Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 11 kur. 149-158
  • Jinsi Tulivyokuja Kujulikana Kuwa Mashahidi wa Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Tulivyokuja Kujulikana Kuwa Mashahidi wa Yehova
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jina Wakristo
  • Majina ya Dharau ya Kubandikwa
  • Uhitaji wa Jina Lenye Kutofautisha
  • Matukio Yaliyoelekeza Kwenye Jina Hilo
  • Jina Jipya
  • Kukubali Daraka
  • Ni Zaidi ya Kibandiko
  • Yehova Analikweza Jina Lake
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • A5 Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo
    Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
  • Kwa Nini Ni Lazima Tujue Jina la Mungu
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Liheshimu Jina Kuu La Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 11 kur. 149-158

Sura ya 11

Jinsi Tulivyokuja Kujulikana Kuwa Mashahidi wa Yehova

KATIKA pindi ya miongo ya mapema ya historia yao ya kisasa, mara nyingi walirejezewa tu kuwa Wanafunzi wa Biblia. Wengine walipouliza juu ya jina la tengenezo, mara nyingi ndugu zetu walikuwa wakijibu, “Sisi ni Wakristo.” Ndugu Russell alijibu swali kama hilo kwa kusema, katika Watch Tower hivi: “Sisi hatujitengi wenyewe na Wakristo wengine kwa kuchukua jina lolote lenye kutofautisha au la pekee. Sisi tunatosheka na jina, Wakristo, ambalo kwalo watakatifu wa mapema walijulikana.”—Toleo la Septemba 1888.

Basi, ilitukiaje kwamba leo tunajulikana kuwa Mashahidi wa Yehova?

Jina Wakristo

Wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo, katika karne ya kwanza na katika nyakati za kisasa pia, wamejirejezea wenyewe na waamini wenzao kuwa “ndugu,” “marafiki,” na “kutaniko la Mungu.” (Mdo. 11:29; 3 Yoh. 14; 1 Kor. 1:2, NW) Pia wamesema juu ya Kristo kuwa ni “Bwana-mkubwa” na wakasema juu yao kuwa “watumwa wa Kristo Yesu” na “watumwa wa Mungu.” (Kol. 3:24; Flp. 1:1; 1 Pet. 2:16, NW) Mitajo hiyo imetumiwa sana ndani ya kutaniko, na imeeleweka vizuri humo.

Katika karne ya kwanza, namna ya maisha iliyotegemea imani katika Yesu Kristo (na kwa kupanuliwa, kutaniko lenyewe) ilirejezewa kuwa “Ile Njia.” (Mdo. 9:2; 19:9, NW) Tafsiri kadhaa za Matendo 18:25 (NW) huonyesha kwamba iliitwa pia “njia ya Yehova.”a Kwa upande mwingine, baadhi ya wale waliokuwa nje ya kutaniko waliiita kwa dharau “farakano la Wanazareti.”—Mdo. 24:5, NW.

Kufikia 44 W.K. au muda mfupi baada ya hapo, wafuasi waaminifu wa Yesu Kristo walianza kujulikana kuwa Wakristo. Wengine hudai kwamba ni watu wa nje waliowabandika jina Wakristo, wakifanya hivyo kwa njia ya kuwavunjia heshima. Hata hivyo, idadi fulani ya watungaji wa kamusi za Biblia na waelezaji hutaarifu kwamba kitenzi kilichotumiwa kwenye Matendo 11:26 hudokeza kwamba ulikuwa mwelekezo au ufunuo wa kimungu. Hivyo, katika New World Translation, andiko hilo husomwa hivi: “Ilikuwa kwanza katika Antiokia kwamba wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo.” (Mifasirio inayofanana na huo inapatikana katika Literal Translation of the Holy Bible, ya Robert Young, Chapa Iliyosahihishwa, ya 1898; The Simple English Bible, ya 1981; na New Testament, ya Hugo McCord, ya 1988.) Kufikia 58 W.K., jina Wakristo likawa lenye kujulikana sana hata na wakuu wa Kiroma.—Mdo. 26:28.

Mitume wa Kristo walipokuwa wangali hai, jina Wakristo lilikuwa lenye kutofautisha na mahususi. (1 Pet. 4:16) Wote waliodai kuwa Wakristo lakini ambao imani zao au mwenendo vilipinga dai lao walifukuzwa kutoka jumuiya ya Kikristo. Hata hivyo, kama vile Yesu alivyokuwa ametabiri, baada ya kifo cha mitume Shetani alipanda mbegu ambazo zilitokeza Wakristo wa mwigo. Watu hao bandia walidai pia kutumia jina Wakristo. (Mt. 13:24, 25, 37-39) Ukristo wenye kuasi imani ulipotumia njia ya kugeuza watu kwa nguvu, wengine walidai kuwa Wakristo ili tu waepuke mnyanyaso. Baada ya wakati, Mzungu yeyote asiyedai kuwa Myahudi, Mwislamu, au Mwatheisti mara nyingi alionwa kuwa Mkristo, bila kujali imani au mwenendo wake.

Majina ya Dharau ya Kubandikwa

Kuanzia karne ya 16 na kuendelea, hali hiyo ilizusha tatizo kwa Warekebishaji wa dini. Kwa kuwa jina Wakristo lilikuwa linatumiwa vibaya sana, wangewezaje kujitofautisha na wengine waliodai kuwa Wakristo?

Mara nyingi walikubali tu kimyakimya kutumia jina la kubandikwa la dharau walilopewa na maadui wao. Hivyo wanatheolojia wenye kumpinga Martin Luther, katika Ujerumani, ndio waliokuwa wa kwanza kutumia jina lake kwa wafuasi wake, wakiwaita Waluther. Wale walioshirikiana na John Wesley, katika Uingereza, walibandikwa jina Wamethodisti kwa sababu walishika kihususa na kufuata wajibu mbalimbali wa kidini kwa utaratibu kuliko ilivyo kawaida. Kwanza Wabaptisti walipinga jina la kubandikwa Anabaptisti (kumaanisha, “Mbatiza-Upya”) lakini hatua kwa hatua wakakubali jina Baptisti ikiwa namna ya kuridhiana.

Namna gani Wanafunzi wa Biblia? Makasisi waliwabandika jina Warusselli na Warutherford. Lakini kukubali jina kama hilo kungechochea roho ya kimafarakano. Haingepatana na karipio walilopewa Wakristo wa mapema na mtume Paulo, ambaye aliandika hivi: “Mmoja asemapo: ‘Mimi ni wa Paulo,’ lakini mwingine asema: ‘Mimi ni wa Apolo,’ je, nyinyi si wanadamu tu [yaani, wenye maoni ya kimwili badala ya yale ya kiroho]?” (1 Kor. 3:4, NW) Baadhi ya watu waliwabandika jina “Wanamapambazuko wa Mileani”; lakini Utawala wa Mileani wa Kristo lilikuwa mojapo tu mafundisho yao. Wengine waliwaita “Watu wa Watch Tower”; lakini hiyo pia haikufaa, kwa kuwa Watch Tower lilikuwa tu mojapo vichapo walivyotumia kuenezea kweli ya Biblia.

Uhitaji wa Jina Lenye Kutofautisha

Baada ya wakati, ikazidi kuwa wazi sana kwamba kuongezea mtajo Wakristo, kutaniko la watumishi wa Yehova kwa kweli lilihitaji jina lenye kutofautisha. Maana ya jina Wakristo ilikuwa imepotoshwa katika akili za umma kwa sababu watu waliodai kuwa Wakristo mara nyingi walikuwa na wazo kidogo tu au hawakuwa na wazo lolote juu ya Yesu Kristo alikuwa nani, yale aliyofundisha, na yale ambayo wao wapaswa kuwa wakifanya ikiwa kwa kweli walikuwa wafuasi wake. Kwa kuongezea, kadiri ndugu zetu walivyofanya maendeleo katika uelewevu wao wa Neno la Mungu, waliona waziwazi uhitaji wa kujitenga na kuwa tofauti na mifumo ya kidini iliyodai kwa udanganyifu kuwa ya Kikristo.

Ni kweli, ndugu zetu mara nyingi walijirejezea kuwa Wanafunzi wa Biblia, na kuanzia katika 1910, walitumia jina International Bible Students Association, kwa habari ya mahali pa mikutano yao. Katika 1914, ili kuepuka mvurugo juu ya shirika lao la kisheria lililokuwa limefanyizwa karibuni lililoitwa International Bible Students Association, walikubali jina Wanafunzi wa Biblia Wenye Kushirikiana kwa ajili ya vikundi vyao vya mahali pao. Lakini ibada yao ilitia ndani mengi zaidi ya kujifunza Biblia. Zaidi ya hilo, walikuwako wengine waliojifunza Biblia—wengine kwa sababu za kidini; wengine, wakiwa wachambuzi; na wengi, wakiwa watu walioiona tu kuwa fasihi bora. Halafu, baada ya kifo cha Ndugu Russell, baadhi ya wale walioshirikiana hapo kwanza walikataa kushirikiana na Watch Tower Society na International Bible Students Association, hata wakapinga kazi ya mashirika hayo. Vikundi hivyo vilivyojitenga vilitumia majina mbalimbali, baadhi yavyo vikishikamana na mtajo Wanafunzi wa Biblia Wenye Kushirikiana. Jambo hilo lilisababisha mvurugo zaidi.

