Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 9/15 kur. 2-7
  • Je, Dini Zote Humpendeza Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Dini Zote Humpendeza Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Watambuliwa kwa Matunda Yao
  • Uhitaji wa Kutahadhari
  • Chunguza Matunda
  • Wakati wa Utendaji wa Kukata Maneno
  • Ibada Ambayo Mungu Anakubali
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Mwisho Wa Dini Ya Uwongo Unakaribia!
    Mwisho Wa Dini Ya Uwongo Unakaribia!
  • Je! Umeipata Dini ya Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Je, Mungu Huzikubali Dini Zote?
    Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 9/15 kur. 2-7

Je, Dini Zote Humpendeza Mungu?

Je, wafikiri kwamba dini zote humpendeza Mungu? Huenda aina yoyote ya ibada unayojua hutia moyo mwenendo mzuri, angalau kwa kiasi fulani. Lakini je, hilo latosha ili kumpendeza Mungu?

WATU fulani husema hivi, ‘Uwe mnyoofu tu katika ibada yako, na Mungu atapendezwa. Kuna wema katika dini zote.’ Kwa kielelezo, Imani ya Bahai imekuwa na maoni hayo kufikia hatua ya kuasilisha kwenye itikadi zayo zile dini kubwa tisa za ulimwengu. Kikundi hicho cha kidini kinaamini kwamba dini zote hizo zina chanzo cha kimungu nazo ni pande mbalimbali za kweli ileile. Hilo lingewezekanaje?

Zaidi, una haki ya kujiuliza jinsi dini ingeweza kumpendeza Mungu huku iwaamurupo washiriki wayo waweke gesi ya neva mahali mbalimbali pa umma, kukiwa na uwezekano wa kuua watu wengi. Shtaka hilo limeelekezwa dhidi ya kikundi kimoja cha kidini huko Japani. Au je, Mungu hupendezwa na dini isababishayo washiriki wayo wajiue? Miaka michache iliyopita, hilo liliwapata wafuasi wa kiongozi wa kidini Jim Jones.

Tukitazama nyuma kwenye nyakati za mapema, huenda kwa kufaa tukauliza hivi, Je, dini zaweza kumpendeza Mungu huku zichocheapo vita, kama vile katika kisa cha Vita ya Miaka Thelathini, iliyopiganwa kuanzia 1618 hadi 1648? Kulingana na The Universal History of the World, yale mapambano ya kidini kati ya Wakatoliki na Waprotestanti yalikuwa “mojawapo vita vibaya zaidi katika historia ya Ulaya.”

Zile Krusedi za kidini kuanzia karne ya 11 hadi karne ya 13 zilitokeza pia umwagikaji wa damu wenye kuchukiza. Kwa kielelezo, katika Krusedi ya kwanza, wale waitwao eti wana-krusedi Wakristo waliwachinja kinyama wakazi Waislamu na Wayahudi wa Yerusalemu.

Fikiria pia, kilichotukia wakati wa lile Baraza la Kuhukumu Wazushi, lililoanza katika karne ya 13 na kudumu kwa miaka ipatayo 600. Maelfu ya watu waliteswa na kuchomwa hadi kifo kwa amri ya viongozi wa kidini. Katika kitabu chake Vicars of Christ—The Dark Side of the Papacy, Peter De Rosa ataarifu hivi: “Kwa jina la papa, [wenye kuhukumu wazushi] walikuwa na lawama la shambulio lenye ukatili zaidi na lenye kuendelea dhidi ya adabu ya kibinadamu katika historia ya jamii [ya kibinadamu].” Kumhusu mhukumu-wazushi Mdominika Torquemada wa Hispania, De Rosa asema hivi: “Akiwa amewekwa rasmi katika 1483, alitawala kimabavu kwa miaka kumi na mitano. Wahasiriwa wake walikuwa zaidi ya 114,000 ambao miongoni mwao 10,220 waliteketezwa.”

Bila shaka, si dini za Jumuiya ya Wakristo pekee zilizo na hatia ya damu. Katika kitabu chake Pensées, mwanafalsafa Mfaransa Blaise Pascal alionelea hivi: “Hakuna kamwe wakati watu hufanya uovu kwa ukamili sana na kwa uchangamfu kama wakati waufanyapo kutokana na usadikisho wa kidini.”

Watambuliwa kwa Matunda Yao

Kwa maoni ya Mungu, kukubalika kwa dini hakutegemei jambo moja tu. Ili dini iwe yenye kukubalika kwake, lazima mafundisho na utendaji wayo upatane na Neno lake la kweli lililoandikwa, Biblia. (Zaburi 119:160; Yohana 17:17) Matunda ya ibada inayokubaliwa na Mungu lazima yapatane na viwango vya Yehova Mungu.

Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu Kristo alionyesha kwamba kungekuwa na manabii wadaio isivyo kweli kumwakilisha Mungu. Yesu alisema hivi: “Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali. Mtawatambua kwa matunda yao. Je! watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti? Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri. Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni. Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua.” (Mathayo 7:15-20) Maneno hayo yaonyesha kwamba twahitaji kuwa macho kiroho. Huenda tukafikiri kwamba kikundi au kiongozi wa kidini hukubaliwa na Mungu na Kristo, lakini twaweza kuwa tumekosea.

Uhitaji wa Kutahadhari

Ingawa dini hudai kuwa na kibali cha Mungu na wahudumu wayo husoma vifungu vya maneno kutoka katika Biblia, hilo halimaanishi kwamba ni aina ya ibada inayompendeza Mungu. Huenda hata viongozi wayo wakafanya mambo yenye kuvutia yafanyayo ionekane kana kwamba Mungu alikuwa akifanya kazi kupitia wao. Hata hivyo, huenda bado dini hiyo ikawa isiyo ya kweli, isiyozaa matunda yakubaliwayo na Mungu. Makuhani Wamisri wafanya-mizungu wa siku ya Musa waliweza kufanya mambo yenye kuvutia, lakini kwa wazi hawakuwa na kibali cha Mungu.—Kutoka 7:8-22.

Leo kama ilivyokuwa wakati uliopita, dini nyingi huendeleza mawazo na falsafa za kibinadamu badala ya kushikamana na yale ambayo Mungu hutangaza kuwa kweli. Basi, lifaalo hasa ni onyo hili la Biblia: “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, kwa jinsi ya mapokeo ya wanadamu, kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo.”—Wakolosai 2:8.

Baada ya kuzungumzia matunda mazuri na mabaya, Yesu alisema hivi: “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.”—Mathayo 7:21-23.

Chunguza Matunda

Basi, kwa wazi, ni muhimu kuyachunguza matunda ya dini kabla ya kukata maneno kwamba hiyo yakubalika kwa Mungu. Kwa mfano, je, dini hiyo yahusika katika siasa? Basi ona maneno haya, yaliyorekodiwa kwenye Yakobo 4:4: “Kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.” Zaidi, Yesu alisema hivi juu ya wafuasi wake wa kweli: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:16) Dini iliyo nzuri machoni pa Mungu haihusiki katika siasa za ulimwengu huu, ambao “hukaa katika [“nguvu ya,” NW] yule mwovu,” kiumbe cha roho kisichoonekana Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Badala ya hivyo, dini aikubaliyo Mungu hutetea kwa uaminifu-mshikamanifu Ufalme wake chini ya Yesu Kristo na hutangaza habari njema ihusuyo serikali hiyo ya kimbingu.—Marko 13:10.

Je, dini yakubaliwa na Mungu ikiwa hiyo hutetea uasi dhidi ya mamlaka? Jibu ni wazi ikiwa twatii shauri hili la mtume Paulo: “Uwakumbushe watu kunyenyekea kwa wenye uwezo na mamlaka, na kutii, na kuwa tayari kwa kila kazi njema.” (Tito 3:1) Bila shaka, Yesu alionyesha kwamba wafuasi wake walipaswa ‘kumpa Kaisari yaliyo ya Kaisari, na yaliyo ya Mungu wampe Mungu.’—Marko 12:17.

Tuseme dini inatia moyo kushiriki katika vita vya mataifa. Petro wa Kwanza 3:11 hutusihi sana ‘tutende mema’ na ‘tutafute amani, tuifuatie sana.’ Dini yaweza kumpendezaje Mungu ikiwa washiriki wayo wako tayari kuua vitani waabudu wenzao wa nchi nyingine? Washiriki wa dini iliyo na kibali cha Mungu huonyesha sifa yake kuu—upendo. Na Yesu alisema hivi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Upendo huo haushiriki lolote pamoja na chuki yenye jeuri ichochewayo katika vita vya mataifa.

Dini ya kweli hubadili watu wenye mielekeo ya kivita wawe wapenda-amani. Hilo lilitabiriwa katika maneno haya: “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4) Badala ya kuropoka maneno ya chuki, wale wazoeao ibada ya kweli hutii amri hii: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.”—Mathayo 22:39.

Wanaozoea dini ya kweli hujitahidi kuishi kupatana na viwango vya juu vya Yehova Mungu, wakikataa kukubali mitindo-maisha isiyo ya adili. Neno la Mungu hutaarifu hivi: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi. Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika Roho wa Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:9-11.

Wakati wa Utendaji wa Kukata Maneno

Ni muhimu kutambua tofauti kati ya ibada isiyo ya kweli na dini ya kweli. Katika kitabu cha Biblia cha Ufunuo, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli hutambulishwa kuwa “Babiloni Mkubwa,” kahaba wa ufananisho “ambaye wafalme wa nchi wamezini naye.” Yeye ana hatia ya damu na anashika kikombe cha dhahabu “kilichojawa na machukizo, na machafu ya uasherati wake.” (Ufunuo 17:1-6, linganisha NW.) Hakuna lolote limhusulo linalokubalika kwa Mungu.

Huu ni wakati wa utendaji wa kukata maneno. Kwa watu wanyoofu walio bado katika Babiloni Mkubwa, Muumba wetu mwenye upendo atoa mwito huu: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.”—Ufunuo 18:4.

Ikiwa unataka kuzoea dini impendezayo Mungu, mbona usipate kufahamiana na Mashahidi wa Yehova vizuri zaidi? Chati inayoandama imeorodhesha baadhi ya itikadi zao, pamoja na sababu zazo za Kimaandiko. Chunguza Biblia yako ili uone ikiwa itikadi za Mashahidi hupatana na Neno la Mungu. Chunguza uone ikiwa dini yao hutokeza aina ya matunda ambayo ungetazamia ibada ya kweli itokeze. Ukiona kwamba inafanya hivyo, utakuwa umepata dini impendezayo Mungu.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

WANAYOAMINI MASHAHIDI WA YEHOVA

ITIKADI MSINGI WA KIBIBLIA

Jina la Mungu ni Yehova Kutoka 6:3; Zaburi 83:18

Biblia ni Neno la Mungu Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16, 17

Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu Mathayo 3:16, 17; Yohana 14:28

Wanadamu hawakutokana na mageuzi Mwanzo 1:27; 2:7

bali waliumbwa

Kifo cha kibinadamu hutokana Warumi 5:12

na dhambi ya mtu wa kwanza

Nafsi hukoma kuwako wakati wa kifo Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4

Helo ni kaburi la kawaida la wanadamu Ayubu 14:13; Ufunuo 20:13,

King James Version

Ufufuo ndio tumaini Yohana 5:28, 29; 11:25;

kwa ajili ya wafu Matendo 24:15

Kristo alitoa uhai wake wa kidunia kuwa Mathayo 20:28;

fidia kwa ajili ya wanadamu watiifu 1 Petro 2:24; 1 Yohana 2:1, 2

Sala lazima zielekezwe kwa Yehova Mathayo 6:9;

pekee kupitia Kristo Yohana 14:6, 13, 14

Sheria za Biblia juu ya maadili 1 Wakorintho 6:9, 10

lazima zitiiwe

Mifano haipaswi kutumiwa katika ibada Kutoka 20:4-6; 1 Wakorintho 10:14

Uwasiliani-roho lazima uepukwe Kumbukumbu la Torati 18:10-12;

Wagalatia 5:19-21

Damu haipaswi kuingizwa mwilini mwa mtu Mwanzo 9:3, 4; Matendo 15:28, 29

Wafuasi wa kweli wa Yesu hujitenga Yohana 15:19; 17:16;

na ulimwengu Yakobo 1:27; 4:4

Wakristo hutoa ushahidi, wakitangaza Isaya 43:10-12; Mathayo 24:14;

habari njema 28:19, 20

Ubatizo kwa kuzamishwa majini kabisa Marko 1:9, 10; Yohana 3:22;

hufananisha kujiweka wakfu kwa Mungu Matendo 19:4, 5

Majina ya vyeo ya kidini hayapatani Ayubu 32:21, 22; Mathayo 23:8-12

na Maandiko

Tunaishi katika “wakati wa mwisho” Danieli 12:4; Mathayo 24:3-14;

2 Timotheo 3:1-5

Kuwapo kwa Kristo hakuonekani Mathayo 24:3; Yohana 14:19;

1 Petro 3:18

Shetani ndiye mtawala asiyeonekana Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19

wa ulimwengu huu

Mungu atauharibu mfumo mbovu Danieli 2:44;

wa mambo uliopo Ufunuo 16:14, 16; 18:1-8

Ufalme wa Mungu chini ya Kristo utaitawala Isaya 9:6, 7; Danieli 7:13, 14;

dunia kwa uadilifu Mathayo 6:10

“Kundi dogo” kutawala mbinguni Luka 12:32; Ufunuo 14:1-4; 20:4

pamoja na Kristo

Wengine wanaokubaliwa na Mungu watapokea Luka 23:43; Yohana 3:16;

uhai wa milele kwenye dunia iliyo paradiso Ufunuo 21:1-4

[Picha katika ukurasa wa 4]

Maelfu ya watu waliuawa wakati wa yale Mabaraza ya Kuhukumu Wazushi

[Picha katika ukurasa wa 6]

Zile Krusedi zilitokeza umwagikaji wa damu wenye kuchukiza

[Picha katika ukurasa wa 7]

Dini ya kweli hujulikana kwa matunda yayo mema

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

Cover: Garo Nalbandian

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki