Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 32 kur. 710-712
  • “Kwa Hilo Wote Watajua Kwamba Nyinyi Ni Wanafunzi Wangu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kwa Hilo Wote Watajua Kwamba Nyinyi Ni Wanafunzi Wangu”
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mpendane Nyinyi kwa Nyinyi”
  • “Kama Vile Nimewapenda Nyinyi”
  • Upendo wa Kikristo Wenye Msingi wa Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Upendo—“Njia Bora Zaidi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Upendo Wako Umepanuka Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Mjengwe na Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 32 kur. 710-712

Sura ya 32

“Kwa Hilo Wote Watajua Kwamba Nyinyi Ni Wanafunzi Wangu”

ILIKUWA Nisani 14, 33 W.K., usiku wa mwisho wa uhai wa kidunia wa Yesu. Yeye alijua kwamba kifo chake kilikaribia, lakini hakuwa akifikiria juu yake mwenyewe. Badala yake, alitumia fursa hiyo kuwatia moyo wanafunzi wake.

Yesu alijua kwamba baada ya kuondoka kwake haingekuwa rahisi kwao. Wao wangekuwa “vitu vya kuchukiwa na mataifa yote” kwa sababu ya jina lake. (Mt. 24:9, NW) Shetani angejaribu kuwagawanya na kuwapotoa. (Luka 22:31) Kwa sababu ya uasi-imani, Wakristo wa mwigo wangetokea. (Mt. 13:24-30, 36-43) Na ‘kwa sababu ya kuongezeka maasi upendo wa wengi ungepoa.’ (Mt. 24:12) Kwa kukabili mambo hayo yote, ni nini kingewashikamanisha pamoja wanafunzi wake wa kweli? Kwanza kabisa, upendo wao kwa Yehova ungekuwa kifungo chenye kuwaunganisha. (Mt. 22:37, 38) Lakini pia wangewajibika kupendana na kufanya hivyo katika njia ambayo ingewatofautisha na ulimwengu mwingine wote. (Kol. 3:14; 1 Yoh. 4:20) Ni upendo wa aina gani ambao Yesu alisema ungewatambulisha waziwazi wafuasi wake wa kweli?

Jioni hiyo ya mwisho, Yesu aliwapa amri hii: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane. Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yn. 13:34, 35, NW) Yesu alizungumza juu ya upendo kwa mara zaidi ya 20 usiku huo. Na mara tatu alitaja amri kwamba ‘wapendane.’ (Yn. 15:12, 17) Kwa wazi, Yesu hakuwa akifikiria tu juu ya mitume wake waaminifu 11 waliokuwa naye jioni hiyo, bali wengineo wote ambao hatimaye wangeukubali Ukristo wa kweli. (Linganisha Yohana 17:20, 21.) Amri ya kupendana ingefuatwa na Wakristo wote wa kweli “siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mt. 28:20, NW.

Lakini je, Yesu alimaanisha kwamba ikiwa mtu yeyote tu mahali popote ulimwenguni alimfadhili na kumpenda mwenzake basi angelitambuliwa kuwa mmoja wa wanafunzi wa kweli wa Yesu?

“Mpendane Nyinyi kwa Nyinyi”

Jioni iyo hiyo, Yesu pia alikuwa na mengi ya kusema kuhusu umoja. “Kaeni katika muungano nami,” akawaambia wanafunzi wake. (Yn. 15:4, NW) Alisali kwamba wafuasi wake “wapate kuwa mmoja,” na akaongeza, “kama vile wewe, Baba, umo katika muungano na mimi na mimi nimo katika muungano na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano na sisi.” (Yn. 17:21, NW) Katika muktadha huo yeye aliwaamuru: “Mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yn. 13:35, NW) Kwa hiyo upendo wao haungeonyeshwa tu kwa marafiki wachache wa karibu au katika kutaniko moja. Akirudia amri ya Yesu, mtume Petro aliandika hivi baadaye: “Mwe na upendo kwa ajili ya ushirika mzima wa akina ndugu [au, ‘ule udugu’].” (1 Pet. 2:17, Kingdom Interlinear; linganisha 1 Petro 5:9.) Kwa hiyo wao wangekuwa udugu wa ulimwenguni pote, uliofungamanishwa pamoja. Upendo wa kipekee ungeonyeshwa kwa wote walio miongoni mwa familia ya waamini ulimwenguni pote kwa sababu wao wangeonwa kuwa ndugu na dada.

Upendo wa aina hiyo ungedhihirishwaje? Katika kupendana kwao, ni nini kingekuwa chenye kubainisha sana, chenye kutofautisha sana, ambacho wengine wangekiona kuwa uthibitisho dhahiri wa Ukristo wa kweli?

“Kama Vile Nimewapenda Nyinyi”

“Umpende jirani yako kama nafsi yako,” ikasema Sheria ya Mungu kwa Israeli miaka zaidi ya 1,500 kabla ya Yesu kuishi duniani. (Law. 19:18) Hata hivyo, upendo huo wa jirani haukuwa aina ya upendo ambao ungetofautisha wafuasi wa Yesu. Yesu alimaanisha upendo ambao ungekuwa zaidi ya kupenda wengine kama wewe mwenyewe.

Kama vile Yesu alivyosema, amri ya kupendana ilikuwa “amri mpya.” Ilikuwa mpya, si kwa sababu ilikuwa ya karibuni zaidi ya Sheria ya Musa, lakini mpya katika kadiri ambayo upendo huo ungeonyeshwa. Mpendane “kama vile nimewapenda nyinyi,” akaeleza Yesu. (Yn. 13:34, NW) Upendo wake kwa wanafunzi wake ulikuwa wenye nguvu, na wa kudumu. Ulikuwa upendo wenye kujidhabihu. Aliudhihirisha kwa kufanya zaidi tu ya matendo mazuri kwao. Aliwalisha kiroho na, ilipohitajika, alitunza mahitaji yao ya kimwili. (Mt. 15:32-38; Mk. 6:30-34) Na ukiwa upeo wa uthibitisho wa upendo wake, alitoa uhai wake kwa ajili yao.—Yn. 15:13.

Huo ndio aina ya upendo ambao “amri mpya” yataka, ule upendo ambao wafuasi wa kweli wa Yesu wangekuwa nao wao kwa wao. (1 Yoh. 3:16) Ni nani leo wanaotoa uthibitisho dhahiri wa kutii ile “amri mpya”? Uthibitisho uliotolewa mapema katika kichapo hiki waelekeza waziwazi kwenye ushirika mmoja wa Wakristo wa ulimwenguni pote.

Wao wanajulikana, si kwa mavazi ya kipekee au desturi zisizo za kawaida, bali kwa shauku yenye nguvu na iliyo changamfu walio nayo wao kwa wao. Wana sifa ya kudhihirisha upendo unaoshinda tofauti za kikabila au mipaka ya kitaifa. Wanajulikana kwamba wao hukataa kupigana wao kwa wao hata wakati mataifa wanamoishi ndani yayo yanapoenda vitani. Wengine wamevutiwa na jinsi wanavyofikiana katika nyakati za taabu, kama vile wakati misiba inapotokea au wakati baadhi ya washiriki wa udugu wao wanaponyanyaswa kwa ajili ya kudumisha uaminifu-maadili kwa Mungu. Wao wako tayari kuvumilia magumu au kukabili hatari ili kusaidia ndugu na dada zao ambao Kristo alitoa uhai wake kwa ajili yao. Na, naam, wao wako tayari kufa kwa ajili ya wenzao. Upendo wanaoonyesha ni wa kipekee katika ulimwengu unaozidi kuwa na ubinafsi. Wao ni Mashahidi wa Yehova.a

Kielelezo kimoja cha upendo huo ukiwa katika tendo ulionwa kufuatia Kimbunga Andrew, kilichoathiri pwani ya Florida, Marekani, katika saa za asubuhi mapema siku ya Jumatatu, Agosti 24, 1992. Kufuatia kimbunga hicho, watu 250,000 waliachwa bila makao. Maelfu ya Mashahidi wa Yehova walikuwa miongoni mwa majeruhi. Karibu na mara hiyo Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilitenda kwa kuagiza halmashauri ya kutoa misaada na ikapanga kutoa fedha za msaada. Waangalizi Wakristo katika eneo lililoathiriwa waliwasiliana upesi na Mashahidi mmoja-mmoja ili kujua mahitaji yao na kutoa msaada. Jumatatu asubuhi, siku ya kimbunga hicho, tayari Mashahidi walioko umbali wa mamia ya kilometa katika South Carolina walikuwa wamepeleka kilori kilichopakiwa jenereta, misumeno-umeme, na maji ya kunywa kuelekea sehemu ya msiba. Siku ya Jumanne, mamia ya wenye kujitolea wa kutoka nje ya mji waliwasili pamoja na ugavi zaidi ambao ulikuwa umetolewa kuwa upaji, ili kusaidia ndugu wenyeji katika kurekebisha Majumba ya Ufalme na makao ya faragha. Mwanamke asiye Shahidi aliyeishi karibu na Jumba la Ufalme alisema hivi kuhusu jitihada za kutoa misaada: “Kwa kweli huu lazima uwe ndio upendo wa Kikristo ambao Biblia husema juu yao.”

Je, upendo wa aina hiyo ungekwisha baada ya tendo moja au mawili ya fadhili? Je, ungeelekezwa tu kwa watu wa kabila au taifa lilelile? Bila shaka sivyo! Nchini Zaire, kwa sababu ya hali mbaya za kisiasa na za kiuchumi, wakati wa 1992 Mashahidi zaidi ya 1,200 huko walipoteza makao yao na mali zao zote. Upesi Mashahidi wengine katika Zaire walienda kuwasaidia. Hata ingawa wao wenyewe wana magumu, walishiriki vitu pia na wakimbizi waliokuja Zaire kutoka Sudan. Upesi, ugavi wa msaada uliwasili kutoka Afrika Kusini na Ufaransa; huo ulitia ndani unga wa mahindi, samaki waliokaushwa, na msaada wa dawa—vitu ambavyo walivihitaji kwelikweli. Msaada uliandaliwa tena na tena, kulingana na hali. Na huku jambo hilo likiendelea, msaada kama huo ulikuwa ukiandaliwa katika nchi nyinginezo nyingi.

Hata hivyo, si kwamba Mashahidi wa Yehova wametosheka kwa sababu ya kuwa na upendo huo. Wanang’amua kwamba, wakiwa wafuasi wa Yesu Kristo, ni lazima waendelee kulinda.

[Maelezo ya Chini]

a Ona Sura ya 19, “Kukua Pamoja Katika Upendo.”

[Blabu katika ukurasa wa 710]

Ni upendo wa aina gani ambao Yesu alisema ungewatambulisha waziwazi wafuasi wake wa kweli?

[Blabu katika ukurasa wa 711]

Wao wangekuwa udugu wa ulimwenguni pote, uliofungamanishwa pamoja

[Sanduku katika ukurasa wa 712]

“Mashahidi Watunza Walio Wao—Na Wengineo”

Chini ya kichwa kikuu hicho, “The Miami Herald” liliripoti juu ya jitihada za kutoa msaada za Mashahidi wa Yehova katika Florida Kusini kufuatia uharibifu ulioletwa na Kimbunga Andrew mnamo Agosti 1992. Makala hiyo ilisema: “Hakuna yeyote katika Homestead anayefunga mlango Mashahidi wa Yehova wanapobisha juma hili—hata ingawa wangali na milango ya kufunga. Mashahidi wenye kujitolea kama 3,000 kotekote nchini wamekutana kwenye sehemu ya msiba, kwanza kusaidia walio wao, kisha kusaidia wengineo. . . . Tani za chakula na ugavi karibu 150 zimepitishwa katika kituo cha kutoa misaada kwenye Jumba la Kusanyiko katika magharibi mwa Wilaya ya Broward hadi kwenye Majumba ya Ufalme mawili katika eneo la Homestead. Kutoka kwa majumba hayo, wafanyakazi huenda kwenye eneo tofauti kila asubuhi ili kurekebisha makao yaliyobomolewa ya ndugu Mashahidi. . . . Jiko la muda hutokeza milo kwa ajili ya watu kama 1,500, mara tatu kila siku. Na si soseji tu na maandazi. Wenye kujitolea huandaliwa mkate uliookwa, lasanya iliyotayarishwa, saladi zilizochanganywa na krimu, supu, chapati na tosti-mayai—zote zikitayarishwa kwa vitu vilivyotolewa upaji.”—Agosti 31, 1992, ukurasa 15A.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki