Habari za Ufalme Na. 35
Je, Watu Wote Watapata Kupendana?
Upendo kwa Jirani Umepoa
MAMILIONI ya watu huhisi hawana uhakika. Ni wenye taabu, na hawana mahali pa kupata msaada. Mwanamke mfanya-biashara aliyestaafu alitoa wazo hili: ‘Jioni moja mjane anayeishi kwenye ghorofa moja nami alibisha mlango wangu na kusema alikuwa mpweke. Nilimwambia kwa upole lakini waziwazi kwamba nilikuwa na shughuli nyingi. Aliomba msamaha kwa kunisumbua akaondoka.’
Kwa kusikitisha, usiku huohuo, mjane huyo alijiua. Baadaye, mwanamke huyo mfanya-biashara alisema kwamba alikuwa amejifunza “somo la maana sana.”
Ukosefu wa upendo kwa jirani mara nyingi ni wenye kuhuzunisha. Wakati wa mapambano ya kikabila katika Bosnia na Herzegovina, zilizokuwa zamani sehemu ya Yugoslavia, watu zaidi ya milioni moja walilazimishwa kuacha makao yao na makumi ya maelfu waliuawa. Na nani? “Jirani zetu,” akaomboleza msichana mmoja ambaye alikuwa ameondoshwa kijijini mwake. “Tuliwajua.”
Katika Rwanda mamia ya maelfu ya watu walichinjwa, mara nyingi na jirani zao wenyewe. “Wahutu na Watutsi [waliishi] pamoja, wakioana, bila kujali au hata kujua ni nani alikuwa Mhutu na ni nani aliyekuwa Mtutsi,” likaripoti gazeti The New York Times. “Kisha jambo fulani likatokea kwa ghafula,” na “mauaji yakaanza.”
Vivyo hivyo, Wayahudi na Waarabu katika Israeli wanaishi pamoja, lakini wengi huchukiana. Hali ni ileile na Wakatoliki na Waprotestanti wengi katika Ireland na idadi yenye kuongezeka ya watu katika nchi nyinginezo. Katika historia, hakujapata kamwe kukosekana upendo katika ulimwengu jinsi hii.
Kwa Nini Upendo kwa Jirani Umepoa?
Muumba wetu atoa jibu. Neno lake, Biblia, huuita wakati tunamoishi kuwa “siku za mwisho.” Hiki ni kipindi ambacho, unabii wa Biblia wasema, watu watakuwa bila “shauku ya kiasili.” Kuhusu “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” pia ziitwazo katika Maandiko “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu Kristo alitabiri kwamba “upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa.”—2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:3, 12.
Kwa hiyo, ukosefu wa upendo wa leo, ni sehemu ya uthibitisho wa kwamba tunaishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu. Kwa furaha, yamaanisha pia kwamba hivi karibuni mahali pa ulimwengu huu wa watu wasiomwogopa Mungu, patachukuliwa na ulimwengu mpya wenye uadilifu uliojaa upendo.—Mathayo 24:3-14; 2 Petro 2:5; 3:7, 13.
Lakini je, tuna sababu ya kuamini kwamba badiliko hilo lawezekana—kwamba watu wote wanaweza kujifunza kupendana na kuishi pamoja wakiwa na amani wao kwa wao?
Upendo kwa Jirani—Ni Uhalisi
Mwanasheria mmoja wa karne ya kwanza alimwuliza yesu, “ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Bila shaka alimtazamia Yesu aseme, ‘Ni Wayahudi wenzako.’ Lakini katika hadithi juu ya Msamaria mwenye ujirani, Yesu alionyesha kwamba watu wa mataifa mengine pia ni jirani zetu.—Luka 10:29-37; Yohana 4:7-9.
Yesu alikazia kwamba, baada ya upendo kwa Mungu, upendo kwa jirani wapaswa kuongoza maisha yetu. (Mathayo 22:34-40) Lakini je, kuna kikundi chochote cha watu ambacho kwa kweli kimewapenda jirani zao? Wakristo wa mapema walifanya hivyo! Walijulikana kwa upendo waliokuwa nao kwa wengine.—Yohana 13:34, 35.
Vipi leo? Je, kuna mtu yeyote anayedhihirisha upendo wa Kikristo? Kichapo Encyclopedia Canadiana chatoa wazo hili: “Kazi ya Mashahidi wa Yehova ni kuamshwa na kuanzishwa tena kwa Ukristo wa kale uliozoewa na Yesu na wanafunzi wake . . . Wote ni ndugu.”
