Tumia Vizuri Vitabu vya Zamani
1 Mwanadamu amehifadhi mamilioni ya vitabu vya zamani kwenye maktaba katika pembe zote za dunia. Hata hivyo, vimekuwa na manufaa gani ya kudumu kwa jamii ya kibinadamu? (Mhu. 12:12) Vichapo vyenye thamani kubwa zaidi ni vile vyenye kukazia fikira Ufalme wa Mungu na kile ambacho huo utafanyia wanadamu. Makutaniko mengi yana akiba ya vitabu hivi vyenye kurasa 192 vya aina mbalimbali, vinavyotolewa kwa bei ya pekee. Januari, tutatolea watu vitabu hivi vya zamani.
2 Ni Vyenye Thamani Sana: Ijapokuwa huenda baadhi yetu tukahisi kwamba vitabu hivi ni vya zamani kwa kulinganishwa na vichapo vyetu vipya, lazima tukumbuke kwamba vina kweli ya Kimaandiko. Ujumbe wa Ufalme ambao vinaeleza bado ni wenye thamani leo, na watu wakiutii, unaweza kuokoa uhai. (Yn. 17:3) Kwa hiyo, twapaswa kujitahidi hata zaidi kutumia vizuri vitabu hivi vya zamani.
3 Jambo linalokazia thamani yake ni lile lililoonwa na mwanamke ambaye alirithi vichapo kadhaa vya zamani vya Watch Tower kutoka kwa nyanya yake. Shahidi mmoja alimwuliza mwanamke huyo kama alijua thamani halisi ya vichapo hivyo. Mwanamke huyo alijibu hivi: “Sijui thamani yake, lakini naweza kujuaje?” Mwanamke huyo alikubali funzo la Biblia, akaja katika kweli, na baadaye alithamini maktaba ya nyanya yake. Vitabu hivyo vya zamani vilithibitika kuwa urithi wenye thamani kama nini!
4 Vigawie Watu: Kuongezea kutoa vitabu vya zamani nyumba hadi nyumba, hakikisha unavitoa unapofanya ziara za kurudia kwa watu ambao wajua wanafurahia kusoma vichapo vyetu, kutia ndani wale ambao huandikisha Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na ambao huchukua magazeti kwa ukawaida. Kuhusu wale unaojifunza Biblia nao, vitabu vya zamani vilivyoteuliwa vyaweza kuandaa ujuzi wa jumla utakaopanua uelewevu wao juu ya kweli. Usisahau kujipatia vitabu vya zamani ambavyo huna katika maktaba yako ya kibinafsi. Katika njia hiyo, utaongeza maktaba ya kitheokrasi yenye thamani, itakayoweza kutumiwa kuboresha vipindi vyako vya funzo la kibinafsi.
5 Badala ya kuweka vitabu vyetu vya zamani akibani, acheni tuvitumie vizuri kuchochea watu tunaowapata ‘wamche Mungu na kuzishika amri zake.’—Mhu. 12:13.