Sura Ya Nane
Muumba Ajifunua—Kwa Manufaa Yetu!
KATI ya ngurumo na radi, watu wapatao milioni tatu walisimama mbele ya mlima mrefu katika Peninsula ya Sinai. Mawingu yalifunika Mlima Sinai, ardhi ikatetemeka. Katika hali hizo zenye kukumbukwa, Musa aliongoza Israeli la kale kufanya agano pamoja na Muumba wa mbingu na dunia.—Kutoka, sura ya 19; Isaya 45:18.
Lakini, kwa nini Muumba wa ulimwengu angejifunua kwa njia ya kipekee kwa taifa moja tu, na isitoshe taifa dogo tu? Musa alitufahamisha hivi: ‘Kwa sababu BWANA anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu.’—Kumbukumbu la Torati 7:6-8.
Taarifa kama hiyo yafunua kwamba Biblia inatupa habari nyingi zaidi kuliko tu mambo ya chanzo cha ulimwengu na maisha duniani. Inasema mengi kuhusu shughuli za Muumba pamoja na wanadamu—katika wakati uliopita, wakati wa sasa, na wakati ujao. Biblia ndicho kitabu ambacho kimesomwa zaidi na kuenezwa zaidi ulimwenguni, na basi kila mtu anayethamini elimu apaswa kufahamu yaliyomo ndani yake. Ebu tuone muhtasari wa yale tuwezayo kupata ndani ya Biblia, kwanza tukikazia akili sehemu ambayo huitwa Agano la Kale. Kwa kufanya hivyo, tutapata pia ufahamu wa ndani wa utu wa Muumba wa ulimwengu aliye pia Mtungaji wa Biblia.
Katika Sura ya 6, “Rekodi ya Kale ya Uumbaji—Je, Unaweza Kuitumaini?,” tuliona kwamba ni masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji ndiyo pekee yaliyo na mambo yahusuyo wazazi wetu wa kale zaidi—ndiyo asili yetu. Kitabu hiki cha kwanza cha Biblia kina mambo mengi sana. Kama yapi?
Hekaya za Kigiriki na nyinginezo hueleza juu ya wakati ambapo miungu na nusu-miungu ilipokuwa na uhusiano na wanadamu. Pia, wataalamu wa asili ya wanadamu waripoti kwamba duniani kote kuna hekaya kuhusu furiko moja la kale lililowafagia wengi wa wanadamu. Kwa haki huenda ukapuuza hekaya kama hizo. Lakini, je, ulijua kwamba ni kitabu cha Mwanzo peke yake hutufunulia historia ambayo baadaye ilitajwa katika hekaya na ngano kama hizo?—Mwanzo, sura ya 6, 7.a
Katika kitabu cha Mwanzo, utasoma pia juu ya wanaume na wanawake—watu wenye kustahiwa walio kama sisi—ambao walijua kwamba Muumba yuko na ambao walifanya mapenzi yake maishani mwao. Utanufaika kujua mambo juu ya wanaume kama Abrahamu, Isaka, na Yakobo, ambao walikuwa miongoni mwa “baba” ambao Musa alitaja. Muumba alimjua Abrahamu akamwita “rafiki yangu.” (Isaya 41:8; Mwanzo 18:18, 19) Kwa nini? Yehova alikuwa amemtazama Abrahamu akawa na uhakika wa kwamba alikuwa na imani. (Waebrania 11:8-10, 17-19; Yakobo 2:23) Mambo aliyojionea Abrahamu yaonyesha kwamba Mungu aweza kufikika. Yeye ana uwezo mkubwa sana, lakini yeye si kani au kisababishi fulani tu kisicho na utu. Yeye ni mtu halisi ambaye wanadamu kama sisi wanaweza kusitawisha uhusiano wenye staha naye—kwa manufaa yetu ya milele.
Yehova alimwahidi Abrahamu hivi: “Na katika uzao wako [“mbegu yako,” NW] mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:18) Hilo laongezea ahadi iliyotolewa wakati wa Adamu kuhusu “mbegu” ijayo. (Mwanzo 3:15) Ndiyo, yale ambayo Yehova alimwambia Abrahamu yalithibitisha tumaini la kwamba mtu fulani—Mbegu—angekuja baadaye na kuwaletea watu wote baraka. Utapata kwamba hicho ndicho kichwa kikuu kinachopatikana kotekote katika Biblia, kikikazia kwamba kitabu hiki si mkusanyo tu wa maandishi tofauti-tofauti ya wanadamu. Na kujua kichwa kikuu cha Biblia kutakusaidia kutambua kwamba Mungu alitumia taifa moja la kale—kwa lengo la kubariki mataifa yote.—Zaburi 147:19, 20.
Jambo la kwamba Yehova alikuwa na lengo hilo katika kushughulika na Israeli laonyesha kwamba ‘yeye si mwenye ubaguzi.’ (Matendo 10:34; Wagalatia 3:14) Isitoshe, hata Mungu alipokuwa akishughulika hasa na wazao wa Abrahamu, watu wa mataifa mengine walikubaliwa kuja na kumtumikia Yehova pia. (1 Wafalme 8:41-43) Na, kama tutakavyoona baadaye, kutobagua kwa Mungu ni kwa namna ya kwamba sisi sote leo—hata tuwe wa kabila gani au taifa gani—tunaweza kumjua na kumpendeza.
Tunaweza kujifunza mengi kutokana na historia ya taifa ambalo Muumba alishughulika nalo kwa karne nyingi. Ebu tugawanye historia hiyo katika sehemu tatu. Tunapozungumzia sehemu hizo, ona jinsi Yehova alivyotenda kwa kupatana na maana ya jina lake, “Yeye Husababisha Iwe,” na jinsi utu wake ulivyodhihirika katika shughuli zake na watu halisi.
Sehemu ya Kwanza—Taifa Lililotawalwa na Muumba
Wazao wa Abrahamu walikuwa watumwa Misri. Hatimaye Mungu alimteua Musa, ambaye aliwaongoza wakapata uhuru mnamo 1513 K.W.K. Israeli lilipopata kuwa taifa, Mungu alikuwa mtawala wake. Lakini mnamo 1117 K.W.K., watu walitaka wawe na mfalme wa kibinadamu.
Ni mambo gani yaliyofanya Musa awe pamoja na Israeli kwenye Mlima Sinai? Kitabu cha Biblia cha Mwanzo chatupa historia hiyo. Mapema, Yakobo (aliyeitwa pia Israeli) alipokuwa anaishi kaskazini-mashariki ya Misri, njaa kuu ilitokea kotekote katika ulimwengu uliojulikana wakati huo. Kwa kuihangaikia familia yake, Yakobo alitafuta chakula huko Misri, ambapo chakula kingi kilihifadhiwa. Akagundua kwamba kumbe yule msimamizi wa chakula alikuwa mwana wake Yosefu, ambaye Yakobo alidhani alikuwa amekufa miaka mingi iliyopita. Yakobo na familia yake wakahamia Misri nao waliombwa wabaki huko. (Mwanzo 45:25–46:5; 47:5-12) Lakini, baada ya kifo cha Yosefu, Farao mpya akawalazimisha wazao wa Yakobo wawe watumwa na ‘kufanya maisha yao kuwa uchungu kwa kazi ngumu; kazi ya chokaa na matofali.’ (Kutoka 1:8-14) Unaweza kusoma masimulizi hayo dhahiri na mengi zaidi katika kitabu cha pili cha Biblia, Kutoka.
Waisraeli walitendwa vibaya kwa miongo mingi, na “kilio chao kikafika juu kwa Mungu.” Lilikuwa jambo la hekima kumgeukia Yehova. Yeye alipendezwa na wazao wa Abrahamu naye aliazimia kutimiza kusudi Lake la kuandaa baraka ya wakati ujao kwa watu wote. Yehova ‘akasikia kuugua kwa Israeli na kuwaangalia,’ jambo linaloonyesha kwamba Muumba anawahurumia watu wanaoonewa na kuteseka. (Kutoka 2:23-25) Alimchagua Musa aongoze Waisraeli kutoka utumwani. Lakini Musa na ndugu yake, Aroni, walipokuja kumwomba Farao wa Misri awaachilie watu hao waliotumikishwa, yeye alijibu hivi kwa ukaidi: “BWANA ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao?”—Kutoka 5:2.
Je, ungeweza kuwazia Muumba wa ulimwengu akitishwa na wito kama huo, hata kama ulitolewa na mtawala wa mamlaka yenye nguvu zaidi kijeshi iliyokuwapo wakati huo? Mungu akawapiga Farao na Wamisri kwa mfululizo wa mapigo. Hatimaye, baada ya pigo la kumi, Farao akakubali kuwaachilia Waisraeli. (Kutoka 12:29-32) Basi, wazao wa Abrahamu wakamjua Yehova kuwa mtu halisi—mtu anayeandaa uhuru kwa wakati wake. Ndiyo, kama jina lake lidokezavyo, Yehova akawa mtimizaji wa ahadi zake katika njia zenye kutazamisha sana. (Kutoka 6:3) Lakini, Farao na Waisraeli bado walikuwa wajifunze hata mengi zaidi kuhusu jina hilo.
Hilo lilitukia kwa sababu Farao alibadili maoni yake upesi. Aliongoza jeshi lake kuwakimbiza kwa bidii wale watumwa waliokuwa wakienda, akiwafikia karibu na Bahari Nyekundu. Waisraeli walinaswa kati ya bahari na jeshi la Misri. Kisha Yehova akaingilia kwa kufungua njia kupitia Bahari Nyekundu. Farao angalipaswa kutambua kwamba huo ulikuwa wonyesho wa uwezo wa Mungu usioweza kushindwa. Badala yake, yeye aliongoza jeshi lake himahima kufuata Waisraeli—akazama na jeshi lake Mungu aliporudisha bahari katika hali yake ya kawaida. Masimulizi yaliyo katika Kutoka hayasemi kihususa jinsi Mungu alivyotimiza matendo hayo. Twaweza kuyaita kwa haki kuwa miujiza kwa sababu matendo hayo na wakati yalipotukia hayangeweza kuongozwa na wanadamu. Kwa hakika, matendo kama hayo hayangemshinda Yule aliyeuumba ulimwengu pamoja na sheria zake zote.—Kutoka 14:1-31.
Tukio hili likawadhihirishia Waisraeli—na hata sisi pia—kwamba Yehova ndiye Mwokoaji atendaye kulingana na jina lake. Lakini, kutokana na masimulizi haya twapaswa kufahamu hata mengi zaidi kuhusu njia za Mungu. Kwa mfano, yeye alitekeleza haki dhidi ya taifa lenye kuonea, na kuonyesha upendo wenye fadhili kwa watu wake ambao kupitia hao Mbegu ingekuja. Kwa habari ya mbegu hiyo, yale tusomayo katika Kutoka ni zaidi ya historia tu ya kale; inahusiana na kusudi la Mungu la kufanya baraka ipatikane kwa wote.
Kuendelea Hadi Bara Lililoahidiwa
Baada ya kuondoka Misri, Musa na watu walivuka jangwa hadi Mlima Sinai. Kile kilichotukia huko kiliongoza shughuli za Mungu na taifa hilo kwa karne nyingi zilizofuata. Yeye aliandaa sheria. Bila shaka, muda mrefu sana kabla ya tukio hilo tayari Muumba alikuwa amefanyiza sheria zenye kuongoza ulimwengu wetu, na sheria hizo zingali zinatumika. Lakini, kwenye Mlima Sinai alimtumia Musa kuandaa sheria za taifa. Twaweza kusoma yale ambayo Mungu alifanya na juu ya mfumo wa Sheria alioandaa katika kitabu cha Kutoka na vile vitabu vitatu vinavyofuata—Mambo ya Walawi, Hesabu, na Kumbukumbu la Torati. Wasomi wanaamini kwamba Musa aliandika pia kitabu cha Ayubu. Tutazungumzia baadhi ya mambo yake makuu katika Sura ya 10.
