Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 6/15 kur. 19-24
  • Muumba Wako—Jifunze Jinsi Alivyo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Muumba Wako—Jifunze Jinsi Alivyo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ajifunua Jinsi Alivyo
  • Mwalimu Mkuu Atusaidia Kumjua Muumba
  • Unaweza Kuwasaidiaje Wengine Wajifunze Kumhusu?
  • Kwa Sababu Gani Ushukuru Muumba?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Muumba Wetu Mtukufu Hutujali!
    Huduma Yetu ya Ufalme—1999
  • Unaweza Kujifunza Nini Juu ya Muumba Katika Kitabu?
    Je, Kuna Muumba Anayekujali?
  • Imarisha Imani Yako Katika Muumba
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 6/15 kur. 19-24

Muumba Wako—Jifunze Jinsi Alivyo

“Nitapitisha wema wangu wote mbele yako, nami nitalitangaza jina la BWANA mbele yako.”—KUTOKA 33:19.

1. Kwa nini Muumba astahili kuheshimiwa?

MTUME Yohana, aliyeandika kitabu cha mwisho cha Biblia, alirekodi tangazo hili kuu kuhusu Muumba: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” (Ufunuo 4:11) Kama makala iliyotangulia ilivyoonyesha, magunduzi ya sayansi ya kisasa mara nyingi huongezea sababu za kuamini kuwepo kwa Muumba wa vitu vyote.

2, 3. (a) Watu wanahitaji nini ili kujifunza juu ya Muumba? (b) Kwa nini si jambo linalopatana na akili kukutana na Muumba binafsi?

2 Japo ni muhimu kukubali kwamba kuna Muumba, ni muhimu vilevile kujifunza jinsi alivyo—kwamba yeye ni mtu halisi, mwenye utu na njia ambazo zinavuta watu kwake. Kwa kadiri ambavyo umefanya hivyo, je, halingenufaisha kupata kumjua zaidi? Hilo halimaanishi kwamba ukutane na yeye binafsi, kwa jinsi ambavyo binadamu hukutana.

3 Yehova ndiye Chanzo cha hata nyota, jua letu likiwa tu nyota yenye ukubwa wa kadiri. Je, ungewazia kujaribu kukaribia jua? Hata kidogo! Watu wengi hata hawataki kulitazama tu kifupi au hata kukaa kwenye mwangaza wake wenye nguvu kwa muda mrefu bila kujifunika. Kiini chake kina joto lipatalo digrii 15,000,000 Selsiasi. Kwa kila sekunde, tanuri hiyo yenye kutokeza nguvu za nyuklia hugeuza tani milioni nne za masi kuwa nishati. Ni sehemu kidogo tu ya nishati hiyo inayofikia dunia ikiwa joto na nuru, lakini kiasi hicho kinadumisha viumbe vyote duniani. Mambo hayo ya msingi yapasa kutustaajabisha juu ya nguvu nyingi sana za Muumba. Kwa kufaa Isaya angeweza kuandika kuhusu ‘ukuu wa uweza wa Muumba, na kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake.’—Isaya 40:26.

4. Musa aliomba nini, na Yehova aliitikiaje?

4 Lakini, je, ulijua kwamba miezi kadhaa baada ya Waisraeli kuondoka Misri mwaka wa 1513 K.W.K., Musa alimwomba Muumba hivi: “Nakusihi unionyeshe utukufu wako.” (Kutoka 33:18) Ukikumbuka kwamba Mungu ndiye Chanzo cha hata jua, unaweza kuelewa ni kwa nini alimwambia Musa: “Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi.” Muumba alimruhusu Musa ajifiche mahali fulani kwenye Mlima Sinai Alipokuwa ‘akipita.’ Kisha Musa akaona “nyuma” ya Mungu, kitamathali, yaani mng’ao fulani uliobaki wa utukufu wa Muumba, au kuwapo kwake.—Kutoka 33:20-23; Yohana 1:18.

