Faraja kwa Walioshuka Moyo
“Viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.” (Warumi 8:22) Kuteseka kwa kibinadamu kulikuwa kwingi wakati hayo yalipoandikwa zaidi ya miaka 1,900 iliyopita. Wengi walikuwa wameshuka moyo. Kwa hiyo, Wakristo walihimizwa hivi: “Semeni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.”—1 Wathesalonike 5:14, New World Translation.
Leo, taabu ya kibinadamu ni kubwa hata zaidi, na watu wengi kuliko wakati mwingine wowote wameshuka moyo. Lakini je, hilo litushangaze? Sivyo hasa, kwani Biblia huzitambulisha hizi kuwa “siku za mwisho” na huziita “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5, NW) Yesu Kristo alitabiri kwamba wakati wa siku za mwisho, kungekuwako “huzuni kuu ya mataifa” na “watu [wangekuwa] wenye kuzimia kwa hofu na tarajio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa.”—Luka 21:7-11, 25-27; Mathayo 24:3-14, NW.
Watu wanapopatwa kwa muda mrefu na wasiwasi, hofu, kihoro, na hisiamoyo nyinginezo zisizofaa kama hizo, mara nyingi wao hushuka moyo. Kisababishi cha mshuko wa moyo au huzuni nyingi mno huenda kikawa kifo cha mpendwa, talaka, kupoteza kazi, au ugonjwa usiokoma. Watu hushuka moyo pia wanapoanza kuhisi hawafai kitu, wanapohisi wamekosa kufaulu na kwamba wametamausha kila mtu. Mtu yeyote aweza kufadhaishwa na hali yenye mkazo, lakini mtu anapoanza kukata tamaa na kukosa kuona suluhisho la hali mabaya, tokeo laweza kuwa mshuko wa moyo mkubwa mno.
Katika nyakati za kale watu walipatwa na hisia zizo hizo. Ayubu alipatwa na ugonjwa na msiba wa kibinafsi. Alihisi Mungu alikuwa amemwacha, kwa hiyo alionyesha kuchukia sana maisha. (Ayubu 10:1; 29:2, 4, 5) Yakobo alishuka moyo juu ya kile kilichoonekana kuwa kifo cha mwana wake, akikataa kufarijiwa akatamani kufa. (Mwanzo 37:33-35) Akihisi kuwa na hatia juu ya kosa zito, Mfalme Daudi aliomboleza hivi: “Mchana kutwa nimekwenda nikihuzunika. Nimedhoofika.”—Zaburi 38:6, 8; 2 Wakorintho 7:5, 6.
Leo, wengi wameshuka moyo kwa sababu ya kujilemeza wenyewe, kwa kujaribu kufuata utaratibu wa kila siku upitao uwezo wao wa kiakili, kihisiamoyo, na wa kimwili. Kwa kadiri ionekanavyo, mkazo pamoja na fikira na hisiamoyo zisizofaa, zaweza kuuathiri mwili na kuchangia ukosefu wa usawaziko wa kemikali katika ubongo, hivyo zikitokeza mshuko wa moyo.—Linganisha Mithali 14:30.
Msaada Wanaohitaji
Epafrodito, Mkristo mmoja wa karne ya kwanza kutoka Filipi, alikuwa ‘ameshuka moyo sana kwa sababu [marafiki wake] walikuwa wamesikia kwamba alikuwa mgonjwa.’ Epafrodito, aliyekuwa amekuwa mgonjwa baada ya kutumwa Roma na marafiki wake akiwa na maandalizi kwa ajili ya Paulo, labda alihisi kwamba alikuwa amewatamausha marafiki wake na kwamba walimwona kuwa mtu asiyefaulu. (Wafilipi 2:25-27; 4:18, NW) Mtume Paulo alisaidiaje?
Alimtuma Epafrodito nyumbani akiwa na barua kwa wale marafiki Wafilipi iliyosema hivi: “Mpokeeni [Epafrodito], basi, katika Bwana, kwa furaha yote, mkawahesabu watu kama huyu kuwa watu wa kuheshimiwa.” (Wafilipi 2:28-30) Jambo la kwamba Paulo alisema kwa kumsifu sana na kwamba Wafilipi walimkaribisha kwa uchangamfu na shauku, kwa hakika ni lazima liwe lilimliwaza Epafrodito na kusaidia kuondoa mshuko wake wa moyo.
Pasipo shaka, shauri la Bibila la “[kusema] kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo” ni bora zaidi. “Unahitaji kujua kwamba wengine wanakujali ukiwa mtu,” akasema mwanamke mmoja aliyekuwa na mshuko wa moyo. “Unahitaji kusikia mtu akisema, ‘Ninaelewa; hali yako itakuwa njema.’”
Mtu ambaye ameshuka moyo mara nyingi huhitaji kuchukua hatua ya kwanza kwa kumtafuta mtu mwenye hisia-mwenzi ambaye yeye aweza kutumainisha siri zake. Mtu huyo apaswa awe msikilizaji mzuri na mwenye saburi nyingi. Yeye apaswa aepuke kumkemea yule aliyeshuka moyo au kusema maneno ya kumhukumu, kama vile, ‘Hupaswi kuhisi hivyo’ au, ‘Huo ni mtazamo mbaya.’ Hisiamoyo za mtu aliyeshuka moyo zaweza kuumizwa upesi, na maneno hayo yenye kuchambua yatamfanya tu ahisi vibaya zaidi juu yake mwenyewe.
Huenda mtu ambaye ameshuka moyo akahisi hafai kitu. (Yona 4:3) Hata hivyo, mtu apaswa akumbuke kwamba jambo la maana sana ni jinsi ambavyo Mungu humthamini mtu. Watu ‘hawakumhesabu Yesu Kristo kuwa kitu,’ lakini hilo halikubadili thamani yake ya kweli kwa Mungu. (Isaya 53:3) Hakikishiwa ya kwamba, jinsi Mungu ampendavyo Mwana wake kipenzi, ndivyo akupenda wewe pia.—Yohana 3:16.
Yesu aliwasikitikia wale waliokuwa katika taabu na alijaribu kuwasaidia waone jinsi wao mmoja mmoja walivyokuwa wenye thamani. (Mathayo 9:36; 11:28-30; 14:14) Alifafanua kwamba Mungu huthamini hata mashomoro wadogo, wasio na maana. “Hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu,” akasema. Yeye huthamani kwa kadiri kubwa zaidi kama nini wanadamu wanaojaribu kufanya mapenzi yake! Yesu alisema hivi juu yao: “Hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote.”—Luka 12:6, 7.
Ni kweli, huenda ikawa vigumu kwa mtu ambaye ameshuka moyo sana, anayelemezwa na udhaifu na upungufu wake mbalimbali, kuamini kwamba Mungu humthamini sana. Huenda akawa na uhakika kwamba hafai kupata upendo na utunzaji wa Mungu. “Mioyo yetu inatuhukumu,” Neno la Mungu hukiri. Lakini je, hilo ndilo linaloamua mambo? La. Mungu ajua kwamba huenda wanadamu wenye dhambi wakafikiri isivyofaa na hata kujihukumu wenyewe. Kwa hiyo Neno lake huwafariji hivi: “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote.”—1 Yohana 3:19, 20.
Ndiyo, Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo huona zaidi ya kuona tu dhambi na makosa yetu. Yeye ajua hali zenye kusababisha makosa, mwendo wote wa maisha yetu, makusudio na nia zetu. Ajua kwamba tulirithi dhambi, ugonjwa, na kifo na kwa hiyo tuna upungufu mwingi ulio mkubwa. Jambo la kwamba tunahisi kuhuzunika na kuudhika na sisi wenyewe ni uthibitisho wenyewe wa kwamba hatutaki kutenda dhambi na kwamba hatujapita kiasi. Biblia husema kwamba ‘tulitiishwa chini ya ubatili’ dhidi ya mapenzi yetu. Kwa hiyo Mungu husikitikia hali yetu yenye kuhuzunisha, na yeye hukumbuka kwa huruma udhaifu wetu mbalimbali.—Warumi 5:12; 8:20.