Halafu, katika 1931, sisi tulikubali kwa moyo jina lenye kutofautisha kikweli Mashahidi wa Yehova. Mtunga-vitabu Chandler W. Sterling huita hilo kuwa “tendo la werevu zaidi ya yote” la J. F. Rutherford, wakati huo akiwa msimamizi wa Watch Tower Society. Kama vile mwandikaji huyo alivyoyaona mambo, hiyo ilikuwa hatua ya werevu si kwa kuandalia tu kikundi jina rasmi, bali pia ilifanya liwe jambo rahisi kufasiri marejezo yote ya Biblia ya maneno “shahidi” na “ushahidi” kuwa yatumika hususa kwa Mashahidi wa Yehova. Kwa kutofautisha, A. H. Macmillan, mshirika wa usimamizi wa wasimamizi watatu wa Watch Tower Society, alisema hivi kuhusu tangazo hilo lililofanywa na Ndugu Rutherford: “Hamna shaka akilini mwangu—wala wakati huo wala sasa—kwamba Bwana alimwongoza katika hilo, na kwamba hilo ndilo jina ambalo Yehova ataka sisi tuitwe, na sisi tunafurahi sana na kuterema sana kuwa nalo.” Mambo ya hakika yanaunga mkono maoni gani? Je, jina hilo lilikuwa ‘tendo la werevu’ la Ndugu Rutherford, au lilikuwa tokeo la mwelekezo wa kimungu?

Matukio Yaliyoelekeza Kwenye Jina Hilo

Ilikuwa katika karne ya nane K.W.K. kwamba Yehova alisababisha Isaya aandike: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” NW], na mtumishi wangu niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye; kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine. . . . Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” NW], nami ni Mungu.” (Isa. 43:10, 12) Kama inavyoonyeshwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, unabii mwingi ulioandikwa na ule wa Isaya una utimizo kuhusiana na kutaniko la Kikristo. (Linganisha Isaya 8:18 na Waebrania 2:10-13; Isaya 66:22 na Ufunuo 21:1, 2.) Hata hivyo, Isaya 43:10, 12 halikuzungumzwa kirefu kamwe katika The Watch Tower wakati wa miaka 40 ya kwanza ya kuchapwa kwalo.

Hata hivyo, baada ya hapo, funzo lao la Maandiko lilielekeza uangalifu wa watumishi wa Yehova kwenye matukio mapya yenye maana. Ufalme wa Mungu, Yesu akiwa Mfalme wa Kimesiya ulikuwa umezaliwa mbinguni katika 1914. Katika 1925, mwaka ambao jambo hilo lilielezwa wazi katika The Watch Tower, ile amri ya kiunabii, katika Isaya sura ya 43, ya kuwa mashahidi wa Yehova ilipewa ufikirio katika matoleo 11 tofauti ya gazeti hilo.

Katika The Watch Tower la Januari 1, 1926, makala kuu ilizungumzia swali lenye kutokeza wito: “Ni Nani Atamheshimu Yehova?” Katika pindi ya miaka mitano iliyofuata, The Watch Tower lilizungumzia kisehemu cha Isaya 43:10-12 katika matoleo 46 mbalimbali na kila wakati likalitumia kuwahusu Wakristo wa kweli.b Katika 1929 ilitajwa kwamba suala kuu linalokabili viumbe wenye akili lahusu kuheshimu jina la Yehova. Na kuhusu daraka walilo nalo watumishi wa Yehova kwa habari ya suala hilo, Isaya 43:10-12 lilitokezwa mara kwa mara lipate kufikiriwa.

Hivyo mambo ya hakika huonyesha kwamba kama tokeo la funzo la Biblia, uangalifu ulikuwa ukivutwa kwa kurudiarudia kwenye wajibu wao wa kuwa mashahidi wa Yehova. Si jina la kikundi fulani lililokuwa likifikiriwa, bali kazi ambayo wangefanya.

Lakini mashahidi hao wangejulikana kwa jina gani? Ni jambo gani lingefaa kwa kufikiria kazi waliyokuwa wakifanya? Neno la Mungu mwenyewe lilielekeza kwenye mkataa gani? Jambo hilo lilizungumzwa kwenye mkusanyiko katika Colombus, Ohio, Marekani, Julai 24-30, 1931.

Jina Jipya

Zile herufi kubwa JW zilionekana kwa njia yenye kutokeza katika jalada la mbele la programu ya mkusanyiko. Zilimaanisha nini? Ilikuwa mpaka Jumapili, Julai 26, ndipo maana yazo ilipoelezwa. Katika siku hiyo Ndugu Rutherford alitoa hotuba ya watu wote “Ufalme, Tumaini la Ulimwengu.” Katika hotuba hiyo, alipokuwa akitambulisha wale ambao hupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu, msemaji huyo alirejezea kipekee jina “Mashahidi wa Yehova” (Jehovah’s Witnesses).

Baadaye siku hiyo Ndugu Rutherford alifuatia hilo kwa hotuba nyingine, ambapo alipokuwa akiitoa alizungumzia sababu jina lenye kutofautisha lilihitajiwa.c Maandiko yenyewe yalielekeza kwenye jina gani? Msemaji alinukuu Matendo 15:14 (NW), ambalo huelekeza uangalifu kwenye kusudi la Mungu la kutwaa watu kutoka mataifa “watu kwa ajili ya jina lake.” Katika hotuba yake alikazia uhakika wa kwamba kama ilivyotaarifiwa kwenye Ufunuo 3:14 (NW), Yesu Kristo ni “shahidi mwaminifu na wa kweli.” Alirejezea Yohana 18:37 (NW), ambapo Yesu alijulisha hivi: “Kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” Alielekeza uangalifu kwenye 1 Petro 2:9, 10 (NW), ambalo husema kwamba watumishi wa Mungu ‘wangetangaza kotekote sifa bora kabisa za yeye aliyewaita nyinyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’ Alitoa sababu kwa kutumia idadi fulani ya maandiko kutoka Isaya, ambayo si yote yalieleweka wazi wakati huo, halafu akafikisha utoaji wake kwenye upeo kwa kutumia Isaya 43:8-12, ambalo hutia ndani utume huu wa kimungu: “‘Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” NW], nami ni Mungu.” Basi, Neno la Yehova mwenyewe lilikuwa likiwaelekeza kwenye mkataa gani? Ni jina gani lingekuwa lenye kupatana na njia ambayo kwa kweli Mungu alikuwa akiwatumia?

Jibu lisilo na shaka lilitiwa katika azimio lililokubaliwa kwa idili katika pindi hiyo.d Azimio hilo lilisema hivi kwa sehemu:

“Ili hali yetu ipate kujulikana, na kwa sababu ya kuamini kwamba hii inapatana na mapenzi ya Mungu, kama yanavyoelezwa katika Neno lake, NA IAZIMIWE kama ifuatavyo:

“KWAMBA, sisi tunampenda sana Ndugu Charles T. Russell kwa ajili ya kazi yake, na kwamba tunatambua kwa furaha kwamba Bwana alimtumia na kubariki sana kazi yake, lakini hatuwezi kupatana na Neno la Mungu kukubali kuitwa kwa jina ‘Warusselli’; kwamba Watch Tower Bible and Tract Society na International Bible Students Association na Peoples Pulpit Association ni majina tu ya mashirika tuliyo nayo kama kampuni ya Wakristo, nasi twayasimamia na kuyatumia kuendesha kazi yetu kwa kutii amri za Mungu, hata hivyo hakuna lolote la majina hayo linaloambatana nasi wala kutuhusu vya kufaa kutumiwa tukiwa jamii ya Wakristo wanaofuata hatua za Bwana na Bwana-Mkubwa wetu, Kristo Yesu; kwamba sisi tu wanafunzi wa Biblia, lakini tukiwa jamii ya Wakristo walio shirika, tunakataa kujitwalia au kuitwa kwa jina ‘Wanafunzi wa Biblia’ au majina mengine kama hayo ili kutambulisha hali yetu halisi mbele za Bwana; twakataa kuchukua au kuitwa kwa jina la binadamu yeyote;

“KWAMBA, kwa kuwa tulinunuliwa kwa damu yenye thamani ya Yesu Kristo Bwana na Mkombozi wetu, aliyehesabiwa kuwa mwadilifu na kuzaliwa na Yehova Mungu na kuitwa kwenye ufalme wake, bila kusitasita twatangaza ushikamano na ujitoaji wetu wote kwa Yehova Mungu na ufalme wake; kwamba sisi tu watumishi wa Yehova Mungu walioagizwa kufanya kazi kwa jina lake, na kwa kutii amri yake, tutoe ushuhuda wa Yesu Kristo, na kujulisha watu kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli na Mweza Yote; kwa hiyo kwa furaha tunalikubali na kulichukua jina ambalo kinywa cha Bwana Mungu kimelitaja, nasi twataka tujulikane na kuitwa kwa jina hili, yaani, mashahidi wa Yehova [Jehovah’s witnesses].—Isa. 43:10-12, NW.”e

Kufuatia kutolewa kwa azimio lote, makofi yenye kuendelea na ya sauti kubwa yalionyesha kwamba wasikilizaji walikubaliana kabisa na yaliyosemwa.

