Sura 111
Ishara ya Siku za Mwisho
KUFIKIA sasa ni alasiri ya Jumanne. Yesu anapoketi juu ya Mlima wa Mizeituni, akitazama hekalu lililo chini, Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana wamjia kwa faragha. Wao wahangaikia hekalu, kwa kuwa Yesu ndipo tu ametabiri kwamba ndani yalo hamna jiwe ambalo litaachwa juu ya jiwe.
Lakini kwa wazi wao wana mengi hata zaidi katika akili zao wakaribiapo Yesu. Majuma machache mapema kidogo, yeye alikuwa amenena juu ya “kuwapo” kwake, wakati ambapo “Mwana wa binadamu apasa kufunuliwa.” Na katika pindi ya mapema kidogo, alikuwa amewaambia juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” Kwa hiyo mitume wana hamu nyingi ya kutaka kujua.
“Tuambie,” wao wasema, “mambo hayo [yenye kutokeza uharibifu wa Yerusalemu na hekalu lalo] yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Kwa kweli, swali lao ni la sehemu tatu. Kwanza, wao wataka kujua juu ya mwisho wa Yerusalemu na hekalu lalo, halafu kuhusu kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme, na hatimaye juu ya mwisho wa mfumo mzima wa mambo.
Katika jibu lake refu, Yesu ajibu sehemu zote tatu za swali hilo. Yeye aandaa ishara ambayo yatambulisha wakati mfumo wa mambo ya Kiyahudi utaisha; lakini aandaa zaidi. Pia atoa ishara ambayo itawaweka chonjo wanafunzi wake wa wakati ujao ili waweze kujua kwamba wanaishi wakati wa kuwapo kwake na karibu na mwisho wa mfumo mzima wa mambo.
Miaka ipitapo, mitume waanza kuona utimizo wa unabiii wa Yesu. Ndiyo, mambo yale yale aliyotabiri yaanza kutukia katika siku yao. Hivyo, Wakristo walio hai miaka 37 baadaye, katika 70 W.K., hawashtukiwi na uharibifu wa mfumo wa Kiyahudi na hekalu lalo.
Hata hivyo, kuwapo kwa Kristo na umalizio wa mfumo wa mambo hakutukii katika 70 W.K. Kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme kwatukia baadaye sana. Lakini wakati gani? Ufikirio wa unabii wa Yesu wafunua hilo.
Yesu atabiri kwamba kutakuwako “vita na ripoti za vita.” “Taifa litainuka dhidi ya taifa,” yeye asema, na kutakuwako upungufu wa chakula, matetemeko ya dunia, na magonjwa ya kipuku. Wanafunzi wake watachukiwa na kuuawa. Manabii wa bandia watainuka na kuongoza wengi vibaya. Kutotii sheria kutaongezeka, na upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa. Wakati uo huo, habari njema za Ufalme wa Mungu zitahubiriwa kuwa ushahidi kwa mataifa yote.
Ingawa unabii wa Yesu unakuwa na utimizo wenye mipaka kabla ya uharibifu wa Yerusalemu katika 70 W.K., utimizo wao mkubwa hutukia wakati wa kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo. Pitio la uangalifu la matukio ya ulimwengu tangu 1914 hufunua kwamba unabii wa Yesu wenye matukio makubwa umekuwa ukipata utimizo mkubwa kuanzia mwaka huo.
Sehemu nyingine ya ishara ambayo Yesu atoa ni kuonekana kwa “kitu cha kunyarafisha kinachosababisha uharibifu.” Katika 66 W.K. kitu hicho cha kunyarafisha (kuchukiza) chatokea kwa namna ya “majeshi yenye kupiga kambi” ya Roma ambayo yazunguka Yerusalemu na kufukua ukuta wa hekalu. Hicho “kitu cha kunyarafisha” chasimama kisipopaswa.
Katika utumizo mkubwa wa ishara, hicho kitu cha kunyarafisha ni Ushirika wa Mataifa na mwandamizi wao, Umoja wa Mataifa. Tengenezo hili kwa ajili ya amani ya ulimwengu huonwa na Jumuiya ya Wakristo kuwa badala ya Ufalme wa Mungu. Lo, ni jambo lenye kunyarafisha kama nini! Kwa hiyo, baada ya muda, mamlaka za kisiasa zenye kushirikiana na UM zitageukia Jumuiya ya Wakristo (Yerusalemu wa ufananisho) na kuiacha ukiwa.
Hivyo Yesu atabiri kwamba: “Kutakuwako dhiki kubwa ya namna ambayo haijatukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena.” Ingawa uharibifu wa Yerusalemu katika 70 W.K. unakuwa dhiki kubwa kweli kweli, kukiwa na watu zaidi ya milioni moja wenye kuripotiwa kuwa waliuawa, si dhiki kubwa kuliko Gharika ya duniani pote katika siku za Noa. Kwa hiyo utimizo mkubwa wa kisehemu hiki cha unabii wa Yesu ungali utatimizwa.
Uhakika Katika Siku za Mwisho
Jumanne, Nisani 11, ikaribiapo kumalizika, Yesu aendelea kuzungumza na mitume wake ishara ya kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme na ya mwisho wa mfumo wa mambo. Yeye awaonya juu ya kukimbilia Makristo wa bandia. Majaribio yatafanywa, yeye asema, ‘kuwaongoza vibaya, ikiwezekana, hata wale wateule.’ Lakini, kama tai wenye kuona mbali, wateule hawa watakusanyika mahali palipo na chakula cha kiroho kilicho cha kweli, yaani, pamoja na Kristo wa kweli wakati wa kuwapo kwake kusikoonekana. Hawataongozwa vibaya wakusanywe pamoja kwa Kristo wa bandia.
Makristo wa bandia waweza kutokea kwa njia yenye kuonekana tu. Kwa kutofautisha, kuwapo kwa Yesu kutakuwa kusikoonekana. Kutatukia wakati wenye kuogopesha sana katika historia ya kibinadamu, kama asemavyo Yesu: “Jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa mwanga wao.” Ndiyo, hiki kitakuwa ndicho kipindi chenye giza lililo jeusi kupita vyote vya kuwako kwa ainabinadamu. Itakuwa kana kwamba jua lilitiwa giza wakati wa mchana, na kana kwamba mwezi haukutoa nuru yao wakati wa usiku.
“Nguvu za mbingu zitatikiswa,” Yesu aendelea. Hivyo aonyesha kwamba mbingu halisi zitakuwa na sura yenye dalili za matazamio mabaya. Mbingu hazitakuwa milki ya nyuni tu, bali zitajawa na ndege za vita, roketi, na vipekua anga za juu. Hofu na jeuri itazidi kitu chochote kilichoonwa katika historia iliyotangulia ya kibinadamu.
Kama tokeo, Yesu asema, kutakuwako “huzuni kuu ya mataifa, yasijue njia ya kutokea kwa sababu ya mngurumo wa bahari na msukosuko wayo, huku watu wakizirai kwa sababu ya hofu na taraja la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa.” Kweli kweli, kipindi hicho cha giza jeusi kuliko vyote vya kuwako kwa binadamu kitaongoza kwenye wakati ambao, kama Yesu asemavyo, “ishara ya Mwana wa binadamu itaonekana katika mbingu, na ndipo makabila yote ya dunia yatajipiga-piga yenyewe kwa ombolezo.”
Lakini si wote watakaokuwa wanaomboleza wakati ‘Mwana wa binadamu ajapo na mamlaka’ kuharibu mfumo huu mbovu wa mambo. “Wateule,” wale 144,000 watakaoshiriki pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa kimbingu, hawataomboleza, wala waandamani wao, wale ambao mapema kidogo Yesu aliwaita “kondoo wengine” wake. Wajapokuwa wanaishi katika kipindi kilicho na giza jeusi kuliko vyote vya historia ya kibinadamu, hawa waitikia kitia-moyo cha Yesu: “Mambo hayo yaanzapo kutukia, jiinueni wima na kuinua vichwa vyenu juu, kwa kuwa ukombozi wenu unakaribia.”
Ili wanafunzi wake ambao wangekuwa wanaishi katika siku za mwisho waweze kupambanua ukaribu wa mwisho, Yesu atoa kielezi hiki: “Utazameni mtini na miti mingine yote: Ikiisha kuchipuka tayari, kwa kuitazama nyinyi mwajua wenyewe kwamba sasa kiangazi kiko karibu. Kwa njia hiyo nyinyi pia, wakati mnapoona mambo haya yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu u karibu. Kweli kweli, mimi nasema kwenu nyinyi, Kizazi hiki hakitapitilia mbali kwa vyovyote mpaka mambo haya yote yatukie.”
Hivyo, wanafunzi waonapo zile sehemu nyingi tofauti-tofauti za ishara zikitimizwa, yawapasa wang’amue kwamba mwisho wa mfumo wa mambo uko karibu na kwamba karibuni Ufalme wa Mungu utafutilia mbali uovu wote. Kwa uhakika, mwisho utatukia katika muda wa maisha wa watu waonao utimizo wa mambo ambayo Yesu atabiri! Akionya kwa upole wale wanafunzi ambao wangekuwa hai wakati wa siku za mwisho zenye umaana mkubwa, Yesu asema:
“Jiangalieni ili mioyo yenu isije ikalemewa na kula kupita kiasi na kunywa kupita kiasi na masumbufu ya maisha, na kwa ghafula siku ile iwafyatukie kama mtego. Kwa maana itawajilia wote wale wanaokaa juu ya uso wa dunia. Endeleeni kukesha, basi, wakati wote mkifanya dua ili nyinyi mpate kufaulu katika kuyakimbia mambo hayo yote ambayo yamekusudiwa yatukie, na katika kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.”
Wale Wanawali Wenye Hekima na Wale Wapumbavu
Yesu amekuwa akijibu ombi la mitume wake la ishara ya kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme. Sasa anaandaa mambo zaidi ya ishara kwa mifano au vielezi vitatu.
Utimizo wa kila kielezi ungekuwa wenye kuonekana kwa wale wanaoishi wakati wa kuwapo kwake. Yeye atanguliza cha kwanza kwa maneno haya: “Ndipo ufalme wa mbingu utafanana na wanawali kumi ambao walitwaa taa zao na kutoka wakamlaki bwana-arusi. Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano walikuwa wenye busara.”
Kwa usemi “ufalme wa mbingu utakuwa kama wanawali kumi,” Yesu hamaanishi kwamba nusu ya wale wanaorithi Ufalme wa kimbingu ni watu wapumbavu na nusu ni wenye busara! Sivyo, bali yeye amaanisha kwamba kuhusiana na Ufalme wa mbingu, kuna upande ulio kama hivi au kama vile, au kwamba mambo kuhusiana na Ufalme yatakuwa kama kitu fulani-fulani.
Wale wanawali kumi wafananisha Wakristo wote ambao wako katika mstari kwa au ambao hudai kuwa katika mstari kwa ajili ya Ufalme wa kimbingu. Ilikuwa wakati wa Pentekoste 33 W.K. kwamba lile kundi la Kikristo lilipewa ahadi ya ndoa kwa Yesu Kristo, Bwana-arusi aliyefufuliwa na kutukuzwa. Lakini ndoa hiyo ingetukia katika mbingu katika wakati fulani ujao usiodhihirishwa.
Katika kielezi kile, wale wanawali kumi wanatoka kwenda wakiwa na kusudi la kumlaki bwana-arusi na kujiunga pamoja naye katika mwandamano wa arusi. Awasilipo, wao wataangazia njia ya mwandamano kwa taa zao, hivyo kumheshimu aletapo bibi-arusi wake kwenye nyumba aliyotayarishiwa. Hata hivyo, Yesu aeleza: “Wale wapumbavu walitwaa taa zao lakini wasitwae mafuta pamoja nao, hali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao. Bwana-arusi alipokuwa anakawia, wote wakasinzia wakalala usingizi.”
Ukawivu mwendelevu wa bwana-arusi huonyesha kwamba kuwapo kwa Kristo akiwa Mfalme anayetawala kungekuwa katika wakati ujao ulio mbali. Hatimaye anakuja kwenye kiti chake cha ufalme katika mwaka 1914. Wakati wa ule usiku mrefu kabla ya hapo, wale wanawali wote wanalala usingizi. Lakini hawakushutumiwa kwa sababu hiyo. Wale wanawali wapumbavu wanashutumiwa kwa kutokuwa na mafuta kwa ajili ya vyombo vyao. Yesu aeleza namna wale wanawali wanavyoamka kabla ya bwana-arusi kuwasili: “Katikati ya usiku barabara kukazuka kilio, ‘Bwana-arusi yupo hapa! Shikeni njia yenu kumlaki.’ Ndipo hao wanawali wote wakainuka na kutayarisha taa zao. Wale wapumbavu wakasema kwa wale wenye busara, ‘Tupeni baadhi ya mafuta yenu, kwa sababu taa zetu zakaribia kuzimika.’ Wale wenye busara wakajibu kwa maneno haya, ‘Labda hakuwezi kuwa yakututosha sisi na nyinyi. Badala ya hivyo, shikeni njia yenu, mwende kwa wale wenye kuyauza mkajinunulie.’”
Mafuta yafananisha kile kinachowaendeleza Wakristo wa kweli wakiwa wanaangaza wakiwa vimulikaji. Hilo ni Neno la Mungu lililovuviwa, ambalo Wakristo wanashika sana, pamoja na roho takatifu, ambayo huwasaidia katika kuelewa Neno hilo. Mafuta hayo ya kiroho huwezesha wale wanawali wenye busara waangaze nuru katika kumkaribisha bwana-arusi wakati wa mwandamano wa kwenda kwenye karamu ya ndoa. Lakini jamii ya wale wanawali wapumbavu haina ndani yao, katika vyombo vyao, yale mafuta ya kiroho yanayohitajiwa. Kwa hiyo Yesu aeleza linalotukia:
“Wakati [hao wanawali wapumbavu] walipokuwa wakienda zao kununua [mafuta], bwana-arusi akawasili, na wale wanawali ambao walikuwa tayari wakaingia ndani pamoja naye kwenye karamu ya ndoa; na mlango ukafungwa. Baadaye wale wengine wa wanawali wakaja pia, wakisema, ‘Bwana, bwana, tufungulie!’ Katika kujibu yeye akasema, ‘Mimi nawaambia ukweli, Mimi siwajui nyinyi.’”
Baada ya Kristo kuwasili akiwa katika Ufalme wake wa kimbingu, jamii ya wale wanawali wenye busara ya Wakristo wa kweli wapakwa-mafuta waamka kwenye pendeleo lao la kuangaza nuru katika ulimwengu huu uliotiwa giza katika kusifu Bwana-arusi aliyerudi. Lakini wale waliofananishwa na wale wanawali wapumbavu wanakuwa hawako tayari kuandaa sifa hii ya kukaribisha. Kwa hiyo wakati ufikapo, Kristo hawafungulii mlango wa karamu ya ndoa katika mbingu. Yeye awaacha nje katika weusi wa usiku mzito zaidi ya wote wa ulimwengu, wakapotee na wafanya kazi wengine wote wa uasi-sheria. “Endeleeni kukesha, basi,” Yesu amalizia, “kwa sababu nyinyi hamjui wala siku ile wala saa ile.”
Kile Kielezi cha Talanta
Yesu aendeleza mazungumzo pamoja na mitume wake katika Mlima wa Mizeituni kwa kuwaambia kielezi kingine, cha pili katika mfululizo wa vielezi vitatu. Siku chache mapema kidogo, alipokuwa Yeriko, alitoa kielezi cha mina kuonyesha kwamba Ufalme ulikuwa ungali mbali katika wakati ujao. Kielezi ambacho asimulia sasa, ingawa kina sehemu kadhaa zenye kufanana, chaeleza katika utimizo wacho utendaji mbalimbali wakati wa kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme. Chatoa kielezi kwamba ni lazima wanafunzi wake wafanye kazi wakiwa wangali duniani ili kuongezea “mali zake.”
Yesu aanza hivi: “Kwa maana hiyo [yaani, hali zenye kuhusiana na Ufalme] ni kama wakati mtu, akiwa karibu kusafiri ng’ambo, aliita watumwa wake na kuwakabidhi mali zake.” Yesu ndiye mtu ambaye, kabla ya kusafiri ng’ambo mbinguni, akabidhi watumwa wake—wanafunzi walio katika mstari wa kupata Ufalme wa kimbingu—mali zake. Mali hizi si mali za kimwili, bali zawakilisha shamba lililolimwa ambamo yeye amejenga uwezekano wa kutokeza wanafunzi zaidi.
Yesu akabidhi mali zake kwa watumwa wake muda mfupi kabla ya kupaa mbinguni. Yeye afanyaje hivyo? Kwa kuwaagiza waendelee kufanya kazi katika shamba lililositawishwa kwa kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwenye sehemu za mbali kabisa za dunia. Ni kama vile Yesu asemavyo: “Alimpa mmoja talanta tano, mwingine mbili, mwingine bado akampa moja, kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe, naye akaenda ng’ambo.”
Hivyo hizo talanta nane—mali za Kristo—zagawanywa kulingana na kadiri za uwezo, au kadiri za uwezekano wa kiroho, za watumwa. Watumwa hao wanasimamia jamii za wanafunzi. Katika karne ya kwanza, jamii iliyopokea talanta tano kwa wazi ilitia ndani mitume. Yesu aendelea kueleza kwamba wale watumwa waliopokea zile talanta tano na mbili walizirudufisha kwa kuhubiri kwao Ufalme na kufanya wanafunzi. Hata hivyo, mtumwa aliyepokea ile talanta moja aliificha katika ardhi.
“Baada ya muda mrefu,” Yesu aendelea kusema, “bwana-mkubwa wa watumwa hao alikuja akafanya hesabu nao.” Haikuwa mpaka karne ya 20, yapata miaka 1,900 baadaye, kwamba Kristo akarudi kufanya hesabu, kwa hiyo, ilikuwa kweli kweli, “baada ya muda mrefu.” Ndipo Yesu aeleza hivi:
“Yule mmoja aliyekuwa amepokea talanta tano akaja mbele na kuleta talanta tano za ziada, akisema, ‘Bwana-mkubwa, wewe ulinikabidhi talanta tano; ona, nilipata talanta tano zaidi.’ Bwana-mkubwa wake akamwambia, ‘Vema, mtumwa mwema na mwaminifu! Wewe ulikuwa mwaminifu juu ya vitu vichache. Mimi nitakuweka juu ya vitu vingi. Ingia ndani ya shangwe ya bwana-mkubwa wako.’” Vivyo hivyo mtumwa aliyepokea talanta mbili alirudufisha talanta zake, na alipokea pongezi na thawabu ile ile.
Ingawa hivyo, watumwa hawa waaminifu huingiaje ndani ya shangwe ya Bwana-mkubwa wao? Basi, shangwe ya Bwana-mkubwa wao, Yesu Kristo, ni ile ya kupokea umiliki wa Ufalme alipoenda ng’ambo kwa Baba yake mbinguni. Kwa habari ya watumwa waaminifu katika nyakati za ki-siku-hizi, wao wana shangwe kubwa katika kuaminishwa madaraka zaidi ya Ufalme, na wanapomaliza mwendo wao wa kidunia, watakuwa na shangwe ya upeo ya kufufuliwa kwenye Ufalme wa kimbingu. Lakini namna gani juu ya mtumwa wa tatu?
“Bwana-mkubwa, mimi nilikujua wewe kuwa u mtu mwenye kutoza sana,” mtumwa huyu alalamika. “Kwa hiyo mimi niliogopa nikaenda na kuficha talanta yako katika ardhi. Hii hapa chukua kilicho chako.” Mtumwa huyo alikataa kimakusudi kufanya kazi katika shamba lililositawishwa kwa kuhubiri na kufanya wanafunzi. Kwa hiyo bwana-mkubwa amwita “mwovu na goigoi” na kutamka hukumu: “Mpokonyeni talanta . . . na mmtupe mtumwa asiyefaa kitu nje ndani ya giza la nje. Huko ndiko kutakuwako kilio chake na kusaga meno yake.” Wale wa jamii hii ya mtumwa mwovu, kwa kutupwa nje, hunyimwa shangwe yoyote ya kiroho.
Hii hutokeza somo zito kwa wote ambao hudai kuwa wafuasi wa Kristo. Ni lazima wafanye kazi ili kuongezea mali za Bwana-mkubwa wao wa kimbingu kwa kuwa na ushiriki kamili katika kazi ya kuhubiri ikiwa wataona shangwe ya kupongezwa na kuthawabishwa, na ikiwa wataepuka kutupwa ndani ya giza lililo nje na uharibifu wa hatimaye. Je! wewe u mwenye bidii ya uendelevu katika habari hii?
Kristo Awasilipo Katika Mamlaka ya Ufalme
Yesu angali pamoja na mitume wake juu ya Mlima wa Mizeituni. Katika kujibu ombi lao la ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo, sasa awaambia kielezi kilicho cha mwisho katika mfululizo wa vielezi vitatu. “Awasilipo Mwana wa binadamu katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye,” Yesu aanza, “ndipo atakapoketi juu ya kiti cha ufalme chake chenye utukufu.”
Wanadamu hawawezi kuona malaika katika utukufu wao wa kimbingu. Kwa hiyo kuwasili kwa Mwana wa binadamu, Yesu Kristo, pamoja na malaika ni lazima kuwe kusikoonekana kwa macho ya kibinadamu. Kuwasili huko kwatukia katika mwaka 1914. Lakini kwa kusudi gani? Yesu aeleza hivi: “Mataifa yote yatakusanywa mbele zake, naye atatenga watu mmoja kutoka kwa mwingine, kama vile mchungaji atengavyo kondoo kutoka kwa mbuzi. Naye ataweka kondoo katika mkono wake wa kulia, bali mbuzi katika kushoto kwake.”
Akisimulia litakalopata wale waliotengwa wawe upande wenye kupendelewa, Yesu asema hivi: “Kisha mfalme atawaambia wale walio mkono wake wa kulia, ‘Njooni nyinyi wenye kubarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi ya ulimwengu.’” Kondoo wa kielezi hiki hawatatawala pamoja na Kristo mbinguni bali watarithi Ufalme katika maana ya kuwa raia zao za kidunia. “Kuwekwa msingi wa ulimwengu” kulitukia wakati Adamu na Hawa walipozaa kwanza watoto ambao wangeweza kunufaika na uandalizi wa Mungu wa kufidia ainabinadamu.
Lakini kwa nini kondoo hutengwa wawe kwenye mkono wa kulia wenye upendeleo wa Mfalme? “Kwa maana mimi nilipata kuwa na njaa,” ajibu mfalme, “na nyinyi mlinipa kitu cha kula; nilipata kuwa na kiu na nyinyi mlinipa kitu cha kunywa. Nilikuwa mgeni na nyinyi mkanipokea kwa ukaribishaji wageni; uchi, na nyinyi mkanivika mavazi. Nilipata kuwa mgonjwa na nyinyi mkanitunza. Nilikuwa gerezani na nyinyi mlinijia.”
Kwa kuwa kondoo wapo duniani, wao wataka kujua ni jinsi gani wangeweza kuwa walimfanyia Mfalme wao wa kimbingu matendo mema jinsi hiyo. Wao wauliza, “Bwana, ni lini tulipokuona wewe una njaa nasi tukakulisha wewe,” wao wauliza, “au mwenye kiu, nasi tukakupa kitu cha kunywa? Ni lini sisi tulipokuona wewe u mgeni na tukakupokea wewe kwa ukaribishaji wageni, au uchi, na kukuvika mavazi wewe? Ni lini tulipokuona wewe u mgonjwa au gerezani na kuja kwako?”
“Kweli kweli, mimi nawaambia nyinyi,” Mfalme ajibu, “kwa kadiri ambayo nyinyi mlifanya hivyo kwa mmoja aliye mdogo zaidi ya wote wa hawa ndugu zangu, nyinyi mlifanya hilo kwangu mimi.” Ndugu za Kristo ni wale waliosalia duniani kati ya wale 144,000 watakaotawala pamoja naye mbinguni. Na kuwafanyia mema, Yesu asema, ni sawa na kumfanyia yeye mema.
Halafu, Mfalme ahutubia wale mbuzi. “Nendeni zenu kutoka kwangu mimi, nyinyi mliolaaniwa, mkaingie katika moto wa milele aliotayarishiwa Ibilisi na malaika zake. Kwa maana mimi nilipata kuwa na njaa, lakini nyinyi hamkunipa chochote cha kula, na nilipata kuwa na kiu, lakini nyinyi hamkunipa chochote cha kunywa. Nilikuwa mgeni, lakini nyinyi hamkunipokea kwa ukaribishaji wageni; uchi, lakini nyinyi hamkunivika mavazi; mgonjwa na katika gereza, lakini nyinyi hamkunitunza mimi.”
Hata hivyo, mbuzi wale walalamika hivi: “Bwana, ni lini tulipokuona wewe ukiwa na njaa au kiu au mgeni au uchi au mgonjwa au gerezani na hatukukuhudumia wewe?” Mbuzi wahukumiwa vikali kwa msingi ule ule ambao kondoo wahukumiwa kwa njia yenye kupendelewa. “Kwa kadiri ambayo nyinyi hamkufanya hivyo kwa mmoja aliye mdogo zaidi ya wote [wa ndugu zangu],” Yesu ajibu, “nyinyi hamkunifanyia mimi hilo.”
Kwa hiyo kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme, kabla tu ya mwisho wa huu mfumo mbovu wa mambo katika ile dhiki kubwa, utakuwa wakati wa hukumu. Wale mbuzi “wataondoka wakaingie katika kukatiliwa mbali milele, bali wale wenye uadilifu [kondoo] wakaingie katika uhai wa milele.” Mathayo 24:2–25:46; 13:40, 49; Marko 13:3-37; Luka 21:7-36; 19:43, 44; 17:20-30; 2 Timotheo 3:1-5; Yohana 10:16; Ufunuo 14:1-3, NW.
▪ Ni kitu gani kinachowasukuma mitume waulize swali lao, lakini kwa wazi ni kitu gani kingine walicho nacho katika akili zao?
▪ Ni sehemu gani ya unabii wa Yesu inatimizwa katika 70 W.K., lakini ni nini hakitukii wakati huo?
▪ Unabii wa Yesu wapata utimizo wa kwanza lini, lakini ni lini unapokuwa na utimizo mkubwa?
▪ Ni nini kitu cha kunyarafisha katika utimizo wacho wa kwanza na wa mwisho?
▪ Kwa nini dhiki kubwa haiwi na utimizo wa mwisho kwa uharibifu wa Yerusalemu?
▪ Ni hali gani za ulimwengu zatia alama kuwapo kwa Kristo?
▪ Ni wakati gani ‘makabila yote ya dunia yanapojipiga-piga yenyewe kwa ombolezo,’ lakini wafuasi wa Yesu watakuwa wakifanya nini?
▪ Yesu aandaa kielezi gani kusaidia wanafunzi wake wa wakati ujao kufahamu wakati mwisho uko karibu?
▪ Ni shauri gani ambalo Yesu aandalia baadhi ya wanafunzi wake ambao wangekuwa wakiishi katika siku za mwisho?
▪ Ni nani wanafananishwa na wale wanawali kumi?
▪ Kundi la Kikristo liliahidiwa ndoa kwa bwana-arusi wakati gani, lakini bwana-arusi awasili wakati gani apeleke bibi-arusi wake kwenye karamu ya ndoa?
▪ Mafuta yawakilisha nini, na kuwa nayo kwawezesha wale wanawali wenye busara wafanye nini?
▪ Karamu ya ndoa inatukia wapi?
▪ Wale wanawali wapumbavu wakosa thawabu gani tukufu, nao wapatwa na nini?
▪ Kielezi cha talanta chafundisha somo gani?
▪ Watumwa ni nani, na mali wanazoaminishwa ni nini?
▪ Ni wakati gani bwana-mkubwa aja kufanya hesabu, naye apata nini?
▪ Ni shangwe gani ambamo watumwa waaminifu waingia, na mtumwa wa tatu, yule mwovu apatwa na nini?
▪ Kwa nini kuwapo kwa Kristo lazima kuwe kusikoonekana, na ni kazi gani ambayo afanya wakati huo?
▪ Kondoo warithi Ufalme katika maana gani?
▪ “Kuwekwa msingi wa ulimwengu” kulitukia wakati gani?
▪ Watu wahukumiwa kuwa kondoo au mbuzi kwa msingi gani?