“BWANA [Yehova, NW] amejaa huruma na neema,” tunahakikishiwa. “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:8, 12, 14) Kwa kweli, Yehova ni “Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.
Msaada ambao wale walioshuka moyo wanahitaji zaidi hutokana na kumkaribia Mungu wao mwenye rehema na kukubali mwaliko wake wa ‘kumtwika mzigo wao.’ Yeye aweza kwa kweli ‘kuhuisha moyo wa wale wanaopondwa.’ (Zaburi 55:22, UV; Isaya 57:15, NW) Kwa hiyo Neno la Mungu hutia moyo kusali, likisema hivi: “Mkimtupia [Yehova] mahangaiko yenu yote, kwa sababu yeye anawajali nyinyi.” (1 Petro 5:7, NW) Naam, kupitia sala na maombi ya kusihi, watu wanaweza kumkaribia Mungu na kufurahia “amani ya Mungu ipitayo akili zote [wazo lote, NW].”—Wafilipi 4:6, 7; Zaburi 16:8, 9.
Marekebisho yafaayo katika mtindo-maisha yaweza pia kumsaidia mtu ashinde hali ya kushuka moyo. Mazoezi ya kimwili, kula chakula kifaacho, kupata hewa safi na pumziko la kutosha, na kuepuka kutazama TV kupita kiasi, hayo yote ni ya maana. Mwanamke mmoja amewasaidia wale walioshuka moyo kwa kuwafanya watembee kwa sulubu. Wakati bibi mmoja mwenye kushuka moyo aliposema: “Mimi sitaki kutembea,” mwanamke huyo alijibu hivi kwa wororo lakini kwa uthabiti: “Ndiyo, utatembea.” Mwanamke huyo aliripoti hivi: ‘Tulitembea mwendo wa kilometa sita. Tuliporudi, alikuwa amechoka, lakini alihisi nafuu. Huwezi kuamini jinsi mazoezi yenye sulubu yalivyo yenye kusaidia mpaka unapoyajaribu.’
Hata hivyo, nyakati nyingine haiwezekani kushinda mshuko wa moyo kabisa, hata wakati ambapo kila kitu kimejaribiwa, kutia na matibabu. “Nimejaribu kila kitu,” akasema mwanamke wa makamo, “lakini mshuko wa moyo waendelea.” Vivyo hivyo, sasa haiwezekani mara nyingi kuwaponya vipofu, viziwi, au vilema. Hata hivyo, wale walioshuka moyo wanaweza kupata faraja na tumaini kwa kusoma kwa ukawaida Neno la Mungu, ambalo huandaa lile tumaini la hakika la kitulizo chenye kudumu cha maradhi yote ya kibinadamu.—Warumi 12:12; 15:4.
Wakati Ambapo Hakuna Atakayeshuka Moyo Tena
Yesu aliposimulia juu ya yale mambo mabaya sana yanayoijia dunia katika siku za mwisho, aliongeza hivi: “Mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:28) Yesu alikuwa akiongea juu ya ukombozi kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, ambamo “viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.”—Warumi 8:21.
Kitakuwa kitulizo kama nini kwa ainakibinadamu kuwekwa huru na mizigo ya wakati uliopita na kuamka kila siku wakiwa na akili nyangavu kama fuwele, wakiwa na hamu sana ya kushughulikia utendaji wa siku hiyo! Hakuna yeyote tena atakayezuiwa na wingu la mshuko wa moyo. Ahadi ya hakika kwa ainabinadamu ni kwamba Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.
Isipokuwa iwe imeonyeshwa vingine, manukuu yote ya Biblia yametoka kwenye Union Version ya Kiswahili.