Habari za Ufalme Na. 34
Kwa Nini Maisha Yamejaa Matatizo Sana?
Je, paradiso isiyo na taabu yawezekana?
MATATIZO MAZITO YANAKUWA MABAYA ZAIDI—KWA NINI?
Watu wamekuwa na matatizo sikuzote. Ingawa wengi walifikiri kwamba tekinolojia ya kisasa ingeyasuluhisha, matatizo mazito yanakuwa mabaya zaidi.
Uhalifu: Ni watu wachache wanaojihisi salama kutembea katika barabara za mjini au hata kukaa nyumbani mwao. Katika nchi moja ya Ulaya, karibu mtu 1 kwa 3 alipatwa na uhalifu mwaka wa majuzi.
Mazingira: Uchafuzi wa hewa, ardhi, na maji umeenea zaidi na zaidi. Katika mataifa yanayositawi, robo ya watu hawana maji safi.
Umaskini: Kuna watu wengi zaidi walio maskini na wenye njaa kuliko wakati mwingine wowote. Zaidi ya asilimia 90 ya watu katika nchi fulani waishi katika umaskini; asilimia 30 ya watu wawezao kufanya kazi ulimwenguni, wapatao milioni 800, hawana kazi au wana kazi za hali ya chini—na idadi hiyo inaongezeka.
Njaa: Hata kama wewe mwenyewe una chakula cha kutosha, mamilioni wanaoongezeka hawana. Katika nchi ambazo hazijasitawi, kila mwaka angalau watu milioni 13, hasa watoto, hufa kutokana na athari za njaa.
Vita: Mamia ya maelfu wameuawa katika ujeuri wa kikabila wa hivi majuzi. Na katika karne ya 20, vita vimeua watu wanaozidi sana milioni mia moja.
Matatizo Mengine: Kwa hayo yaliyo juu, ongeza mvunjiko wa familia unaozidi kuwa mbaya, mama wengi zaidi wasiofunga ndoa, ongezeko la ukosefu wa makao, kuenea kwa matumizi ya dawa za kulevya, kuenea sana kwa ukosefu wa adili. Kwa kufaa, mmoja aliyekuwa mshiriki wa washauri wa serikali ya Marekani alisema hivi: “Kuna ishara nyingi mno za . . . ustaarabu uliooza.” Katika kipindi kimoja cha majuzi cha miaka 30, idadi ya watu wa Marekani iliongezeka kwa asilimia 41, lakini uhalifu wenye jeuri uliongezeka kasi kufikia asilimia 560, uzazi haramu ukaongezeka kwa asilimia 400, talaka kwa asilimia 300, ujiuaji wa matineja kwa zaidi ya asilimia 200. Na ndivyo ilivyo hali katika mataifa mengine.
Kwa Nini Matatizo Yamekuwa Mabaya Zaidi?
Muumba wetu aandaa jibu. Neno lake lataja nyakati hizi zenye kujaa matatizo kuwa “siku za mwisho,” pindi ambayo “nyakati zilizo ngumu kushughulika nazo” zingekuwapo. (2 Timotheo 3:1, New World Translation) Siku za mwisho wa nini? Biblia yasema kuhusu “mwisho wa ulimwengu.”—Mathayo 24:3, King James Version.
Matatizo ya leo yanayozidi kuongezeka ni uthibitisho wa wazi kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo wakaribia, kutia na mwisho wa uovu na wale wanaousababisha. (Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5; Ufunuo 12:7-12) Karibuni Mungu ataingilia mambo na kuhakikisha kwamba matatizo yote ya leo yamesuluhishwa kabisa.—Yeremia 25:31-33; Ufunuo 19:11-21.
DINI ZA ULIMWENGU HUU ZIMESHINDWA
Badala ya kusaidia kusuluhisha matatizo ya leo, mifumo ya kidini ya ulimwengu huu huyaongeza. Wakati wa vita, Wakatoliki huua Wakatoliki, Waprotestanti huua Waprotestanti—kwa mamilioni. Muda usio mrefu uliopita katika Rwanda, ambako wengi zaidi ni Wakatoliki, watu waliuana kwa maelfu ya mamia! (Ona picha iliyo kushoto.)
