Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • gt sura 132
  • Kwenye Mkono wa Kuume wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwenye Mkono wa Kuume wa Mungu
  • Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Habari Zinazolingana
  • Kwenye Mkono wa Kuume wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Kristo Akiwa Kwenye Mkono wa Kuume wa Mungu
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Wakienda Damasko
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
  • Je, Watu Wanaofanya Mabaya Wanaweza Kubadilika?
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
Pata Habari Zaidi
Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
gt sura 132

Sura 132

Kwenye Mkono wa Kuume wa Mungu

KUMIMINWA kwa roho takatifu katika siku ya Pentekoste ni uthibitisho kwamba Yesu amefika mbinguni. Njozi aliyopewa mwanafunzi Stefano muda mfupi baadaye inathibitisha pia kwamba Yeye amefika huko. Kabla tu ya Stefano kupigwa kwa mawe kwa ajili ya kutoa kwake ushuhuda kwa uaminifu, apaaza sauti hivi: “Tazama! naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu.”

Anapokuwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu, Yesu angojea amri hii kutoka kwa Baba yake: “Nenda hali ukitiisha katikati ya adui zako.” Lakini kwa sasa, mpaka wakati ufike wa kuwachukulia maadui wake hatua, Yesu afanya nini? Atawala, au kumiliki juu ya wanafunzi wake wapakwa-mafuta, akiwaongoza katika utendaji wao wa kuhubiri na kuwatayarisha wawe, kwa njia ya ufufuo, wafalme washirika pamoja naye katika Ufalme wa Baba yake.

Kwa mfano, Yesu ateua Sauli (ambaye baadaye ajulikana zaidi kwa jina lake la Kiroma, Paulo) aongoze kazi ya kufanya wanafunzi katika nchi nyinginezo. Sauli ni mwenye bidii katika Sheria ya Mungu, hata hivyo anaongozwa vibaya na viongozi wa kidini Wayahudi. Kama tokeo, si kwamba Sauli akubaliana tu na kuuawa kwa Stefano bali yeye aenda Dameski kwa ruhusa ya kuhani mkuu Kayafa ili awakamate na kuwaleta Yerusalemu wanaume na wanawake wowote anaowapata huko ambao ni wafuasi wa Yesu. Hata hivyo, Sauli anapokuwa njiani, ghafula nuru yenye kung’aa yaangaza kumzunguka pande zote, naye aanguka chini.

“Sauli, Sauli, mbona waniudhi [kwa nini unaninyanyasa mimi, NW]?” sauti kutoka chanzo kisichoonekana yauliza. “U nani wewe, Bwana?” Sauli auliza.

“Mimi ndimi Yesu unayeniudhi [ambaye unaninyanyasa, NW] wewe,” laja jibu.

Sauli, ambaye amepofushwa na nuru hiyo ya kimuujiza, aambiwa na Yesu aingie Dameski na kungojea maagizo. Halafu Yesu amtokea Anania katika njozi, ambaye ni mmoja wa wanafunzi wake. Kuhusu Sauli, Yesu amwambia Anania hivi: “Huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli.”

Kweli kweli, akiwa na utegemezo wa Yesu, Sauli (anayejulikana sasa kwa jina Paulo) pamoja na waeneza evanjeli wengine wapata mafanikio makubwa katika kazi yao ya kuhubiri na kufundisha. Kwa kweli, karibu miaka 25 baada ya kutokewa na Yesu barabarani kwenda Dameski, Paulo aandika kwamba “habari njema” (NW) ‘zimehubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.’

Baada ya miaka mingine mingi kupita, Yesu amwandalia mtume wake mpendwa, Yohana, njozi mfululizo. Kupitia njozi hizo ambazo Yohana aeleza katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo, kwa kweli, ni kana kwamba yeye aishi na kumwona Yesu akirudi katika mamlaka ya Ufalme. Yohana asema kwamba “kwa kuvuviwa” (NW) yeye asafirishwa kusonga mbele katika wakati hadi “siku ya Bwana.” Hiyo ni “siku” gani?

Kujifunza kwa uangalifu unabii mbalimbali wa Biblia, kutia na unabii wa Yesu mwenyewe kuhusu siku za mwisho, kwafunua kwamba “siku ya Bwana” ilianza katika mwaka wenye maana sana kihistoria wa 1914, ndiyo, katika kizazi hiki! Kwa hiyo ni katika 1914 kwamba Yesu alirudi bila kuonekana, bila kujionyesha hadharani kwa njia yenye kutazamisha na watumishi wake waaminifu wakiwa ndio tu wanaotambua kurudi kwake. Katika mwaka huo Yehova alimpa Yesu amri aende akitiisha katikati ya maadui wake!

Akitii amri ya Baba yake, Yesu alisafisha mbingu kwa kumwondosha Shetani na roho wake waovu, akiwatupa chini duniani. Baada ya kuona hilo likitukia katika njozi, Yohana asikia sauti ya kimbingu ikitangaza hivi: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake.” Ndiyo, katika 1914 Kristo alianza kutawala akiwa Mfalme!

Hiyo ni habari njema kama nini kwa waabudu wa Yehova mbinguni! Wanahimizwa hivi: “Shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo.” Lakini hali ikoje kwa wale walio duniani? “Ole wa nchi na bahari!” yaendelea sauti kutoka mbinguni, “kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”

Sasa hivi sisi tumo katika wakati huo mchache. Kwa sasa watu wanatenganishwa ama ili waingie ulimwengu mpya wa Mungu ama ili waharibiwe. Ukweli ni kwamba, yatakayokupata wewe yanaamuliwa sasa kwa jinsi unavyoitikia habari njema za Ufalme wa Mungu ambao unahubiriwa ulimwenguni pote chini ya mwelekezo wa Kristo.

Wakati kutenganishwa kwa watu kumalizikapo, Yesu Kristo atatumika akiwa Wakili wa Mungu aondolee mbali kutoka dunia mfumo wote wa mambo wa Shetani na wale wanaouunga mkono. Yesu atatimiza kuondolewa huko kwa uovu wote katika vita inayoitwa katika Biblia Har–Magedoni. Baadaye, Yesu, akiwa ndiye Mtu mkuu zaidi ya wote katika ulimwengu wote mzima kufuata Yehova Mungu mwenyewe, atamkamata Shetani na roho wake waovu na kuwafunga kwa miaka elfu katika “abiso,” (NW) yaani, hali ya kutotenda kama ya kifo. Matendo 7:55-60; 8:1-3; 9:1-19; 16:6-10; Zaburi 110:1, 2, NW; Waebrania 10:12, 13; 1 Petro 3:22; Luka 22:28-30; Wakolosai 1:13, 23; Ufunuo 1:1, 10; 12:7-12; 16:14-16; 20:1-3; Mathayo 24:14; 25:31-33.

▪ Baada ya Yesu kupaa mbinguni, akaa wapi, naye angojea nini?

▪ Yesu atawala juu ya nani baada ya kupaa mbinguni, na utawala wake wadhihirikaje?

▪ “Siku ya Bwana” ilianza wakati gani, na ni jambo gani lililotukia ilipoanza?

▪ Ni kazi gani ya kutenganisha inayoendelea sasa ambayo inahusu kila mmoja wetu kibinafsi, na kutenganishwa kunafanywa kwa msingi gani?

▪ Kazi ya kutenganisha inapoisha, ni matukio gani yatafuata?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki