Somo la 1
Jinsi Unavyoweza Kujua Yale Ambayo Mungu Anataka
Ni habari gani ya maana iliyomo katika Biblia? (1)
Mtungaji wa Biblia ni nani? (2)
Kwa nini ujifunze Biblia? (3)
1. Biblia ni zawadi yenye thamani sana kutoka kwa Mungu. Ni kama barua kutoka kwa baba mwenye upendo kwa watoto wake. Hiyo hutuambia kweli kumhusu Mungu—yeye ni nani na viwango vyake ni nini. Hueleza jinsi ya kukabiliana na matatizo na jinsi ya kupata furaha ya kweli. Biblia pekee hutuambia kile ambacho ni lazima tufanye ili kumpendeza Mungu.—Zaburi 1:1-3; Isaya 48:17, 18.
2. Biblia iliandikwa na watu tofauti-tofauti wapatao 40 kwa kipindi cha miaka 1,600, kuanzia 1513 K.W.K. Imefanyizwa kwa vitabu vidogo 66. Wale walioandika Biblia walipuliziwa na Mungu. Waliandika mawazo yake, si yao wenyewe. Kwa hiyo Mungu aliye mbinguni ndiye Mtungaji wa Biblia, si binadamu yeyote duniani.—2 Timotheo 3:16, 17; 2 Petro 1:20, 21.
3. Mungu alihakikisha kwamba Biblia ilinakiliwa kwa usahihi na kuhifadhiwa. Biblia zaidi zimechapwa kuliko kitabu kingine chochote. Si kila mtu atakayefurahi kukuona ukijifunza Biblia, lakini usiruhusu hilo likuzuie. Wakati ujao wako wa milele wategemea kupata kwako kumjua Mungu na kufanya mapenzi yake ujapokuwa upinzani wowote.—Mathayo 5:10-12; Yohana 17:3.