Je, Yesu angeenda vitani akiwa na bunduki au upanga na kuua wanafunzi wake kwa sababu walikuwa wa taifa tofauti na lake? La hasha! “Ampendaye Mungu,” Biblia yasema, “ampende na ndugu yake.” (1 Yohana 4:20, 21) Dini za ulimwengu huu zimeshindwa kufanya hivyo. “Wanakiri ya kwamba wanamjua Mungu, bali kwa matendo yao wanamkana.”—Tito 1:16.
Na zaidi, kwa kutoshikilia hasa viwango vya Biblia vya maadili, dini za ulimwengu huchangia mvunjiko mkubwa wa maadili duniani pote.
Yesu alisema kwamba ungeweza kutambua dini ya uwongo kutokana na dini ya kweli ‘kwa matunda yayo’—kwa mambo ambayo washiriki wayo hufanya. Pia alisema: “Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni.” (Mathayo 7:15-20) Neno la Mungu latuhimiza tutoroke dini inayozaa matunda mabaya kwani yakabili uharibifu.—Ufunuo 18:4.
Dini ya Kweli Haijashindwa
Dini ya kweli “huzaa matunda mazuri,” hasa upendo. (Mathayo 7:17; Yohana 13:34, 35) Ni udugu gani uliounganika wa kimataifa wa Wakristo unaoonyesha upendo kama huo? Ni nani hukataa kuua wale wa dini yao, au mtu yeyote yule?—1 Yohana 3:10-12.
Mashahidi wa Yehova wana sifa ya kuzaa yale “matunda mazuri.” Duniani pote, katika nchi zaidi ya 230, ‘wao wamefua panga zao kuwa majembe.’ (Isaya 2:4) Upendo wao kwa watu waonyeshwa vilevile na utii wao kwa amri ya Kristo ya kuhubiri “habari njema” za Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote. (Mathayo 24:14) Wao pia hutenda na kutetea maadili ya juu yafundishwayo katika Biblia.—1 Wakorintho 6:9-11.
Dini ya kweli haijashindwa. Hiyo huelekeza watu kwa yule Mmoja wa pekee awezaye kusuluhisha matatizo ya mwanadamu. Karibuni huyo Mmoja ataleta ulimwengu mpya kabisa. Huyo Mmoja ni nani? (Tafadhali angalia ukurasa wa nyuma.)
PARADISO ISIYO NA MATATIZO NI HAKIKA
Kama ungeweza, je, hungesuluhisha matatizo yote yanayopata wanadamu? Bila shaka ungefanya hivyo! Je, tufikirie kwamba Muumba wetu mwenye upendo, ambaye pekee ana uwezo na hekima ya kusuluhisha matatizo ya wanadamu, hatafanya hivyo?
Biblia yafunua kwamba Mungu ataingilia mambo ya binadamu akitumia serikali yake ya kimbingu iliyo mikononi mwa Yesu Kristo. Hiyo ‘itavunja vipande vipande’ serikali zenye ufisadi duniani. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Na kwa nini? Akimwambia Mungu, mtunga-zaburi ajibu hivi: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.”—Zaburi 83:18.
Ulimwengu huu uishapo, je, kutakuwa na waokokaji? “Ulimwengu unapita,” Biblia yasema, “lakini yeye afanyaye mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (1 Yohana 2:17, NW) Waokokaji hao wataishi milele wapi? “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele,” Biblia yajibu.—Zaburi 37:9-11, 29; Mithali 2:21, 22.
Katika ulimwengu mpya wa Mungu, “mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Hakuna uhalifu, umaskini, njaa, ugonjwa, huzuni, au kifo! Lo! hata wafu wataishi tena! “Kutakuwa na ufufuo.” (Matendo 24:15) Na dunia yenyewe itageuzwa kuwa paradiso halisi.—Isaya 35:1, 2; Luka 23:43.
Ni lazima tufanye nini ili tupate uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu? Yesu alisema: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Mamilioni ya watu wenye mioyo ya haki ulimwenguni pote wanatwaa ujuzi huo. Huo huwawezesha kukabili matatizo yao mengi ya kibinafsi sasa, na la maana zaidi, unawapa uhakika kamili kwamba matatizo wasiyoweza kusuluhisha yatasuluhishwa kabisa katika ulimwengu mpya wa Mungu.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]
Picha ya WHO ya P. Almasy
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Jerden Bouman/Sipa Press