema.
Martha anapinga, akiwa bado haelewi Yesu anakusudia kufanya nini. “Bwana,” yeye anasema, “ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne.”
Lakini Yesu anauliza: “Mimi sikukuambia ya kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?”
Hivyo jiwe linaondolewa. Halafu Yesu anainua macho yake na kusali hivi: “Baba, nakushukuru kwa kuwa umenisikia. Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia sikuzote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma.” Yesu anasali peupe ili watu wajue kwamba analokaribia kufanya litatimizwa kupitia nguvu zilizopokewa kutoka kwa Mungu. Kisha anapaaza sauti hivi: “Lazaro, njoo huku nje.”
Hapo, Lazaro anatokea. Mikono na nyayo zake zingali zimefungwa kwa vitambaa vya maziko, na uso wake umefunikwa kwa kitambaa. “Mfungueni, mkamwache aende zake,” Yesu anasema.
Wanapoona muujiza huo, wengi wa Wayahudi waliokuwa wamekuja kufariji Mariamu na Martha wanatia imani katika Yesu. Hata hivyo, wengine wanaenda zao na kuwaambia Mafarisayo jambo ambalo limetukia. Wao na wakuu wa makuhani wanapanga mara hiyo kuwe na mkutano wa mahakama kuu ya Kiyahudi, ile Sanhedrini.
Sanhedrini inatia ndani kuhani mkuu wa wakati wa sasa, Kayafa, pamoja na Mafarisayo na Masadukayo, wakuu wa makuhani, na wale ambao hapo kwanza walikuwa makuhani wakuu. Hao wanaomboleza hivi: “Tunafanya [tufanye, NW] nini? Maana mtu huyu afanya ishara nyingi. Tukimwacha hivi, watu wote watamwamini; na Warumi watakuja, watatuondolea mahali petu na taifa letu.”
Ingawa viongozi wa kidini wanakiri kwamba Yesu “anafanya ishara nyingi,” wanachohangaikia tu ni cheo na mamlaka yao wenyewe. Kufufuliwa kwa Lazaro ni pigo kubwa hasa kwa Masadukayo, kwa kuwa hawaamini katika ufufuo.
Kayafa, ambaye labda ni Sadukayo, sasa anajitokeza kunena, akisema: “Ninyi hamjui neno lo lote; wala hamfikiri ya kwamba yafaa mtu mmoja afe kwa ajili ya watu, wala lisiangamie taifa zima.”
Mungu alitumia uvutano juu ya Kayafa aseme hilo, kwa maana baadaye mtume Yohana aliandika hivi: “Neno hilo yeye [Kayafa] hakulisema kwa nafsi yake.” Jambo ambalo Kayafa alimaanisha hasa ni kwamba Yesu alipasa kuuawa ili kumzuia Yeye asiendelee kudhoofisha vyeo vyao vya mamlaka na umashuhuri. Hata hivyo, kulingana na Yohana, ‘Kayafa alitabiri [alitoa unabii, NW] ya kwamba Yesu atakufa si kwa ajili ya taifa hilo tu; lakini pamoja na hayo awakusanye watoto wa Mungu waliotawanyika.’ Na, kweli kweli, ni kusudi la Mungu kwamba Mwana wake afe akiwa ukombozi kwa ajili ya wote.
Sasa Kayafa anafaulu kutumia uvutano juu ya Sanhedrini ile ifanye mipango ya kuua Yesu. Lakini Yesu, yawezekana kwa kupashwa habari na Nikodemo, mshiriki wa Sanhedrini aliye na urafiki kwake, anaondoka huko. Yohana 11:38-54.
▪ Kwa nini Yesu anasali peupe kabla ya kufufua Lazaro?
▪ Wale walioona ufufuo huu wanauitikiaje?
▪ Ni nini kinachofunua uovu wa washiriki wa Sanhedrini?
▪ Kusudi la Kayafa lilikuwa nini, lakini Mungu alimtumia kutoa unabii juu ya nini?