Sura ya 3
Mashahidi wa Kikristo wa Yehova Katika Karne ya Kwanza
“MTAKUWA mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Mdo. 1:8, NW) Kwa maneno hayo ya kuaga, Yesu aliwapa wanafunzi wake utume wa kuwa mashahidi. Lakini mashahidi wa nani? “Mashahidi wangu,” akasema Yesu. Je, maneno hayo yamaanisha kwamba hawakupaswa kuwa mashahidi wa Yehova? Hata!
Kwa kweli, wanafunzi wa Yesu walipewa pendeleo lisilo na kifani—lile la kuwa mashahidi wa wote wawili, Yehova na Yesu. Wakiwa Wayahudi waaminifu, wanafunzi wa mapema wa Yesu walikuwa tayari ni mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Lakini sasa walipaswa kutoa ushahidi pia kwa habari ya fungu muhimu la Yesu katika kutakaswa kwa jina la Yehova kupitia Ufalme Wake wa Kimesiya. Kutoa ushahidi hivyo juu ya Yesu, kulimtukuza Yehova. (Rum. 16:25-27; Flp. 2:9-11) Walishuhudia kwamba Yehova hakuwa amesema uwongo, kwamba baada ya miaka zaidi ya 4,000 alikuwa hatimaye amemwinua Mesiya, au Kristo, aliyekuwa ameahidiwa kwa muda mrefu!
Mashahidi wa Kikristo wa Yehova katika karne ya kwanza walipewa pia daraka lisilo na kifani—daraka ambalo ni la Wakristo wa kweli mpaka leo hii.
“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”
Baada ya ufufuo wa Yesu kutoka kwa wafu, aliwatokea wanafunzi wake waliokuwa wamekusanyika kwenye mlima mmoja katika Galilaya. Huko, Yesu alieleza daraka lao: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi. Na, tazameni! mimi nipo pamoja nanyi siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20, NW) Fikiria yaliyohusika katika utume huu mzito.
“Nendeni,” akasema Yesu. Lakini kuenda kwa nani? Kwa “watu wa mataifa yote.” Hii ilikuwa amri mpya, hasa yenye ugumu kwa waamini Wayahudi. (Linganisha Matendo 10:9-16, 28.) Kabla ya siku za Yesu, Wasio-Wayahudi walipokewa wakati wao walipokuja Israeli kwa sababu ya kupendezwa na ibada ya kweli. (1 Fal. 8:41-43) Mapema kidogo katika huduma yake, Yesu alikuwa amewaambia mitume ‘waenende, wahubiri,’ lakini kwa “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli” tu. (Mt. 10:1, 6, 7, NW) Sasa, waliamriwa waendee watu wa mataifa yote. Kwa kusudi gani?
“Mkafanye wanafunzi,” Yesu akaamuru. Ndiyo, wanafunzi wake walipewa utume wa kufanya wengine kuwa wanafunzi. Hiyo yahusisha nini? Mwanafunzi ni mtu anayefunzwa, mfunzwa—hata hivyo, si mfundishwa tu bali mshikamani. Mwanafunzi hukubali mamlaka ya Yesu si kwa kumwamini tu kwa ndani bali pia kwa nje kwa kumtii yeye. Kulingana na Theological Dictionary of the New Testament, neno la Kigiriki lililofasiriwa “mwanafunzi” (ma·the·tesʹ) “hudokeza kuwapo kwa ufungamano wa kibinafsi ambao huongoza maisha yote ya yule anayesimuliwa kuwa [mwanafunzi].”
“Kuwafundisha,” akaongezea Yesu, “kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” Ili kusitawisha ufungamano wa kibinafsi kwa Yesu, ni lazima mtu afundishwe “kushika mambo yote” ambayo Kristo ameamuru, kutia na amri yake ya kuihubiri “habari njema hii ya ufalme.” (Mt. 24:14, NW) Ni kwa jinsi hiyo tu yeye aweza kuwa mwanafunzi katika maana ya kweli ya neno hilo. Na wale tu ambao hukubali fundisho hilo na kuwa wanafunzi wa kweli ndio hubatizwa.
“Mimi nipo pamoja nanyi,” Yesu akawahakikishia, “siku zote mpaka ule umalizio wa mfumo wa mambo.” Fundisho la Yesu hufaa sikuzote, haliwi kuukuu kamwe. Kwa msingi huo, Wakristo hadi leo hii wanawajibika kuwafanya wengine kuwa wanafunzi.
Hivyo utume mzito ulipewa wafuasi wa Kristo, yaani, kutenda kazi ya kufanya wanafunzi miongoni mwa mataifa yote. Ingawa hivyo, ili wafanye wanafunzi wa Kristo ilikuwa lazima watoe ushahidi kwa habari ya jina na Ufalme wa Yehova, kwa maana hivyo ndivyo Kielelezo chao, Yesu, alivyokuwa ametenda. (Luka 4:43; Yn. 17:26) Hivyo, wale waliokubali fundisho la Kristo na kuwa wanafunzi walikuja kuwa mashahidi wa Kikristo wa Yehova. Kuwa shahidi wa Yehova hakukuwa tena jambo la kuzaliwa—ndani ya taifa la Kiyahudi—bali la kujichagulia. Wale waliokuja kuwa mashahidi walifanya hivyo kwa sababu walimpenda Yehova na walitaka kwa moyo mweupe kujitiisha kwa utawala wake wa enzi kuu.—1 Yoh. 5:3.
Lakini je, mashahidi wa Kikristo wa Yehova katika karne ya kwanza walitimiza utume wao wa kutumikia wakiwa mashahidi wa Mungu na Kristo na ‘kuwafanya watu wa mataifa yote kuwa wanafunzi’?
“Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia”
Muda mfupi baada ya kuwapa wanafunzi wake utume wao, Yesu alirudi kwenye makao ya kimbingu ya Baba yake. (Mdo. 1:9-11) Siku kumi baadaye, siku ya Pentekoste 33 W.K., ile kazi kubwa ya kufanya wanafunzi ikaanza. Yesu alimimina roho takatifu iliyoahidiwa juu ya wanafunzi wake wenye kungojea. (Mdo. 2:1-4; linganisha Luka 24:49 na Matendo 1:4, 5.) Hiyo iliwajaza bidii ya kuhubiri juu ya Kristo mfufuliwa na kurudi kwake kwa wakati ujao akiwa na mamlaka ya Ufalme.
Kulingana kabisa na maagizo ya Yesu, wanafunzi hao wa karne ya kwanza walianza kushuhudia kwao juu ya Mungu na Kristo mlemle katika Yerusalemu. (Mdo. 1:8) Akiongoza, kwenye Sikukuu ya Pentekoste, mtume Petro ‘aliwatolea ushahidi kamili’ maelfu ya waadhimishi Wayahudi kutoka mataifa mengi. (Mdo. 2:5-11, 40) Upesi idadi ya waamini wanaume peke yao ilikuwa karibu 5,000. (Mdo. 4:4; 6:7) Baadaye, Filipo alijulisha Wasamaria “habari njema ya ufalme wa Mungu na juu ya jina la Yesu Kristo.”—Mdo. 8:12, NW.
Lakini kulikuwa kazi nyingi zaidi ya kufanya. Kuanzia 36 W.K., na kuongoka kwa Kornelio, Asiye-Myahudi mtahiriwa, habari njema zilianza kuenea kwa watu wa mataifa yote wasio-Wayahudi. (Matendo, sura ya 10) Kwa kweli, zilienea haraka sana hivi kwamba kufikia kama 60 W.K., mtume Paulo angeweza kusema kwamba habari njema hizo zilikuwa ‘imehubiriwa katika viumbe vyote chini ya mbingu.’ (Kol. 1:23, NW) Hivyo, kufikia mwisho wa karne ya kwanza, wafuasi waaminifu wa Yesu walikuwa wamefanya wanafunzi kotekote katika Milki ya Roma—katika Asia, Ulaya, na Afrika!
