Somo la 2
Mungu Ni Nani?
Mungu wa kweli ni nani, na jina lake ni nani? (1, 2)
Yeye ana mwili wa aina gani? (3)
Ni zipi zilizo sifa zake zenye kutokeza? (4)
Je, tutumie sanamu na mifano katika kumwabudu? (5)
Ni njia gani mbili ambazo twaweza kujifunza kumhusu Mungu? (6)
1. Watu huabudu vitu vingi. Lakini Biblia hutuambia kwamba kuna Mungu mmoja tu wa KWELI. Yeye aliumba kila kitu mbinguni na duniani. Kwa sababu alitupa sisi uhai, yeye ndiye Mmoja pekee ambaye twapaswa kuabudu.—1 Wakorintho 8:5, 6; Ufunuo 4:11.
2. Mungu ana majina mengi ya cheo lakini ana jina moja tu. Jina hilo ni YEHOVA. Katika Biblia zilizo nyingi, jina la Mungu limeondolewa na mahali palo pamechukuliwa na majina ya cheo BWANA au MUNGU. Lakini Biblia ilipoandikwa, jina Yehova lilipatikana ndani yayo karibu mara 7,000!—Kutoka 3:15; Zaburi 83:18.
3. Yehova ana mwili, lakini huo si kama wetu. “Mungu ni Roho,” Biblia husema. (Yohana 4:24) Roho ni namna ya uhai iliyo bora zaidi ya yetu. Hakuna binadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote. Yehova huishi mbinguni, lakini aweza kuona vitu vyote. (Zaburi 11:4, 5; Yohana 1:18) Lakini, roho takatifu ni nini? Hiyo si mtu kama vile Mungu. Badala ya hivyo, hiyo ni kani ya utendaji ya Mungu.—Zaburi 104:30.
4. Biblia hutufunulia utu wa Yehova. Hiyo hutuonyesha kwamba sifa zake zenye kutokeza ni upendo, haki, hekima, na nguvu. (Kumbukumbu la Torati 32:4; Ayubu 12:13; Isaya 40:26; 1 Yohana 4:8) Biblia hutuambia kwamba yeye pia ni mwenye rehema, mwenye fadhili, mwenye kusamehe, mkarimu, na mwenye subira. Sisi, tukiwa kama watoto watiifu, twapaswa tujaribu kumwiga.—Waefeso 5:1, 2.
5. Je, tuinamie au kusali kuelekea sanamu, picha, au mifano katika ibada yetu? La! (Kutoka 20:4, 5) Yehova asema kwamba ni lazima tumwabudu yeye pekee. Yeye hatashiriki utukufu wake pamoja na yeyote mwingine au chochote kingine. Sanamu hazina nguvu za kutusaidia.—Zaburi 115:4-8; Isaya 42:8.
6. Twaweza kupataje kumjua Mungu vizuri zaidi? Njia moja ni kwa kuchunguza vitu ambavyo yeye ameumba na kufikiria sana yale ambayo hivyo hutuambia. Viumbe vya Mungu hutuonyesha kwamba yeye ana nguvu na hekima nyingi. Twaona upendo wake katika vyote ambavyo yeye ameumba. (Zaburi 19:1-6; Warumi 1:20) Njia nyingine ambayo twaweza kujifunza kumhusu Mungu ni kwa kujifunza Biblia. Katika hiyo yeye hutuambia mengi zaidi kuhusu Mungu ni wa aina gani. Yeye hutuambia pia kuhusu makusudi yake na yale ambayo anataka tufanye.—Amosi 3:7; 2 Timotheo 3:16, 17.
Pictures katika ukurasa wa 5]
Twajifunza kumhusu Mungu kutoka uumbaji na kutoka Biblia