Sura 7
Alilofanya Mungu ili Kuokoa Wanadamu
1, 2. (a) Akida Mroma alikujaje kung’amua ni nani aliyekuwa Mwana wa Mungu? (b) Sababu gani Yehova alimruhusu Yesu afe?
ALASIRI moja ya masika karibu miaka 2,000 iliyopita, akida mmoja Mroma alitazama wanaume watatu wakifa vifo vyenye maumivu makali na vya polepole. Askari-jeshi huyu akamtambua mmoja wao hasa—Yesu Kristo. Yesu alikuwa amepigiliwa misumari kwenye mti wa mateso wa mbao. Anga ya adhuhuri ilikuwa yenye giza wakati wa kifo chake ulipokaribia. Alipokufa, dunia ilitikisika kwa nguvu, na askari-jeshi huyu akapaaza sauti hivi: “Hakika mtu huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”—Marko 15:39.
2 Mwana wa Mungu! Askari-jeshi huyo alisema kweli. Yeye alikuwa ametoka tu kushuhudia jambo la maana zaidi lililopata kutendeka duniani wakati wowote ule. Kwenye pindi nyinginezo, Mungu mwenyewe alikuwa amemwita Yesu Mwana wake mpendwa. (Mathayo 3:17; 17:5) Sababu gani Yehova alikuwa amemruhusu Mwana wake afe? Kwa sababu hiyo ilikuwa njia ya Mungu ya kuokoa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo.
KUCHAGULIWA KWA AJILI YA KUSUDI LA PEKEE
3. Sababu gani ilifaa kwamba Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu achaguliwe kwa ajili ya kusudi la pekee kuhusiana na wanadamu?
3 Kama vile tumetangulia kujifunza katika kitabu hiki, Yesu alikuwako kabla ya kuwa binadamu. Yeye aitwa “Mwana mzaliwa-pekee” wa Mungu kwa sababu Yehova alimuumba moja kwa moja. Baada ya hapo Mungu alimtumia Yesu kufanya vitu vingine vyote viweko. (Yohana 3:18, NW; Wakolosai 1:16, NW) Yesu alipenda hasa jamii ya kibinadamu. (Mithali 8:30, 31) Si ajabu kwamba Yehova alimchagua Mwana wake mzaliwa-pekee ili kutimiza kusudi la pekee wakati wanadamu walipokuja kuwa chini ya hukumu ya kifo!
4, 5. Kabla ya Yesu kuja duniani, Biblia ilifunua nini juu ya Mbegu ya Kimesiya?
4 Alipokuwa akitamka hukumu juu ya Adamu, Hawa, na Shetani katika bustani ya Edeni, Mungu alisema juu ya Mwokoaji wa wakati ujao kuwa “mbegu.” Mbegu hii, au uzao, ingekuja kuondoa maovu mabaya ambayo Shetani Ibilisi, yule “nyoka wa zamani,” alikuwa amesababisha. Kwa kweli, hiyo Mbegu iliyoahidiwa ingemponda Shetani na wote wale waliomfuata.—Mwanzo 3:15; 1 Yohana 3:8; Ufunuo 12:9.
5 Kwa muda wa karne zilizopita, Mungu alifunua hatua kwa hatua mengi zaidi juu ya hiyo Mbegu, iliyoitwa pia Mesiya. Kama vile ionyeshwavyo katika chati kwenye ukurasa 37, unabii mwingi sana ulitoa habari zaidi juu ya sehemu nyingi za maisha yake duniani. Kwa mfano, yeye angevumilia kutendwa vibaya sana ili kutimiza daraka lake katika kusudi la Mungu.—Isaya 53:3-5.
SABABU KWA NINI MESIYA ANGEKUFA
6. Kulingana na Danieli 9:24-26, Mesiya angetimiza nini, na kwa jinsi gani?
6 Unabii ambao umerekodiwa kwenye Danieli 9:24-26 ulitabiri kwamba Mesiya—Mtiwa-Mafuta wa Mungu—angetimiza kusudi kubwa. Yeye angekuja duniani “ili kukomesha makosa, na kuishiliza dhambi, na kufanya upatanisho [“ufunikaji,” NW] kwa ajili ya uovu, na kuleta haki” milele. Mesiya angeondoa hukumu ya kifo kutoka kwa wanadamu waaminifu. Lakini yeye angefanyaje hilo? Unabii huo unaeleza kwamba yeye ‘angekatiliwa mbali,’ au kuuawa.
7. Sababu gani Wayahudi walitoa dhabihu za wanyama, nazo zilitangulia kuonyesha kivuli cha nini?
7 Waisraeli wa kale walifahamu wazo la kufunikwa kwa kosa. Katika ibada yao chini ya Sheria ambayo Mungu aliwapa kupitia Musa, wao walitoa kwa kawaida dhabihu za wanyama. Hizo ziliwakumbusha watu wa Israeli kwamba wanadamu wanahitaji kitu fulani cha kufunika dhambi zao. Mtume Paulo alitoa muhtasari wa kanuni hiyo kwa njia hii: “Pasipo kumwaga damu hakuna ondoleo [“msamaha,” NW].” (Waebrania 9:22) Wakristo hawako chini ya Sheria ya Kimusa pamoja na matakwa yayo, kama vile dhabihu. (Warumi 10:4; Wakolosai 2:16, 17) Wanajua pia kwamba dhabihu za wanyama haziwezi kutoa msamaha wa dhambi wenye kudumu na ulio kamili. Badala ya hivyo, matoleo hayo ya kidhabihu yalitangulia kuonyesha kivuli cha dhabihu yenye thamani zaidi—ile ya Mesiya, au Kristo. (Waebrania 10:4, 10; linganisha Wagalatia 3:24.) Hata hivyo, huenda ukauliza, ‘Je, kweli ilikuwa lazima Mesiya afe?’
8, 9. Ni mambo gani yenye thamani yaliyopotezwa na Adamu na Hawa, na matendo yao yaliathirije wazao wao?
8 Ndiyo, Mesiya alipaswa afe ikiwa wanadamu wangeokolewa. Ili kuelewa ni sababu gani, ni lazima tufikirie mambo yaliyotokea huko nyuma katika bustani ya Edeni na tujaribu kuelewa uzito wa yale ambayo Adamu na Hawa walipoteza walipoasi dhidi ya Mungu. Wao walikuwa wamewekewa uhai wa milele mbele yao! Wakiwa watoto wa Mungu, wao walifurahia pia uhusiano wa moja kwa moja naye. Lakini walipokataa katakata utawala wa Yehova, walipoteza yote hayo wakaleta dhambi na kifo juu ya jamii ya kibinadamu.—Warumi 5:12.
9 Ilikuwa kana kwamba wazazi wetu wa kwanza walikuwa wameponda mali nyingi mno, wakijiingiza katika deni kubwa mno. Adamu na Hawa walipitisha deni hilo kwa wazao wao. Kwa sababu hatukuzaliwa tukiwa wakamilifu na bila dhambi, kila mmoja wetu ni mwenye dhambi na anakufa. Tunapokuwa wagonjwa au kusema jambo fulani lenye kudhuru ambalo tungetamani tufute, tunapatwa na matokeo ya deni letu tulilorithi—kutokukamilika kwa binadamu. (Warumi 7:21-25) Tumaini letu pekee ni kupata tena yale ambayo Adamu alipoteza. Hata hivyo, hatuwezi kuchuma uhai mkamilifu wa kibinadamu. Kwa kuwa wanadamu wote wasio wakamilifu hutenda dhambi, sisi sote tunachuma kifo, si uhai.—Warumi 6:23.
10. Ni nini kilichohitajiwa ili kukomboa yale ambayo Adamu alipoteza?
10 Hata hivyo, je, kuna lolote ambalo lingeweza kutolewa kwa kubadilishana na uhai ambao Adamu alipoteza? Kiwango cha Mungu cha haki chadai usawaziko, “nafsi kwa nafsi.” (Kutoka 21:23, NW) Kwa hiyo ilikuwa lazima uhai utolewe ili kulipia uhai uliopotezwa. Si uhai tu wowote ule ambao ungefaa. Zaburi 49:7, 8 husema hivi juu ya wanadamu wasio wakamilifu: “Hakuna mtu awezaye kumkomboa ndugu yake, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake, (maana fidia ya nafsi zao ina gharama, wala hana budi kuiacha hata milele).” Basi je, hiyo hali ni ile isiyo na tumaini? La, hasha.
11. (a) Neno “fidia” humaanisha nini katika Kiebrania? (b) Ni nani pekee angeweza kukomboa wanadamu, na sababu gani?
11 Katika lugha ya Kiebrania, neno “fidia” humaanisha kiasi kinacholipwa ili kumkomboa mwenye kutekwa na huonyesha pia kitu kinacholingana. Ni mwanadamu tu mwenye uhai wa kibinadamu ulio mkamilifu ndiye angeweza kutoa kinacholingana na alichopoteza Adamu. Baada ya Adamu, mwanadamu mkamilifu pekee kuzaliwa duniani alikuwa Yesu Kristo. Kwa sababu hiyo, Biblia humwita Yesu “Adamu wa mwisho” na hutuhakikishia kwamba Kristo ‘alijitoa mwenyewe kuwa fidia inayolingana kwa ajili ya wote.’ (1 Wakorintho 15:45, NW; 1 Timotheo 2:5, 6, NW) Ingawa Adamu aliwapitishia watoto wake kifo, Yesu alipitisha uhai wa milele. Wakorintho wa Kwanza 15:22 hueleza hivi: “Kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa.” Kwa kufaa basi, Yesu huitwa “Baba wa milele.”—Isaya 9:6, 7.
JINSI FIDIA ILIVYOLIPWA
12. Yesu akaja kuwa Mesiya lini, naye alifuatia mwendo gani wa maisha baada ya hapo?
12 Katika vuli ya 29 W.K., Yesu alimwendea Yohana mtu wa ukoo wake ili abatizwe na hivyo ajitoe kufanya mapenzi ya Mungu. Kwenye pindi hiyo Yehova alimtia Yesu mafuta kwa roho takatifu. Kwa njia hiyo Yesu akawa Mesiya, au Kristo, mwenye kutiwa mafuta na Mungu. (Mathayo 3:16, 17) Ndipo Yesu akaanza huduma yake ya muda wa miaka mitatu na nusu. Alisafiri kotekote katika nchi yake, akihubiri juu ya Ufalme wa Mungu na kukusanya wafuasi waaminifu. Hata hivyo, kama ilivyotabiriwa, upinzani dhidi yake ukaongezeka upesi.—Zaburi 118:22; Matendo 4:8-11.
13. Ni mambo gani yaliyoongoza kwenye kifo cha Yesu akiwa mshika-uaminifu-maadili?
13 Yesu alifichua kwa moyo mkuu unafiki wa viongozi wa kidini, nao walijaribu kumuua. Hatimaye walitunga njama mbaya iliyohusisha usaliti, kukamatwa isivyofaa, kesi isiyo halali, na shtaka bandia la uchochezi. Yesu alipigwa makofi, alitemewa mate, alidhihakiwa, na kupigwa mijeledi iliyokusudiwa kurarua nyama ya mwili wake. Ndipo gavana Mroma Pontio Pilato akamhukumia kifo kwenye mti wa mateso. Alipigiliwa misumari kwenye nguzo ya mbao na kutundikwa hapo wima. Kila mvuto wa pumzi uliumiza sana, na ilichukua muda wa saa nyingi kabla ya yeye kufa. Muda wote wa jaribu hilo kali, Yesu alidumisha uaminifu-maadili mkamilifu kwa Mungu.
14. Sababu gani Mungu alimruhusu Mwana wake ateseke na kufa?
14 Basi, ikawa katika Nisani 14, 33 W.K., Yesu akatoa uhai wake “iwe fidia ya wengi.” (Marko 10:45; 1 Timotheo 2:5, 6) Kutoka mbinguni, Yehova angeweza kuona Mwana wake mpendwa akiteseka na kufa. Sababu gani Mungu aliruhusu jambo hilo baya litendeke? Alifanya hivyo kwa sababu alipenda jamii ya kibinadamu. Yesu alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kifo cha Yesu chatufundisha pia kwamba Yehova ni Mungu mwenye haki kamilifu. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Huenda wengine wakajiuliza sababu gani Mungu hakuachia mbali kanuni zake za haki zilizotaka nafsi kwa nafsi na kupuuza bei iliyotakwa na mwendo wa Adamu wenye dhambi. Sababu ni kwamba sikuzote Yehova hufuata sheria zake na huzitegemeza, hata kwa gharama kubwa juu yake mwenyewe.
15. Kwa kuwa isingekuwa haki kuruhusu kuwako kwa Yesu kukome daima, Yehova alifanya nini?
15 Haki ya Yehova ilitaka pia kwamba kifo cha Yesu kiwe na tokeo lenye furaha. Kwa vyovyote vile, je, ingekuwa haki kumruhusu Yesu mwaminifu alale milele katika kifo? Bila shaka sivyo! Maandiko ya Kiebrania yalikuwa yametoa unabii kwamba mwaminifu-mshikamanifu wa Mungu asingeendelea kuwa kaburini. (Zaburi 16:10; Matendo 13:35) Yeye alilala katika kifo kwa sehemu za siku tatu, ndipo Yehova Mungu akamfufua kwenye uhai akiwa kiumbe wa roho mwenye uweza.—1 Petro 3:18.
16. Yesu alifanya nini aliporudi mbinguni?
16 Kwenye kifo chake, Yesu alisalimisha uhai wake wa kibinadamu kwa wakati wote. Alipofufuliwa ili kuishi mbinguni, alikuja kuwa roho mwenye kutoa uhai. Zaidi ya hayo, Yesu alipopaa kwenda mahali palipo patakatifu zaidi ya patakatifu katika ulimwengu wote mzima, aliunganishwa tena na Baba yake mpendwa akamtolea Yeye thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa njia rasmi. (Waebrania 9:23-28) Hapo ndipo thamani ya uhai huo wenye bei ingeweza sasa kutumiwa kwa niaba ya wanadamu watiifu. Hilo lamaanisha nini kwako?
FIDIA YA KRISTO NA WEWE
17. Tunaweza kujinufaishaje na msamaha kwa msingi wa dhabihu ya Kristo ya fidia?
17 Fikiria njia tatu ambazo dhabihu ya fidia ya Kristo inakunufaisha hata sasa. Kwanza, inaleta msamaha wa dhambi. Kupitia imani katika damu iliyomwagwa ya Yesu, tuna “ukombozi wetu [“kupitia fidia,” NW],” ndiyo, “masamaha ya dhambi.” (Waefeso 1:7) Kwa hiyo hata ikiwa tumetenda dhambi nzito, tunaweza kumwomba Mungu msamaha kwa jina la Yesu. Tukitubu kwelikweli, Yehova anatumia kwetu thamani ya dhabihu ya fidia ya Mwana wake. Mungu hutusamehe, akitupa sisi baraka ya dhamiri njema, badala ya kutekeleza adhabu ya kifo tunayojiletea kwa kutenda dhambi.—Matendo 3:19; 1 Petro 3:21.
18. Dhabihu ya Yesu hututolea tumaini kwa njia gani?
18 Pili, dhabihu ya fidia ya Kristo hutoa msingi wa tumaini letu kwa wakati ujao. Katika ono, mtume Yohana aliona kwamba “mkutano [“umati,” NW] mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu” ungeokoka mwisho wenye msiba unaokuja wa mfumo huu wa mambo. Sababu gani wao wataokoka wakati Mungu anapowaharibu wengine wengi sana? Malaika alimwambia Yohana kwamba wale wa umati mkubwa walikuwa “wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Yesu Kristo. (Ufunuo 7:9, 14) Maadamu tunadhihirisha imani katika damu iliyomwagwa ya Yesu Kristo na kuishi kulingana na matakwa ya kimungu, sisi tutakuwa safi machoni pa Mungu na tutakuwa na tumaini la uhai udumuo milele.
19. Dhabihu ya Kristo huthibitishaje kwamba yeye na Baba yake wanakupenda wewe?
19 Tatu, dhabihu ya fidia ni upeo wa ithibati ya mwisho ya upendo wa Yehova. Kifo cha Kristo kilionyesha wazi sana yale matendo mawili makubwa zaidi ya upendo katika historia ya ulimwengu wote mzima: (1) Upendo wa Mungu katika kumtuma Mwana wake kufa kwa niaba yetu; (2) Upendo wa Yesu katika kujitoa kwa hiari kuwa fidia. (Yohana 15:13; Warumi 5:8) Tukidhihirisha imani kwelikweli, upendo huo unatumika kwa kila mmoja wetu. Mtume Paulo alisema hivi: “Mwana wa Mungu . . . alinipenda akajitoa nafsi yake kwa ajili yangu.”—Wagalatia 2:20; Waebrania 2:9; 1 Yohana 4:9, 10.
20. Sababu gani tunapaswa kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu?
20 Kwa hiyo, acheni tuonyeshe shukrani yetu kwa ajili ya upendo ulioonyeshwa na Mungu na Kristo kwa kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Kufanya hivyo huongoza kwenye uhai udumuo milele. (Yohana 3:36) Hata hivyo, wokovu wetu siyo sababu yenye maana zaidi kuliko zote ya uhai na kifo cha Yesu duniani. La, hangaiko lake la kwanza lilikuwa suala kubwa hata zaidi, linalohusu ulimwengu wote mzima. Kama vile tutakavyoona katika sura ifuatayo, suala hilo linahusu sisi sote kwa sababu linaonyesha sababu kwa nini Mungu ameruhusu uovu na kuteseka kuendelee kwa muda mrefu sana katika ulimwengu huu.
TAHINI UJUZI WAKO
Sababu gani Yesu alipaswa kufa ili kuokoa wanadamu?
Fidia ililipwaje?
Unanufaika katika njia zipi kutokana na fidia?
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 67]