Sura Ya Kwanza
Ni Nini Kinachoweza Kufanya Maisha Yako Yawe na Maana Zaidi?
JE, UMEPATA kuwazia kufurahia maisha bora, iwe ni nyumbani kwenu au katika kisiwa fulani? Wengi wetu tumepata kuwazia hivyo pindi moja au nyingine.
Mnamo 1891, mchoraji mmoja Mfaransa Paul Gauguin alienda kutafuta maisha kama hayo katika visiwa vinavyoitwa Polinesia ya Ufaransa. Lakini upesi alikabiliwa na uhalisi wa maisha. Maisha yake ya zamani ya kuponda raha na anasa yalimletea yeye na wengine maradhi na kuteseka. Alipohisi kwamba alikuwa anakaribia kufa, alichora picha ambayo imetajwa kuwa “wonyesho bora zaidi wa mwisho wa uwezo wa kuchora.” Kitabu Paul Gauguin 1848-1903—The Primitive Sophisticate chasema hivi: “Utendaji wa wanadamu ulio katika mchoro huo wahusisha maisha yote, tokea kuzaliwa hadi kifo . . . Yeye alikuwa akionyesha kwamba maisha yalikuwa fumbo kubwa.”
Gauguin aliuita mchoro huo “Twatoka Wapi? Sisi Ni Nini? Twaelekea Wapi?”a
Huenda ikawa umewahi kufikiria maswali kama hayo. Watu wengi wanaofikiri huyauliza. Baada ya kutaja maendeleo ya mwanadamu katika mambo ya kisayansi na kiufundi, mhariri mmoja wa The Wall Street Journal aliandika hivi: “Tumfikiriapo mwanadamu mwenyewe, na magumu anayokabili, na fungu lake katika ulimwengu huu, hatujafanya maendeleo makubwa tangu mwanzo wa mwanadamu. Bado hatujui sisi ni nani na kwa nini tunaishi na twaelekea wapi.”
Ni kweli kwamba watu fulani wana shughuli nyingi za kutunza familia zao, kupata riziki, kusafiri, au kufuatia mapendezi mengine ya kibinafsi kwa sababu hawajui umaana mwingine wa maisha. Pindi moja Albert Einstein alisema hivi: “Mtu aonaye kwamba maisha yake hayana maana hakosi furaha tu bali pia hastahili kuishi.” Kwa kupatana na mawazo hayo, wengine hujaribu kufanya maisha yao yawe na maana kwa kufuatia uchoraji, utafiti wa kisayansi, au jitihada za kutoa msaada wa kibinadamu ili kuondoa kuteseka. Je, wewe wajua wengine ambao wako hivyo?
Inaeleweka kwamba maswali ya msingi kuhusu maana ya maisha huzuka. Ni wazazi wangapi ambao baada ya kuona mtoto wao akifa kutokana na malaria au maradhi mengine huuliza, Kwa nini kuna kuteseka kwingi hivi? Je, kuna sababu yoyote? Maswali kama hayo huwatatanisha vijana wengi, wanaume kwa wanawake, ambao huona umaskini, maradhi, na ukosefu wa haki. Vita vikatili mara nyingi huwafanya watu wajiulize ikiwa maisha yanaweza kuwa na maana.
Hata kama hujateseka hivyo, huenda ukakubaliana na Profesa Freeman Dyson, aliyesema hivi: “Mawazo yangu yanapatana na mawazo ya watu wengi wenye kuheshimika ninapouliza tena maswali [ambayo yule mtu wa Biblia] Ayubu aliuliza. Kwa nini tunateseka? Kwa nini ulimwengu hauna haki? Ni nini kusudi la maumivu na msiba?” Huenda wewe pia ukataka kujua majibu.
Kuyapata majibu yenye kuridhisha kwa hakika kwaweza kutusaidia sasa kupata maana ya maisha. Profesa mmoja aliyevumilia hali za kutisha za kambi ya mateso ya Auschwitz alisema: “Hakuna kitu chochote ulimwenguni . . . kiwezacho kumsaidia sana mtu aokoke hata hali zilizo ngumu zaidi kama kujua kwamba maisha ya mtu yana maana.” Yeye alihisi kwamba hata hali ya akili ya mtu inahusiana na utafutaji huu wa kujua maana ya maisha.
Katika karne ambazo zimepita, wengi wametafuta majibu hayo kupitia dini. Baada ya Gautama (mwanzilishi wa Ubudha) kumwona mgonjwa, mzee, na mfu, yeye alitafuta kufahamu, au maana ya hayo, katika dini lakini bila kuamini kuna Mungu halisi. Wengine wameendea makanisa yao.
Lakini, vipi kuhusu watu leo? Wengi hukazia sayansi akili, wakipuuza dini na kuona kuwa “Mungu” hafai. “Kadiri sayansi ifanyavyo maendeleo,” chaeleza kitabu Religion and Atheism, “ndivyo inavyozidi kuonekana kwamba kumfikiria Mungu kunapungua. Mungu amekuwa kama Mtu Asiye na Makao.”
Kwa Nini Watu Wanapuuza Kuwapo kwa Muumba?
Kwa hakika, mwelekeo wa kupuuza dini au Mungu ulianza na falsafa za watu ambao walisisitiza kwamba kusababu pekee kunatosha. Charles Darwin alihisi kwamba nadharia ya “kusalimika kwa viumbe bora na kufa kwa visivyo bora” yatoa sababu ya kuwapo kwa viumbe ulimwenguni kuliko wazo la kuwapo kwa Muumba. Sigmund Freud alifundisha kwamba Mungu alikuwa ndoto tu. Na wazo la kwamba ‘Mungu amekufa’ lilitokea wakati wa Friedrich Nietzsche hadi siku zetu. Falsafa za nchi za Mashariki zinasema vivyo hivyo. Walimu wa Ubudha wasisitiza kwamba hakuna haja ya kujifunza kuhusu Mungu. Kwa habari ya Dini ya Shinto, Profesa Tetsuo Yamaori alisema kwamba “miungu ni binadamu tu.”
Ingawa kuna shaka nyingi juu ya kuwapo kwa Muumba, je, yafaa kuwa na shaka hizo? Yaelekea unajua mifano ya ‘mambo ya hakika ya kisayansi’ ambayo yalidumu katika wakati uliopita na ambayo baada ya muda yalithibitishwa kuwa si sahihi hata kidogo. Maoni kama vile ‘Dunia ni tambarare’ na ‘Ulimwengu wote mzima huzunguka dunia yetu’ yalidumu kwa karne nyingi, lakini sasa tunajua ya kwamba maoni hayo yalikosea kabisa.
Vipi kuhusu mawazo ya baadaye ya kisayansi? Kwa mfano, mwanafalsafa wa karne ya 18, David Hume—akikana kuwapo kwa Muumba—hakuweza kutoa maelezo yoyote yanayofafanua chanzo cha ubuni tata wa uhai ulio duniani. Nadharia ya Darwin ilionyesha jinsi namna mbalimbali za uhai zilivyotokea, lakini haikueleza jinsi uhai ulivyoanza au maisha yanamaanisha nini kwetu.
Basi, wanasayansi na watu wengi wa kawaida wanaona kwamba kuna kitu kinachokosekana. Huenda ikawa nadharia za kisayansi zinaweza kufafanua jinsi uhai ulivyoanza, lakini maswali muhimu ni kusudi la uhai ni nini? Hata watu ambao wamekua wakiamini kwamba kuna Muumba wanaathiriwa. Msichana mmoja wa Ulaya ambaye ni mwanafunzi wa historia alisema hivi: “Kwa maoni yangu, Mungu amekufa. Ikiwa kwa kweli yeye yupo, ulimwengu haungekuwa umevurugika hivi: Watu wasio na hatia wanakufa njaa; aina mbalimbali za wanyama zinatoweka . . . Wazo la kwamba kuna Muumba ni upuuzi mtupu.” Kwa kufikiria hali zilizo duniani, wengi hawawezi kuelewa kwamba ikiwa kuna Muumba, mbona habadili mambo yawe mazuri.
Lakini, ni lazima tukiri kwamba sababu inayofanya wengi wakatae kuwapo kwa Muumba ni kwamba wao hawataki kuamini kuwa yeye yupo. Mtu mmoja wa Ulaya mwenye kiwanda alimwambia mwajiriwa mmoja hivi: “Hata kama Mungu mwenyewe angeniambia kwamba ni lazima nibadili maisha yangu, bado nisingebadilika. Nataka kuishi maisha yangu jinsi nipendavyo.” Kwa wazi, wengine huona kwamba kukiri kwamba kuna Muumba mwenye mamlaka kungepingana na uhuru wao au mtindo wa maisha ambao wao hupendelea. Huenda wakasema, ‘Naamini tu kile ninachoona, na siwezi kuona Muumba yeyote asiyeonekana.’
Mbali na sababu ambayo imefanya watu ‘wapuuze Muumba,’ kungali kuna maswali kuhusu maisha na maana yake. Siku moja baada ya mwanadamu kutua kwenye mwezi, mwanatheolojia Karl Barth aliulizwa kuhusu matimizo hayo makubwa ya kiufundi. Yeye alisema hivi: “Maendeleo hayo makubwa ya mwanadamu kutua kwenye mwezi hayasuluhishi matatizo yoyote ambayo hufanya nikose usingizi.” Leo mwanadamu anapaa angani na kufanya maendeleo makubwa ya haraka kwa mambo ya kompyuta. Hata hivyo, watu wenye kufikiri huona uhitaji wa kuwa na kusudi, jambo ambalo linafanya maisha yawe na maana.
Twawaomba watu ambao huwa tayari kupokea mawazo mapya wafikirie jambo hili. Kitabu Belief in God and Intellectual Honesty chasema kwamba mtu ambaye ana ‘akili yenye kufuatia haki’ huwa “tayari kuchunguza kile anachoamini kuwa kweli” na “kufikiria ifaavyo uthibitisho mwingine upatikanao.”
Katika habari tutakayozungumzia, ‘uthibitisho huo upatikanao’ unaweza kutusaidia kuona ikiwa kwa kweli kuna Muumba aliyeanzisha uhai na ulimwengu wote mzima. Na ikiwa kuna Muumba, Yeye aweza kuwa mtu wa aina gani? Je, Muumba aweza kuwa na utu unaohusiana na maisha zetu? Kufikiria jambo hili kwaweza kutusaidia kuona jinsi maisha zetu ziwezavyo kuwa zenye maana zaidi na zenye kuthawabisha.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa Kifaransa D’où venons-nous? Que sommes-nous? Où allons-nous?
[Picha ya ukurasa mzima katika kurasa za 4]
[Picha katika ukurasa wa 6]
Mchoro wa Gauguin ulizusha maswali kuhusu maana ya maisha