5. Muumba aliridhisha ombi la Musa kwa njia gani, akithibitisha nini?

5 Tamaa ya Musa ya kutaka kumjua Muumba vizuri iliridhishwa. Kwa wazi akisema kupitia malaika, Mungu alipita karibu na Musa na kutangaza: “BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.” (Kutoka 34:6, 7) Jambo hilo laonyesha kwamba kupata kumjua Muumba vizuri zaidi hakuhusishi kutazama umbo lake halisi bali kufahamu zaidi jinsi alivyo, utu wake na sifa zake.

6. Mfumo wetu wa kinga wastaajabisha kwa njia gani?

6 Njia moja tunayoweza kumfahamu Mungu ni kwa kutambua sifa zake kutokana na uumbaji wake. Fikiria mfumo wako wa kinga ya mwili. Toleo moja la Scientific American lililohusu mfumo wa kinga lilisema hivi: “Tokea wakati wa kabla ya kuzaliwa hadi kifo, mfumo wa kinga huwa chonjo nyakati zote. Molekuli na chembe nyingi tofauti-tofauti . . . hutukinga dhidi ya vimelea na viini. Bila kinga hizo, wanadamu hawawezi kuishi.” Mfumo huo ulianzaje? Makala moja katika gazeti hilo ilisema hivi: “Chembe nyingi tofauti-tofauti zinazoshirikiana kwa ustadi sana, ambazo hukinga mwili dhidi ya mashambulizi ya viini na virusi, hutokana na chembe za awali ambazo hutokea majuma tisa hivi baada ya mimba kutungwa.” Mwanamke aliye mja-mzito hupitishia kijusu chake kinachokua mfumo fulani wa kinga. Baadaye, kupitia maziwa ya matiti, yeye pia huandalia mtoto wake chembe za kinga na kemikali zenye manufaa.

7. Tunaweza kufikiria nini kuhusu mfumo wetu wa kinga, jambo linalotufanya tufikie uamuzi gani?

7 Kuna sababu nzuri ya kufikia uamuzi wa kwamba mfumo wako wa kinga unashinda kitu kingine chochote ambacho tiba ya kisasa inaweza kuandaa. Basi, jiulize, ‘Jambo hilo ladokeza nini juu ya Mwanzilishi na Mwandaaji wa mfumo huo?’ Mfumo huo, ambao ‘hutokea kwa mara ya kwanza majuma tisa hivi baada ya mimba kutungwa’ na ambao upo tayari kulinda mtoto ambaye ametoka kuzaliwa, kwa kweli waonyesha hekima na hali ya kufikiria kimbele. Lakini je, tunaweza kujifunza hata mengi zaidi kuhusu Muumba kutokana na mfumo huu wa kinga? Wengi wetu hukata kauli gani kuhusu Albert Schweitzer na wengine ambao walitoa maisha zao ili wawatibu maskini? Kwa kawaida watu kama hao wenye huruma nyororo ya kusaidia wenye uhitaji huonwa kuwa wema. Kwa kulinganisha, twaweza kukata kauli gani juu ya Muumba, ambaye amewapa matajiri kwa maskini mfumo wa kinga? Ni wazi kwamba yeye ni mwenye upendo, asiye na ubaguzi, mwenye huruma nyororo, na mwenye haki. Je, jambo hilo halipatani na ufafanuzi wa Muumba ambao Musa alisikia?

Ajifunua Jinsi Alivyo

8. Yehova hujifunua kwetu kwa njia gani ya kipekee?

8 Lakini, kuna njia nyingine ya kupata kumjua Muumba wetu vizuri zaidi—kupitia Biblia. Hilo ni jambo muhimu hasa kwa sababu kuna mambo yanayomhusu ambayo wala sayansi wala ulimwengu hauwezi kamwe kufunua na mambo mengine yaliyo wazi sana katika Biblia. Mfano mmoja wa jambo ambalo wala sayansi wala ulimwengu hauwezi kufunua ni jina binafsi la Muumba. Ni Biblia tu inayotaja jina la Muumba na umaana wa jina hilo. Katika hati-kunjo za Kiebrania za Biblia, jina lake latokea mara 7,000 hivi likiwa limeandikwa kwa konsonanti nne ambazo zaweza kuandikwa YHWH au JHVH, nalo kwa kawaida hutamkwa Yehova kwa Kiswahili.—Kutoka 3:15; 6:3.

