Maisha na Huduma ya Yesu
Kwenye Mkono wa Kuume wa Mungu
KUMWAGWA kwa roho takatifu katika Pentekoste ni ushuhuda kwamba Yesu amefika mbinguni. Njozi iliyopewa kwa mwanafunzi Stefano muda mfupi baadaye inathibitisha pia kwamba Yeye amefika huko. Kabla tu Stefano hajapigwa kwa mawe kwa ajili ya kutoa kwake ushuhuda kwa uaminifu, apaaza sauti hivi: “Tazama! naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu.”
Wakati yuko kwenye mkono wa kuume wa Mungu, Yesu angojea amri kutoka kwa Baba: “ Uwe na enzi kati ya adui zako.” Lakini wakati wa sasa, mpaka yeye apigane dhidi ya adui zake, Yesu afanya nini? Atawala au amiliki, juu ya wanafunzi wake wapakwa-mafuta, akiwaongoza katika utendaji wao wa kuhubiri, na kwa ufufuo akiwatayarisha kuwa wafalme washiriki pamoja naye katika Ufalme wa Baba yake.
Kwa mfano, Yesu achagua Sauli (anayejulikana vizuri baadaye kwa jina lake la Kiroma, Paulo) kutanguliza kazi ya kufanya wanafunzi katika mabara mengine. Sauli ni mwenye bidii katika Sheria ya Mungu, hata hivyo anaongozwa vibaya na viongozi wa kidini wa Kiyahudi. Kama tokeo, Sauli hakubaliani tu na uuaji wa Stefano lakini aenda Dameski akiwa na mamlaka kutoka kwa Kayafa kuhani wa juu ili kuleta Yerusalemu wanaume na wanawake wowote walio wafuasi wa Yesu wenye kushikwa ambao amewapata huko. Hata hivyo, Sauli anapokuwa njiani, nuru yenye kung’aa inamwangaza kotekote kumzunguka, naye aanguka chini.
“Sauli, Sauli, mbona waniudhi?” sauti kutoka chanzo kisichoonekana yauliza. “U nani wewe, Bwana?” Sauli auliza.
“Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe,” laja jibu.
Sauli, ambaye amepofushwa na nuru ya kimuujiza, aambiwa na Yesu aingie Dameski na angojee maagizo. Halafu Yesu amtokea Anania mwanafunzi wake mmoja, katika njozi. Kuhusu Sauli, Yesu amwambia Anania hivi: “Huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli.”
Kweli kweli, wakiwa na utegemezo wa Yesu, Sauli (anayejulikana sasa kuwa Paulo) na waevanjeli wengine hufanikiwa sana katika kazi yao ya kuhubiri na kufundisha. Kwa hakika, karibu miaka 25 baada ya kutokewa na Yesu katika barabara akielekea Dameski, Paulo aandika kwamba “habari njema” (NW) ‘imehubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.’
Baada ya miaka mingine mingi kupita, Yesu aandaa mfululizo wa njozi kwa mtume wake mpendwa Yohana. Kupitia njozi hizo ambazo Yohana aeleza katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo, yeye, kwa kweli, aishi kumwona Yesu akirudi katika mamlaka ya Ufalme. Yohana asema kwamba “kwa kupuliziwa roho” alisafirishwa mbele katika wakati wa “siku ya Bwana.” Hiyo ni “siku” gani?
Funzo lenye uangalifu la unabii wa Biblia, kutia na unabii wa Yesu mwenyewe kuhusu siku za mwisho, hufunua kwamba “siku ya Bwana” ilianza katika mwaka wa maana sana kihistoria wa 1914, naam, katika kizazi hiki! Kwa hiyo katika 1914 ndipo Yesu aliporudi bila kuonekana, bila mshindo wa kupiga matarumbeta peupe na kurudi kwake kukifahamiwa na watumishi wake waaminifu tu. Katika mwaka huo, Yehova alimpa Yesu amri aende akitiisha katikati ya adui zake!
Akitii amri ya Baba yake, Yesu alisafisha mbingu zitokwe na Shetani na roho waovu wake, akiwatupa duniani. Baada ya kuona hayo yakitokea, katika njozi Yohana asikia sauti ya kimbingu ikitangaza hivi: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake!” Naam, katika 1914 Kristo alianza kutawala akiwa Mfalme!
Hiyo ni habari njema kama nini kwa waabudu wa Yehova mbinguni! Wanahimizwa hivi: “Shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo.” Lakini hali ikoje kwa wale walio duniani? “Ole wa nchi na bahari,” yaendelea sauti kutoka mbinguni, “kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”
Tuko katika wakati huo mchache sasa hivi. Watu kwa sasa wanatenganishwa ama kuingia ulimwengu mpya wa Mungu ama kupata uharibifu. Ukweli ni kwamba, mwisho wako unaamuliwa sasa kwa jinsi unavyoitikia habari njema ya Ufalme wa Mungu ambao unahubiriwa ulimwenguni pote chini ya mwelekezo wa Yesu.
Wakati kutenganishwa kwa watu kumemalizwa, Yesu Kristo atatumika akiwa Wakili wa Mungu ili kuondolea dunia mfumo wote mzima wa mambo ya Shetani na wale wote wanaouunga mkono. Yesu atatimiza kuondoa huko kwa uovu wote katika vita inayoitwa katika Biblia Har–Magedoni. Baada ya hayo, Yesu, Mtu mkuu kupita wote katika ulimwengu wote mzima wa pili kwa Yehova Mungu mwenyewe, atamkamata Shetani na roho waovu wake na kuwafunga kwa miaka elfu katika “abiso” (NW), yaani, hali ya kutotenda kama ya kifo. Matendo 7:55-60; 8:1-3; 9:1-19; 16:6-10; Zaburi 110:1, 2, NW; Waebrania 10:12, 13; 1 Petro 3:22; Luka 22:28-30; Wakolosai 1:13, 23; Ufunuo 1:1, 10; 12:7-12; 16:14-16; 20:1-3; Mathayo 24:14; 25:31-33.
◆ Baada ya Yesu kupaa mbinguni, yuko mahali gani, naye angojea nini?
◆ Yesu atawala juu ya nani baada ya kupaa mbinguni, na kutawala kwake kwaonyeshwaje?
◆ “Siku ya Bwana” ilianza wakati gani, na ni jambo gani lililotokea ilipoanza?
◆ Ni kazi gani ya kutenganisha leo ambayo inahusu kila mmoja wetu binafsi, na kutenganisha kunafanywa kwa msingi gani?
◆ Kazi ya kutenganisha iishapo, ni matukio gani yatakayofuata?