Yaliyomo Katika Hicho Kitabu
Huenda mtu anayeingia katika maktaba kwa mara ya kwanza akapata unamna-namna wa vitabu kuwa wenye kutatanisha. Lakini kwa kufafanuliwa kidogo jinsi ambavyo vitabu vimepangwa, anapata kujua upesi jinsi ya kupata vitabu hususa. Vivyo hivyo, unaweza kupata mambo hususa katika Biblia kwa urahisi zaidi unapoelewa jinsi ambavyo yaliyomo katika Biblia yamepangwa.
NENO “Biblia” limetolewa katika neno la Kigiriki bi·bliʹa, lililomaanisha “makunjo ya mafunjo” au “vitabu.”1 Kwa kweli Biblia ni mkusanyo wa—maktaba ya —vitabu 66, ambavyo kuandikwa kwavyo kulienea kwa muda wa miaka ipatayo 1,600, kutoka mwaka wa 1513 K.W.K. hadi karibu mwaka wa 98 W.K.
Vitabu 39 vya kwanza, karibu robo tatu za yaliyomo katika Biblia, vinajulikana kuwa Maandiko ya Kiebrania, kwa kuwa viliandikwa katika lugha hiyo hasa. Vitabu hivyo vyaweza kwa ujumla kugawanywa katika vikundi vitatu: (1) Vya kihistoria, Mwanzo hadi Esta, vitabu 17; (2) Vya kishairi, Ayubu hadi Wimbo Ulio Bora, vitabu 5; na (3) Vya kiunabii, Isaya hadi Malaki, vitabu 17. Maandiko ya Kiebrania hutia ndani historia ya mapema ya dunia na wanadamu na pia historia ya taifa la Israeli la kale tangu mwanzo walo hadi karne ya tano K.W.K.
Vitabu 27 vinavyobaki vinajulikana kuwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kwa kuwa viliandikwa katika Kigiriki, lugha ya kimataifa ya hiyo siku. Kwa msingi vimepangwa kulingana na habari vilivyo nayo: (1) vitabu 5 vya kihistoria—Gospeli na Matendo, (2) zile barua 21, na (3) Ufunuo. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hukazia mafundisho na utendaji mbalimbali wa Yesu Kristo na wanafunzi wake katika karne ya kwanza W.K.