Kwa kuwa mashahidi wa Kikristo wa Yehova katika karne ya kwanza walitimiza mengi sana kwa muda mfupi kadiri hiyo, maswali yatokea: Je, walikuwa wamepangwa kitengenezo? Ikiwa ndivyo, jinsi gani?
Tengenezo la Kutaniko la Kikristo
Kuanzia wakati wa Musa na kuendelea, taifa la Kiyahudi lilikuwa katika msimamo wa pekee sana—lilitumikia likiwa kutaniko la Mungu. Kutaniko hilo lilikuwa limepangwa kitengenezo na Mungu kwa hali ya juu likiwa chini ya wanaume wazee, wakuu, waamuzi, na maofisa. (Yos. 23:1, 2) Lakini taifa la Kiyahudi lilipoteza msimamo walo wenye kupendelewa kwa sababu lilimkataa Mwana wa Yehova. (Mt. 21:42, 43; 23:37, 38; Mdo. 4:24-28) Siku ya Pentekoste 33 W.K., kutaniko la Kikristo la Mungu lilichukua mahali pa kutaniko la Israeli.a Kutaniko hilo la Kikristo lilipangwaje kitengenezo?
Tayari katika siku ya Pentekoste, wanafunzi walikuwa ‘wakijitoa wenyewe kwa ufundishaji wa mitume,’ kuonyesha kwamba walianza wakiwa na muungamano ambao msingi wao ni fundisho. Kuanzia siku ya kwanza hiyo, walikutana pamoja “kwa umoja.” (Mdo. 2:42, 46, NW) Kazi ya kufanya wanafunzi ilipoenea, makutaniko ya waamini yalianza kufanyika, kwanza katika Yerusalemu halafu nje ya Yerusalemu. (Mdo. 8:1; 9:31; 11:19-21; 14:21-23, NW) Ilikuwa desturi yao kukusanyika pamoja hadharani na vilevile katika makao ya faragha.—Mdo. 19:8, 9; Rum. 16:3, 5; Kol. 4:15, NW.
Ni nini kilichozuia kutaniko la Kikristo lenye kupanuka lisiwe ushirika usiofungamana wa makutaniko ya mahali yenye kujitegemea? Yaliungamanishwa chini ya Kiongozi mmoja. Tangu mwanzo, Yesu Kristo alikuwa ndiye Bwana na Kichwa cha kutaniko aliyewekwa rasmi, naye alitambuliwa kuwa hivyo na makutaniko yote. (Mdo. 2:34-36; Efe. 1:22) Kutoka mbinguni, Kristo alielekeza mambo ya kutaniko lake duniani kwa bidii. Jinsi gani? Kwa njia ya roho takatifu na malaika, aliyopewa na Yehova atumie kwa hiari yake.—Mdo. 2:33; linganisha Matendo 5:19, 20; 8:26; 1 Pet. 3:22, NW.
Kristo alikuwa na kitu kingine cha kutumia kwa hiari yake ili kudumisha muungamano wa kutaniko la Kikristo—baraza lenye kuongoza lionekanalo. Mwanzoni, mitume waaminifu wa Yesu ndio waliojumlika kuwa baraza lenye kuongoza. Baadaye, likatia ndani wanaume wazee wengine wa kutaniko la Yerusalemu na vilevile mtume Paulo, hata ingawa yeye hakukaa Yerusalemu. Kila kutaniko lilitambua mamlaka ya baraza kuu hilo la wanaume wazee na kulitegemea kwa mwelekezo wakati masuala ya kitengenezo au ya kimafundisho yalipotokea. (Mdo. 2:42; 6:1-6; 8:14-17; 11:22; 15:1-31) Tokeo likawa nini? “Makutaniko yakaendelea kufanywa imara katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.”—Mdo. 16:4, 5, NW.
Baraza lenye kuongoza, chini ya mwelekezo wa roho takatifu, lilisimamia kuwekwa rasmi kwa waangalizi na wasaidizi, watumishi wa huduma, ili kutunza kila kutaniko. Hao walikuwa wanaume waliotimiza sifa za kiroho zilizotumika katika makutaniko yote, si viwango vilivyowekwa kulingana na mahali tu. (1 Tim. 3:1-13; Tito 1:5-9; 1 Pet. 5:1-3) Waangalizi walihimizwa wafuate Maandiko na kutii uongozi wa roho takatifu. (Mdo. 20:28; Tito 1:9) Wote katika kutaniko walitiwa moyo ‘wawatii wenye kuwaongoza.’ (Ebr. 13:17) Kwa njia hiyo muungamano ulidumishwa si ndani ya kila kutaniko tu bali pia ndani ya kutaniko zima la Kikristo.
Miongoni mwa mashahidi wa Kikristo wa Yehova wa karne ya kwanza, hata ingawa wanaume fulani walishika vyeo vya madaraka, hakukuwa na tofauti inayokuwa kati ya makasisi na watu wa kawaida.Wote walikuwa ndugu; kulikuwa na Kiongozi mmoja tu, Kristo.—Mt. 23:8, 10.
Watambulishwa na Mwenendo Mtakatifu na Upendo
Ushuhuda wa mashahidi wa karne ya kwanza wa Yehova haukuwa wa “tunda la midomo” tu. (Ebr. 13:15) Uanafunzi uliongoza maisha yote ya shahidi wa Kikristo. Kwa hiyo, si kwamba tu Wakristo hao walipiga mbiu ya imani zao, bali imani zao ziligeuza maisha zao pia. Waliondolea mbali utu wa zamani pamoja na mazoea yao yenye dhambi na kujitahidi kujivika utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu. (Kol. 3:5-10) Walikuwa wasema-kweli na wafuataji-haki, na vilevile wenye bidii na wenye kutegemeka. (Efe. 4:25, 28) Walikuwa safi kiadili—ukosefu wa adili katika ngono ulikatazwa katakata. Ndivyo na ulevi na ibada ya sanamu. (Gal. 5:19-21) Basi, ni kwa sababu nzuri kwamba Ukristo ulikuja kujulikana kuwa “Ile Njia,” njia au namna ya maisha yaliyotegemea hasa imani katika Yesu, kufuata kwa ukaribu hatua zake.—Mdo. 9:1, 2; 1 Pet. 2:21, 22, NW.
Hata hivyo, sifa moja yatokeza wazi juu ya nyingine zote—upendo. Wakristo wa mapema walionyesha hangaiko lenye upendo la mahitaji ya waamini wenzao. (Rum. 15:26; Gal. 2:10) Walipendana si kama walivyojipenda wenyewe bali zaidi ya walivyojipenda wenyewe. (Linganisha Wafilipi 2:25-30.) Hata walikuwa tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake. Lakini hilo halikushangaza. Kwani Yesu hakuwa tayari kuwafia wao? (Yn. 15:13; linganisha Luka 6:40.) Yeye angeweza kuwaambia wanafunzi wake hivi: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane. Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yn. 13:34, 35, NW) Kristo aliamuru kwamba wafuasi wake waonyeshe upendo huo wa kujidhabihu; na wanafunzi wake wa karne ya kwanza waliifuata sana amri hiyo.—Mt. 28:20.
“Si Sehemu ya Ulimwengu”
Ili kutimiza daraka lao la kufanya wanafunzi na kuwa mashahidi wa Mungu na Kristo, Wakristo wa karne ya kwanza hawangeweza kujiruhusu wakengeushwe fikira na mambo ya kilimwengu; ilikuwa lazima waendelee kukazia fikira utume wao. Hakika Yesu alikuwa amefanya hivyo. Yeye alimwambia Pilato hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yn. 18:36, NW) Tena aliwaambia wanafunzi wake waziwazi hivi: “Nyinyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yn. 15:19, NW) Basi, kama Yesu, Wakristo wa mapema waliendelea kujitenga na ulimwengu; hawakuhusika katika siasa wala vita. (Linganisha Yohana 6:15.) Wala hawakunaswa katika njia za ulimwengu—kufuatia kwao vitu vya kimwili kwa hamu nyingi na kujihusisha kwao kupita kiasi katika anasa.—Luka 12:29-31; Rum. 12:2; 1 Pet. 4:3, 4.
Kwa sababu waliendelea kujitenga na ulimwengu, mashahidi wa Kikristo wa karne ya kwanza walikuwa jamii tofauti ya watu. Aandika hivi mwanahistoria E. G. Hardy katika kitabu chake Christianity and the Roman Government: “Wakristo walikuwa wageni na wasafiri katika ulimwengu uliowazunguka; uenyeji wao ulikuwa mbinguni; ufalme walioutumainia haukuwa wa ulimwengu huu. Hivyo kutopendezwa na mambo ya umma kulikotokana na jambo hilo kulikuwa jambo lenye kuonekana wazi katika Ukristo pale mwanzoni.”
Kunyanyaswa kwa Ajili ya Uadilifu
“Mtumwa si mkubwa zaidi kuliko bwana-mkubwa wake.” Yesu akaonya. “Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia.” (Yn. 15:20, NW) Kabla ya kifo chake juu ya mti wa mateso, Yesu alipatwa na mnyanyaso mkali. (Mt. 26:67; 27:26-31, 38-44) Na kulingana kabisa na onyo lake, upesi wanafunzi wake walitendwa vivyo hivyo. (Mt. 10:22, 23) Lakini kwa nini?
Haikuchukua muda mrefu kwa Wakristo wa mapema kukaziwa fikira na wengine. Wao walikuwa watu wenye kanuni za juu za maadili na uaminifu-maadili. Waliendesha kazi ya kufanya wanafunzi kwa ujasiri wa kusema na bidii; tokeo ni kwamba, maelfu ya watu waliacha mifumo ya dini bandia wakawa Wakristo. Walikataa kuhusika katika mambo ya kilimwengu. Walikataa kujiunga katika ibada ya maliki. Basi, haishangazi kwamba upesi walikuja kuwa shabaha ya mnyanyaso mkali wenye kuchochewa na viongozi wa dini bandia na watawala wa kisiasa waliopashwa habari vibaya. (Mdo. 12:1-5; 13:45, 50; 14:1-7; 16:19-24) Ingawa hivyo, hao walikuwa ni mawakili wa kibinadamu tu wa yule mnyanyasi halisi—“nyoka wa awali,” Shetani. (Ufu. 12:9, NW; linganisha Ufunuo 12:12, 17.) Lengo lake? Kuukandamiza Ukristo na ile kazi yao ya kutoa ushahidi kwa ujasiri.
Lakini hakuna kiasi chochote cha mnyanyaso ambacho kingeweza kuifumba midomo ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova wa karne ya kwanza! Wao walikuwa wamepokea utume wao wa kuhubiri kutoka kwa Mungu kupitia Kristo, nao walikuwa wamepiga moyo konde kumtii Mungu kuliko wanadamu. (Mdo. 4:19, 20, 29; 5:27-32) Walitegemea nguvu ya Yehova, wakiwa na uhakika kwamba yeye angethawabisha mashahidi wake waaminifu-washikamanifu kwa sababu ya uvumilivu wao.—Mt. 5:10; Rum. 8:35-39; 15:5.
Historia huthibitisha kwamba mnyanyaso uliofanywa na wenye mamlaka wa Milki ya Roma ulishindwa kufutilia mbali mashahidi wa Kikristo wa Yehova wa mapema. Asema hivi Yosefo, mwanahistoria Myahudi wa karne ya kwanza W.K.: “Na hilo kabila la Wakristo, lililoitwa hivyo kulingana na jina [la Yesu], lingali mpaka leo hii [kama 93 W.K.] halijatoweka.”—Jewish Antiquities, XVIII, 64 (iii, 3).
Hivyo, rekodi ya ushuhuda wa mashahidi wa Kikristo wa Yehova katika karne ya kwanza inafunua sifa kadhaa zenye kutambulika wazi: Wao walitimiza kwa ujasiri na kwa bidii utume wao wa kutoa ushahidi juu ya Mungu na Kristo na kutenda kazi ya kufanya wanafunzi; wao walikuwa na muundo wa kitengenezo ambamo wote walikuwa ndugu, bila tofauti ya makasisi na watu wa kawaida; wao walishikamana na kanuni za juu za maadili na walipendana; wao walijitenga na njia na mambo ya kilimwengu; na wao walinyanyaswa kwa ajili ya uadilifu.
Ingawa hivyo, kufikia mwisho wa karne ya kwanza, lile kutaniko moja la Kikristo lenye muungamano lilitishwa na hatari kubwa yenye madhara ya kisirisiri.
[Maelezo ya Chini]
a Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, “kutaniko” nyakati fulani hutumiwa katika maana ya ujumla, likirejezea kutaniko lote la Kikristo (1 Kor. 12:28, NW); huenda pia likarejezea kikundi cha mahali fulani katika jiji fulani au katika makao ya mtu fulani.—Mdo. 8:1, NW; Rum. 16:5, NW.
[Blabu katika ukurasa wa 26]
Wanafunzi wapya walipaswa wawe wafuasi watiifu, sio waamini wasiotenda
[Blabu katika ukurasa wa 27]
Kuwa shahidi wa Yehova hakukuwa tena jambo la kuzaliwa bali la kujichagulia
[Blabu katika ukurasa wa 28]
Kufikia mwisho wa karne ya kwanza, mashahidi wa Kikristo wa Yehova walikuwa wamefanya wanafunzi katika Asia, Ulaya, na Afrika!
[Blabu katika ukurasa wa 29]
Miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza, hakukuwa na tofauti inayokuwa kati ya makasisi na watu wa kawaida
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
Ukristo Ulienea kwa Sababu ya Kuhubiri kwa Bidii
Kwa kuchochewa na bidii ambayo haingeweza kuzimwa, mashahidi wa Kikristo wa Yehova wa mapema walitumia juhudi iliyo kubwa kabisa katika kupiga mbiu ya habari njema kwa mapana makubwa zaidi yaliyowezekana. Edward Gibbon, katika “The Decline and Fall of the Roman Empire,” aandika kwamba “bidii ya Wakristo hao . . . iliwasambaza kotekote katika kila mkoa na katika karibu kila jiji la milki ile [ya Roma].” Asema Profesa J. W. Thompson katika “History of the Middle Ages”: “Ukristo ulikuwa umeenea kwa haraka ajabu katika ulimwengu wa Roma. Kufikia mwaka 100 labda kila mkoa uliopakana na Mediterania ulikuwa na jumuiya ya Kikristo ndani yao.”
[Sanduku katika ukurasa wa 30]
‘Ushindi Wenye Shangwe wa Ukristo’
Vyanzo visivyo vya Kibiblia huthibitisha kwamba mwenendo mzuri na upendo ulikuwa sifa ya Wakristo wa mapema. Mwanahistoria John Lord alitaarifu hivi: “Ushindi wa kweli wenye shangwe wa Ukristo ulionekana katika kufanya wale waliodai kufuata mafundisho yao wawe watu wema. . . . Tuna ushuhuda wa kwamba wao walikuwa na maisha zisizo na lawama, walikuwa na maadili yasiyoweza kusutwa, walikuwa raia wema, na walikuwa na adabu zenye wema wa Kikristo.”—“The Old Roman World.”
[Picha katika ukurasa wa 31]
Baraza kuu lenye kuongoza lilisaidia kuandalia makutaniko mwelekezo, lakini yote yalitegemea Kristo kuwa Kiongozi wao mmoja
[Picha katika ukurasa wa 32]
Wakristo wa mapema walikuwa shabaha ya mnyanyaso mkali