Kwa Sababu Gani Ushukuru Muumba?
MTU YE YOTE anayekosa kuonyesha kuthamini fadhili alizoonyeshwa kwa kawaida anaonwa kuwa asiyefikiria au asiye na tabia nzuri. Kama ilivyo, kati ya watu wanaostahili zaidi shukrani zetu kwa ajili ya kutuonyesha fadhili, wazazi wetu ndio wa kwanza. Inatambulikana ulimwenguni pote kwamba watoto wanapaswa kuwashukuru wazazi wao kwa kuwazaa na kwa kuwapa chakula, mavazi, nyumba, elimu, na kadhalika.
Hata hivyo, ingawa tuna deni la wazazi wetu, deni letu kwa Muumba wetu ni kubwa hata zaidi. Kwa sababu gani? Kwa sababu tumepokea faida nyingi zaidi kutoka kwake.
Kuonyesha hilo: Tunawashukuru wazazi wetu kwa kutuzaa. Lakini kwanza kabisa uzima wetu haukutoka kwao. Walitupokeza uzima tu, kwa maana Muumba hasa ndiye chanzo cha uzima. (Zaburi 36:9) Pia sisi tunawathamini wazazi wetu kwa kutupa vitu vya lazima maishani. Lakini, ingawa mambo hayo ya lazima yalinunuliwa kwa pesa zao wenyewe au kwa jasho lao, wao hawakuumba vitu hivyo vinavyohitajiwa. Kwa hiyo, tuna sababu kubwa zaidi kuhisi tuna deni la Muumba wetu.
Kama isingekuwa Yeye aliyeumba dunia na kufanya maandalizi yayo yote ya kutegemeza uzima wa kibinadamu, hakuna kiasi cho chote cha pesa wala jitihada ya jasho ingeweza kututunza tukiwa hai. Ni kama Mkristo mtume Paulo alivyotajia Wagiriki katika Athene wa kale: “[Muumba] ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote. Kwa maana [kwa] yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai.”—Matendo 17:25, 28.
Yajapokuwa yote ambayo Muumba amefanya na anafanyia wanadamu, mamilioni leo wanampuuza kabisa na kwa hakika hawamshukuru yeye kwa ajili ya faida nyingi ambazo wamepokea. Wengine, ingawa wanakubali bila kutaka kwamba lazima kuwe Muumba, wanatia jitihada ndogo tu kujifunza zaidi juu yake au mapenzi yake. Wengine ambao hesabu yao ni mamilioni, hata wanakanusha kuna Muumba, wakidai kwamba vitu vyote vilijitokeza vyenyewe tu. Maskini wanakosa shukrani kama nini! Ukosefu huo wa kuthamini ni mojapo vionyesho kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Lakini, sisi binafsi tunaweza na tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa Muumba wetu.
Zawadi Bora za Muumba
Kadiri tunavyofahamiana vizuri zaidi na Yule aliyefanya vitu vyote, ndivyo tunavyotambua kwamba yeye ni Mtoaji wa “kila zawadi njema.” (Yakobo 1:17, NW; Ufunuo 4:11) Kama ilivyo, wengi wa wale wasioonyesha shukrani kwa Muumba wanajaribu kutetea mwendo wao kwa kudai kwamba kwa kuwa hakuna mwanadamu aliyepata kumwona Yeye, hatuwezi kuwa na hakika kwamba Yeye yuko. Ni kweli, Muumba mkuu haonekani kwa macho yetu kwa sababu yeye ni Roho, na macho yetu hayawezi kuona watu au vitu vilivyomo katika makao ya kiroho. (Yohana 4:24) Lakini hali ya mwanadamu ya kutoweza kumwona Muumba kwa kweli si sababu nzuri ya kuchukua maandalizi Yake ya ukarimu hila shukrani na kukataa kukubali sisi tuna deni Lake.
Tuseme ungekuja nyumbani siku moja na kukuta kwamba mtu fulani alikuachia mfuko mkubwa wa matunda matamu. Kesho yake kikapu cha mboga za kutoka shambani kiachwe, na keshoye upewe vipande vizuri vya nyama. Kisha jambo hilo liendelee hivyo kwa juma zima, na barua yo yote isiachwe kamwe ya kumtambulisha mpaji. Je! ungekata kauli kwamba zawadi hizo zote zilijitokeza “kiasili” ati kwa sababu tu hukumwona mtu ye yote akiacha chakula hicho? Badala yake, je, si ungeuliza kwa bidii kati ya marafiki na watu wa ukoo, ukijaribu kutambua mpaji huyo mwenye fadhili ili uweze kumtolea shukrani za unyofu?
Ndivyo ilivyo na Muumba wetu. Ingawa yeye haonekani kwa macho ya kibinadamu, upendo wake, fadhili na ukarimu kuwaelekea wanadamu unathibitishwa vya kutosha na uumbaji wake wa ajabu unaotosheleza mahitaji yetu katika kila njia. Ni kama mtume Paulo alivyowatajia wakaaji wa Listra wa kale: “[Mungu] hakujiacha pasipo ushuhuda, kwa kuwa alitenda mema, akiwapeni mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akiwashibisha mioyo yenu chakula na furaha.” (Matendo 14:17) Kwa hiyo inafaa tu kwamba tukubali deni letu kwa Muumba na utegemeo wetu kwa maandalizi yake maishani. Zaidi ya hilo, je, hatupaswi kumtafuta kwa bidii zaidi ya tunavyoweza kumtafuta yule mpaji wa zawadi asiyejulikana wa mfano wetu?—Matendo 17:26, 27.
