Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 6/15 kur. 3-6
  • Unaweza Kuacha Kushuka Moyo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unaweza Kuacha Kushuka Moyo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UNALOWEZA KUFANYA
  • JITIHADA INATAKIWA
  • LAZIMA WENGINE WAWASTAHIMILI WALIOSHUKA MOYO
  • “Mseme kwa Kuzifariji Nafsi Zilizoshuka Moyo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Jinsi ya Kusaidia Walioshuka Moyo Wapate Shangwe Tena
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Faraja kwa Walioshuka Moyo
    Faraja kwa Walioshuka Moyo
  • Kulishinda Pigano Dhidi ya Mshuko wa Moyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 6/15 kur. 3-6

Unaweza Kuacha Kushuka Moyo

WANADAMU wote wanashuka moyo. Mtu anaposhuka moyo mara kwa mara tu, hilo si jambo la kumtia wasiwasi. Bali, inakuwa ishara ya kumwonyesha achukue hatua ya kufanya jambo linalofaa aache kushuka moyo. Vipindi hivyo vifupi ambapo mtu anahuzunika sana si kushuka moyo kwa njia halisi. Mabaya kama kufiwa na mpendwa, kupoteza kazi, kupungukiwa na pesa, kupatwa na mikasa mibaya, na mambo kama hayo, yanavumiliwa na watu wengi baada ya wakati mfupi. Lakini yanashusha kweli kweli mioyo ya watu wachache.

Makala moja inayozungumza juu ya kushuka moyo katika gazeti Science World (Ulimwengu wa Sayansi) la Desemba 16, 1975, inamtaja Dakt. Nathan S. Kline, ambaye ni Mtaalamu wa Matibabu ya Akili katika Columbia University mjini New York, akisema kwamba dalili inayoonekana sana katika watu wengi kuonyesha wameshuka moyo kweli kweli siyo hali yenyewe ya kushuka moyo, bali ni anhedonia (ambalo ni neno lililotokana na Kigiriki), naye analieleza neno hilo kuwa na maana ya “kutokuwa na furaha wala raha. Kutoweza kufurahia mambo yanayofanya maisha yapendeze.”

Makala hiyo inaendelea kusema kwamba dalili nyingine ya kushuka moyo ni kupoteza hamu ya kula, kisha mtu anapunguka uzito wa mwili wake. Anashindwa kulala, na hata akilala vizuri usiku, bado anajisikia amechoka. Anashindwa kukaza fikira juu ya kazi anayofanya. Kwa upande mwingine, wengine walioshuka moyo wanalala kupita kiasi, wakitumia wakati mwingi wakiwa kitandani. Kulala kunakuwa njia yao ya kuepuka magumu ya maisha.

Ili ujikaze uache kushuka moyo, kwanza jaribu kuangalia sababu zinazokushusha moyo, kisha uchunguze maoni na makusudi yako ya ndani. Angalia uone kama kweli umepatwa na mambo mabaya sana au unajisikitikia tu. Vilevile, kwa kuwa mtu anaweza kushushwa moyo na mambo ya kimwili, angalia uone kama mwili unashindwa kutumia vizuri chakula unachokula, kama damu yako haina sukari ya kutosha, kama una upungufu wa damu, kama chembe fulani za damu yako zinaongezeka kwa njia isiyofaa, kama una ugonjwa wa sukari, au ugonjwa mwingine unaoweza kukulegeza na kukuvunja moyo. Angalia uone kama umeshuka moyo kwa sababu ya nia yako mwenyewe, kisha uone ni mambo gani yanayokulemea hata ushuke moyo hivyo. Huenda ukakuta kwamba wewe unafurahia kushuka moyo kwa sababu ya kutaka kujisikitikia.

UNALOWEZA KUFANYA

Unaweza kufanya nini, hasa ikiwa hukushuka moyo kwa sababu ya ugonjwa? Ingawa mganga wa akili anaweza kukusaidia nyakati nyingine, msaada ulio bora zaidi na wenye kudumu unaweza kupatikana katika Biblia na kundi la Kikristo. Kwa sababu gani? Kwa sababu Mungu ndiye aliyeumba mwili na akili ya kibinadamu na basi analijua umbo la mwanadamu. Mtunga zaburi alisema hivi: “Ee [Yehova], umenitafuta na kunijua. Unajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu, unafahamu wazo langu toka mbali. Unatafuta njia yangu na kulala kwangu, na unajua njia zangu zote.” (Zab. 139:1-3, ZSB) Basi, dawa ya akili iliyo bora zaidi ni mashauri ya Mungu.

Basi, jambo kubwa zaidi ambalo mwenye kushuka moyo anahitaji kufanya ni kumpelekea Yehova Mungu sala. Daudi mtumishi wa Mungu alishuka sana moyo mara nyingi, nyakati nyingine kwa sababu ya makosa yake mwenyewe, na tena kwa sababu adui zake walikuwa karibu kumkamata wamwue. Alisali kwa bidii nyingi katika hali hizo. Wakati mmoja alionyesha alivyokata tamaa katika ombi alilomtolea Mungu:

“Unirehemu, Ee [Yehova]; maana nimekauka; uniponyeshe, Ee [Yehova], maana mifupa yangu imefazaika. Nafsi yangu imefazaika sana vilevile; nawe, Ee [Yehova], hata wakati gani? Rudi, Ee [Yehova], uokoe nafsi yangu, uniokoe kwa ajili ya wema wako. Maana katika mauti hapana ukumbusho juu yako, katika Hadeze nani atakayekupa sante? Nimechoka kwa kuugua kwangu; kila usiku ninanyeshea kitanda changu maji; ninatia malalo yangu maji kwa machozi yangu.”​—Zab. 6;2-6, ZSB.

Tunajua kutokana na maandishi ya Biblia kwamba Mungu alimjibu Daudi sala zake na kumtia nguvu asonge mbele na kutimiza mambo ya maana. Hata tukiona kwamba hakuna mwanadamu anayefahamu tunavyojisikia, tunajua kwamba Mungu anafahamu. Anasema hivi juu yake mwenyewe: “Akili zake hazitafutikani. Anawapa nguvu wenye kuzima roho, naye anamwongezea uwezo yeye asiye na nguvu. . . . Wao wanaongojea [Yehova] watapata nguvu mpya; watapanda juu na mabawa kama tai; watapiga mbio na hawatachoka; watatembea, wala hawatazimia roho.”​—Isa. 40:28-31, ZSB.

Mtume Paulo anashauri hivi: “Mudumu sana katika maombi, mukiangalia ndani yao pamoja na kushukuru.” (Kol. 4:2, ZSB) Lakini huenda ukajisikia ukilemewa na mambo yote. Ikiwa ndivyo, mkumbuke Yona akizama baharini, huku mimea ya baharini ikijikunja katika kichwa chake. ‘Nafsi yake ilikuwa ikizimia.’ Lakini alisali. Baadaye, alikasirika sana na kukata tamaa kwa sababu ya kuwa na nia mbaya. Aliona afadhali kufa kuliko kuishi. Hata hivyo, alisali. Nyakati zote hizo mbili alikombolewa.​—Yona 2:5-7; 4:1-8.

Lakini huenda ukashuka sana moyo hata ujisikie huwezi kumpelekea Mungu sala. Huenda ukajisikia kwamba hustahili kumfikia Mungu. Ili tupate faraja katika hali hiyo, mtume Yohana aliandika hivi:

“Kwa hivi tutafahamu ya kwamba tuko wa kweli, nasi tutatuliza mioyo yetu mbele yake, ikiwa mioyo yetu inatuhukumu; kwa maana Mungu ni mukubwa kuliko mioyo yetu, naye anajua yote. Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu, tuna imani mbele ya Mungu; na lo lote tunaloomba, tunalipokea kwake, kwa kuwa tunashika amri zake, na kutenda maneno yanayopendeza machoni mwake. Na hii ndiyo amri yake, kwamba tuamini jina la Mwana wake Yesu Kristo, na kupendana sisi kwa sisi, kana alivyotupa amri.”​—1 Yohana 3:19-23, ZSB.

Hapo Yohana anatuambia kwamba wakati moyo wetu wenyewe unapoelekea kutuhukumu, tunapojisikia hatustahili kumpelekea Mungu sala, sivyo Mungu anavyojisikia juu yetu. Mungu anaweza kuiona na kuifahamu huzuni nyingi tuliyo nayo. Anajua kwamba hatutaki kuwa na huzuni. Tukijua hivyo, tutayaondoa mashaka au woga tulio nao kisha tumwendee Mungu na kumweleza huzuni yote tuliyo nayo. Yeye atatusikia na kutuhurumia, kisha atachukua hatua asawazishe akili zetu tena.​—1 Yohana 4:17, 18; 1 Pet. 3:12.

Lakini, ikiwa huwezi kujipa moyo wa kusali, unaweza kupata msaada kwa kuwaendea wazee wa kundi la Kikristo. Yakobo ndugu mzazi na Yesu anatuambia hivi: “Mutu wa kwenu amekuwa na ugonjwa [wa kiroho]? aite wazee wa kanisa; nao waombe juu yake, na kumupakaa mafuta kwa jina la Bwana. Na kule kuomba kwa imani kutaokoa mugonjwa yule, na Bwana atamusimamisha; na kama amefanya zambi, atasamehewa.”​—Yak. 5:14, 15, ZSB.

Zaidi ya kusali, ipate hekima na faraja nzuri itakayokupa usawa kwa kulisoma Neno la Mungu na kulifikiria sana kila siku. Ukijisikia hutaki kusoma, mwambie mtu fulani akusomee. Kuzungumza yanayosomwa kutakuchangamsha sana.​—Yos. 1:8; Zab. 63:6, 7; 77:12.

JITIHADA INATAKIWA

Katika hayo yote lazima pia uwe na nia ya kutaka kuacha kushuka moyo. Hata wengine wakikusaidia na kukutolea sala, lazima wewe ujitahidi kwa imani. Yesu alimwambia Petro maneno yafuatayo ambayo yalimpata baadaye, alipokuwa akitabiri namna ambavyo angemkana: “Nimekuombea, imani yako isipunguke; na wakati unapogeuka, usubutishe ndugu zako.” (Luka 22:32, ZSB; linganisha Luka 22:54-62.) Ilimpasa Petro ahurumie ndugu zake Wakristo pia, ambao walihitaji kutiwa moyo na kusaidiwa baada ya Yesu kufa, tena alipaswa awe na tamaa ya kuwasaidia. Kupendezwa na wengine ndio mmojawapo misaada mikubwa zaidi ya kuacha kushuka moyo. Wafikirie walio karibu nawe, ufikirie mahitaji yao na wajibu ulio nao kwao. Kwa kadiri fulani wao pia wanajisikia vibaya kwa sababu ya hali yako ya kushuka moyo. Fikiria namna watakavyofurahi ukiacha kukata tamaa.

Usidhani kwamba hali yako ni tofauti na ya watu wote, kwamba mzigo wako unakulemea mno, hata uwe ni wa namna gani. Usidhani haiwezekani kuivumilia hali hiyo kwa tumaini la kuishinda. Mtume Paulo alieleza habari za hali moja iliyoshusha sana moyo. Anasema kwamba, Katika Asia . . . tulilemewa sana kuliko nguvu zetu, hata tulikata tamaa ya kuishi. Ndiyo, sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti ndani yetu, ya kwamba, tusijitegemee wenyewe, lakini tutegemee Mungu anayefufua wafu.” (2 Kor. 1:8, 9, ZSB) Paulo aliwahakikishia Wakristo Wakorintho, ambao pia walivumilia mateso, kwamba halikuwa jambo lisilowezekana kuokoka dhiki yao: “Jaribu halikuwapata ninyi ila lililo kwa watu wote; lakini Mungu ni mwaminifu, asiyewaacha ninyi kujaribiwa kuliko munavyoweza; lakini pamoja na lile jaribu atafanya njia ya kukimbia, ili muweze kulivumilia.” (1 Kor. 10:13, ZSB) Hakuna hali tusiyoweza kuondolewa na Mungu tukionyesha imani.

Hata ukijisikia kwamba hakuna mtu anayeifahamu hali yako​—ukijisikia umeachwa na kila mtu, pata faraja kutokana na maneno ya Daudi: “Kama baba yangu mwenyewe na mama yangu mwenyewe angeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” (Zab. 27:10, NW) Bila shaka, ndugu zako katika kundi la Kikristo hawatakuacha. Ni kweli kwamba nyakati nyingine huenda ukadhani mashauri wanayokupa yanaonyesha hawafahamu namna unavyojisikia. Wanapojaribu kukuchochea ujitahidi kujisaidia, huenda ukadhani wanakuwa wagumu mno. Lakini kumbuka wanajaribu kukusaidia, tena ukiwa katika hali ya kushuka moyo utaelekea kuudhika kwa wepesi zaidi. Wewe uthamini msaada wanaokupa na kujitahidi uwezavyo ufuate mashauri wanayokutolea.

Tena, jitahidi uwezavyo ushirikiane na Wakristo wenzako. Wao wana roho ya Mungu na wanaweza kukuhimiza katika upendo na kazi nzuri. Palipo na roho ya Yehova pana uhuru​—uhuru wa kutokuwa katika utumwa wa kushuka moyo. (Ebr. 10:24; 2 Kor. 3:17) Epuka kujitenga na watu wengine. (Mit. 18:1) Wakaribishe rafiki zako wakutembelee. Uhudhurie mikutano ya Kikristo.​—Ebr. 10:25.

Kwa kuwa mtu anapokuwa ameshuka moyo hana furaha, lazima ajaribu kufurahia mambo mema aliyo nayo pamoja na mambo aliyoona. Kaza fikira zako juu ya mambo yanayokufanya ushukuru na kufurahi; yaondoe mawazo ya kufikiria ubaya tu wa mambo. (Flp. 4:8) Kufanya hivyo kutakusaidia uepuke magonjwa yanayoweza kuletwa na hali ya kushuka moyo, au, ikiwa umeshuka moyo kwa sababu ya ugonjwa, kufikiria mambo mazuri kunaweza kukupunguzia taabu yako. Huenda ukapata msaada kwa kukaa siku au juma chache katika mazingira tofauti​—mahali fulani pa kupendeza pasipokukumbusha nyakati zote juu ya taabu yako. Madaktari (waganga) wanakubali kwamba “moyo wa furaha ni dawa nzuri: lakini roho inayovunjika inakausha mifupa.” Vilevile ni kweli kwamba “moyo wa furaha unaleta uso wa furaha: lakini kwa huzuni ya moyo roho inavunjika.”​—Mit. 17:22; 15:13, ZSB.

LAZIMA WENGINE WAWASTAHIMILI WALIOSHUKA MOYO

Kwa upande wa watu wa ukoo na rafiki, lazima wakumbuke kwamba ni vigumu mtu aliyeshuka moyo kujisaidia mwenyewe. Ni jambo la maana pia kuvumilia, kutodhani kwamba mtu aliyeshuka moyo anajaribu kusumbua-sumbua wengine. Nyakati zote sema naye kwa fadhili na upendo. Lakini, ziko nyakati ambazo huenda ukahitaji kusema naye kwa imara ili kumsadikisha kwamba anahitaji kujitahidi.

Wale waliomo katika kundi la Kikristo wanapaswa kufanya yote wawezayo kumfariji na kumsaidia mtu aliyekata tamaa. Tumieni hekima mwone ni wakati gani mnapopaswa kumtembelea na namna ya kufanya hivyo, lakini msivunjike moyo asipoitikia jitihada zenu upesi. Msimwachilie mtu huyo mkidhani hawezi kusaidiwa. Katika kundi la kwanza la Kikristo kulikuwa na watu walioshuka moyo, wakamfanya mtume Paulo aandike hivi: “Tunawatia moyo, ndugu, mwaonye kwa upole wasio na utaratibu, mseme kwa kuzifariji nafsi zilizoshuka moyo, mwasaidie waliolegea, mwe wastahimilivu kwa watu wote,” tena, “Nyosheni mikono iliyolegea, na magoti yenye kupooza.”​—1 The. 5:14, NW; Ebr. 12:12, ZSB.

Kila mtu, katika moyo wake, anataka kuwa mwenye furaha. Tukijua hivyo, tutamhurumia asiye na furaha, huku tukijua kwamba jambo linalomzuia kuwa na furaha ni kizuizi anachokiona kuwa kikubwa sana. Tukiwa na tamaa nyingi ya kumsaidia, tutajaribu kukijua kizuizi hicho ikiwezekana, kisha tujitahidi tuwezavyo kumrudishia furaha yake. Kwa upande mwingine, mtu mwenye huzuni, aliyeshuka moyo, lazima ajitahidi kuwa na hali yenye furaha katika akili yake, huku akikubali msaada wa upole anaopewa na kujitahidi arudie hali yake ya kawaida, kwanza kwa kusali kisha kwa kuchukua hatua zinazoonekana kuwa za lazima.

Blurb katika ukurasa wa 5

“Usidhani kwamba hali yako ni tofauti na ya watu wote, kwamba mzigo wako unakulemea mno, hata uwe ni wa namna gani.”

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Hakuna hali tusiyoweza kuondolewa na Mungu tukionyesha imani.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki