SURA YA SABA
Je, Kuna Mwasi Nyumbani?
1, 2. (a) Yesu alitoa kielezi gani ili kukazia ukosefu wa uaminifu wa viongozi wa kidini Wayahudi? (b) Ni jambo jipi kuhusu wabalehe tuwezalo kujifunza kutokana na kielezi cha Yesu?
SIKU chache kabla ya kifo chake, Yesu aliuliza kikundi cha viongozi Wayahudi swali lenye kuchochea fikira. Alisema hivi: “Nyinyi mwafikiri nini? Mtu alikuwa na watoto wawili. Akimwendea wa kwanza, akasema, ‘Mtoto, nenda kafanye kazi leo katika shamba la mizabibu.’ Kwa kujibu, huyu akasema, ‘Hakika nitakwenda, bwana,’ lakini hakutoka aende. Akimkaribia wa pili, akasema lilelile. Kwa kujibu, huyu akasema, ‘Hakika sitakwenda.’ Baadaye alihisi majuto na kutoka akaenda. Ni yupi wa hao wawili aliyefanya mapenzi ya baba yake?” Viongozi Wayahudi wakajibu: “Huyo wa mwisho.”—Mathayo 21:28-31.
2 Hapa Yesu alikuwa akikazia ukosefu wa uaminifu wa viongozi Wayahudi. Wao walikuwa kama mwana wa kwanza, wakiahidi kufanya mapenzi ya Mungu kisha wakikosa kutimiza ahadi yao. Lakini wazazi wengi watatambua kwamba kielezi cha Yesu kilitegemea uelewevu mzuri wa maisha ya familia. Kama vile alivyoonyesha vema sana, mara nyingi ni jambo gumu kujua yale ambayo vijana wanafikiri au kutabiri lile watakalofanya. Huenda kijana akasababisha matatizo mengi wakati wa ubalehe wake kisha akue akiwa mtu mzima mwenye kuchukua madaraka, anayestahiwa sana. Hili ni jambo la kukumbuka tunapozungumza juu ya tatizo la uasi wa kitineja.
MWASI NI NANI?
3. Kwa nini wazazi wasifanye haraka kumwainisha mtoto wao kuwa mwasi?
3 Mara kwa mara, huenda ukasikia juu ya matineja ambao huasi kabisa dhidi ya wazazi wao. Hata huenda ukajua kibinafsi juu ya familia ambayo katika hiyo tineja anaonekana kuwa asiyeweza kudhibitiwa. Hata hivyo, si jambo rahisi sikuzote kujua kama mtoto kwa kweli ni mwasi. Zaidi ya hayo, huenda ikawa jambo gumu kuelewa ni kwa nini watoto wengine huasi na wengine—hata katika nyumba iyo hiyo—hawaasi. Wazazi wakishuku kwamba huenda mmoja wa watoto wao akawa anasitawika kuwa mwasi kabisa, wao wanapaswa kufanya nini? Ili kujibu hilo, ni lazima kwanza tuongee kuhusu ni nani aliye mwasi.
4-6. (a) Mwasi ni nani? (b) Wazazi wakumbuke nini ikiwa mara kwa mara tineja wao anakosa?
4 Kwa kusema kisahili, mwasi ni mtu anayekosa kutii kimakusudi na bila kubadilika au anayekinza na kukaidi mamlaka iliyo juu zaidi. Bila shaka, ‘upumbavu umefungwa ndani ya moyo wa mtoto.’ (Mithali 22:15) Kwa hiyo watoto wote hukinza mamlaka ya wazazi na ya wengine wakati mmoja au mwingine. Hili liko hivyo hasa katika wakati wa ukuzi wa kimwili na wa kihisia-moyo unaoitwa ubalehe. Badiliko katika maisha ya mtu yeyote yule litasababisha mkazo, na ubalehe ni wakati wa mabadiliko mengi. Mwana au binti yako tineja anatoka utoto na kuingia barabara inayoelekea kwenye utu mzima. Kwa sababu hiyo, katika miaka ya ubalehe, wazazi na watoto wengine huwa na wakati mgumu kupatana. Mara nyingi wazazi hujaribu kisilika kupunguza mwendo wa badiliko hilo, huku matineja hutaka kuongeza mwendo wa badiliko hilo.
5 Tineja aliye mwasi hukataa katakata kanuni za wazazi. Lakini, kumbuka kwamba vitendo vichache vya kutokutii havimfanyi mtu awe mwasi. Na kwa habari ya mambo ya kiroho, huenda watoto fulani mwanzoni wakaonyesha kupendezwa kidogo au wasionyeshe kupendezwa na kweli ya Biblia, lakini huenda wasiwe waasi. Ukiwa mzazi, usifanye haraka kumwainisha mtoto wako kuwa mwasi.
6 Je, miaka ya ubalehe ya vijana wote ni yenye uasi dhidi ya mamlaka ya wazazi? La, hasha. Kwa kweli, uthibitisho ungeonekana kuonyesha kwamba ni matineja wachache tu ambao huonyesha uasi mzito wa ubalehe. Bado, namna gani mtoto anayeasi kwa ushupavu na bila kubadilika? Ni mambo gani huenda yakachochea uasi huo?
MAMBO YANAYOSABABISHA UASI
7. Mazingira ya kishetani yanaweza kumvutaje mtoto aasi?
7 Jambo kuu linalosababisha uasi ni mazingira ya kishetani ya ulimwengu. “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Ulimwengu uliomo katika nguvu ya Shetani umesitawisha utamaduni wenye kudhuru ambao ni lazima Wakristo washindane nao. (Yohana 17:15) Sehemu kubwa ya utamaduni huo ni wenye kukosa adhabu zaidi, wenye hatari zaidi, na wenye kujaa mavutano mabaya zaidi leo kuliko wakati uliopita. (2 Timotheo 3:1-5, 13) Wazazi wasipoelimisha, wasipoonya, na wasipolinda watoto wao, vijana wanaweza kushindwa kwa urahisi na “roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” (Waefeso 2:2) Jambo linalohusiana na hili ni msongo wa marika. Biblia husema: “Rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Vivyo hivyo, yeye anayeendelea kushirikiana na wale waliojaa roho ya ulimwengu huu anaelekea kuvutwa na roho hiyo. Vijana hutaka msaada wa daima ikiwa watathamini kwamba kutii kanuni za kimungu ndio msingi wa maisha yaliyo bora kabisa.—Isaya 48:17, 18.
8. Ni mambo gani ambayo huenda yakaongoza mtoto kwenye uasi?
8 Jambo jingine linalosababisha uasi huenda likawa hali ya nyumbani. Kwa kielelezo, ikiwa mzazi mmoja ni mraibu wa alkoholi, hutumia vibaya madawa, au ni mjeuri kuelekea mzazi yule mwingine, maoni ya tineja juu ya maisha yanaweza kupotoshwa. Hata katika nyumba zilizo tulivu kwa kulinganishwa, uasi unaweza kutokea wakati mtoto anapohisi kwamba wazazi wake hawapendezwi naye. Hata hivyo, uasi wa kitineja hausababishwi sikuzote na mavutano ya nje. Watoto fulani hukataa katakata kanuni za wazazi wajapokuwa na wazazi wanaotumia kanuni za kimungu na ambao huwakinga, kwa kadiri kubwa, na ulimwengu unaowazunguka. Kwa nini? Labda kwa sababu ya mzizi mwingine wa matatizo yetu—kutokamilika kwa kibinadamu. Paulo alisema hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Adamu alikuwa mwasi mwenye ubinafsi, naye aliwaachia wazao wake wote urithi mbaya. Vijana fulani huchagua kuasi tu, kama vile babu yao alivyofanya.
ELI MWENYE UENDEKEVU NA REHOBOAMU MWENYE UZUIFU
9. Ni njia gani zenye kupita kiasi katika kumlea mtoto ambazo huenda zikamchochea mtoto aasi?
9 Jambo jingine ambalo limeongoza kwenye uasi wa kitineja ni maoni yasiyo na usawaziko juu ya kulea mtoto kwa upande wa wazazi. (Wakolosai 3:21) Wazazi fulani wenye kudhamiria huwazuia na kuwatia watoto wao nidhamu kwa ukali. Wengine ni wenye uendekevu, wakikosa kuandaa miongozo ambayo ingemlinda mbalehe wao asiye na uzoefu. Si rahisi sikuzote kuwa na usawaziko kati ya njia hizo mbili zenye kupita kiasi. Na watoto tofauti wana mahitaji tofauti. Huenda mmoja akahitaji kuangaliwa zaidi kuliko mwingine. Bado, vielelezo viwili vya Biblia vitasaidia kuonyesha hatari za kuwa wenye kupita kiasi ama kwa habari ya uzuifu ama uendekevu.
10. Kwa nini Eli, ingawa yaelekea alikuwa kuhani mwaminifu wa cheo cha juu, alikuwa mzazi asiyefaa?
10 Eli kuhani wa cheo cha juu wa Israeli la kale alikuwa baba. Alitumikia kwa miaka 40, bila shaka akiwa na ujuzi sana wa Sheria ya Mungu. Yaelekea Eli alifanya wajibu wake wa kawaida wa kikuhani kwa uaminifu sana na hata huenda akawa aliwafundisha kikamili wana wake, Hofni na Finehasi, Sheria ya Mungu. Hata hivyo, Eli alikuwa mwenye kubembeleza sana wana wake. Hofni na Finehasi walitumikia wakiwa makuhani wenye kufanya kazi rasmi, lakini walikuwa “watu wasiofaa kitu,” wenye kupendezwa tu na kuridhisha hamu zao na tamaa zao zisizo za adili. Hata hivyo, walipofanya vitendo vya fedheha kwenye kiwanja kitakatifu, Eli hakuwa na moyo mkuu wa kuwaondosha wasiwe makuhani tena. Aliwapa karipio tu lisilo na nguvu. Kwa uendekevu wake, Eli aliwaheshimu wana wake zaidi ya Mungu. Likiwa tokeo, wana wake waliasi dhidi ya ibada safi ya Yehova na nyumba yote ya Eli ilipatwa na msiba.—1 Samweli 2:12-17, 22-25, 29; 3:13, 14; 4:11-22.
11. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo kibaya cha Eli?
11 Watoto wa Eli walikuwa watu wazima tayari wakati mambo hayo yalipotendeka, lakini historia hii inakazia hatari ya kunyima nidhamu. (Linganisha Mithali 29:21.) Huenda wazazi fulani wakadhani uendekevu ndio upendo, wakishindwa kuweka na kutekeleza amri zilizo wazi, zenye upatano, na zinazofaa. Wanapuuza kutumia nidhamu yenye upendo, hata wakati kanuni za kimungu zinapovunjwa. Kwa sababu ya uendekevu huo, huenda watoto wao wakakosa hatimaye kuelekeza uangalifu kwenye mamlaka ya wazazi au ya aina yoyote nyingineyo.—Linganisha Mhubiri 8:11.
12. Rehoboamu alifanya kosa gani katika kutumia mamlaka?
12 Rehoboamu huonyesha kielelezo cha njia ile nyingine ya kupita kiasi katika kutumia mamlaka. Yeye alikuwa mfalme wa mwisho wa ufalme wa Israeli uliounganika, lakini yeye hakuwa mfalme mwema. Rehoboamu alikuwa amerithi nchi ambayo watu wayo hawakuwa na uradhi kwa sababu ya mizigo yenye kulemea waliyowekewa na babake, Sulemani. Je, Rehoboamu alionyesha uelewevu? La. Kikundi cha wajumbe kilipomwomba aondoe baadhi ya hiyo mizigo yenye uonevu, yeye alishindwa kutii shauri lenye ukomavu kutoka kwa washauri wake wenye umri mkubwa zaidi naye akaamuru kwamba nira ya watu hao ifanywe kuwa nzito zaidi. Kiburi chake kilichochea uasi wa yale makabila kumi ya kaskazini, na ufalme huo ukagawanywa mara mbili.—1 Wafalme 12:1-21; 2 Mambo ya Nyakati 10:19.
13. Wazazi wanaweza kuepukaje kosa la Rehoboamu?
13 Wazazi wanaweza kujifunza baadhi ya masomo ya maana kutokana na usimulizi wa Biblia juu ya Rehoboamu. Wao wanahitaji ‘kumtafuta Yehova’ katika sala na kuchunguza njia zao za kulea watoto kupatana na kanuni za Biblia. (Zaburi 105:4) “Jeuri [“uonevu wenyewe,” NW] humpumbaza mwenye hekima,” yasema Mhubiri 7:7. Mipaka iliyofikiriwa vizuri huwapa wabalehe nafasi ya kukua huku ikiwalinda dhidi ya madhara. Lakini watoto hawapaswi waishi katika hali iliyo ngumu na yenye kubana mno hivi kwamba wanazuiwa wasisitawishe kiasi kifaacho cha kujitegemea na kujitumaini. Wazazi wanapojaribu kupata usawaziko kati ya uhuru wa kiasi na mipaka imara iliyofafanuliwa kwa wazi, matineja walio wengi hawataelekea sana kuasi.
KUTIMIZA MAHITAJI YA MSINGI KWAWEZA KUZUIA UASI
Yaelekea, watoto watakua wawe wenye uthabiti zaidi ikiwa wazazi wao wanawasaidia wakabiliane na matatizo yao ya utineja
14, 15. Wazazi waoneje ukuzi wa mtoto wao?
14 Ingawa wazazi hushangilia wanapoona kijana wao akikua kimwili kutoka utoto hadi utu mzima, huenda wakahisi kusumbuka wakati mtoto wao mbalehe anapoanza kutoka katika hali ya kutegemea wengine hadi hali ya kujitegemea ifaavyo. Katika kipindi hiki cha badiliko, usishangae ikiwa pindi fulani-fulani tineja wako anakuwa kidogo mshupavu au si mwenye ushirikiano. Kumbuka kwamba lengo la wazazi Wakristo linapaswa kuwa kumlea Mkristo mkomavu, aliye thabiti, na mwenye kuchukua madaraka.—Linganisha 1 Wakorintho 13:11; Waefeso 4:13, 14.
15 Hata liwe ni jambo gumu jinsi gani, wazazi wanahitaji kuvunja tabia ya kukataa ombi lolote kutoka kwa mbalehe wao la kutaka kujitegemea zaidi. Mtoto anahitaji kukua awe mtu binafsi, kwa njia bora. Kwa kweli, kuanzia umri mchanga kwa kulinganishwa, matineja fulani huanza kusitawisha mtazamo wa utu mzima sana. Kwa kielelezo, Biblia husema juu ya Mfalme mchanga Yosia: “Naye akali mchanga [wa umri wa miaka 15], alianza kumtafuta Mungu wa Daudi.” Tineja huyu mwenye kutokeza alikuwa kwa wazi mtu mwenye kuchukua madaraka.—2 Mambo ya Nyakati 34:1-3.
16. Watoto wapewapo madaraka ya kuongezeka, ni lazima wang’amue nini?
16 Hata hivyo, uhuru huleta daraka la kutoa hesabu. Kwa hiyo, mruhusu kijana wako anayetokea kuwa mtu mzima aone matokeo ya baadhi ya maamuzi na hatua zake. Kanuni hii “lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia,” inahusu matineja na pia watu wazima. (Wagalatia 6:7) Watoto hawawezi kukingwa milele. Lakini, namna gani ikiwa mtoto wako ataka kufanya jambo fulani lisilokubalika kabisa? Ukiwa mzazi mwenye kuchukua madaraka, ni lazima useme, “La.” Na, ingawa huenda ukazieleza sababu, kusiwe na sababu ya kubadili la yako iwe ndiyo. (Linganisha Mathayo 5:37.) Hata hivyo, jaribu kusema “La” kwa njia yenye utulivu na ya kiasi, kwa maana “jawabu la upole hugeuza hasira.”—Mithali 15:1.
17. Ni nini baadhi ya mahitaji ya tineja ambayo mzazi apaswa kutimiza?
17 Vijana wahitaji usalama wa nidhamu isiyo na ugeugeu hata ikiwa hawakubaliani kwa utayari sikuzote na vizuizi na amri. Ni jambo la kufadhaisha ikiwa amri zinabadilishwa mara nyingi, ikitegemea njia ambayo mzazi anahisi wakati huo. Zaidi, matineja wakipokea kitia-moyo na msaada, kama uhitajiwavyo, katika kukabiliana na hali ya kuwa na shaka, haya, au ukosefu wa kujitumaini, yaelekea wao watakua wawe wenye uthabiti zaidi. Matineja huthamini pia wanapopokea hali ya kutumainiwa ambayo wamechuma.—Linganisha Isaya 35:3, 4; Luka 16:10; 19:17.
18. Ni nini baadhi ya kweli zenye kutia moyo kuhusu matineja?
18 Wazazi wanaweza kufarijiwa kwa kujua kwamba amani, uthabiti, na upendo unapokuwako katika nyumba, kwa kawaida watoto husitawi. (Waefeso 4:31, 32; Yakobo 3:17, 18) Kwa kweli, vijana wengi wameshinda hata mazingira mabaya ya nyumbani, wakiwa wametoka katika familia zenye uraibu wa alkoholi, ujeuri, au uvutano mwingine wenye kudhuru, nao wamekua wakawa watu wazima walio wazuri. Kwa sababu hiyo, ukiandaa nyumba ambako matineja wako wanahisi usalama na wanajua kwamba watapokea upendo, shauku, na uangalifu—hata ikiwa utegemezo huo unafuatana na vizuizi vifaavyo na nidhamu inayopatana na kanuni za Kimaandiko—wanaelekea sana kukua wawe watu wazima utakaoonea fahari.—Linganisha Mithali 27:11.
WATOTO WAINGIAPO HALI NGUMU
19. Ingawa wazazi wapaswa kuzoeza mvulana katika njia apaswaye kwenda, mtoto anakuwa na daraka gani?
19 Kwa hakika kuwa wazazi wema kunaleta matokeo ya maana. Mithali 22:6 yasema: “Mlee mtoto [“zoeza mvulana,” NW] katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” Hata hivyo, namna gani watoto walio na matatizo mazito ijapokuwa wana wazazi wema? Je, hili lawezekana? Ndiyo. Lazima maneno ya mithali yaeleweke kulingana na mistari mingine inayokazia daraka la mtoto ‘kusikiliza’ na kutii wazazi. (Mithali 1:8) Ni lazima mzazi na mtoto pia washirikiane katika kutumia kanuni za Kimaandiko ikiwa kutakuwa na upatano katika familia. Wazazi na watoto wasipofanya kazi pamoja, kutakuwa na magumu.
20. Watoto wanapokosea kwa sababu ya kutofikiri, ni njia gani ambayo ingekuwa yenye hekima kwa wazazi kufuata?
20 Wazazi waitikieje wakati tineja anapokosea na kuingia taabani? Ndipo, kijana anapohitaji hasa msaada. Wazazi wakikumbuka kwamba wanashughulikia kijana asiye na uzoefu, wao watakinza kwa urahisi zaidi mwelekeo wa kuitikia kwa njia ya kupita kiasi. Paulo alishauri watu wakomavu kutanikoni hivi: “Hata ingawa mtu achukua hatua fulani isiyo ya kweli kabla ya yeye kuijua, nyinyi mlio na sifa za ustahili wa kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole.” (Wagalatia 6:1) Wazazi wanaweza kufuata utaratibu huohuo wanaposhughulika na kijana anayefanya kosa kwa sababu ya kutofikiri. Huku wakieleza kwa wazi kwa nini mwenendo wake ulikuwa mbaya na jinsi awezavyo kuepuka kurudia hilo kosa, ni lazima wazazi waeleweshe wazi kwamba ni mwenendo huo wenye kosa ulio mbaya, si kijana.—Linganisha Yuda 22, 23.
21. Kwa kufuata kielelezo cha kutaniko la Kikristo, wazazi wapaswa waitikieje watoto wao wakifanya dhambi nzito?
21 Namna gani ikiwa uhalifu wa kijana ni mzito sana? Katika hali hiyo mtoto anahitaji msaada wa pekee na mwelekezo wenye ustadi. Mshiriki wa kutaniko anapofanya dhambi nzito, anatiwa moyo atubu na kuwaendea wazee ili apate msaada. (Yakobo 5:14-16) Mara anapotubu, wazee hufanya kazi naye ili kumponya kiroho. Katika familia daraka la kumsaidia tineja ambaye amekosa ni la wazazi, ingawa huenda wakahitaji kulizungumza jambo pamoja na wazee. Bila shaka wao hawapaswi kujaribu kuficha baraza la wazee dhambi zozote nzito zilizofanywa na mmoja wa watoto wao.
22. Kwa kumwiga Yehova, wazazi watajaribu kudumisha mtazamo gani mtoto wao akifanya kosa zito?
22 Tatizo zito linalohusisha watoto wa mtu mwenyewe ni gumu sana. Wakiwa wamefadhaika kihisia-moyo, huenda wazazi wakahisi kumtisha kwa hasira mtoto mkaidi; lakini hili huenda likamtia tu uchungu. Kumbuka kwamba wakati ujao wa kijana huyu huenda ukategemea jinsi anavyotendewa katika wakati huu mgumu. Kumbuka pia, kwamba Yehova alikuwa tayari kusamehe wakati watu wake walipoacha njia iliyo sawa—ikiwa tu wangetubu. Sikiliza maneno yake yenye upendo: “Haya, njoni, tusemezane, asema BWANA. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.” (Isaya 1:18) Hicho ni kielelezo bora kama nini kwa wazazi!
23. Kunapokuwa na dhambi nzito ambayo mmoja wa watoto wao amefanya, wazazi watendeje, nao waepuke nini?
23 Kwa hiyo, jaribu kumtia moyo yule aliye mkaidi abadili mwendo wake. Tafuta shauri timamu kutoka kwa wazazi wenye uzoefu na wazee wa kutaniko. (Mithali 11:14) Jaribu kutotenda kwa misukumo tu na kusema au kufanya mambo ambayo yangefanya iwe vigumu kwa mtoto wako kurudi kwako. Epuka hasira na uchungu usiodhibitiwa. (Wakolosai 3:8) Usikate tamaa upesi. (1 Wakorintho 13:4, 7) Huku ukichukia ubaya, epuka kuwa mgumu na mwenye uchungu kuelekea mtoto wako. La maana zaidi, wazazi wapaswa wajitahidi kuweka kielelezo bora na kuweka imani yao katika Mungu ikiwa imara.
KUMSHUGHULIKIA MWASI ALIYEAZIMIA
24. Ni hali gani yenye kuhuzunisha ambayo nyakati nyingine hutokea katika familia ya Kikristo, na mzazi aitikieje?
24 Katika visa fulani huwa wazi kwamba kijana amefanya uamuzi dhahiri kuasi na kukataa katakata kanuni za Kikristo. Basi jambo lipaswalo kukaziwa sasa ni kudumisha au kujenga upya maisha ya familia ya wale wanaosalia. Uwe mwangalifu kwamba huelekezi nishati zako zote kwa mwasi, hivyo ukipuuza wale watoto wengine. Badala ya kujaribu kuficha wengine wa familia tatizo hilo, lizungumze hilo pamoja nao kwa kadiri inayofaa na kwa njia ya kuhakikishia.—Linganisha Mithali 20:18.
25. (a) Kwa kufuata kiolezo cha kutaniko la Kikristo, huenda wazazi wakahitaji kuchukua hatua gani ikiwa mtoto anakuwa mwasi mwenye kuazimia? (b) Wazazi wakumbuke nini ikiwa mmoja wa watoto wao aasi?
25 Mtume Yohana alisema hivi juu ya mmoja anayekuwa mwasi asiyeweza kurekebishwa katika kutaniko: “Msimpokee kamwe nyumbani mwenu wala kusema salamu kwake.” (2 Yohana 10) Huenda wazazi wakahisi ni lazima kumchukulia mtoto wao wenyewe hatua kama hiyo, ikiwa ni wa umri wa kutosha kisheria na amekuwa mwasi kabisa. Ingawa hatua hiyo huenda ikawa ngumu na ya kuumiza, ni ya muhimu nyakati nyingine ili kulinda wengine wa familia. Nyumba yako inahitaji ulinzi na usimamizi wenye kuendelea. Kwa hiyo, endelea kudumisha mipaka ya mwendo iliyofafanuliwa wazi, na bado yenye kiasi. Wasiliana na wale watoto wengine. Pendezwa na jinsi wanavyofanya shuleni na kutanikoni. Pia, waache wajue kwamba ingawa hukubaliani na matendo ya yule mtoto mwasi, wewe humchukii. Laumu lile tendo baya badala ya yule mtoto. Wana wawili wa Yakobo walipoiletea familia fedheha kwa sababu ya tendo lao katili, Yakobo alilaani hasira yao jeuri, si wana wenyewe.—Mwanzo 34:1-31; 49:5-7.
26. Wazazi wenye kudhamiria wanaweza kupata faraja kutokana na nini ikiwa mmoja wa watoto wao aasi?
26 Huenda ukahisi una daraka kwa lile ambalo limetendeka katika familia yako. Lakini ikiwa umefanya yote uwezavyo kwa sala, ukifuata shauri la Yehova vema kadiri ulivyoweza, hakuna uhitaji wa kujichambua isivyofaa. Farijiwa na uhakika wa kwamba hakuna awezaye kuwa mzazi mkamilifu, lakini ulijaribu kwa kudhamiria kuwa mzazi mwema. (Linganisha Matendo 20:26.) Kuwa na mwasi kabisa katika familia ni jambo la kuvunja moyo, lakini iwapo jambo hilo lakupata, uwe na uhakikishio kwamba Mungu anaelewa naye hatawaacha mbali kamwe watumishi wake wenye kujitoa. (Zaburi 27:10) Kwa hiyo azimia kuweka nyumba yako ikiwa mahali salama, pa kiroho kwa watoto wanaosalia.
27. Wakikumbuka mfano wa mwana mpotevu, wazazi wa mtoto mwasi wanaweza kutumaini nini sikuzote?
27 Zaidi ya hayo, hupaswi kamwe kukata tumaini. Jitihada zako za hapo awali katika mazoezi yafaayo huenda hatimaye zikavuta moyo wa mtoto anayepotea na kumfanya arudie akili zake timamu. (Mhubiri 11:6) Familia nyingine kadhaa za Kikristo zimekuwa na ono lilo hilo kama wewe, na zimeona watoto wazo wakaidi wakirudi, sawa na alivyoona yule baba katika mfano wa Yesu wa mwana mpotevu. (Luka 15:11-32) Huenda wewe ukaona jambo lilo hilo.