Kichapo hicho chamaanisha nini? Chamaanisha kwamba Mashahidi wa Yehova hawaruhusu chochote—iwe ni jamii, taifa, au malezi ya kikabila—kiwasababishe kuchukia jirani zao. Wala hawawezi kuua mtu yeyote, kwa kuwa wamefua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu kwa njia ya kitamathali. (Isaya 2:4) Kwa kweli, Mashahidi, wanajulikana kwa kuchukua hatua ya kwanza kusaidia jirani zao.—Wagalatia 6:10.
Si ajabu uhariri katika Sacramento Union ya California uliandika hivi: “Yatosha kusema kwamba ikiwa ulimwengu wote ungeishi kwa imani ya Mashahidi wa Yehova umwagikaji wa damu na chuki ungekoma, na upendo ungetawala kama mfalme.” Mwandikaji katika gazeti Ring la Hungaria alisema hivi: “Nimekuja kuamua kwamba ikiwa Mashahidi wa Yehova ndio wangalikuwa wakiishi duniani peke yao, vita vingalikoma, na kazi pekee za polisi zingekuwa kuongoza magari na kutoa pasi.”
Ingawa hivyo, ni jambo lenye kukubalika kwamba, badiliko la ulimwenguni pote litahitajiwa ikiwa watu wote watapendana. Badiliko hilo litakujaje? (Tafadhali ona ukurasa wa mwisho.)
Watu Wote Watakapopendana
SALA aliyofundisha Yesu Kristo yaonyesha kwamba badiliko kubwa sana liko karibu. Katika Mahubiri yake ya Mlimani yenye kujulikana sana, Yesu alitufundisha kusali: “Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatimizwe duniani, kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:10, King James Version.
Ufalme wa Mungu ni nini? Ni serikali halisi, ambayo inatawala kutoka mbinguni. Ndiyo sababu unaitwa “ufalme wa mbingu.” Yesu, yule “Mkuu wa Amani,” amewekwa rasmi na Baba yake kuwa mtawala wa huo ufalme.—Mathayo 10:7; Isaya 9:6, 7, New World Translation; Zaburi 72:1-8.
Ufalme wa Mungu ujapo, ni nini kitakachoupata ulimwengu huu wenye kujawa na chuki? ‘Ufalme utavunja vipande vipande na kuziharibu’ serikali zote fisadi za ulimwengu huu. (Danieli 2:44) Biblia hufafanua hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali . . . , lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17.
Kuhusu ulimwengu mpya wa Mungu, Biblia husema: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:9-11, 29; Mithali 2:21, 22) Huo utakuwa wakati mtukufu kama nini! “Kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.” (Ufunuo 21:4) Hata wafu wataishi tena, na dunia yote itageuzwa iwe paradiso halisi.—Isaya 11:6-9; 35:1, 2; Luka 23:43; Matendo 24:15.
Ili tuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu, lazima tupendane, kama tu Mungu atufundishavyo tupendane. (1 Wathesalonike 4:9) Mwanafunzi wa Biblia wa Mashariki alisema: “Natazamia kwa hamu wakati ambapo, watu wote watakuwa wamejifunza kupendana, kama Biblia inavyoahidi.” Nasi twaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atatimiza ahadi zake! “Nimenena,” yeye asema, “nami nitafanya.”—Isaya 46:11.
Lakini ili ufurahie baraka hizo chini ya Ufalme wa Mungu, lazima utwae ujuzi wa Biblia, kama mamilioni ya watu walio na moyo wenye kufuatia haki ulimwenguni pote wanavyofanya. (Yohana 17:3) Broshua yenye kurasa 32 Mungu Anataka Tufanye Nini? itakusaidia. Jipatie nakala moja kwa kujaza kipande cha tangazo kilicho kwenye ukurasa uliotangulia na kukipeleka kwenye anwani iliyo karibu zaidi na nyumbani kwako.
□ Ningependa kupokea broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?
□ Tafadhali wasilianeni nami kuhusu funzo la Biblia nyumbani bila malipo.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]
Mpiga-risasi stadi kutoka mafichoni na maziko katika Bosnia: Reuters/Corbis-Bettmann