Sanduku La Swali
◼ Ni vichapo gani vinavyopaswa kuwekwa katika maktaba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?
Wingi wa vichapo vya kiroho umeandaliwa kwa manufaa ya watu wa Mungu. Kwa kuwa watangazaji wengi hawana hivi kibinafsi, maktaba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kwenye Jumba la Ufalme huandaa njia ya kufanya utafiti katika vichapo ambavyo huenda visipatikane. Hivyo, yapaswa kuwa imeandaliwa vifaa ifaavyo kukiwa na tafsiri mbalimbali za Biblia, vichapo vya karibuni vya Sosaiti, nakala za Huduma ya Ufalme Yetu, mabuku yaliyojalidiwa ya The Watchtower na Awake!, na Watch Tower Publications Index. Kwa kuongezea, kamusi nzuri ya kisasa yapaswa kuongezwa. Ikiwa vyaweza kupatikana, ensaiklopedia, atlasi, au vitabu vya marejezeo kuhusu sarufi na historia vyaweza kuwa vyenye mafaa. Hata hivyo, hangaikio letu kubwa lapaswa kuwa kwenye vichapo vinavyoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45.
Katika visa fulani imeripotiwa kwamba vitabu visivyofaa vimewekwa katika maktaba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Haingefaa kutia ndani habari ya hadithi zenye kubuniwa, ufafanuzi wa Biblia wenye kukazia uhakiki wa Biblia, au vitabu vya falsafa au uwasiliani-roho. Maktaba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi yapaswa kutia ndani habari tu ambayo itawezesha wale wenye kuitumia kusonga mbele kiroho kwa kuendelea.—1 Tim. 4:15.
Mwangalizi wa shule ana daraka la kutunza maktaba, ijapokuwa ndugu mwingine anaweza kupewa mgawo wa kumsaidia kuitunza. Anapaswa kuangalia kwamba maktaba ina vichapo vya karibuni, vichapo vipya vikiongezwa mara tu vinapopatikana. Kila kitabu chapaswa kuandikwa waziwazi kwenye jalada la ndani jina la kutaniko lacho. Kila mwaka, vitabu hivyo vyapaswa kuangaliwa kuona kama vyovyote vyahitaji kurekebishwa au vipya kuwekwa mahali pavyo.
Kila mtu aweza kushirikiana katika kutunza maktaba. Kwapaswa kuwa na uangalifu katika kushughulikia na kutumia vitabu. Watoto hawapaswi kuruhusiwa kucheza navyo, wala mtu yeyote kuvitia alama. Ishara sahili ifaayo yaweza kuwekwa iwe kikumbusha kwamba vitabu havipaswi kutolewa kwenye Jumba la Ufalme.
Kukiwa na makutaniko mapya yanayofanyizwa daima, yamkini kwamba maktaba nyingi si kubwa. Watangazaji fulani walio na vichapo vyetu vya zamani huenda wakafikiria kuvichangia kutaniko. Wazee huenda wakataka kuagiza kuchapwa tena kwa mabuku yaliyojalidiwa ya Watchtower ya Sosaiti. Kwa njia hizi, maktaba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi itathibitika kuwa yenye mafaa sana katika kusaidia wote wafunue hazina zilizositirika za Neno la Mungu, ambazo hutoa ujuzi, hekima, na uelewevu.—Mit. 2:4-6.