“Hata Hivyo Imo Katika Mwendo!”
“BIBLIA hufundisha jinsi ya kwenda mbinguni, siyo jinsi mbingu zinavyopiga mwendo,” akasema Galileo Galilei mwanasayansi na mbuni Mwitaliano wa karne ya 16. Mawazo kama hayo yalimwingiza katika hitilafiano pamoja na Kanisa Katoliki la Kiroma, lililomtisha kumtesa na kumfunga gerezani. Miaka 350 hivi baadaye, kanisa lilipitia jinsi lilivyomtendea Galileo. Lile lililotukia siku ya Galileo limeitwa “Kabiliano kati ya sayansi inayoamini yanayochunguzika tu na ushupavu wa kijinga.”
Leo, watafutaji kweli waweza kujifunza kutokana na ono la Galileo. Lakini ni kwa nini kabiliano la jinsi hiyo lilitukia? Uchunguzi wa maoni ya sayansi yaliyokubaliwa wakati wake utaandaa jibu.
Katikati mwa karne ya 16, dunia ilifikiriwa kuwa ndicho kitovu cha ulimwengu wote mzima. Sayari zilidhaniwa kuwa zilizunguka katika duara kamili. Ingawa hayakuthibitishwa kwa njia za kisayansi, mawazo hayo yalikubaliwa katika imani kuwa kweli thabiti. Kwa kweli, sayansi pamoja na “mawazo yayo ya kifumbo” ilikuwa haitengeki na dini.
Galileo alizaliwa katika ulimwengu wa jinsi hiyo kwa familia iliyostahiwa katika Pisa katika 1564. Baba yake alimtaka ajifunze utibabu, lakini mvulana huyo mwenye udadisi alisisimuliwa sana na hesabu. Baadaye, akiwa profesa wa sayansi, alivumbua kanuni fulani za inesha (kutobadilika mwendo kwa gimba). Maelezo ya darubini za mapema za Uholanzi yalipomfikia, alifanyia umbo hilo maendeleo mengi na kujifanyia chombo chake mwenyewe cha hali bora zaidi. Aliielekeza mbinguni na kuchapisha yale aliyojifunza katika kitabu chake cha kwanza, Sidereus Nuncius (Mjumbe wa Kinyota), akijulisha kizazi chake juu ya miezi minne ya Jupita. Katika 1611 aliitwa aende Roma, ambapo alionyesha mavumbuo yake kwa Collegio Romano (Chuo cha Kiroma) cha Kiyesuiti. Walimheshimu kwa baraza ambalo katika hilo walikiri mavumbuo yake.
Mafundisho Yapingwa na Kanisa
Kwa kusikitisha, kabla ya Galileo kuondoka Roma, Kardinali Myesuiti mashuhuri Bellarmine, alianzisha upelelezi wa mafundisho ya Galileo. Galileo aliamini kwamba uumbaji unaongozwa na sheria ambazo wanadamu wanaweza kujifunza kwa uchunguzi. Kanisa Katoliki lilipinga maoni hayo.
Hata wengine wenye elimu ya nyota hawakukubaliana na maoni ya Galileo. Waliamini kwamba haingewezekana darubini ionyeshe hali halisi ya mbingu na kwamba ubuni huo ulikuwa danganyo. Padri mmoja hata alidokeza kwamba nyota zilizoonwa zilikuwa zimeingizwa katika kioo cha darubini! Galileo alipovumbua milima ya mwezi, akihakikisha kwamba viumbe vya mbinguni havikuwa matufe ya mviringo kamili, padri Clavius alibisha kwamba mwezi ulikuwa katika chombo cha fuwele, hivi kwamba, ingawa mtu angeweza kuiona milima, bado ulikuwa mpira kamili! “Wazo hilo,” akasema Galileo kwa kujibu, “si la hakika bali ni fikira bandia ambayo akili inapenda kuwazia-wazia tu.”
Upendezi uliomsukuma Galileo kusoma “Kitabu cha Asili,” kama alivyouita uchunguzi wa kujifunza uumbaji, ulimwongoza kwenye kitabu cha Nicolaus Copernicus Mpolandi mwenye elimu ya nyota. Katika 1543, Copernicus alikuwa amechapisha kitabu kilichotoa hoja kwamba dunia ilikuwa ikizunguka jua. Galileo alikubaliana na hilo. Hata hivyo, hilo lilifanya Galileo awe mshindani dhidi ya sayansi, siasa, na dini madhubuti ya siku yake.