9. Jina binafsi la Muumba linamaanisha nini, na tunaweza kufikia uamuzi gani juu ya jambo hili?

9 Ili tumjue Muumba vizuri, twahitaji kutambua kwamba yeye si “Kianzilishi tu cha Kwanza” wala “MIMI NIKO” asiyeeleweka. Jina lake binafsi laonyesha jambo hilo. Jina hilo ni namna ya kitenzi cha Kiebrania kinachomaanisha “kuwa” au “thibitika kuwa.”a (Linganisha Mwanzo 27:29; Mhubiri 11:3, NW.) Jina la Mungu lamaanisha “Yeye Husababisha Iwe” nalo lakazia kwamba yeye hukusudia na kuchukua hatua. Kwa kujua jina hilo na kulitumia, tunaweza kufahamu vema zaidi kwamba yeye hutimiza ahadi zake na kutekeleza makusudi yake.

10. Tunaweza kupata ufahamu gani muhimu katika rekodi ya kitabu cha Mwanzo?

10 Biblia ndiyo iwezayo kutoa ujuzi juu ya makusudi na utu wa Mungu. Rekodi ya kitabu cha Mwanzo yafunua kwamba pindi moja wanadamu walikuwa na amani na Mungu, nao walikuwa na tazamio la maisha marefu yenye umaana. (Mwanzo 1:28; 2:7-9) Kwa kupatana na umaana wa jina lake, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atamaliza kuteseka na mfadhaiko ambao wanadamu wamekabili kwa muda mrefu. Twasoma hivi juu ya kutimiza kusudi lake: “Ulimwengu halisi ulifadhaishwa, si kwa tamaa yake, bali kwa mapenzi ya Muumba, ambaye kwa kuufanya hivyo, aliupa tumaini ya kwamba huenda siku moja upate . . . kufanywa ushiriki uhuru mtakatifu wa watoto wa Mungu.” —Waroma 8:20, 21, The New Testament Letters, cha J. W. C. Wand.

11. Kwa nini tunaweza kufikiria masimulizi ya Biblia, na mojawapo ya masimulizi hayo yana mambo gani?

11 Biblia inaweza kutusaidia pia kumjua Muumba vizuri zaidi kwa sababu inafunua matendo yake alipokuwa akishughulika na Israeli la kale. Fikiria mfano unaohusu Elisha na Naamani, aliyekuwa mkuu wa jeshi la Wasiria wenye uhasama. Usomapo simulizi hilo kwenye 2 Wafalme sura ya 5, utaona kwamba msichana Mwisraeli aliyetekwa alisisitiza kwamba Naamani angeweza kuponywa ukoma wake kwa msaada wa Elisha katika Israeli. Naamani alienda huko akidhani kwamba Elisha atapunga mikono kwa kufuatia mafumbo fulani ya kuponesha. Badala yake, Elisha alimwambia Msiria huyo akaoge ndani ya Mto Yordani. Ingawa ilibidi watumishi wa Naamani wamsadikishe akubali kufanya hivyo, alipooga aliponywa. Naamani alitoa zawadi zenye thamani, naye Elisha akazikataa. Baadaye mshiriki mmoja wa Elisha akamwendea Naamani kisirisiri na kwa kutumia udanganyifu akapata baadhi ya zawadi hizo zenye thamani. Akapigwa kwa ukoma kwa sababu ya kutofuatia haki. Hili ni simulizi lenye kuvutia la kuonyesha hali ya kibinadamu, ambalo linaweza kutufundisha.

12. Tunaweza kufikia uamuzi gani kuhusu Muumba katika simulizi la Elisha na Naamani?

12 Kwa njia yenye kuvutia, simulizi hilo laonyesha kwamba Muumba Mtukufu wa ulimwengu hakujiona kuwa wa maana sana asiweze kumpendelea msichana mdogo, sifa iliyo tofauti kabisa na desturi za tamaduni nyingi leo. Pia linathibitisha kwamba Muumba haonyeshi upendeleo kwa jamii moja au taifa moja. (Matendo 10:34, 35) Kwa kupendeza, badala ya kutarajia watu watumie ujanja—ambalo ni jambo la kawaida kwa “waponyaji” fulani wa wakati uliopita na wa sasa—Muumba alionyesha hekima ya ajabu sana. Alijua namna ya kuponya ukoma. Pia alionyesha ufahamu na haki kwa kutoruhusu udanganyifu wowote ufaulu. Je, jambo hili vilevile halipatani na utu wa Yehova ambao Musa alisikia? Japo simulizi hilo la Biblia ni fupi, tunaweza kuona kwa kadiri kubwa kama nini jinsi Muumba alivyo!—Zaburi 33:5; 37:28.

13. Toa kielelezo cha jinsi tuwezavyo kupata masomo muhimu katika masimulizi ya Biblia.

13 Masimulizi mengine kuhusu matendo ya Waisraeli yasiyoonyesha shukrani na jinsi Mungu alivyotenda yanathibitisha kwamba kwa kweli Yehova anajali. Biblia yasema kwamba Waisraeli walimjaribu Yehova tena na tena, wakimhuzunisha na kumtia uchungu. (Zaburi 78:40, 41) Kwa hiyo, Muumba ana hisia, naye anajali kile ambacho wanadamu wanafanya. Pia kuna mengi ya kujifunza katika masimulizi ya watu mmoja-mmoja walio mashuhuri. Daudi alipochaguliwa kuwa mfalme wa Israeli, Mungu alimwambia Samweli: “Wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Ndiyo, Muumba hutazama jinsi tulivyo kwa ndani, si sura tu ya nje. Jambo hilo laridhisha kama nini!

14. Tusomapo Maandiko ya Kiebrania, tunaweza kunufaika kwa kufanya nini?

14 Vitabu 39 vya Biblia viliandikwa kabla ya wakati wa Yesu, na yafaa tuvisome. Kusudi halipasi kuwa kujifunza tu masimulizi ya Biblia au historia. Kama kweli tunataka kujifunza jinsi Muumba wetu alivyo, tunapaswa kutafakari masimulizi hayo, labda kwa kufikiria, ‘Tukio hili lafunua nini kuhusu utu wake? Ni sifa zake zipi zinazodhihirika hapa?’b Kufanya hivyo kwaweza hata kuwasaidia wenye kutilia shaka waone kwamba ni lazima Biblia iwe imetokana na Mungu, jambo ambalo linawawekea msingi wa kupata kumjua Mtungaji wake mwenye upendo vizuri zaidi.

Mwalimu Mkuu Atusaidia Kumjua Muumba

15. Kwa nini matendo ya Yesu na mafundisho yake yawe yenye kufundisha?

15 Ni kweli kwamba watu ambao hutilia shaka kuwapo kwa Muumba au ambao humwona Mungu kuwa kitu kisicho dhahiri huenda wakawa hawaijui Biblia vizuri. Labda umekutana na watu ambao hawajui kama Musa aliishi kabla ya Mathayo au baada yake na ambao hawajui matendo na mafundisho ya Yesu. Jambo hilo lahuzunisha sana kwa sababu mtu aweza kujifunza mengi sana kuhusu Muumba kutokana na Mwalimu Mkuu, Yesu. Kwa kuwa alikuwa na uhusiano wa karibu na Mungu, yeye angeweza kufunua jinsi Muumba wetu alivyo. (Yohana 1:18; 2 Wakorintho 4:6; Waebrania 1:3) Naye alifanya hivyo. Hata pindi moja alisema: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 14:9.

16. Mazungumzo ya Yesu pamoja na mwanamke Msamaria yatoa kielelezo cha nini?

16 Fikiria mfano huu. Pindi moja Yesu alipokuwa amechoka kwa sababu ya kusafiri, aliongea na mwanamke Msamaria karibu na Sikari. Alimweleza kweli za ndani, akikazia uhitaji wa ‘kumwabudu Baba kwa roho na kweli.’ Wayahudi wa wakati huo waliepukana na Wasamaria. Tofauti na hivyo, Yesu alionyesha utayari wa Yehova wa kukubali wanaume na wanawake wenye mioyo myeupe wa mataifa yote, kama tulivyoona katika kisa cha Elisha na Naamani. Tunapaswa kufarijika kwamba Yehova hana uhasama wa kishupavu wa kidini ambao umejaa ulimwenguni leo. Pia twaweza kuona kwamba Yesu alikuwa tayari kumfundisha mwanamke, na katika kisa hiki mwanamke aliyekuwa akiishi na mwanamume asiye mume wake. Badala ya kumshutumu, Yesu alimtendea kwa adhama, kwa njia ambayo kwa kweli ingeweza kumsaidia. Baadaye, Wasamaria wengine walimsikiliza Yesu na kukata kauli hivi: “Twajua kwamba mtu huyu kwa hakika ndiye mwokozi wa ulimwengu.”—Yohana 4:2-30, 39-42; 1 Wafalme 8:41-43; Mathayo 9:10-13.

17. Simulizi la ufufuo wa Lazaro laonyesha nini?

17 Ebu tufikirie kielelezo kingine cha jinsi tunavyoweza kujifunza kuhusu Muumba kwa kufahamu matendo na mafundisho ya Yesu. Fikiria pindi ile ambapo rafiki ya Yesu, Lazaro, alipokufa. Awali Yesu alikuwa amethibitisha uwezo wake wa kuwafufua wafu. (Luka 7:11-17; 8:40-56) Lakini, alitendaje alipomwona dada ya Lazaro, Maria, akiomboleza? Yesu “akapiga kite katika roho na kuwa mwenye kutaabika.” Yeye alijali na hakujitenga; “akatokwa na machozi.” (Yohana 11:33-35) Na hilo halikuwa wonyesho tu wa hisia. Yesu alisukumwa kuchukua hatua nzuri—akamfufua Lazaro. Unaweza kuwazia jinsi jambo hilo lilivyowasaidia mitume wafahamu hisia na matendo ya Muumba. Linapasa kutusaidia na kusaidia wengine pia kuelewa utu wa Muumba na njia zake.

18. Watu wanapaswa kuhisije juu ya kujifunza Biblia?

18 Hakuna sababu ya kuaibika kusoma Biblia na kujifunza zaidi kuhusu Muumba wetu. Biblia si kitabu kisichotumika. Yohana aliisoma akawa mshiriki wa karibu wa Yesu. Baadaye aliandika: “Twajua kwamba Mwana wa Mungu amekuja, na yeye ametupa sisi uwezo wa akili ili tupate ujuzi juu ya aliye wa kweli. Na sisi tumo katika muungano na aliye wa kweli, kwa njia ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli na uhai udumuo milele.” (1 Yohana 5:20) Ona kwamba kutumia “uwezo wa akili” ili kupata ujuzi wa “aliye wa kweli,” Muumba, kwaweza kutuongoza kwenye “uhai udumuo milele.”

Unaweza Kuwasaidiaje Wengine Wajifunze Kumhusu?

19. Ni hatua zipi ambazo zimechukuliwa ili kuwasaidia watu wenye kutilia shaka?

19 Watu wengine wanahitaji kujua mengi zaidi ndipo waamini kwamba kuna Muumba mwenye huruma anayetujali ndipo watambue jinsi alivyo. Kuna mamilioni ya watu ambao bado wanatilia shaka kuhusu Muumba au ambao maoni yao juu yake hayapatani na yale yanayopatikana katika Biblia. Unaweza kuwasaidiaje? Kwenye mikusanyiko ya wilaya na ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova iliyofanywa katika kipindi cha 1998/1999, chombo kipya chenye kufaa kilitolewa katika lugha nyingi—kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?

20, 21. (a) Kitabu cha Muumba kinaweza kutumiwaje kwa mafanikio? (b) Simulia mambo yaliyoonwa ya jinsi ambavyo kitabu Muumba tayari kimethibitika kuwa chenye matokeo.

20 Hicho ni kichapo ambacho kitaimarisha imani yako mwenyewe juu ya Muumba wetu na uthamini wako juu ya utu wake na njia zake. Kwa nini hili ni jambo la hakika? Kwa sababu kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kimetayarishwa hasa kwa malengo hayo. Jambo kuu linalokaziwa katika kitabu hicho chote ni “Ni Nini Kinachoweza Kufanya Maisha Yako Yawe na Maana Zaidi?” Habari hii imeandaliwa kwa njia ya kwamba hata watu wenye elimu nyingi sana watapata ikiwa yenye kuvutia. Lakini, habari hiyo inagusia tamaa ambazo sisi sote tunazo. Kuna habari zenye kuvutia na zenye kushawishi wasomaji wanaotilia shaka kuwapo kwa Muumba. Kitabu hicho hakichukulii kwamba msomaji anaamini kuna Muumba. Wenye kutilia shaka kuhusu kuwapo kwa Muumba watavutiwa na uvumbuzi na hoja za kisayansi za karibuni. Mambo hayo yataimarisha pia imani ya wale wanaoamini Mungu.

21 Unapojifunza kitabu hiki kipya, itaonekana kwamba sehemu zake zinatoa pitio la historia ya Biblia kwa njia inayokazia sehemu mbalimbali za utu wa Mungu, kikisaidia wasomaji wamjue Mungu vizuri zaidi. Wengi ambao tayari wamekisoma wameeleza jinsi ambavyo wameona ukweli wa jambo hilo. (Ona makala ifuatayo, ukurasa wa 25-26.) Na iwe hivyo kwako pia unapokisoma kitabu hicho na kukitumia kuwasaidia wengine kupata kumjua Muumba wao vizuri zaidi.

[Maelezo ya Chini]

a Alipokuwa mhariri mkuu wa The Catholic Biblical Quarterly, msomi mmoja Myesuiti M. J. Gruenthaner alisema kwamba kitenzi hiki kinahusishwa na maneno yanayohusu kitenzi kinachofanana nacho, ya kwamba “hakidokezi kamwe wazo la kuwapo kwa njia ya kuwaziwa tu bali sikuzote kitenzi hicho humaanisha kuwapo halisi au kufahamiwa, yaani kujidhihirisha kwa njia thabiti.”

b Wazazi wasimuliapo watoto wao masimulizi ya Biblia, wao waweza kuwasaidia kwa kutokeza maswali kama hayo. Kwa njia hiyo vijana wanaweza kumfahamu Mungu, na vilevile kujifunza kutafakari Neno lake.

Je, Ulitambua?

◻ Musa alimfahamuje Yehova vizuri zaidi kwenye Mlima Sinai?

◻ Kwa nini kujifunza Biblia ni msaada wa kujua jinsi alivyo Mungu?

◻ Tusomapo Biblia, tunaweza kufanya nini ili tumkaribie Muumba wetu zaidi?

◻ Unapanga kutumiaje kitabu Muumba?

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mfumo wetu wa kinga wadokeza nini kuhusu Muumba wetu?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Sehemu ya Hati-Kunjo za Bahari ya Chumvi, ikionyesha zile herufi za Tetragramatoni (jina la Mungu katika Kiebrania)

[Hisani]

Courtesy of the Shrine of the Book, Israel Museum, Jerusalem

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyotenda kwa kuona huzuni ya Maria?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki