Kwa Nini Tunakufa?
“Juu ya vichwa vya milima ni kimya sasa, katika vichwa vya miti hausikii sauti hata kidogo; ndege wanalala katika miti: ngoja; karibuni kama hawa utapumzika.”—JOHANN WOLFGANG VON GOETHE, MSHAIRI MJERUMANI.
1, 2. (a) Watu waliumbwa wakiwa na tamaa gani? (b) Watu wawili wa kwanza walifurahia maisha ya namna gani?
MUNGU aliumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuishi milele. Kwa kweli, Biblia husema kwamba ameweka “milele vilevile ndani ya mioyo yao.” (Muhubiri 3:11) Lakini Mungu alifanya zaidi kuliko kuwapa tu wanadamu tamaa ya kuishi milele. Yeye pia aliwatolea uwezekano wa kuishi milele.
2 Wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, waliumbwa wakamilifu, bila kasoro akilini au mwilini. (Kumbukumbu 32:4) Fikiri—hakukuwa maumivu yenye kuendelea wala uchungu, hakukuwa hofu yenye kutisha wala mahangaiko! Zaidi tena, Mungu aliwaweka katika makao-paradiso yenye kupendeza. Mungu alikusudia kwamba mtu aweze kuishi milele na halafu dunia ingejaa na uzao wake mkamilifu. (Mwanzo 1:31; 2:15) Basi, kwa nini tunakufa?
Kutotii Kwaleta Kifo
3. Uzima wa milele wa Adamu na Hawa ulitegemea nini?
3 Mungu alimuamuru Adamu hivi: “Wa kila muti wa shamba unaweza kula; lakini wa muti wa kujua uzuri na ubaya usile kwa maana siku unapokula, hakika utakufa.” (Mwanzo 2:16, 17) Kwa hiyo, uzima wa milele wa Adamu na Hawa ulitiliwa sharti; ulitegemea utii wao kwa Mungu.
4. Adamu na Hawa walipofanya dhambi, kwa nini walipoteza tazamio la kuishi milele katika Paradiso?
4 Lakini, kwa huzuni Adamu na Hawa hawakutii sheria ya Mungu. (Mwanzo 3:1-6) Kwa kufanya hivyo, wakawa wafanya dhambi, kwa kuwa “dhambi ni uasi-sheria.” (1 Yohana 3:4) Matokeo ni kwamba Adamu na Hawa hawakuwa tena kamwe na tazamio la uzima wa milele. Kwa nini? Kwa sababu “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Hivyo, alipotamka hukumu juu ya Adamu na Hawa, Mungu alisema: “Mavumbi wewe, na utarudi kwa mavumbi.” Ndipo wazazi wetu wa kwanza wakafukuzwa katika makao yao ya kiparadiso. Siku hiyo walipotenda dhambi, Adamu na Hawa wakaanza polepole lakini kwa uthabiti hatua ya kifo.—Mwanzo 3:19, 23, 24.
“Kifo Kikasambaa kwa Watu Wote”
5. Namna gani kifo kilisambaa kwa jamii yote ya kibinadamu?
5 Sasa Adamu na Hawa wakawa na dhambi iliyoingia sana katika jeni zao. Kwa hiyo, hawangeliweza kutokeza uzao wenye kukamilika, kama vile chombo cha kupikia mkate chenye kasoro hakiwezi kutokeza kitu chenye kukamilika. (Yobu 14:4) Kweli, kila kuzaliwa kwa mtu kwahakikisha kwamba wazazi wetu wa kwanza walipoteza afya kamilifu na uzima wa milele kwao wenyewe na kwa uzao wao. Mtume Mkristo Paulo aliandika: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12; linganisha Zaburi 51:5.
6. Kwa nini tunakufa?
6 Leo wanasayansi hawajui hakika kwa nini watu huzeeka na kufa. Lakini, Biblia hufasiria kwamba tunakufa kwa sababu tunazaliwa tukiwa wenye dhambi, tukiwa tumerithi hali hii kutoka wazazi wetu wa kwanza wa kibinadamu. Lakini, jambo gani hutufikia tunapokufa?