Ni Nini Kimepata Upendo wa Jirani?
MAMILIONI ya watu wako hoi, wameogopa, na wako katika hali yenye kusikitisha sana na bila namna. “Mimi hula peke yangu, hutembea peke yangu, hulala peke yangu na kuzungumza peke yangu,” akaomboleza mtu mmoja. Ni watu wachache ambao wako tayari kujaribu na kutendea kwa upendo watu wenye uhitaji.
Mwanamke mmoja mfanya-biashara aliyestaafu alisema: ‘Jioni moja mjane aishiye kwenye orofa moja na mimi alibisha mlango wangu akasema kwamba alikuwa mpweke. Nikamwambia kwa upole lakini kwa wazi kwamba nilikuwa na shughuli. Akaomba radhi kwa kunisumbua akaondoka.’
Mwanamke huyo akaendelea kusema: ‘Nilifurahi sana kwamba sikunaswa na mwanamke huyo mchoshi. Jioni iliyofuata, rafiki yangu mmoja alinipigia simu akiuliza kama namjua mwanamke fulani katika jengo letu ambaye alikuwa amejiua usiku uliotangulia. Kama tayari hujakisia, basi ni yule mwanamke aliyebisha mlango wangu.’ Baadaye, mwanamke huyo mfanya-biashara akasema alijifunza “somo kubwa sana.”
Inajulikana sana kwamba watoto wachanga ambao hawaonyeshwi upendo wanaweza kufa. Watoto wakubwa kidogo pia wanaweza kufa wasipoonyeshwa upendo. Msichana mmoja mrembo mwenye umri wa miaka 15 aliandika hivi katika barua ya kujiua: “Upendo unamaanisha kutokuwa mpweke tena.”
Msiba wa Kisasa
Gazeti Newsweek liliripoti hivi miaka michache iliyopita lilipokuwa likieleza juu ya chuki ya kikabila: “‘Umchukie jirani yako’ inaonekana kuwa ndiyo shime ya mwaka huu.” Katika yale mapambano nchini Bosnia na Herzegovina, ambayo zamani ilikuwa sehemu ya Yugoslavia, zaidi ya watu milioni moja walilazimishwa kuhama makwao, na makumi ya maelfu waliuawa. Nani kawaua? “Majirani wetu,” akaomboleza msichana mmoja ambaye alikuwa amefukuzwa kutoka kwenye kijiji chao. “Tuliwajua.”
“Tulikuwa tukikaa pamoja kwa amani,” mwanamke mmoja akasema akirejezea Wahutu na Watutsi 3,000 waliokuwa wakiishi katika kijiji cha Ruganda. Gazeti la The New York Times lilisema: “Hadithi ya kijiji hiki ni hadithi ya Rwanda: Wahutu na Watutsi wakiishi pamoja, wakioana wao kwa wao, bila kujali na bila kujua ni nani aliye Mhutu au aliye Mtutsi. Halafu mambo yakabadilika,” “mauaji yakaanza.”
Vivyo hivyo, Wayahudi na Waarabu huishi pamoja katika Israeli, lakini wengi wanachukiana. Kotekote katika karne hii ya 20, hali kama hizo zimetokea nchini Ireland ya Kaskazini, katika India na Pakistan, katika Malasia na Indonesia, na kati ya jamii tofauti-tofauti nchini Marekani—ndiyo, kotekote ulimwenguni tunamoishi.
Mtu aweza kutaja mifano mingi ya chuki ya kikabila na ya kidini. Ulimwengu haujapata kamwe kukosa upendo kwa kadiri hii.
Ni Nani Anayelaumika?
Chuki, kama ilivyo na upendo, hufundishwa. Wimbo mmoja wenye kupendwa wasema kwamba watoto “hufundishwa kabla haijawa kuchelewa mno/ Kabla hujawa na miaka sita au saba au nane/ Kuchukia watu wote ambao jamaa zako wanachukia.” Ni wakati huu hasa ndipo chuki hufundishwa. Hasa makanisa yameshindwa kufundisha wafuasi wake wawe na upendo.
Gazeti la Ufaransa Le Monde liliuliza hivi: “Mtu aweza kukosaje kufikiri kwamba Watutsi na Wahutu waliokuwa vitani katika Burundi na Rwanda walizoezwa na wamishonari walewale wa Kikristo na kuhudhuria makanisa yaleyale?” Kwa kweli, kulingana na National Catholic Reporter, “asilimia 70 ya [Rwanda] ni Wakatoliki.”
Mapema katika karne hii, nchi za Ulaya Mashariki ziligeukia Ukomunisti usioamini kuwapo kwa Mungu. Kwa nini? Mnamo 1960 mkuu wa kitivo kimoja cha mambo ya kidini katika Prague, Chekoslovakia, alisema: “Ni sisi, sisi Wakristo pekee, ambao tumefanya Ukomunisti uibuke. . . . Kumbuka kwamba pindi moja Wakomunisti walikuwa Wakristo. Ikiwa hawaamini kwamba kuna Mungu mwenye haki, ni kosa la nani?”
Ebu fikiria mambo ambayo makanisa yalifanya wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Brigedia-Jenerali wa Uingereza Frank Crozier alisema hivi kuhusu vita hiyo: “Makanisa ya Kikristo ndiyo wachochezi wakuu wa umwagikaji wa damu, nasi tumewatumia sana.” Baadaye, baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, The New York Times lilisema: “Kwa wakati uliopita mabaraza ya viongozi Wakatoliki wenyeji karibu kila wakati yaliunga mkono vita vya mataifa yao, wakibariki vikosi vya vita na kutoa sala nyingi kwa ajili ya ushindi, ilhali kikundi kingine cha maaskofu upande ule mwingine kilisali peupe ili nao wapate ushindi.”
Lakini, Yesu Kristo alidhihirisha upendo katika matendo yake yote, na mtume Paulo aliandika: “Nyinyi wenyewe hufundishwa na Mungu kupendana.” (1 Wathesalonike 4:9) “Wakristo wa kweli ni ndugu na dada katika Yesu Kristo,” akasema mwandikaji mmoja wa gazeti Sun la Vancouver. “Hawawezi kamwe kuumizana kimakusudi.”
Kwa wazi, makanisa yamechangia sana ukosefu wa upendo uliopo leo. Makala moja iliyochapishwa katika gazeti India Today ilisema: “Uhalifu mwingi wenye ukatili zaidi umefanywa kwa jina la dini.” Lakini, kuna sababu kubwa inayofanya kizazi chetu kijulikane kuwa kisichojali kabisa wengine.
Sababu Ambayo Imefanya Upendo Upoe
Muumba wetu ana jibu. Neno lake, Biblia, laita wakati tunamoishi kuwa “siku za mwisho.” Unabii wa Biblia wasema kwamba hiki ni kipindi ambacho watu ‘hawangekuwa na shauku ya kiasili.’ Kuhusu hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” ambazo pia zimeitwa katika Maandiko kuwa “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu Kristo alitabiri kwamba “upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa.”—2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:3, 12.
Basi, ukosefu wa upendo ni sehemu ya uthibitisho wa kwamba tunaishi katika siku za mwisho za ulimwengu huu. Kwa furaha, hiyo pia yamaanisha kwamba ulimwengu huu wa watu wasiomcha Mungu karibuni utabadilishwa na ulimwengu mpya unaotawalwa na upendo.—Mathayo 24:3-14; 2 Petro 3:7, 13.
Lakini, je, kweli tuna sababu za kuamini kwamba badiliko kama hilo lawezekana—kwamba tutaweza kuishi katika ulimwengu ambamo watu wote watapendana na kuishi pamoja kwa amani?