Ingawa Kanisa Katoliki lilitumia elimu ya nyota ya Copernicus kuweka tarehe, kama ya Ista, maoni ya Copernicus hayakuwa yamekubaliwa rasmi. Baraza la kanisa lilikuwa limeunga mkono nadharia ya Aristotle kwamba dunia ilikuwa kitovu cha ulimwengu wote mzima. Hata hivyo, mawazo mapya ya Galileo yalipinga sifa na nguvu yao.
Ingawa wanasayansi mmoja mmoja kutoka upande mmoja wa Ulaya hadi mwingine walijitahidi kuthibitisha mfumo wa Copernicus, waliridhika na kuzungumza juu yalo miongoni mwa wanasayansi wengine. Kwa msingi huo Kanisa Katoliki liliwaacha. Galileo hakuandika katika Kilatini bali katika Kiitaliano cha watu wa kawaida na hivyo akafanya uvumbuzi wake mbalimbali ujulikane na wote. Makasisi walihisi kwamba hakuwa akiwapinga wao tu bali Neno la Mungu.
Si Kitabu cha Mafundisho ya Sayansi
Bila shaka, kuvumbua mambo ya hakika juu ya ulimwengu wote mzima kwa kweli si kupinga Neno la Mungu. Wanafunzi wa Neno hilo hutambua kwamba Biblia si kitabu cha mafundisho ya sayansi, ingawa ni sahihi inapogusia mambo ya kisayansi. Iliandikwa kwa ajili ya ukuzi wa kiroho wa waamini, si ili kuwafundisha fizikia au sayansi yoyote nyingine ya kiasili. (2 Timotheo 3:16, 17) Galileo alikubali hilo. Alidokeza kwamba kuna aina mbili za lugha: maneno hususa ya sayansi na maneno ya kila siku ya waandishi waliopuliziwa roho. Aliandika hivi: “Katika Maandiko ni lazima . . . mambo yaeleweshwe wazi kwa ufahamu wa watu wa kawaida, kusema mambo mengi ambayo huonekana kutofautiana (katika maana ya maneno) na kweli kamili.”
Kuna mifano ya hilo katika maandiko mbalimbali ya Biblia. Moja ni Ayubu 38:6, ambapo Biblia husema juu ya dunia ikiwa na “misingi” na ‘jiwe la pembeni.’ Wengine walitumia hilo vibaya kuwa ushuhuda kwamba dunia imesimama imara. Maneno kama hayo hayakusudiwi yawe maelezo ya kisayansi ya dunia, bali, yanalinganisha kishairi kuumbwa kwa dunia na ujenzi wa nyumba, Yehova akiwa ndiye Mjenzi Mkubwa.
Akiwa mwandishi habari za maisha za watu, L. Geymonat aonyesha katika kitabu chake Galileo Galilei: “Wanatheolojia wenye maoni mamoja tu waliotaka sayansi isipite mpaka yenye msingi wa usababu wa Kibiblia wangeletea Biblia yenyewe sifa mbaya tu.” Kwa sababu za ubinafsi watu washupavu walifanya hivyo barabara. Barua ilipelekwa kwa Makao Matakatifu ikitoa mwito kuwe na uchunguzi wa Galileo.
Katika Februari 19, 1616, wanatheolojia Wakatoliki walitolewa mawazo mawili: (1) “jua ni kitovu cha ulimwengu wote mzima” na (2) “dunia si kitovu cha ulimwengu wote mzima.” Katika Februari 24 walitoa hukumu kwamba mawazo hayo ni ya upumbavu na ya uzushi. Galileo aliamuriwa asishikilie au kufundisha nadharia za jinsi hiyo. Vitabu vyake kadhaa na vya wengine vilizuiliwa kwa muda.
Galileo alinyamazishwa. Si kwamba Kanisa Katoliki lilimpinga tu bali rafiki zake hawakuwa na uwezo wa kumsaidia. Hakuwa na la kufanya ila kujitoa kufanya utafiti tu. Kama papa asingebadilishwa katika 1623, huenda ikawa hatungalisikia juu yake tena. Hata hivyo, askofu mpya, Urban 8, alikuwa mtu mwenye akili na muunga mkono wa Galileo. Galileo alipata habari kwamba papa asingekataza kitabu kipya. Hata alikutana na papa. Baada ya ule ulioonekana kuwa utayari wa kusikia maoni mapya, Galileo alianza kufanyia kazi kitabu hicho.
Ingawa kitabu Dialogue Concerning the Two Chief World Systems kilichapishwa kwanza chini ya leseni ya Katoliki katika 1632, uchangamfu wa kipapa ulififia upesi. Akiwa na umri wa miaka 70, Galileo aliitwa aje mbele ya Baraza la Kuhukumu Wazushi kwa mara ya pili. Kwanza shtaka la kushukiwa kuwa mzushi lilihitaji kwamba elezo litolewe kuhusu mamlaka iliyotolewa na kanisa ya kuchapisha kitabu hicho, na ilidaiwa kwamba Galileo alificha kwa udanganyifu kupigwa marufuku kwa mapema kwa mafundisho ya Copernicus. Kwa kuwa kitabu Dialogue kililinganisha mifumo ya elimu ya nyota, kutia na ule wa Copernicus, kilidaiwa kwamba kilikiuka marufuku.
Galileo aliitikia kwamba kitabu chake kilimchambua Copernicus. Hilo lilikuwa teto dhaifu, kwani katika kitabu hicho hoja yenye kusadikisha sana ilikuwa imetolewa kumwunga mkono Copernicus. Isitoshe, maneno ya papa yalikuwa yameonyeshwa yakisemwa na punguani wa mwisho katika kitabu hicho, Simplicio, hivyo akimuudhi Papa Urban 8.
Galileo Ahukumiwa Kuwa Mzushi
Galileo alipatikana kuwa na hatia. Akiwa tayari mgonjwa na akiwa ametishwa kuteswa asipokana maneno ya kwanza, aliyakana. Akiwa amepiga magoti aliapa hivi: “Ninakana kwa kiapo . . . makosa na uzushi uliosemwa . . . sitasema kamwe . . . mambo kama hayo ambayo yaweza kuniweka chini ya shuku kama hiyo.” Kwa kupendeza, hekaya husema kwamba alipoinuka, aliipiga dunia na kung’ong’oneza, “Eppur si muove! [Na hata hivyo imo katika mwendo!]”
Hukumu ilikuwa kufungwa gerezani na vitubio hadi kifo chake, kilichotukia miaka tisa baadaye. Barua aliyoandika katika 1634 ilisema hivi: “Si wazo lolote langu lililoanza vita hiyo, bali ni kukosa kwangu upendeleo wa Wayesuiti.”
Katika 1822 marufuku kwa kitabu chake yaliondolewa. Lakini haikuwa mpaka 1979 ndipo Papa John Paul 2 alipolirudia tena swala hilo na kukubali kwamba Galileo alikuwa “amefanywa ateseke sana . . . na watu na matengenezo ya Kanisa.” Katika gazeti la Vatikani, L’Osservatore Romano, Mario D’Addio, mshirika mashuhuri wa tume ya pekee iliyowekwa na Papa John Paul 2 iangalie tena hukumu ya Galileo ya 1633, alisema hivi: “Ule ulioitwa eti uzushi wa Galileo hauonekani kuwa na msingi wowote, ama wa kitheolojia ama chini ya sheria ya kanisa.” Kulingana na D’Addio, mahakama ya Baraza la Kuhukumu Wazushi iliruka mipaka ya mamlaka yayo—nadharia za Galileo hazikuvunja sehemu yoyote ya imani. Gazeti la Vatikani lilikiri kwamba hukumu ya Galileo la uzushi haikuwa na msingi wowote.
Tunajifunza nini kutokana na ono la Galileo? Mkristo apaswa atambue kwamba Biblia si kitabu cha mafundisho ya sayansi. Ikionekana kana kwamba kuna hitilafiano kati ya Biblia na sayansi, yeye hahitaji kujaribu kupatanisha kila “tofauti.” Kwa vyovyote, imani ya Kikristo ina msingi wa “neno la Kristo,” si wa mamlaka ya kisayansi. (Warumi 10:17) Isitoshe, sayansi inabadilika daima. Nadharia inayoonekana kupinga Biblia na inayopendwa na wengi leo huenda kesho ikavumbuliwa kuwa yenye makosa na kukataliwa.
Hata hivyo, wakitumia kisa cha Galileo kuonyesha jinsi dini hukandamiza sayansi, wanasayansi wangefanya vema kukumbuka kwamba uvumbuzi wa Galileo haukukubaliwa na shirika la utafiti la siku yake. Kinyume na mawazo ya wengi wa siku yake, Biblia haikupingana na kweli hiyo. Neno la Mungu halikuhitaji kusahihishwa. Tatizo lilisababishwa na ufasiri mbaya wa Biblia wa Kanisa Katoliki.
Kila mtu apaswa asukumwe na upatano mzuri sana na sheria ya kiasili iliyo katika ulimwengu wote mzima amthamini Muumba, Yehova Mungu, hata zaidi. Galileo aliuliza hivi: “Je! Kazi ya Muumba ina ubora mdogo kuliko Neno lake?” Mtume ajibu hivi: “Mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake.”—Warumi 1:20.