Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ba kur. 4-5
  • Kitabu Kinachowakilishwa Vibaya

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu Kinachowakilishwa Vibaya
  • Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kupata Maana ya Kweli ya Mafungu ya Kibiblia
  • Kuwakilishwa Vibaya na Dini
  • “Hata Hivyo Imo Katika Mwendo!”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Galileo
    Amkeni!—2015
  • Mgogoro Kati ya Galileo na Kanisa
    Amkeni!—2003
  • Sayansi na Dini Mwanzo wa Ubishi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
Pata Habari Zaidi
Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote
ba kur. 4-5

Kitabu Kinachowakilishwa Vibaya

“Fundisho la mwendo maradufu wa dunia izungukapo mhimili wayo na izungukapo jua si la kweli, na lapinga kabisa Maandiko Matakatifu.” Ndivyo lilivyotaarifu baraza liitwalo Congregation of the Index la Kanisa Katoliki ya Kiroma katika amri ya mwaka wa 1616.1 Je, kwa kweli Biblia hupinga mambo ya hakika ya kisayansi? Au imewakilishwa vibaya?

KATIKA majira ya baridi kali ya mwaka wa 1609/1610, Galileo Galilei aligeuza kuelekea mbingu darubini-upeo yake iliyotoka tu kufanyiwa maendeleo, naye akavumbua miezi minne ya angani ikizunguka sayari Sumbula. Kile alichoona kilidhoofisha kabisa dhana iliyoenea ya kwamba lazima magimba yote ya kimbingu yaizunguke dunia. Mapema, mwaka wa 1543, mwastronomia wa Poland Nicolaus Copernicus alikuwa ametoa nadharia ya kwamba sayari zinalizunguka jua. Galileo alithibitisha kwamba hiyo ilikuwa kweli ya kisayansi.

Hata hivyo, kwa wanatheolojia Wakatoliki, maoni hayo yalikuwa uzushi. Hilo kanisa lilikuwa limeamini kwa muda mrefu kwamba dunia ilikuwa kitovu cha ulimwengu wote mzima.2 Maoni hayo yalitegemea fasiri halisi ya maandiko yaliyoonyesha dunia kuwa imewekwa imara “juu ya misingi yake, ili isitikisike milele.” (Zaburi 104:5, Biblia Habari Njema) Akiwa ameitwa aende Roma, Galileo alifika mbele ya Baraza la Kuhukumu Wazushi. Kwa kuhojiwa chini ya hali ngumu, alilazimishwa aache mambo yote aliyokuwa amevumbua, na alitumia sehemu iliyobaki ya maisha yake akiwa amezuiliwa nyumbani.

Mwaka wa 1992, miaka ipatayo 350 baada ya kifo cha Galileo, Kanisa Katoliki lilikiri hatimaye kwamba kumbe alikuwa amesema kweli.3 Lakini ikiwa Galileo alikuwa amesema kweli, je, Biblia ilikuwa imekosea?

Kupata Maana ya Kweli ya Mafungu ya Kibiblia

Galileo aliamini Biblia kuwa kweli. Uvumbuzi wake wa kisayansi ulipopinga fasiri iliyoenea ya mistari fulani ya Biblia, alisababu kwamba wanatheolojia walikuwa wakikosa maana ya kweli ya hayo mafungu. Kwa vyovyote, “kweli mbili haziwezi kupingana kamwe,” akaandika.4 Alidokeza kwamba maneno dhahiri ya sayansi hayapingi maneno ya kila siku ya Biblia. Lakini wanatheolojia hawakuweza kujiruhusu washawishike. Walisisitiza kwamba taarifa zote za Kibiblia juu ya dunia zapasa kuchukuliwa kihalisi. Tokeo ni kwamba, hawakukataa tu uvumbuzi mbalimbali wa Galileo bali pia walikosa maana ya kweli ya maneno hayo ya Kimaandiko.

Kwa kweli, akili ya kawaida yapaswa ituambie kwamba Biblia irejezeapo “pembe nne za dunia,” haimaanishi kwamba waandikaji wa Biblia waliiona dunia kuwa mraba kihalisi. (Ufunuo 7:1) Biblia imeandikwa katika lugha ya watu wa kawaida, mara nyingi ikitumia tamathali za usemi zilizo dhahiri. Kwa hiyo isemapo juu ya dunia kuwa na “pembe nne,” “msingi” wenye kudumu, “nguzo,” na ‘jiwe la pembeni,’ Biblia haitoi ufafanuzi wa kisayansi wa dunia; kwa wazi inasema kwa njia ya kulinganisha vitu, kama vile tufanyavyo mara nyingi katika usemi wa kila siku.a—Isaya 51:13; Ayubu 38:6, BHN.

Katika kitabu chake kiitwacho Galileo Galilei, mwandika wasifu L. Geymonat, alisema hivi: “Wanatheolojia wasio tayari kupokea mawazo mapya ambao walitaka kuiwekea sayansi mipaka kwa msingi wa sababu za kibiblia wangefanya tu Biblia yenyewe isiaminiwe.”5 Na ndivyo walivyofanya. Kwa kweli, ni fasiri ya wanatheolojia iliyowekea sayansi mipaka, si Biblia yenyewe.

Vivyo hivyo, wale leo wafuatao kanuni za msingi za kidini huipotosha Biblia wanaposisitiza kwamba dunia iliumbwa katika siku sita za muda wa saa 24. (Mwanzo 1:3-31) Maoni hayo hayapatani wala na sayansi wala na Biblia. Katika Biblia, sawa na katika usemi wa kila siku, neno “siku” ni neno la kunyumbuka, likionyesha sehemu za wakati zenye muda tofauti-tofauti. Kwenye Mwanzo 2:4, siku zote sita za uumbaji zinarejezewa kuwa “siku” moja iliyotia ndani mambo yote. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “siku” katika Biblia laweza kumaanisha “wakati mrefu” tu.6 Kwa hiyo, hakuna sababu ya Kibiblia kusisitiza kwamba siku za uumbaji zilikuwa za muda wa saa 24 kila moja. Kwa kufundisha vingine, wale wafuatao kanuni za msingi huiwakilisha Biblia vibaya.—Ona pia 2 Petro 3:8.

Muda wa karne zote zilizopita, mara nyingi wanatheolojia wameipotosha Biblia. Chunguza baadhi ya njia ambazo dini za Jumuiya ya Wakristo zimewakilisha vibaya mambo ambayo Biblia husema.

Kuwakilishwa Vibaya na Dini

Mara nyingi matendo ya wale wasemao wanaifuata Biblia huharibu sifa njema ya kitabu wanachodai kustahi sana. Wale waitwao Wakristo isivyofaa wamemwaga damu ya mmoja na mwenzake katika jina la Mungu. Hata hivyo, Biblia huwaonya kwa upole wafuasi wa Kristo “wapendane.”—Yohana 13:34, 35; Mathayo 26:52.

Makasisi fulani hukumba mali za vikundi vyao kwa udanganyifu, wakiwavuta kwa maneno matamu ili wapate kutoka kwao fedha zilizochumwa kwa jasho—tofauti sana na agizo hili la Kimaandiko: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mathayo 10:8; 1 Petro 5:2, 3.

Kwa wazi, Biblia haiwezi kuhukumiwa kulingana na maneno na matendo ya wale wanaoinukuu tu au wanaodai kuishi kulingana nayo. Huenda basi mtu aliye tayari kupokea mawazo mapya akataka kujivumbulia yale ambayo Biblia husema hasa na kwa nini ni kitabu chenye kutokeza sana.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa kielelezo, hata leo waastronomia wenye kuona mambo kihalisi zaidi watasema juu ya “kupanda” na “kushuka” kwa jua, nyota, na vikundinyota—ingawa kwa hakika, hizo huonekana kujongea kwa sababu tu ya kuzunguka kwa dunia.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Mbili kati ya darubini-upeo za Galileo

[Picha katika ukurasa wa 5]

Galileo akikabili mahakimu wake wa baraza la kuhukumu wazushi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki