Sura 92
Wakoma Kumi Waponywa Wakati wa Safari ya Mwisho ya Yesu Kwenda Yerusalemu
YESU anakatiza jitihada za Sanhedrini za kumuua kwa kuondoka Yerusalemu na kusafiri kwenda kwenye jiji la Efraimu, pengine kilometa 24 hivi kaskazini-mashariki ya Yerusalemu. Abaki huko pamoja na wanafunzi wake, mbali na maadui wake.
Hata hivyo, wakati wa Sikukuu ya Kupitwa ya 33 W.K. unakaribia, na upesi Yesu yumo mwendoni tena. Asafiri kupitia Samaria na kukwea kuingia katika Galilaya. Hii ndiyo ziara yake ya mwisho katika eneo hili kabla ya kifo chake. Anapokuwa katika Galilaya, yaelekea yeye na wanafunzi wake wanajiunga na wengine wanaoenda Yerusalemu kwa ajili ya mwadhimisho wa Sikukuu ya Kupitwa. Wanashika njia ipitayo wilaya ya Perea, mashariki ya Mto Yordani.
Mapema katika safari hii, wakati Yesu anapoingia katika kijiji kimoja katika Samaria au katika Galilaya, anakutana na wanaume kumi wenye ukoma. Ugonjwa huu mbaya sana hula polepole sehemu za mwili wa mtu—vidole vyake vya mikono na miguu, masikio yake, pua yake, na midomo yake. Ili kulinda usalama wa wengine wasiambukizwe, Sheria ya Mungu husema hivi kuhusu mwenye ukoma: “Atafunika mdogo wake wa juu, naye atapiga kelele, Ni najisi, ni najisi. Sikuzote ambazo pigo li ndani yake, yeye atakuwa mwenye unajisi; . . . atakaa peke yake.”
Wale wenye ukoma kumi wanashika vizuizi vya Sheria kwa wenye ukoma na kubaki mbali na Yesu. Hata hivyo, wao wanapiga kelele kwa sauti kubwa hivi: “Ee Yesu, Bwana mkubwa, Uturehemu!”
Akiwaona kwa umbali, Yesu aamuru: “Enendeni, mkajionyeshe kwa makuhani.” Yesu asema hivyo kwa sababu Sheria ya Mungu huwapa makuhani mamlaka ya kuwatangaza waliopona ugonjwa wao kuwa ni wenye ukoma walioponywa. Kwa njia hii hao wanapata kibali cha kuishi tena pamoja na watu wenye afya.
Wale wenye ukoma kumi wana uhakika na nguvu za kimuujiza za Yesu. Kwa hiyo wanaenda mbio kuona makuhani, hata ingawa hawajaponywa bado. Wakiwa njiani, imani yao katika Yesu inathawabishwa. Wanaanza kuhisi afya yao iliyorudhishwa!
Kenda kati ya wale wenye ukoma waliotakaswa waendelea na safari yao, lakini yule mwenye ukoma mwingine, Msamaria, anarudi kumtafuta Yesu. Kwa nini? Kwa sababu yeye anashukuru sana kwa yale yaliyompata. Asifu Mungu kwa sauti kubwa, na anapompata Yesu, anaanguka miguuni pake, na kumshukuru.
Katika kujibu Yesu anasema: “Hawakutakaswa wote kumi? Wale kenda wa wapi? Je! hawakuonekana waliorudi kumpa Mungu utukufu ila mgeni [mtu wa taifa jingine, NW] huyu?”
Kisha amwambia yule mtu wa Samaria: “Inuka, enenda zako, imani yako imekuokoa.”
Tunaposoma juu ya Yesu akiponya wale wenye ukoma kumi, inatupasa tuweke moyoni lile somo linalodokezwa na swali lake: “Wale kenda wa wapi?” Kule kutokuwa na shukrani kulikoonyeshwa na wale kenda ni udhaifu mzito. Je! sisi, kama yule Msamaria, tutajionyesha kuwa wenye shukrani kwa vitu tunvyopokea kutoka kwa Mungu, kutia na ahadi hakika ya uhai wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu? Yohana 11:54, 55; Luka 17:11-19; Walawi 13:16, 17, 45, 46; Ufunuo 21:3, 4.
▪ Yesu anakatizaje jitihada za kumuua?
▪ Halafu Yesu anasafiri wapi, na safari yake inaishia wapi?
▪ Kwa nini wale wenye ukoma wanasimama mbali, na kwa nini Yesu awaambia waende kwa makuhani?
▪ Ni somo gani tunapaswa kujifunza kutokana na ono hili?