Kusitawisha Uthamini kwa Ajili ya Muumba
Ni wakati tumepata kumjua Muumba na tunaweza kuthamini kweli kweli yale ambayo ametufanyia ndipo tutakapoguswa moyo tumpende na kumtii yeye. Ingawa mamilioni leo wanadai wanamwamini Mungu, ni wazi kutokana na ambavyo wengi wanaishi kwamba si wengi wenye uthamini wa kweli wa kutoka moyoni kwa ajili ya Mfanyizaji wao. Lakini si lazima sisi tukose shukrani kama wao. Kwa hiyo ulizo ambalo lapasa kutupendeza sisi ni hili, Tunawezaje kusitawisha uthamini mwingi kwa ajili ya Muumba Mkuu wetu?
Kwanza kabisa, tutafaidika kufikiria faida nyingi ambazo tumepokea kwa Muumba. Yeye alitupa sisi uhai wetu, hata ingawa kwa wakati huu maisha ya binadamu ni ya muda mfupi. (Zaburi 90:10) Pia uthamini wetu utaongezwa tukitafakari juu ya uhakika wa kwamba Yehova Mungu ametoa pia maandalizi ya ukarimu ya kutegemeza wanadamu na namna nyingine za uhai duniani. Ni kama mtunga zaburi alivyosema kwa kuthamini: “Nchi imeshiba mazao ya kazi zako. Huyameesha majani kwa makundi, na maboga kwa matumizi ya mwanadamu; ili atoe chakula katika nchi. . . . Ee [Yehova], jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.”—Zaburi 104:10-24.
Wanadamu wana sababu kubwa hata zaidi za kuwa wenye shukrani kwa Mungu, kwa maana wanadamu wamepewa mengi zaidi ya wanyama. Kati ya viumbe wote duniani, wanadamu peke yao ndio wenye uweza wa kufikiri, kuthamini uzuri na viwango vya kiroho, na zaidi ya yote, kumjua na kumwabudu Muumba. Iko hivyo kwa sababu mwanadamu peke yake ndiye aliyeumbwa kwa mfano wa Mungu na amepewa sifa zinazoonyesha jinsi zilivyo zile za Yehova Mungu. (Mwanzo 1:27) Kwa hiyo, tunaweza kuona si furaha za kimwili peke yake bali pia furaha zenye kina kirefu zaidi na zenye kudumu zaidi. Ni mwanadamu peke yake anayeweza kuthamini muziki mzuri, vitabu, mashairi, uchoraji wa kutumia rangi na namna nyingine nyingi za uchoraji. Ni mwanadamu peke yake anayejua furaha ya mazungumzo mazuri yenye kujenga, na pia kujiona ametimiza jambo wakati amefanya jambo linalofaa sana.
Pia jambo linalomfanya mwanadamu tofauti ni tamaa ya uzima wa milele. Hiyo ni tamaa iliyotiwa ndani ya moyo wa kibinadamu na Muumba mwenye upendo. (Mhubiri 3:11) Lakini hilo si tumaini la bure tu ambalo haliwezi kutimizwa. Badala yake, kwa sababu ya upendo mkubwa wa Muumba kwa wanadamu, tayari amefanya mipango yote ya lazima kwa ajili ya wanadamu kufurahia uzima wa milele duniani katikati ya hali zenye kupendeza za kiparadiso. Ndiyo, Mungu amefanya hilo liwezekane kwa upendo kupitia dhabihu ya ukombozi ya Mwanaye, Yesu Kristo.—Warumi 5:12; 6:23; 1 Yohana 2:1, 2.
Ingawa furaha nyingi inapatikana wakati mahitaji yetu ya kimwili, kiakili na kimoyoni yanatimizwa, baraka kubwa zaidi inatokana na kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho. (Mathayo 5:3) Kama ilivyo tunataka kujua chanzo chetu, mahali ambako tunaelekea na ni kusudi gani ambalo Muumba analo kwa ajili ya dunia na wanadamu. Zaidi ya hayo, tunatamani kumjua Mfanyizaji wetu na kufurahia uhusiano mzuri pamoja na yeye. Kwa furaha, wale ambao wanatambua uhitaji wao wa kiroho na ambao wanatenda ili kuutosheleza katika njia inayofaa wanaweza kupata furaha yenye kina kirefu na ya kudumu ambayo haijulikani kwa watu wenye kufikiria mambo ya kimwili.—1 Wakorintho 2:6-16.
Uhitaji wetu wa kiroho ukitoshelezwa tunakuwa na amani ya kweli ya moyo na akili na kadiri kubwa ya furaha, hata ingawa tunaishi katika ulimwengu wenye taabu zisizopata kuonekana tena. La maana zaidi, kutambua uhitaji wetu wa kiroho kunaweza kutokeza baraka kubwa zaidi ambayo mwanadamu anaweza kupata—uzima wa milele katika mfumo mpya wa mambo wenye uadilifu wa Mungu.—Yohana 3:16; Wafilipi 4:6, 7; 2 Petro 3:13.
Kumfahamu Vizuri Zaidi Muumba Wetu
Ikiwa tunasadiki kwamba Muumba mwenye upendo na mkarimu yuko, je, si jambo la akili kwamba tungetamani kumjua vizuri zaidi na kuonyesha kuthamini kwetu fadhili zake za upendo kwa kufanya mambo yanayompendeza yeye? Kwa kuangalia uumbaji mzuri sana wa Mungu, tunaweza kutambua baadhi ya sifa zake nzuri, kama vile upendo, ukarimu, huruma, hekima na uwezo. (Warumi 1:20) Hata hivyo, maandishi kutoka kwa Mungu yanahitajiwa ikiwa tutajifunza juu ya mawazo na makusudi yake kuwaelekea wanadamu. Kuongezea hayo, maandishi hayo yapasa kutuambia sisi juu ya mambo ambayo Mungu alifanya wakati uliopita na ambayo atafanya bado kwa ajili ya kubariki wanadamu.
Kwa furaha, tuna maandishi hayo katika kitabu kile kinachoenezwa zaidi ya kingine katika historia ya kibinadamu—Neno la Mungu, Biblia. Ni mapenzi ya Muumba kwamba viumbe wake waweze kuwa na maarifa sahihi juu yake na kusitawisha upendo mwingi kwa ajili yake kwa kujifunza Neno lake na kutafakari juu yake. Kwa njia hiyo wanaweza kujifunza juu ya matendo mengi ya ajabu ya Mungu na wanaweza kuthamini sehemu mbalimbali za utu wake mzuri ajabu.—Yoshua 1:8.
Kumwonyesha Mungu Kuthamini Kwetu
Funzo la bidii la Neno la Mungu ni la lazima ikiwa tunataka kusitawisha uthamini mwingi wa Muumba. Kwa kadiri tunavyojifunza zaidi juu ya Yehova na sifa zake nzuri zilizo nyingi, ndivyo tunavyovutwa kwake. Tunajawa na upendo na kuvutiwa na Mungu huyo mwenye fadhili, upendo na aliye wa ajabu. Zaidi ya hayo, huenda tukachochewa tuonyeshe tunavyohisi kama mtunga zaburi, ambaye alisema: “Nitayakumbuka matendo ya [Yehova]; naam, nitayakumbuka maajabu yako ya kale. Pia nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako. Ee Mungu, njia yako i katika utakatifu; ni nani aliye mungu mkuu kama Mungu? Wewe ndiwe Mungu ufanyaye maajabu.”—Zaburi 77:11-14.
Basi, tunawezaje kuonyesha kuthamini kwetu kwa moyoni kwa Muumba Mkuu? Upendo wetu kwa ajili yake na shukrani kwa ajili ya fadhili zake za upendo zapasa kutuchochea tumtumikie kwa hiari. Twapaswa kuliona hilo si kama daraka tu bali zaidi tulione kuwa furaha. Utumishi huo wa furaha, wa kutaka, anaupenda Yehova, kwa maana mtunga zaburi aliongozwa na Mungu aseme: “Mtumikieni [Yehova] kwa furaha; njoni mbele zake kwa kuimba.”—Zaburi 100:2.
Je! si chanzo kikubwa cha furaha kumtumikia mtu tunayempenda kweli kweli? Hakika ndivyo. Na hakika ndivyo ilivyo kuhusu utumishi wetu kwa Yehova, Muumba Mkuu.
Bila shaka, kumtumikia Yehova kunatia mengi zaidi ya mtu kuishi maisha safi na kutofanya yaliyo mabaya maishani mwake. Mwenendo wa kimungu ni wa lazima, lakini utumishi wetu kwa Muumba pia unatia ndani kumsifu kwa tendo na kwa furaha. Ina maana ya kuwaambia wengine juu ya matendo makuu ya Yehova na makusudi makuu yake, kama yanavyofunuliwa katika Maandiko Matakatifu.
Kwa hiyo wote wenye uthamini wa kweli kwa ajili ya Muumba wetu wa ajabu watakuwa wenye furaha sana kuitikia mwito huu wa furaha wa mtunga zaburi: “Mwimbieni [Yehova], libarikini jina lake, tangazeni wokovu wake siku kwa siku. Wahubirini mataifa habari za utukufu wake, na watu wote habari za maajabu yake. Kwa kuwa [Yehova] ni mkuu mwenye kusifiwa sana.” (Zaburi 96:2-4) Kwa utumishi huo wa furaha wewe, kama vile wengine wengi, unaweza kuonyesha kwa usadikishi kwamba unathamini kweli kweli yale ambayo Muumba amekufanyia.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Onyesha kwamba unathamini maandalizi ya Yehova
Neno la Mungu
ibada takatifu
chakula kinachofaa