Hata leo hii, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanajua au wanajaribu kufuata zile Amri Kumi, ambazo ndizo mwongozo mkuu wa maadili wa huu mfumo kamili wa Sheria. Lakini, sheria hizo zina mielekezo mingine mingi ambayo huvutia watu kwa ubora wake. Inaeleweka kwamba sheria nyingi zilihusu maisha ya Waisraeli wakati huo, kama vile sheria za usafi wa kimwili, usafi wa kiafya, na zenye kuhusu maradhi. Ingawa awali zilikusudiwa zitumiwe na watu wa kale, sheria hizo huonyesha mambo ya kisayansi ambayo wataalamu wa kibinadamu wamegundua tu katika karne moja hivi iliyopita. (Mambo ya Nyakati 13:46, 52; 15:4-13; Hesabu 19:11-20; Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Kwa kufaa huenda mtu akauliza, Inawezekanaje kwamba sheria za Israeli la kale zilionyesha ujuzi na hekima zilizoshinda kwa mbali zile zilizojulikana na mataifa ya wakati huo? Jibu lenye kupatana na akili ni kwamba sheria hizo zilitoka kwa Muumba.
Sheria pia zilisaidia kuhifadhi vizazi vya familia na kuweka wajibu wa kidini ambao ungefuatwa na Waisraeli mpaka wakati ambapo ile Mbegu ingetokea. Kwa kukubali kufanya yale yote ambayo Mungu alikuwa amesema, waliwajibika kuishi kwa kupatana na Sheria hiyo. (Kumbukumbu la Torati 27:26; 30:17-20) Ni kweli kwamba wao hawangeweza kushika Sheria kikamilifu. Na hata hiyo ilikuwa na kusudi zuri. Mtaalamu mmoja wa sheria alieleza baadaye kwamba Sheria ilifanya “mikiuko-sheria iwe dhahiri, mpaka mbegu iwasili ambayo kwayo ahadi ilikuwa imetolewa.” (Wagalatia 3:19, 24) Basi mfumo wa Sheria uliwafanya wawe watu walio tofauti, uliwakumbusha kwamba walihitaji ile Mbegu, au Mesiya, na kuwatayarisha wamkaribishe.
Waisraeli, waliokuwa wamekusanyika kwenye Mlima Sinai, walikubali kushika mfumo wa Sheria wa Mungu. Basi wao wakafanya kile Biblia inachokiita agano, au mapatano. Agano hilo lilifanywa kati ya taifa hilo na Mungu. Japo walifanya agano hilo kwa hiari, wao wakawa wenye shingo ngumu. Kwa mfano, wao walifanyiza ndama ya dhahabu ili iwakilishe Mungu. Hiyo ilikuwa dhambi kwa sababu ibada ya sanamu ilivunja moja kwa moja zile Amri Kumi. (Kutoka 20:4-6) Isitoshe, walilalamika juu ya maandalizi waliyopewa, walimwasi kiongozi wao (Musa) aliyewekwa rasmi na Mungu, na kujiingiza katika ukosefu wa adili pamoja na wanawake wa kigeni walioabudu sanamu. Lakini kwa nini mambo haya yatupendeze, sisi tunaoishi mbali sana na wakati wa Musa?
Tena, hii si historia tu ya kale. Masimulizi ya Biblia kuhusu matendo ya Israeli yasiyo na shukrani na jinsi Mungu alivyotenda yaonyesha kwamba kwa kweli yeye anajali. Biblia yasema kwamba Waisraeli walimjaribu Yehova “tena na tena,” wakimfanya “ahuzunike” na kumtia “uchungu.” (Zaburi 78:40, 41, NW) Kwa hiyo, twaweza kuwa na uhakika wa kwamba Muumba ana hisia na kwamba yeye anajali kile ambacho wanadamu wanafanya.
Kwa maoni yetu sisi wanadamu, huenda mtu akafikiri kwamba kosa la Israeli lingefanya Mungu afutilie mbali agano lake na labda achague taifa jingine ili atimize ahadi yake. Lakini hakufanya hivyo. Badala yake, yeye aliwaadhibu wakosaji hao waliokuwa waovu lakini akawaonyesha rehema taifa zima lililopotoka. Ndiyo, Mungu aliendelea kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa ahadi aliyompa rafiki yake mwaminifu Abrahamu.
Baada ya muda mfupi, Israeli lilikaribia Kanaani, ambayo Biblia huita Bara Lililoahidiwa. Lilikuwa limekaliwa na watu wenye matendo mapotovu sana kiadili. Muumba alikuwa ameruhusu miaka 400 ipite bila kuwaingilia, lakini sasa aliamua kwa haki kulipatia Israeli la kale bara hilo. (Mwanzo 15:16; ona pia “Mungu Mwenye Wivu—Katika Maana Gani?,” ukurasa wa 132-133.) Kwa matayarisho Musa aliwatuma wapelelezi 12 kwenye bara hilo. Kumi kati yao hawakuonyesha imani katika nguvu ya Yehova ya kuokoa. Ripoti yao iliwasukuma watu wanung’unike dhidi ya Mungu na kufanya hila ya kutaka kurudi Misri. Tokeo likawa kwamba Mungu akawahukumu watu watange-tange jangwani kwa miaka 40.—Hesabu 14:1-4, 26-34.
Hukumu hiyo ilitimiza nini? Kabla ya kifo chake, Musa aliwahimiza wana wa Israeli wakumbuke ile miaka ambayo Yehova aliwanyenyekeza. Musa aliwaambia: “Nawe fikiri moyoni mwako, ya kuwa kama vile baba amrudivyo mwanawe, ndivyo BWANA, Mungu wako, akurudivyo.” (Kumbukumbu la Torati 8:1-5) Japo walitenda kwa njia ya kumtukana, Yehova aliwatunza, akionyesha kwamba wao hawangeweza kujitegemea. Kwa mfano, wao waliokoka kwa sababu aliandalia taifa hilo mana, vitu vyenye kulika vyenye ladha kama ya keki zenye asali. Kwa wazi, wao wangalijifunza mengi kutokana na mambo waliyojionea jangwani. Hayo yangalithibitisha umuhimu wa kumtii Mungu wao mwenye rehema na kumtegemea.—Kutoka 16:13-16, 31; 34:6, 7.
Baada ya kifo cha Musa, Mungu alimpa Yoshua utume wa kuongoza Israeli. Mwanamume huyo shujaa aliye mwaminifu-mshikamanifu aliingiza taifa hilo Kanaani na kwa moyo mkuu akaanza kuliteka. Kwa kipindi kifupi sana, Yoshua alishinda wafalme 31 na kukalia sehemu kubwa ya Bara Lililoahidiwa. Unaweza kupata masimulizi haya yenye kuvutia katika kitabu cha Yoshua.
Utawala Bila Mfalme wa Kibinadamu
Kotekote katika safari yao jangwani na katika miaka ya mapema wakiwa katika Bara Lililoahidiwa, taifa hilo liliongozwa na Musa kisha Yoshua. Waisraeli hawakuhitaji mfalme wa kibinadamu, kwa kuwa Yehova alikuwa ndiye Mwenye Enzi Kuu wao. Yeye alifanya maandalizi ya wanaume wazee waliowekwa rasmi wasikize kesi za kisheria kwenye malango ya jiji. Wao walidumisha utaratibu na kuwasaidia watu kiroho. (Kumbukumbu la Torati 16:18; 21:18-20) Kitabu cha Ruthu chatuonyesha kifupi jinsi wanaume hao wazee walivyoshughulikia kesi moja ya kisheria kwa kutegemea sheria iliyopatikana katika Kumbukumbu la Torati 25:7-9.
Katika miaka iliyopita, mara nyingi taifa hilo halikumpendeza Mungu kwa sababu mara kwa mara hawakumtii nao waligeukia miungu ya Wakanaani. Lakini, hali ilipokuwa mbaya sana na wakamwitia Yehova awape msaada, yeye aliwakumbuka. Aliwateua waamuzi wenye kuchukua uongozi katika kukomboa Israeli, wakiwaokoa kutokana na majirani wao wenye kuwadhulumu. Kitabu kiitwacho Waamuzi chaonyesha dhahiri matendo ya waamuzi 12 miongoni mwa waamuzi hao wenye moyo mkuu.—Waamuzi 2:11-19; Nehemia 9:27.
Rekodi hiyo inasema hivi: “Siku hizo hapakuwa na mfalme katika Israeli; kila mtu alifanya yaliyokuwa ni mema machoni pake mwenyewe.” (Waamuzi 21:25) Taifa lilikuwa na viwango vya maadili vilivyokuwa katika Sheria, basi kwa msaada wa wanaume wazee na maagizo kutoka kwa makuhani, watu walikuwa na msingi wa ‘kufanya yaliyokuwa ni mema machoni pao’ na wawe salama. Na zaidi, mfumo wa Sheria uliandaa tabenakulo, au hema lenye kubebeka, ambamo dhabihu zilitolewa. Ibada ya kweli ilikuwa ikifanywa huko nayo ilisaidia kuunganisha taifa wakati huo.
Sehemu ya Pili—Ufanisi Chini ya Wafalme
Samweli alipokuwa mwamuzi katika Israeli, watu walidai kwamba wanataka mfalme wa kibinadamu. Wafalme wa kwanza watatu—Sauli, Daudi, na Solomoni—walitawala kwa miaka 40 kila mmoja, tokea mwaka wa 1117 hadi 997 K.W.K. Israeli likafikia kilele cha utajiri na utukufu, na Muumba alichukua hatua muhimu za kutayarisha utawala kwa ajili ya Mbegu ijayo.
Akiwa mwamuzi na nabii, Samweli alitunza vema hali ya kiroho ya Israeli, lakini wana wake walikuwa tofauti. Hatimaye watu wakamsisitizia Samweli hivi: “Basi, tufanyie mfalme atuamue, mfano wa mataifa yote.” Yehova akamweleza Samweli umaana wa madai yao: “Isikilize sauti ya watu hawa . . . kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao.” Yehova aliona kimbele matokeo yenye kuhuzunisha ya jambo hilo. (1 Samweli 8:1-9) Lakini, kwa kupatana na dai lao, yeye alimteua mtu mmoja mwenye kiasi aliyeitwa Sauli kuwa mfalme wa Israeli. Japo alianza vizuri, baada ya kuwa mfalme, Sauli alionyesha mitazamo iliyopotoka, akakiuka amri za Mungu. Nabii wa Mungu akatangaza kwamba ufalme huo ungepewa mtu anayekubalika machoni pa Yehova. Jambo hilo lapasa kutukazia jinsi Muumba anavyothamini utii kutoka moyoni.—1 Samweli 15:22, 23.
Daudi, ambaye angekuwa mfalme afuataye wa Israeli, alikuwa mwana mchanga zaidi katika familia moja ya kabila la Yuda. Kuhusu chaguo hilo lenye kushangaza, Mungu alimwambia Samweli: “Wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Je, haitii moyo kwamba Muumba hutazama jinsi tulivyo ndani, bali si sura ya nje? Lakini, Sauli alikuwa na mawazo yake mwenyewe. Tokea wakati ambapo Yehova alimchagua Daudi awe mfalme wa wakati ujao, Sauli alishikwa na kichaa—akiwa na mori ya kumwua Daudi. Yehova hakuruhusu jambo hilo litendeke, na hatimaye Sauli na wana wake wakafa vitani dhidi ya watu waitwao Wafilisti.
Daudi alitawala akiwa mfalme katika jiji la Hebroni. Kisha akateka Yerusalemu na kuhamisha makao yake makuu huko. Pia alipanua mipaka ya Israeli kufikia kiwango kamili ambacho Mungu alikuwa ameahidi kuwapa wazao wa Abrahamu. Unaweza kusoma juu ya kipindi hiki (na historia ya wafalme wa baadaye) katika vitabu sita vya historia vya Biblia.b Vitabu hivyo vinafunua kwamba maisha ya Daudi yalikuwa pia na matatizo. Kwa mfano, akishindwa na tamaa ya kibinadamu, alifanya uzinzi na yule Bath-sheba mrembo kisha akafanya makosa mengine ya kufunika dhambi yake. Akiwa Mungu wa haki, Yehova hangepuuza tu kosa la Daudi. Lakini kwa sababu ya toba ya moyoni ya Daudi, Mungu hakutaka adhabu ya Sheria itumiwe kikamili; lakini, bado Daudi angepata matatizo mengi ya familia kwa sababu ya dhambi zake.
Kupitia matatizo hayo yote, Daudi akamjua Mungu kuwa mtu halisi—mtu mwenye hisia. Yeye aliandika hivi: ‘BWANA yu karibu na wote wamwitao naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.’ (Zaburi 145:18-20) Weupe wa moyo wa Daudi na ujitoaji wake waonyeshwa wazi katika nyimbo tamu alizotunga, ambazo zimefanyiza karibu nusu ya kitabu cha Zaburi. Mamilioni ya watu wamefarijika na kutiwa moyo na mashairi hayo. Ebu fikiria jinsi Daudi alivyokuwa karibu na Mungu, kama ionyeshwavyo katika Zaburi 139:1-4: “Ee BWANA, umenichunguza na kunijua. Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu; umelifahamu wazo langu tokea mbali. . . . Maana hamna neno ulimini mwangu usilolijua kabisa, BWANA.”
Daudi hasa alifahamu nguvu ya Mungu ya kuokoa. (Zaburi 20:6; 28:9; 34:7, 9; 37:39) Kila wakati alipojionea nguvu hiyo, tumaini lake kwa Yehova lilikua. Unaweza kuona uthibitisho wa jambo hilo katika Zaburi 30:5; 62:8; na 103:9. Au soma Zaburi 51, ambayo Daudi alitunga baada ya kukaripiwa kwa kutenda dhambi na Bath-sheba. Inafariji kama nini kujua kwamba tunaweza kujieleza kwa utayari kwa Muumba, tukiwa na uhakika wa kwamba yeye hana kiburi bali yuko tayari kusikiliza kwa unyenyekevu! (Zaburi 18:35; 69:33; 86:1-8) Daudi hakupata uthamini huo kupitia mambo aliyojionea tu. Aliandika hivi: “Nimeyatafakari matendo yako yote, naziwaza kazi za mikono yako.”—Zaburi 63:6; 143:5.
Yehova alifanya agano la kipekee na Daudi kwa ajili ya ufalme wa milele. Labda Daudi hakuelewa umaana hasa wa agano hilo, lakini kutokana na mambo madogo-madogo yaliyorekodiwa baadaye katika Biblia, twaweza kuona kwamba Mungu alikuwa akionyesha kwamba Mbegu iliyoahidiwa ingekuja katika nasaba ya Daudi.—2 Samweli 7:16.
Mfalme Solomoni Mwenye Hekima na Umaana wa Maisha
Solomoni, mwana wa Daudi alijulikana sana kwa hekima yake, nasi twaweza kunufaika nayo kwa kusoma vitabu vyenye kutumika sana maishani vya Mithali na Mhubiri.c (1 Wafalme 10:23-25) Hasa kitabu cha Mhubiri ni chenye msaada sana kwa watu ambao wanatafuta umaana wa maisha, kama tu alivyofanya Mfalme Solomoni mwenye hekima. Akiwa mfalme wa kwanza Mwisraeli aliyezaliwa katika familia ya kifalme, Solomoni alikuwa na mambo mengi sana ambayo angeweza kufanya. Pia alianzisha miradi mitukufu ya ujenzi, alikuwa na vyakula vya aina nyingi mezani pake, na kufurahia muziki na ushirika wa waandamani wenye kutokeza sana. Lakini, akaandika hivi: “Nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, yote ni ubatili.” (Mhubiri 2:3-9, 11) Alimaanisha nini?
Solomoni aliandika: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.” (Mhubiri 12:13, 14) Kwa kupatana na hayo, Solomoni alijishughulisha na mradi wa miaka saba, wa kujenga hekalu tukufu, ambamo watu wangemwabudu Mungu.—1 Wafalme, sura ya 6.
Kwa miaka mingi utawala wa Solomoni ulikuwa wenye amani na wingi wa vitu. (1 Wafalme 4:20-25) Lakini, bado moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Yehova kama moyo wa Daudi. Solomoni alioa wake wengi wa kigeni akawaruhusu wafanye moyo wake uelekee miungu yao. Hatimaye Yehova akasema: “Hakika nitaurarua ufalme usiwe wako . . . Nitampa mwana wako kabila moja, kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu, na kwa ajili ya Yerusalemu.”—1 Wafalme 11:4, 11-13.
Sehemu ya Tatu—Ufalme Wagawanywa
Baada ya kifo cha Solomoni, mnamo 997 K.W.K., makabila kumi ya kaskazini yalijitenga. Hayo yalifanyiza ufalme wa Israeli, ambao Waashuru waliuteka mnamo 740 K.W.K. Wafalme wa Yerusalemu walitawala makabila mawili. Ufalme huu, Yuda, ulidumu mpaka Wababiloni walipolishinda Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. na kuwateka wakazi. Yuda ukawa ukiwa kwa miaka 70.
Solomoni alipokufa, mwana wake Rehoboamu akatwaa mamlaka na kufanya maisha yawe magumu kwa watu. Hilo lilitokeza maasi, na makabila kumi yalijitenga na kuwa ufalme wa Israeli. (1 Wafalme 12:1-4, 16-20) Katika miaka iliyopita, ufalme huu wa kaskazini haukushikamana na Mungu wa kweli. Watu walizoea kuinamia sanamu za ndama ya dhahabu au waliingia katika namna nyinginezo za ibada isiyo ya kweli. Baadhi ya wafalme waliuawa na utawala wa familia zao kupinduliwa na wanyakuaji. Yehova alivumilia kwa subira sana, akiwatuma tena na tena manabii wa kuonya taifa hilo kwamba lingepatwa na msiba iwapo lingeendelea na uasi wao. Vitabu vya Hosea na Amosi viliandikwa na manabii ambao ujumbe wao hasa ulikazia ufalme huu wa kaskazini. Hatimaye, mnamo 740 K.W.K., Waashuru walileta msiba ambao manabii wa Mungu walikuwa wametabiri.
Kule kusini, mfuatano wa wafalme 19 wa nyumba ya Daudi walitawala Yuda hadi mwaka wa 607 K.W.K. Mfalme Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia walitawala kama vile baba yao wa kale Daudi alivyotawala, nao walimpendeza Yehova. (1 Wafalme 15:9-11; 2 Wafalme 18:1-7; 22:1, 2; 2 Mambo ya Nyakati 17:1-6) Wafalme hao walipotawala, Yehova alibariki taifa hilo. Kitabu The Englishman’s Critical and Expository Bible Cyclopædia chaonelea hivi: “Desturi kuu tukufu ya Y[uda] ilikuwa ni hekalu, ukuhani, sheria iliyoandikwa, ambazo zote ziliwekwa na Mungu, na kutambua kwamba Mungu mmoja tu wa kweli Yehova ndiye mfalme wao halisi wa kitheokrasi. . . . Kushika sheria . . . kulitokeza mfululizo wa wafalme wazuri wenye hekima . . . Kwa hiyo Y[uda] ulidumu kwa muda mrefu kuliko ufalme wa kaskazini.” Wafalme hao wazuri walikuwa wachache sana kwa kulinganisha na wale ambao hawakutembea katika njia ya Daudi. Lakini, Yehova aliongoza mambo ili ‘Daudi, mtumishi wake apate kuwa na taa sikuzote mbele zake katika Yerusalemu, mji ule aliouchagua Mungu aweke jina lake huko.’—1 Wafalme 11:36.
Kuelekea Uharibifu
Manase alikuwa mmojawapo wa wafalme wa Yuda ambao waliacha ibada ya kweli. “Akampitisha mwanawe motoni, akatazama bao, akafanya uganga, akajishughulisha na hao wenye pepo wa utambuzi, na wachawi; akafanya mabaya mengi machoni pa BWANA, hata kumkasirisha.” (2 Wafalme 21:6, 16) Mfalme Manase aliwashawishi watu wake “wakazidi kufanya mabaya kuliko mataifa, aliowaharibu BWANA.” Baada ya kumwonya Manase na watu wake kwa kurudia-rudia, Muumba akatangaza: “Nitaifuta Yerusalemu, kama mtu afutavyo sahani.”—2 Mambo ya Nyakati 33:9, 10; 2 Wafalme 21:10-13.
Ukiwa kama utangulizi, Yehova aliwaruhusu Waashuru wamkamate Manase na kumchukua mateka akiwa amefungwa pingu za shaba. (2 Mambo ya Nyakati 33:11) Akiwa uhamishoni Manase akatambua makosa yake na ‘kujinyenyekeza sana mbele za Mungu wa baba zake.’ Yehova alitendaje? “[Mungu] akayasikia maombi yake; akamrudisha tena Yerusalemu katika ufalme wake. Ndipo Manase akajua ya kwamba BWANA [“Yehova,” NW] ndiye Mungu.” Mfalme Manase na mjukuu wake, Mfalme Yosia, wote walifanya marekebisho yaliyotakikana. Lakini, bado taifa hilo halikuacha kabisa upotovu mwingi wa kiadili na wa kidini.—2 Mambo ya Nyakati 33:1-20; 34:1–35:25; 2 Wafalme, sura ya 22.
Jambo la muhimu ni kwamba Yehova aliwatuma manabii wenye bidii wakatangaze maoni yake juu ya mambo yaliyokuwa yakitendeka.d Yeremia alisimulia maneno ya Yehova: “Tokea siku ile baba zenu walipotoka katika nchi ya Misri hata leo, nimewatuma watumishi wangu wote manabii kwenu ninyi, nikiamka mapema kila siku, na kuwatuma.” Lakini watu hawakumsikiliza Mungu. Wao walitenda vibaya hata zaidi ya baba zao! (Yeremia 7:25, 26) Yeye aliwaonya kwa kurudia-rudia “kwa sababu aliwahurumia watu wake.” (Italiki ni zetu.) Bado walikataa kutii. Basi akaruhusu Wababiloni waharibu Yerusalemu na kulifanya ukiwa mnamo 607 K.W.K. Kwa miaka 70 lilibaki ukiwa.—2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16; Yeremia 25:4-11.
Pitio hili fupi la matendo ya Mungu lapasa kutusaidia kutambua hangaiko la Yehova na shughuli zake zenye haki pamoja na taifa lake. Yeye hakuachilia tu mambo na kungoja kuona kile ambacho watu wangefanya, kana kwamba hakujali. Yeye alijaribu kuwasaidia. Unaweza kuthamini ni kwa nini Isaya alisema hivi: “Ee BWANA, wewe u baba yetu . . . sisi sote tu kazi ya mikono yako.” (Isaya 64:8) Kwa kupatana na hayo, wengi leo hurejezea Muumba kuwa “Baba,” kwa kuwa yeye hutenda kama vile baba wa kibinadamu mwenye upendo na mwenye kupendezwa na mambo atendavyo. Hata hivyo, yeye hutambua pia kwamba ni lazima tuchukue daraka la mwendo wetu na matokeo yake.
Baada ya taifa hilo kuwa utekwani kwa kipindi cha miaka 70 Babiloni, Yehova Mungu alitimiza unabii wake wa kurudisha Yerusalemu. Watu waliachiliwa huru na kuruhusiwa kurudi nyumbani ili ‘kuijenga nyumba ya BWANA Yerusalemu.’ (Ezra 1:1-4; Isaya 44:24–45:7) Vitabu kadhaa vya Bibliae vyazungumzia urudisho huo, kujengwa upya kwa hekalu, na matukio yaliyofuata. Mojawapo ya vitabu hivyo, Danieli, hasa ni chenye kupendeza kwa sababu kilitoa unabii juu ya wakati hasa ambapo ile Mbegu, au Mesiya, ingetokea, nacho kilitabiri matukio ya ulimwengu ya wakati wetu.
Hatimaye hekalu lilijengwa upya, lakini Yerusalemu lilikuwa katika hali yenye kusikitisha. Kuta zake na malango yake yalikuwa yamekuwa magofu. Basi Mungu akawateua wanaume kama vile Nehemia ili awatie moyo Wayahudi na kuwapanga. Sala ambayo twaweza kusoma katika Nehemia sura ya 9 inajumlisha ifaavyo shughuli za Yehova pamoja na Waisraeli. Inaonyesha kwamba Yehova ni ‘Mungu aliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema.’ Sala hiyo inaonyesha pia kwamba Yehova hutenda kwa kupatana na viwango vyake vikamilifu vya haki. Hata wakati ambapo ana sababu nzuri ya kudhihirisha uwezo wake wa kutekeleza hukumu, yeye yu tayari kutenda kwa haki na kwa upendo. Kuweza kwake kufanya hivyo kwa usawaziko na kwa njia yenye kuvutia kwahitaji hekima. Kwa wazi, shughuli za Muumba pamoja na taifa la Israeli, zapasa kutuvuta kwake na kutuchochea kutaka kufanya mapenzi yake.
Sehemu hii ya Biblia (Agano la Kale) imalizikapo, Yuda, pamoja na hekalu lake Yerusalemu, lilirudishwa lakini likiwa chini ya utawala wa kipagani. Basi, lile agano la Mungu pamoja na Daudi kuhusu “mbegu” ambayo ingetawala “milele” lingetimizwaje? (Zaburi 89:3, 4; 132:11, 12, linganisha NW.) Wayahudi bado walikuwa wakitazamia kutokea kwa “Masihi aliye mkuu” ambaye angewaweka huru watu wa Mungu na kuweka ufalme wa kitheokrasi (wenye kutawalwa na Mungu) duniani. (Danieli 9:24, 25) Lakini, je, hilo lilikuwa kusudi la Yehova? Kama sivyo, Mesiya aliyeahidiwa angeletaje wokovu? Na jambo hilo latuhusuje leo? Sura ifuatayo itazungumzia masuala haya muhimu.
[Maelezo ya Chini]
a Majina ya vitabu vya Biblia yana maandishi mazito ili kusaidia kutambua yaliyomo.
b Vitabu hivyo ni 1 Samweli, 2 Samweli, 1 Wafalme, 2 Wafalme, 1 Mambo ya Nyakati, na 2 Mambo ya Nyakati.
c Pia aliandika Wimbo Ulio Bora, shairi la mapenzi linalokazia uaminifu-mshikamanifu wa mwanamke kijana kwa mchungaji mnyenyekevu.
d Vitabu kadhaa vya Biblia vina ujumbe kama huo uliopuliziwa. Vitabu hivyo vinatia ndani Isaya, Yeremia, Maombolezo, Ezekieli, Yoeli, Mika, Habakuki, Sefania. Vitabu vya Obadia, Yona, na Nahumu vilikazia mataifa jirani ambayo shughuli zao ziliathiri watu wa Mungu.
e Hivi vitabu vya historia na unabii vyatia ndani Ezra, Nehemia, Esta, Hagai, Zekaria, na Malaki.
[Sanduku katika ukurasa wa 126, 127]
Miujiza—Je, Unaweza Kuiamini?
“Haiwezekani kukubali tekinolojia ya kisasa kama vile taa za umeme, redio na maendeleo ya kitiba, na wakati huohuo kuamini roho na miujiza ya Agano Jipya.” Maneno hayo ya mwanatheolojia Mjerumani Rudolf Bultmann yaonyesha maoni ya watu wengi leo juu ya miujiza. Je, una maoni kama hayo kuhusu miujiza iliyorekodiwa katika Biblia, kama ule ambao Mungu aligawanya Bahari Nyekundu?
Kamusi The Concise Oxford Dictionary yafafanua “muujiza” kuwa “tukio lisilo la kawaida ambalo limesababishwa na nguvu zipitazo za wanadamu.” Tukio kama hilo lisilo la kawaida lahusisha kuvurugwa kwa utaratibu wa asili, jambo linalofanya wengi wasiamini miujiza. Lakini, kile kionekanacho kuwa kuvunja sheria ya asili chaweza kuelezwa kwa kufikiria sheria nyinginezo za asili zinazohusika.
Kwa mfano, gazeti New Scientist liliripoti kwamba wataalamu wawili wa fizikia katika Chuo Kikuu cha Tokyo walitumia sumaku yenye nguvu sana kwenye mrija uliolazwa ambao ulitiwa maji kwa kiasi. Maji yalikimbilia miisho ya huo mrija, sehemu ya katikati ikakauka. Tukio hilo, lililogunduliwa mnamo 1994, linatokea kwa sababu maji husukumwa kihafifu na sumaku. Tukio hilo lililothibitishwa la maji kutoka penye nguvu nyingi za sumaku hadi mahali ambapo hapana nguvu nyingi za sumaku limeitwa Athari ya Moses. Gazeti New Scientist lilisema kwamba: “Ni rahisi kusukuma-sukuma maji—ikiwa una sumaku kubwa ya kutosha. Na ikiwa hivyo, karibu kitu chochote kinawezekana.”
Bila shaka, mtu hawezi kusema kwa uhakika kabisa njia ambayo Mungu alitumia kugawanya Bahari Nyekundu kwa ajili ya Waisraeli. Lakini, Muumba ajua kabisa sheria zote za asili. Yeye angeweza kudhibiti kwa urahisi sehemu fulani ya sheria moja kwa kutumia sheria nyinginezo ambazo alifanyiza. Kwa wanadamu, matokeo yaweza kuonekana kuwa ya kimuujiza, hasa kama hawakujua vizuri sheria zilizohusika.
Kuhusu miujiza iliyo katika Biblia, Akira Yamada, profesa mstaafu wa Chuo Kikuu cha Kyoto nchini Japani, asema: “Ingawa ni sahihi kusema kwamba [muujiza] hauwezi kueleweka kwa sasa kutokana na maoni ya kisayansi ambayo mtu amejihusisha nayo (au maoni ya sasa ya sayansi), ni makosa kukata kauli kwamba haukufanyika, kwa kutegemea tu fizikia bora ya kisasa au elimu bora ya kisasa ya Biblia. Miaka kumi tokea sasa, sayansi ya kisasa ya leo itakuwa sayansi iliyopita. Kadiri sayansi ifanyavyo maendeleo haraka ndivyo uongezekavyo uwezekano wa kwamba wanasayansi wa leo watakuwa wakidhihakiwa hivi, ‘Wanasayansi wa miaka kumi iliyopita walishikilia hili na hili.’”—Gods in the Age of Science.
Akiwa Muumba, akiweza kuratibu sheria zote za asili, Yehova aweza kutumia uwezo wake ili kufanyiza miujiza.
[Sanduku katika ukurasa wa 132, 133]
Mungu Mwenye Wivu—Katika Maana Gani?
“Yehova, ambaye jina lake ni Wivu, yeye ni Mungu mwenye wivu.” Twaweza kusoma maneno hayo katika Kutoka 34:14 (NW), lakini yanamaanisha nini?
Neno la Kiebrania lililotafsiriwa “wivu” laweza kumaanisha “kudai ujitoaji usiohusisha wengine, kutovumilia ushindani.” Katika maana nzuri inayonufaisha viumbe wake, Yehova ni mwenye wivu kuhusu jina lake na ibada yake. (Ezekieli 39:25) Bidii yake ya kutimiza kile ambacho jina lake lawakilisha yamaanisha kwamba yeye atatekeleza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu.
Kwa mfano, ebu fikiria hukumu yake dhidi ya watu walioishi katika bara la Kanaani. Msomi mmoja aeleza mambo haya yenye kushtua: “Ibada ya Baali, Ashtorethi, na miungu mingine ya Kanaani ilikuwa na desturi zenye kushangaza sana; mahekalu yao yalikuwa vitovu vya upotovu wa maadili. . . . Wakanaani waliabudu kwa kujiingiza sana katika ibada ya ukosefu wa adili, . . . kisha, waliwaua watoto wao wa kwanza kuwa dhabihu kwa miungu iyo hiyo.” Wataalamu wa mambo ya kale wamegundua magudulia yenye mabaki ya watoto waliotolewa dhabihu. Ingawa Mungu aliona kosa la Wakanaani katika siku za Abrahamu, yeye aliwaonyesha subira kwa miaka 400, akiwaruhusu muda wa kutosha wa kubadilika.—Mwanzo 15:16.
Je, Wakanaani walijua uzito wa kosa lao? Wao walikuwa na dhamiri ya kibinadamu, ambao wanasheria hutambua kuwa msingi wa ulimwenguni pote wa maadili na haki. (Waroma 2:12-15) Japo hayo, Wakanaani waliendelea kutoa dhabihu zenye kuchukiza za watoto na matendo yaliyopotoka ya kingono.
Kwa haki yake yenye usawaziko, Yehova aliazimia kwamba bara hilo lilihitaji kutakaswa. Hilo halikuwa uchinjaji wa jamii nzima-nzima. Wakanaani, wakiwa watu mmoja-mmoja kama vile Rahabu na vikundi-vikundi kama vile Wagibeoni, ambao walikubali kwa hiari viwango vya juu vya maadili vya Mungu hawakuuawa. (Yoshua 6:25; 9:3-15) Rahabu akaja kuwa katika nasaba ya kifalme iliyoelekeza kwa Mesiya, na wazao wa Wagibeoni walikuwa na pendeleo la kuhudumu katika hekalu la Yehova.—Yoshua 9:27; Ezra 8:20; Mathayo 1:1, 5-16.
Basi, mtu atafutapo habari kamili inayotegemea mambo ya hakika, ni rahisi kumwona Yehova kuwa Mungu avutiaye na mwenye haki, mwenye wivu katika njia nzuri inayonufaisha viumbe wake waaminifu.
[Picha katika ukurasa wa 123]
Muumba aliwakomboa watu waliofanywa kuwa watumwa na kuwatumia kutekeleza kusudi lake
[Picha katika ukurasa wa 129]
Kwenye Mlima Sinai taifa la kale la Israeli liliingia katika uhusiano wa agano pamoja na Muumba
[Picha katika ukurasa wa 130]
Kushika amri za Muumba zisizo na kifani kulisaidia watu wake wafurahie Bara Lililoahidiwa
[Picha katika ukurasa wa 136]
Unaweza kuzuru eneo lililo kusini mwa ukuta wa Yerusalemu ambapo Mfalme Daudi alifanyiza makao yake makuu