Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • T-74 kur. 1-6
  • Je, Mungu Atahukumu Watu kwa Moto wa Mateso?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Mungu Atahukumu Watu kwa Moto wa Mateso?
  • Je, Mungu Atahukumu Watu kwa Moto wa Mateso?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Fundisho Lisilopatana na Akili
  • Fundisho Hatari
  • Adhabu ya Dhambi Ni Nini?
  • Thawabu kwa Ajili ya Mema
  • Je, Watu Wabaya Watateketezwa Milele?
    Amkeni!—2009
  • Kuchunguza kwa Makini Mapokeo Fulani Kuhusu Kifo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Tunapaswa “Kumjibu Kila Mtu” Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Je, Kweli Kuna Mahali Penye Moto wa Mateso?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Je, Mungu Atahukumu Watu kwa Moto wa Mateso?
T-74 kur. 1-6

Je, Mungu Atahukumu Watu kwa Moto wa Mateso?

Je, umewahi kuona mtu akiteswa? Tunatumaini kwamba hujawahi. Kumtesa mtu kimakusudi ni jambo lenye kuchukiza sana. Hata hivyo, namna gani Mungu mwenyewe kumtesa mtu? Je, kweli anaweza kumtesa mtu? Dini nyingi zinafundisha kwamba Mungu hufanya hivyo.

Hebu wazia jambo hili lenye kuogofya: Mtu anakaangwa kwenye kikaangio chenye moto mkali. Kwa sababu ya maumivu yake makali analia kwa nguvu sana akiomba ahurumiwe, lakini hakuna anayemsikiliza. Anazidi kuteswa, saa baada ya saa, siku nenda siku rudi—mfululizo!

Hata mtu huyo awe amefanya kosa gani, je, hungemsikitikia? Vipi yule aliyeagiza ateswe? Je, kweli ana upendo? Haiwezekani! Mtu mwenye upendo huwa na huruma naye huwasikitikia wengine. Baba mwenye upendo anaweza kuwatia nidhamu watoto wake, lakini hawezi kamwe kuwatesa!

Hata hivyo, dini nyingi hufundisha kwamba Mungu huwatesa watenda-dhambi katika moto wa milele. Tendo hilo linaitwa eti ni hukumu ya Mungu. Ikiwa ni kweli, ni nani basi aliyetengeneza mahali hapo pabaya sana pa mateso ya milele? Na ni nani anayepasa kulaumiwa kwa sababu ya maumivu makali ambayo watu wanapata humo? Basi, majibu pia ni wazi. Ikiwa kuna mahali kama hapo, Mungu ndiye aliyepatengeneza, naye ndiye anayepasa kulaumiwa kwa sababu ya mambo yanayotendeka humo.

Je, unakubaliana na jambo hilo? Bibliaa inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Je, Mungu mwenye upendo anaweza kuwatesa watu kwa njia ambayo hata wanadamu wenyewe wanaiona kuwa yenye kuchukiza sana? Haiwezekani!

Fundisho Lisilopatana na Akili

Hata hivyo, watu wengi wanaamini kwamba waovu wataenda motoni ambapo watateswa milele. Je, fundisho hilo linapatana na akili? Mwanadamu anaweza kuishi miaka 70 au 80. Hata ikiwa mtu alifanya uovu mkubwa sana maisha yake yote, je, angestahili kuteswa milele? Hapana. Haingekuwa haki hata kidogo kumtesa mtu milele kwa sababu ya dhambi alizofanya katika maisha yake mafupi.

Ni nani anayejua ukweli wa mambo kuhusu yanayotupata baada ya kufa? Ni Mungu tu anayeweza kutueleza, naye amefanya hivyo katika Neno lake lililoandikwa, Biblia, iliyotangulia kutajwa. Biblia inasema hivi: “Anavyokufa [mnyama], ndivyo anavyokufa [mwanadamu]; nao wote wana roho moja . . . Wote wanaenda mahali pamoja. Wote wametoka katika mavumbi, nao wote wanarudi mavumbini.” (Mhubiri 3:19, 20) Andiko hilo halitaji moto wa mateso. Wanapokufa, wanadamu hurudi mavumbini katika hali ya kutokuwapo.

Ili mtu ateseke, lazima awe na fahamu. Je, wafu wana fahamu? Hapana. “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe, wala hawana malipo tena, kwa maana kumbukumbu lao limesahauliwa.” (Mhubiri 9:5) Basi, wafu ambao “hawajui lolote kamwe,” hawawezi kupatwa na maumivu makali ya moto wa mateso.

Fundisho Hatari

Watu fulani hudai kwamba fundisho la moto wa mateso, liwe ni la kweli au si la kweli, lina faida. Kwa nini? Wanasema kwamba fundisho hilo huwazuia watu wasifanye makosa. Je, hilo ni kweli? Je, kiwango cha uhalifu katika maeneo ambayo watu wanaamini kwamba kuna moto wa mateso ni cha chini kuliko katika sehemu nyingine? Hata! Kusema kweli, fundisho la moto wa mateso ni fundisho hatari sana. Je, mtu anayeamini kwamba Mungu anawatesa watu atayaona mateso kuwa jambo lenye kuchukiza? Kwa nini aone hivyo? Wale wanaomwamini mungu mkatili mara nyingi huwa wakatili kama mungu wao.

Vyovyote vile, mtu anayetumia akili hawezi kukubali kwamba kuna mahali penye moto wa mateso. Hilo ni jambo lisilopatana na akili hata kidogo. Halipatani kamwe na utu wa kibinadamu. Isitoshe, Neno la Mungu halisemi kwamba kuna mahali kama hapo. Mtu anapokufa, “hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.”—Zaburi 146:4.

Adhabu ya Dhambi Ni Nini?

Je, hilo linamaanisha kwamba hatuadhibiwi kwa sababu ya dhambi zetu? Hapana, sivyo ilivyo. Mungu wetu mtakatifu huwaadhibu watenda-dhambi, lakini hawatesi. Nao watenda-dhambi wanapotubu, yeye huwasamehe. Adhabu ya dhambi ni nini? Biblia inatoa jibu la moja kwa moja: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu. Tunapotenda dhambi hatustahili tena kupata zawadi hiyo, nasi hufa.

Huenda ukauliza: ‘Je, hiyo ni haki kweli? Kwani, kila mtu hufa!’ Hilo ni kweli kwa sababu sisi sote ni watenda-dhambi. Kwa kweli, hakuna yeyote anayestahili kuishi. “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

Huenda kufikia sasa unajiuliza: ‘Ikiwa sisi sote hutenda dhambi, na kwa hiyo sisi sote hufa, kuna haja gani ya kujaribu kuwa wema? Inaonekana kwamba mtu mwovu hutendewa sawasawa na yule anayejitahidi kumtumikia Mungu.’ Lakini sivyo ilivyo. Ingawa sisi sote ni watenda-dhambi, Mungu huwasamehe wale wanaotubu kikweli na kujaribu kubadili mwenendo wao. Yeye hutupa thawabu tunapojitahidi ‘kufanya upya akili zetu’ na kufanya mema. (Waroma 12:2) Kweli hizo hutupa tumaini zuri ajabu.

Thawabu kwa Ajili ya Mema

Tunapokufa huwa hatupo tena. Lakini hilo halimaanishi kwamba huo ndio mwisho wa mambo yote. Ayubu aliyekuwa mwaminifu alijua kwamba angeenda kaburini baada ya kufa. Lakini hebu sikiliza jinsi alivyomwomba Mungu: “Laiti ungenificha katika Kaburi, kwamba ungenificha mpaka hasira yako igeuke, kwamba ungeniwekea kikomo cha wakati na kunikumbuka! Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena? . . . Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu.”—Ayubu 14:13-15.

Ayubu aliamini kwamba ikiwa angekuwa mwaminifu mpaka wakati wa kufa kwake, Mungu angemkumbuka na kumfufua. Hivyo ndivyo watumishi wote wa Mungu wa nyakati za kale walivyoamini. Yesu mwenyewe alithibitisha tumaini hilo aliposema hivi: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.”—Yohana 5:28, 29.

Ufufuo huo utaanza wakati gani? Kulingana na Biblia, utaanza karibuni sana. Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba katika mwaka wa 1914, ulimwengu huu uliingia katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Hivi karibuni, Mungu ataondolea mbali uovu na kuanzisha ulimwengu mpya chini ya utawala wa kimbingu. Watu wengi wanauita wakati huo ‘mwisho wa ulimwengu.’—Mathayo, sura ya 24; Marko, sura ya 13; Luka, sura ya 21; Ufunuo 16:14.

Kisha dunia nzima itakuwa paradiso inayokaliwa na watu ambao walijitahidi kikweli kumtumikia Mungu. Watu waovu hawatateketezwa katika moto, lakini hawatakuwapo katika Paradiso inayokuja. Katika Zaburi 37:10, 11, tunasoma hivi: “Mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”

Je, hayo yote ni ndoto tu? Hapana, ni ahadi ya Mungu. Katika Biblia tunasoma hivi: “Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’”—Ufunuo 21:3, 4.

Je, unaamini maneno hayo? Unapaswa kuyaamini. Neno la Mungu hutimia sikuzote. (Isaya 55:11) Tunakuhimiza ujifunze mengi zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia. Ikiwa ungependa wakusaidie, tafadhali waandikie ukitumia mojawapo ya anwani zilizo hapa chini.

Isipokuwa imeonyeshwa vingine, Maandiko yote yamenukuliwa kutoka katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

[Maelezo ya chini]

a Kulingana na Uislamu, Biblia ina vitabu vinavyoitwa Taurati, Zaburi, na Injili. Angalau aya 64 za Kurani zinasema kwamba vitabu hivyo ni Neno la Mungu, nazo hukazia umuhimu wa kuvisoma na kutekeleza amri zake. Watu fulani hudai kwamba Taurati, Zaburi, na Injili zimepotoshwa. Wale wanaodai hivyo ni kana kwamba wanasema Mungu hawezi kulihifadhi Neno lake mwenyewe.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki