Somo la 4
Ibilisi Ni Nani?
Shetani Ibilisi—alitoka wapi? (1, 2)
Shetani huwaongozaje watu vibaya? (3-7)
Kwa nini umkinze Ibilisi? (7)
1. Neno “ibilisi” lamaanisha mtu asemaye uwongo mbaya sana kumhusu mtu mwingine. “Shetani” lamaanisha adui au mpinzani. Haya ni majina aliyopewa adui mkuu wa Mungu. Hapo kwanza, alikuwa malaika mkamilifu mbinguni pamoja na Mungu. Hata hivyo, baadaye, alijiona sana akataka ibada iliyo milki ya Mungu kwa haki.—Mathayo 4:8-10.
2. Malaika huyo, Shetani, aliongea na Hawa kupitia nyoka. Kwa kumwambia uwongo, alimfanya mwanamke huyo asimtii Mungu. Hivyo Shetani alishambulia kile kiitwacho “enzi kuu” ya Mungu, au cheo akiwa Aliye Juu Zaidi Sana. Shetani alitia shaka kama Mungu hutawala kwa njia inayostahili na kwa faida kamili ya raia Zake. Shetani alitia shaka pia kama binadamu yeyote angeweza kuendelea akiwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Mungu. Kwa kufanya hivyo, Shetani alijifanya mwenyewe adui wa Mungu. Hiyo ndiyo sababu alikuja kuitwa Shetani Ibilisi.—Mwanzo 3:1-5; Ayubu 1:8-11; Ufunuo 12:9.
3. Shetani hujaribu kudanganya watu ili wamwabudu yeye. (2 Wakorintho 11:3, 14) Njia moja ambayo yeye huongoza watu vibaya ni kupitia dini bandia. Dini ikifundisha uwongo kumhusu Mungu, hiyo kwa kweli hutumikia kusudi la Shetani. (Yohana 8:44) Huenda watu ambao ni washiriki wa dini bandia wakaamini kwa moyo mweupe kwamba wanamwabudu Mungu wa kweli. Lakini kwa kweli wanamtumikia Shetani. Yeye ni ‘mungu wa ulimwengu huu.’—2 Wakorintho 4:4.
4. Uwasiliani-roho ni njia nyingine ambayo Shetani huleta watu chini ya nguvu zake. Huenda wakaomba roho hao wawalinde, wawadhuru wengine, watabiri wakati ujao, au wafanye miujiza. Shetani ndiye kani yenye uovu inayotokeza mazoea haya. Ili kumpendeza Mungu, ni lazima tusihusike hata kidogo na uwasiliani-roho.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Matendo 19:18, 19.
5. Shetani pia huwaongoza watu vibaya kupitia kiburi cha kupita kiasi cha kuwa wa jamii fulani na ibada ya matengenezo ya kisiasa. Wengine huhisi kwamba taifa au jamii yao ni bora kuliko ya wengine. Lakini hiyo si kweli. (Matendo 10:34, 35) Watu wengine hutazamia matengenezo ya kisiasa yasuluhishe matatizo ya binadamu. Kwa kufanya hivi, wanakataa katakata Ufalme wa Mungu. Huo ndio suluhisho pekee la matatizo yetu.—Danieli 2:44.
6. Njia nyingine ambayo Shetani huongoza watu vibaya ni kwa kuwashawishi na tamaa zenye dhambi. Yehova hutuambia tuepuke mazoea yenye dhambi kwa sababu yeye ajua yatatudhuru. (Wagalatia 6:7, 8) Huenda watu wengine wakakutaka ujiunge nao katika mazoea hayo. Lakini, kumbuka kwamba ni Shetani kwa kweli ambaye akutaka uyafanye mambo haya.—1 Wakorintho 6:9, 10; 15:33.
7. Huenda Shetani akatumia mnyanyaso au upinzani ili akufanye umwache Yehova. Huenda baadhi ya wapendwa wako wakakasirika sana kwa sababu unajifunza Biblia. Huenda wengine wakakudhihaki. Lakini una deni kwa nani la uhai wako? Shetani ataka kukuogopesha ili uache kujifunza kumhusu Yehova. Usimruhusu Shetani ashinde! (Mathayo 10:34-39; 1 Petro 5:8, 9) Kwa kumkinza Ibilisi, unaweza kumfurahisha Yehova na kuonyesha kwamba waunga mkono enzi kuu Yake.—Mithali 27:11.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Dini bandia, uwasiliani-roho, na utukuzo wa taifa, huongoza watu vibaya
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mkinze Shetani kwa kuendelea kujifunza kumhusu Yehova