Kukubali Daraka

Ilikuwa heshima kama nini kuitwa jina la Mungu pekee wa kweli, Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima! Lakini daraka laambatana na jina hilo. Ni daraka ambalo vikundi vingine vya kidini havitaki. Kama vile Ndugu Rutherford alivyosema katika hotuba yake: “Wenye furaha ni hao ambao waweza kutwaa jina ambalo hakuna mtu yeyote chini ya mbingu alitakaye isipokuwa wale ambao wamejitoa kabisa na bila masharti kwa Yehova.” Hata hivyo, inafaa kama nini kwamba watumishi wa Yehova waitwe jina la kibinafsi la Mungu, kwamba walijulishe, na kwamba lishirikishwe kwa njia yenye kutokeza na kupigiwa mbiu kwa kusudi lake!

Kikundi chochote au mtu mmoja-mmoja yeyote ambaye husema kwa jina la Yehova hujiweka chini ya wajibu wa kuwasilisha neno lake kwa njia ya kweli. (Yer. 23:26-28) Lazima wajulishe si maandalizi tu ya Yehova kwa ajili ya kubariki wapendao uadilifu bali pia hukumu zake juu ya wale watendao mambo yasiyo ya uadilifu. Kama vile Yehova alivyoamuru manabii wake katika nyakati zilizopita, ndivyo na leo, mashahidi wake lazima wasiondoe chochote kutoka neno la Mungu kwa kushindwa kulijulisha. (Yer. 1:17; 26:2; Eze. 3:1-11) Lazima wapige mbiu ya “mwaka wa nia njema kwa upande wa Yehova na siku ya kisasi kwa upande wa Mungu wetu.” (Isa. 61:1, 2, NW) Wale waliokuwa wakikubali azimio hilo lililo juu walitambua daraka hilo, na katika sehemu ya pili ya azimio hilo, walijulisha hivi:

“Tukiwa mashahidi wa Yehova kusudi letu moja tu na la pekee ni kuwa watiifu kabisa kwa amri zake; kujulisha kwamba yeye pekee ndiye Mungu Mweza Yote na wa kweli; kwamba Neno lake ni la kweli na kwamba jina lake lastahili heshima na utukufu wote; kwamba Kristo ni Mfalme wa Mungu, ambaye yeye amemweka juu ya kiti cha ufalme cha mamlaka; kwamba ufalme wake sasa umekuja, na katika kutii amri za Bwana lazima sisi tujulishe sasa habari njema hizi kuwa ushuhuda au ushahidi kwa mataifa na kuarifu watawala na watu juu ya tengenezo katili na lenye uonevu la Shetani, na hasa kwa habari ya ‘Jumuiya ya Wakristo,’ ambayo ndiyo sehemu yenye uovu zaidi ya tengenezo hilo lionekanalo, na juu ya kusudi la Mungu la kuharibu hivi karibuni tengenezo la Shetani, tendo hilo kuu litafuatwa upesi na Kristo Mfalme akiletea vikundi vyote vya watu watiifu wa dunia amani na ufanisi, uhuru na afya, furaha na uhai wa milele; kwamba ufalme wa Mungu ndilo tumaini la ulimwengu, hakuna jingine, na kwamba ujumbe huu lazima utolewe na wale wanaotambulishwa kuwa mashahidi wa Yehova.

“Kwa unyenyekevu twaalika watu wote ambao wamejitoa kabisa kwa Yehova na ufalme wake wajiunge katika kupigia wengine mbiu ya habari hizi njema, ili viwango vyenye uadilifu vya Bwana viinuliwe juu, na kwamba watu wa ulimwengu wapate kujua mahali pa kupata kweli na tumaini kwa ajili ya kitulizo; na zaidi ya yote, kwamba lile jina kuu na takatifu la Yehova Mungu lipate kutetewa na kutukuzwa.”

Si katika Colombus, Ohio, katika Marekani tu, bali kufika mbali sana Australia kwamba wasikilizaji walipiga makofi ghafula waliposikia tangazo la jina hilo jipya. Katika Japani, baada ya saa nyingi za jitihada, ni kisehemu kifupi tu cha programu kilichonaswa katika redio ya masafa mafupi katika usiku wa manane. Mara hiyo kikatafsiriwa. Hivyo kile kikundi kidogo cha huko kilisikia azimio hilo na kishindo cha makofi. Matsue Ishii alikuwapo pamoja nao, na kama alivyoandika baadaye, ‘waliinua kilio cha shangwe kupatana na ndugu zao katika Marekani.’ Kufuatia kusanyiko katika Columbus, makusanyiko na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika nchi zote ambako walikuwa wakiendeleza huduma yao wajionyesha wenyewe kuwa wakubaliana kabisa na azimio hilo. Kutoka Norway, ikiwa kielelezo kimoja, ilikuja ripoti hii: “Kwenye mkusanyiko wetu wa mwaka . . . katika Oslo sisi sote tuliinuka kwa miguu yetu na kwa idili kubwa tuliinua sauti ‘Ndiyo,’ tulipokuwa tukikubali jina letu jipya ‘mashahidi wa Yehova.’”

Ni Zaidi ya Kibandiko

Je, ulimwengu kwa ujumla ungejua kwamba ndugu zetu walikuwa wamekubali jina hilo jipya? Ndiyo, kwelikweli! Hotuba ambayo tangazo la jina letu lilitolewa kwanza iliwakilishwa katika muunganisho wa redio uliopata kuwa mkubwa zaidi kufikia wakati huo. Kuongezea, azimio lililoonyesha jina hilo jipya lilitiwa ndani ya kijitabu The Kingdom, the Hope of the World. Kufuatia mkusanyiko, Mashahidi wa Yehova waligawanya mamilioni ya nakala za kijitabu hicho katika lugha nyingi katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, Afrika, Asia, na visiwa vya bahari. Zaidi ya kutoa nakala nyumba hadi nyumba, walifanya jitihada ya pekee kuitia mikononi mwa kila mkuu wa serikali, mwanabiashara mashuhuri, na kasisi. Baadhi yao waliokuwa wangali hai katika 1992 walikumbuka vema ushiriki wao katika kampeni hiyo yenye umaana.

Si wote waliokipokea vizuri kijitabu hicho. Eva Abbott akumbuka kwamba alipokuwa akiondoka nyumbani mwa kasisi mmoja katika Marekani, kijitabu hicho kilitupwa hewani na kuanguka chini mbele yake. Yeye hakutaka kukiacha hapo, hivyo akakichukua; lakini mbwa mkubwa alinguruma, akakinyakua mkononi mwake, na kukipeleka kwa bwana-mkubwa wake, yule kasisi. Dada huyo alisema: “Kile ambacho sikuweza kupeleka, mbwa huyo alikipeleka!”

Martin Poetzinger, ambaye baadaye alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikumbuka hivi: “Nyuso zenye kushangaa zilionekana kwenye kila mlango tulipojijulisha wenyewe kwa maneno haya: ‘Nimekujia leo nikiwa mmoja wa mashahidi wa Yehova.’ Watu walikuwa wakitikisa vichwa vyao au kuuliza: ‘Lakini nyinyi mngali wanafunzi wa Biblia, sivyo? Au je, mmejiunga na farakano jingine?’” Hatua kwa hatua hali hiyo ikabadilika. Miongo kadhaa baada ya kuanza kutumia jina lao lenye kutofautisha, Ndugu Poetzinger aliandika: “Ni badiliko kubwa kama nini! Kabla sijasema neno watu hutaja: ‘Lazima uwe mmoja wa mashahidi wa Yehova.’” Ndiyo, sasa wanajua jina hilo.

Jina hilo halikuwa kibandiko tu. Awe kijana au mzee, wa kiume au wa kike, wote kati ya Mashahidi wa Yehova hushiriki katika kazi ya kutoa ushahidi kwa Yehova na kusudi lake tukufu. Kama tokeo, C. S. Braden, profesa wa historia ya kidini, aliandika: “Mashahidi wa Yehova wameieneza dunia kihalisi kwa kutoa kwao ushahidi.”—These Also Believe.

Ijapokuwa kazi ya kutoa ushahidi iliyofanywa na ndugu zetu kabla ya kukubali jina Mashahidi wa Yehova ilikuwa ya duniani pote, kwa kutazama nyuma yaonekana kwamba Yehova alikuwa akiwatayarisha kwa ajili ya kazi kubwa hata zaidi—kukusanywa kwa umati mkubwa ambao ungehifadhiwa ukiwa hai kupitia Har–Magedoni, ukiwa na fursa ya kuishi milele katika dunia iliyo paradiso.

[Maelezo ya Chini]

a New World Translation of the Holy Scriptures; A Literal Translation of the New Testament . . . From the Text of the Vatican Manuscript, ya Herman Heinfetter; na tafsiri sita katika Kiebrania. Ona pia kielezi-chini cha Matendo 19:23 katika New World Translation of the Holy Scriptures.

b Miongoni mwa makala kuu za Watch Tower zilizotangazwa wakati wa kipindi hicho zilikuwa “Yehova na Kazi Zake,” “Heshimu Jina Lake,” “Watu kwa Ajili ya Jina Lake,” “Jina Lake Latukuzwa,” “Shahidi Wa-Kweli na Mwaminifu,” “Msifu Yehova!” “Pendezwa na Yehova,” “Yehova Mkuu Kupita Wote,” “Kutetewa kwa Jina Lake,” “Jina Lake,” na “Mwimbie Yehova.”

c Ona makala “Jina Jipya,” katika The Watch Tower la Oktoba 1, 1931.

d The Watch Tower, Septemba 15, 1931, kur. 278-279.

e Ijapokuwa ushahidi waonyesha kwa njia yenye kusadikisha kwenye mwelekezo wa Yehova katika uteuzi wa jina Mashahidi wa Yehova, Mnara wa Mlinzi la Kiingereza (Februari 1, 1944, kur. 42-43; Oktoba 1, 1957, uku. 607) na kitabu “New Heavens and a New Earth” (kur. 231-237) baadaye vilitaja kwamba jina hilo silo lile “jina jipya” lirejezewalo kwenye Isaya 62:2; 65:15; na Ufunuo 2:17, ingawa jina hilo lapatana na uhusiano mpya unaorejezewa katika maandiko hayo mawili katika Isaya.

[Blabu katika ukurasa wa 149]

“Wanafunzi kwa uongozi wa kimungu waliitwa Wakristo”

[Blabu katika ukurasa wa 150]

Jina Wakristo likawa limepotoshwa katika akili za umma

[Blabu katika ukurasa wa 150]

Hawakuwa Wanafunzi wa Biblia tu

[Blabu katika ukurasa wa 157]

“Ninyi ni mashahidi wangu, asema BWANA [“Yehova,” “NW”], nami ni Mungu”

[Sanduku katika ukurasa wa 151]

Jina Mashahidi wa Yehova Katika Mabara ya Amerika

Kiarabu ش‍هود ‍ي‍هوه‍

Kiarmenia Եհովայի Վկաներ

Kichina 耶和華見證人

Kiingereza Jehovah’s Witnesses

Kifaransa Témoins de Jéhovah

Kigiriki Μάρτυρες του Ιεχωβά

Kigreenland Jehovap Nalunaajaasui

Kiitalia Testimoni di Geova

Kijapani エホバの証人

Kikorea 여호와의 증인

Kipapiamento Testigonan di Jehova

Kipoland Świadkowie Jehowy

Kireno Testemunhas de Jeová

Kisamoa Molimau a Ieova

Kihispania Testigos de Jehová

Kisranantongo Jehovah Kotoigi

Kitagalogi Mga Saksi ni Jehova

Kivietnam Nhân-chứng Giê-hô-va

[Sanduku katika ukurasa wa 152]

Wengine Waliliona

Si “The Watch Tower” pekee lililoonyesha kutoka Biblia kwamba Yehova angekuwa na mashahidi duniani. Kama kielelezo, H. A. Ironside, katika kitabu “Lectures on Daniel the Prophet” (kilitangazwa kwanza katika 1911), alirejezea kwa wale ambao kwao ahadi zenye thamani kuu za Isaya sura ya 43 zingetimizwa na kusema: “Hao watakuwa mashahidi wa Yehova, wakishuhudia nguvu na utukufu wa Mungu mmoja wa kweli, wakati Jumuiya ya Wakristo iliyoasi imani itakuwa imeachwa kwenye lile danganyo lenye nguvu iamini uwongo wa Mpinga-Kristo.”

[Sanduku katika ukurasa wa 153]

Jina Mashahidi wa Yehova Katika Nchi za Mashariki na Visiwa vya Pasifiki

Kibengali যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kibikoli, Kisebuano, Kihiligaynoni,

Kisamar-Leyte, Kitagalogi Mga Saksi ni Jehova

Kibislama Ol Wetnes blong Jeova

Kichina 耶和華見證人

Kiingereza Jehovah’s Witnesses

Kifiji Vakadinadina i Jiova

Kigujarati যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kihindi যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kihiri Motu Iehova ena Witness Taudia

Kiiloko Dagiti Saksi ni Jehova

Kiindonesia Saksi-Saksi Yehuwa

Kijapani エホバの証人

Kikannada যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kikorea 여호와의 증인

Kimalayalami যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kimarathi যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kimarshall Dri Kennan ro an Jeova

Kimyanmar ယေဟောဝါသက်သေများ

Kinepali যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kipidgini cha New Guin ea Ol Witnes Bilong Jehova

Kiniue Tau Fakamoli a Iehova

Kipalau reSioning er a Jehovah

Kipangasinani Saray Tasi nen Jehova

Kiponape Sounkadehde kan en Siohwa

Kirarotonga Au Kite o Iehova

Kirusi Свидетели Иеговы

Kisamoa, Kituvalu Molimau a Ieova

Kisinhali যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kipidgini cha Visiwa vya Solomon all’gether Jehovah’s Witness

Kitahiti Ite no Iehova

Kitamili যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kitelugu যিহোবাব সাক্ষীদেব

Kithailand พยานพระยะโฮวา

Kitonga Fakamo‘oni ‘a Sihova

Kitruki Ekkewe Chon Pwarata Jiowa

Kiurdu

Kivietnam Nhân-chứng Giê-hô-va

Kiyapu Pi Mich Rok Jehovah

[Sanduku katika ukurasas wa 154]

Jina Mashahidi wa Yehova Katika Afrika

Kiafrikaani Jehovah se Getuies

Kiamhari የይሖዋ ምሥክሮች

Kiarabu شهود يهوه

Chicheŵa Mboni za Yehova

Cibemba Inte sha kwa Yehova

Kiefịki Mme Ntiense Jehovah

Kiingereza Jehovah’s Witnesses

Kiewe Yehowa Ðasefowo

Kifaransa Témoins de Jéhovah

Kiga Yehowa Odasefoi

Kiguni Kunnudetọ Jehovah tọn lẹ

Kihausa Shaidun Jehovah

Kiigbo Ndịàmà Jehova

Kiluba Ba Tumoni twa Yehova

Kinyarwanda Abahamya ba Yehova

Kirundi Ivyabona vya Yehova

Kikisi Seiyaa Jɛhowaa

Kikwanyama Eendombwedi daJehova

Lingala Batemwe ya Jéhovah

Kiganda Abajulirwa ba Yakuwa

Kimalagasi Vavolombelon’i Jehovah

Kimoore A Zeova Kaset rãmba

Kindonga Oonzapo dhaJehova

Kireno Testemunhas de Jeová

Kisango A-Témoin ti Jéhovah

Kisepedi Dihlatse tša Jehofa

Kisesotho Lipaki tsa Jehova

Kishona Zvapupu zvaJehovha

Silozi Lipaki za Jehova

Kiswahili Mashahidi wa Yehova

Kitigirinya ናይ የሆዋ መሰኻኽር

Tshiluba Bantemu ba Yehowa

Kitsonga Timbhoni ta Yehova

Kitswana Basupi ba ga Jehofa

Kitwi Yehowa Adansefo

Kivenda Ṱhanzi dza Yehova

Xhosa amaNgqina kaYehova

Kiyoruba Ẹlẹ́rìí Jehofa

Kizulu oFakazi BakaJehova

[Sanduku katika ukurasas wa 154]

Jina Mashahidi wa Yehova Katika Ulaya na Mashariki ya Kati

Kialbania Dëshmitarët e Jehovait

Kiarabu شهود يهوه

Kiarmenia Եհովայի Վկաներ

Kibulgaria Свидетелите на Йехова

Kikroatia Jehovini svjedoci

Kicheki svĕdkové Jehovovi

Kidenmark Jehovas Vidner

Kiholanzi Jehovah’s Getuigen

Kiingereza Jehovah’s Witnesses

Kiestonia Jehoova tunnistajad

Kifinland Jehovan todistajat

Kifaransa Témoins de Jéhovah

Kijerumani Jehovas Zeugen

Kigiriki Μάρτυρες του Ιεχωβά

Kiebrania עדי־יהוה

Kihungaria Jehova Tanúi

Kiiceland Vottar Jehóva

Kiitalia Testimoni di Geova

Kimakedonia, Kiserbia Јеховини сведоци

Kimalta Xhieda ta’ Jehovah

Kinorway Jehovas vitner

Kipoland Świadkowie Jehowy

Kireno Testemunhas de Jeová

Kirumania Martorii lui Iehova

Kirusi Свидетели Иеговы

Kislovaki Jehovovi svedkovia

Kislovenia Jehovove priče

Kihispania Testigos de Jehová

Kisweden Jehovas vittnen

Kituruki Yehova’nın Şahitleri

Kiukrainia Свідки Єгови

[Picha katika ukurasa wa 155]

Zile herufi J W (bila maelezo) zilikuwa zenye kutokeza kwenye mkusanyiko wa 1931. Maana yazo ilifunuliwa katika hotuba yenye kusisimua juu ya jina jipya

[Picha katika ukurasa wa 156]

Walijivunia kujulisha wengine kwamba wao walikuwa Mashahidi wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki