Jambo Gani Huifikia Nafsi Wakati wa Kifo?
“Fundisho la kwamba nafsi ya mwanadamu ni isiyoweza kufa na kwamba itaendelea kuwako baada ya kufa kwa mtu na kuharibika kwa mwili wake ni mojapo wa fundisho la msingi la falsafa na teolojia ya Ukristo.”—“NEW CATHOLIC ENCYCLOPEDIA.”
1. New Catholic Encyclopedia chakubali nini kuhusu kuokoka kifo kwa nafsi?
LAKINI, rejezeo hilo hilo lakubali kwamba “wazo la kuendelea kuishi kwa nafsi baada ya kifo halitambulikani kabisa katika Biblia.” Hivyo, basi, Biblia kwa kweli hufundisha nini kuhusu jambo ambalo huifikia nafsi wakati wa kifo?
Wafu Hawajui Lolote
2, 3. Wafu wanayo hali gani, na ni maandiko gani yanayofunua hilo?
2 Hali ya wafu yaonyeshwa wazi kwenye Muhubiri 9:5, 10, ambapo twasoma hivi: “Wafu hawajui kitu . . . hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima ndani ya kaburi.” Kwa hiyo, kifo ni hali ya kutokuwako. Mtunga-Zaburi aliandika kwamba wakati mtu anapokufa, “anarudia udongo wake; siku ileile mafikili yake yanapotea.”—Zaburi 146:4.
3 Basi, wafu hawajui lolote, ni wasiotenda. Alipotamka hukumu juu ya Adamu, Mungu alisema: “Mavumbi wewe, na utarudi kwa mavumbi.” (Mwanzo 3:19) Kabla ya Mungu kumfanya kutoka katika mavumbi ya ardhi na kumpa uhai, Adamu hakuwako. Adamu alipokufa, alirudi katika hali ileile. Adhabu yake ilikuwa kifo—na si kuhama kwenda makao mengine.
Nafsi Yaweza Kufa
4, 5. Toa mifano kutoka Biblia, inayoonyesha kwamba nafsi yaweza kufa.
4 Adamu alipokufa, jambo gani liliifikia nafsi yake? Kumbuka kwamba katika Biblia neno “nafsi” kwa kawaida huelekeza kwa mtu. Basi, tunaposema kwamba Adamu alikufa, tunamaanisha kwamba nafsi iliyoitwa Adamu ilikufa. Kwa mtu ambaye huamini katika kutoweza kufa kwa nafsi hilo linaweza kuonekana kuwa jambo geni. Hata hivyo, Biblia yaeleza hivi: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4) Walawi 21:1 husimulia juu ya “nafsi iliyokufa” (“wafu,” Zaïre Swahili Bible). Na wanaziri waliambiwa kwamba wasikaribie “nafsi yoyote iliyokufa” (“maiti,” ZSB).—Hesabu 6:6.
5 Rejezeo linalofanana na hilo kuhusu nafsi lapatikana kwenye 1 Wafalme 19:4. Eliya mwenye kutaabishwa vikali sana ‘alianza kuomba kwamba nafsi yake iweze kufa.’ Vivyo hivyo, Yona aliendelea kuomba kwamba nafsi yake iweze kufa, naye alirudilia kusema hivi: “Ni vema kwangu kufa kuliko kuishi.” (Yona 4:8) Na Yesu alitumia usemi “kuua nafsi,” ambao Zaïre Swahili Bible huutafsiri “kuua.” (Marko 3:4) Basi, kifo cha nafsi chamaanisha tu kifo cha mtu.
‘Kutoka’ na ‘Kurudi’
6. Biblia inamaanisha nini isemapo kwamba nafsi ya Raheli ilikuwa “ikitoka“?
6 Lakini namna gani kuhusu kifo chenye kutia huzuni cha Raheli, kilichotukia alipokuwa akizaa mwana wake wa pili? Tunasoma kwenye Mwanzo 35:18 hivi: “Na ilikuwa wakati alipokuwa akikata roho [nafsi yake ilikuwa ikimtoka, NW] (kwa sababu alikufa) akaita jina lake Benoni; lakini baba yake alimwita Benyamina.” Je! andiko hili lamaanisha kwamba Raheli alikuwa na kiumbe kingine cha ndani ambacho kiliondoka wakati wa kufa kwake? La, Hasha! Kumbuka, neno “nafsi” laweza kuelekeza kwa uhai alio nao mtu. Basi, katika kisa hiki “nafsi” ya Raheli ilimaanisha tu “uhai” wake. Ndiyo sababu Biblia zingine hutafsiri usemi huu ‘nafsi yake ilikuwa ikimtoka’ kuwa ‘uhai wake ulikuwa ukitoka’ (Knox), “alivuta pumzi yake ya mwisho” (Jerusalem Bible), na ‘uhai wake ulimtoka’ (Bible in Basic English). Hakuna jambo fulani linaloonyesha kwamba sehemu ya kifumbo ya Raheli iliendelea kuishi baada ya kifo chake.
7. Katika njia gani yasemwa kwamba nafsi ya mwana aliyefufuliwa wa mjane “ilimurudia”?
7 Jambo lenye kufanana na hilo ni ufufuo wa mwana wa mjane, unaorekodiwa kwenye 1 Wafalme sura ya 17. Katika mstari wa 22, twasoma kwamba kadiri Eliya alivyosali kwa ajili ya kijana, “BWANA [Yehova, NW] alisikiliza sauti ya Eliya; roho [nafsi, NW] ya mutoto ilimurudia, akafufuka.” Mara nyingine tena, neno “nafsi” lamaanisha “uhai.” Hivyo, New American Standard Bible husomwa: “Uhai wa mtoto ukamrudia naye akaishi tena.” Ndiyo, ulikuwa uhai, wala si kitu chenye kivuli, uliomrudia tena kijana huyo. Hilo lapatana na yale Eliya alimwambia mama ya mtoto huyo: “Tazama, mwana wako [mtu kamili] anaishi.”—1 Wafalme 17:23.
Shaka la Wazo la “Hali ya Katikati”
8. Watu wengi wanaojidai kuwa Wakristo wanaamini jambo gani litatokea wakati wa ufufuo?
8 Wengi wanaokiri kuwa Wakristo wanaamini kwamba kutakuwa na ufufuo wakati ujao ambapo mwili utaungana na nafsi zisizoweza kufa. Ndipo, wafufuliwa watakuwa mbele ya tokeo lao la mwisho—ama thawabu kwa wale waliyoongoza uhai wao vizuri au kisasi kwa waovu.
9. Usemi “hali ya katikati” wamaanisha nini, nao wengine husema jambo gani huifikia nafsi katika kipindi hicho?
9 Wazo hili laonekana kuwa jepesi. Lakini wale wanaoshikamana na imani ya kutoweza kufa kwa nafsi wanayo matatizo ya kufasiria jambo linaloifikia nafsi kati ya wakati wa kufa na wakati wa ufufuo. Kwa kweli, hii “hali ya katikati,” kama itwavyo kwa kawaida, imechochea kufikiri-fikiri kwa karne nyingi. Wengine husema kwamba katika kipindi hicho nafsi huenda kwenye pirigatori, ambapo yaweza kutakaswa na dhambi ndogo na hivyo kuwa yenye kustahili kuingia mbinguni.a
10. Kwa nini haipatani na maandiko kuamini kwamba nafsi zinaendelea kukaa kwa muda katika pirigatori baada ya kifo, na namna gani jambo lililompata Lazaro lahakikisha hilo?
10 Walakini, kama tulivyoona, nafsi ni mtu mwenyewe. Mtu anapokufa, nafsi inakufa. Kwa hiyo, hakuna maisha yenye ufahamu baada ya kifo. Kwa kweli, Lazaro alipokufa, Yesu Kristo hakusema kwamba alikuwa katika pirigatori, katika Limbo, au katika “hali ya katikati” nyingine yoyote. Badala yake, Yesu alisema tu: “Lazaro analala usingizi.” (Yohana 11:11, ZSB) Bila shaka, Yesu, aliyejua kweli kuhusu jambo linaloipata nafsi wakati wa kifo, aliamini kwamba Lazaro hakuwa na ufahamu, hakuwako.
Roho Ni Nini?
11. Kwa nini neno “roho” halingeweza kuelekeza kwa sehemu ya mtu isiyo na mwili inayookoka kifo?
11 Biblia yasema kwamba wakati mtu anapokufa, “pumuzi [roho, NW] yake inatoka, anarudia udongo wake.” (Zaburi 146:4) Je! hilo lamaanisha kwamba roho isiyo na mwili huondoka kihalisi na kuendelea kuishi baada ya kifo cha mtu? Haiwezekani iwe hivyo, kwa kuwa mtunga-zaburi asema tena: “Siku ile ile mafikili yake yanapotea” (“fikira zake hukoma,” New English Bible). Basi, roho ni nini, na namna gani ‘inamtoka’ mtu wakati wa kufa kwake?
12. Katika Biblia, maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa “roho” yamaanisha nini?
12 Katika Biblia, maneno yaliyotafsiriwa “roho” (Kiebrania, ruʹach; Kigiriki, pneuʹma) kwa msingi yamaanisha “pumzi.” Hivyo, badala ya ‘roho yake inatoka,’ tafsiri ya R. A. Knox yatumia usemi “pumzi yauacha mwili wake.” (Zaburi 145:4, Knox) Lakini, neno “roho” lamaanisha mengi zaidi kuliko tendo la kupumua. Kwa mfano, katika kuelezea uharibifu wa uhai wa binadamu na mnyama wakati wa Garika la ulimwenguni pote, Mwanzo 7:22 husema: “Wote waliokuwa na pumuzi ya roho [kani, NW] [au, roho; Kiebrania: ruʹach] ya uzima kwa pua yao, wa wote waliokuwa katika inchi kavu, wakakufa.” Basi, “roho” yaweza kuelekeza kwa kani ya uhai ambayo hutenda katika viumbe vyote vinavyoishi, wanadamu na wanyama, na ambayo hutegemezwa na kupumua.
13. Katika njia gani roho yaweza kulinganishwa na mkondo wa umeme?
13 Tutoe kielezo: Mkondo wa umeme hutoa nguvu kwa vifaa mbalimbali. Mkondo ukisimama, vifaa vinaacha kufanya kazi. Mkondo hauwi chombo kingine kinachoachana na vifaa. Jambo lenye kufanana, mtu anapokufa, roho yake inaacha kuzitia nguvu chembe za mwili. Roho haiuachi mwili na kuendelea mpaka makao mengine.—Zaburi 104:29.
14, 15. Namna gani roho hurudi kwa Mungu wakati wa kifo?
14 Basi, kwa nini Muhubiri 12:7 hueleza kwamba mtu anapokufa, “roho inarudi kwa Mungu aliyeitoa”? Je! hilo lamaanisha kwamba roho yasafiri kihalisi kupitia anga kwenda mpaka aliko Mungu? Haimaanishi hivyo. Kumbuka, roho ni kani ya uhai. Mara tu hiyo kani ya uhai kuondoka, Mungu pekee ndiye anao uwezo wa kuirudisha tena. Basi, roho “inarudi kwa Mungu” katika maana ya kwamba tumaini lolote la uhai kwa wakati ujao kumhusu mtu huyo sasa linabaki kabisa kwa Mungu.
15 Mungu pekee ndiye awezaye kuirudisha roho, au kani ya uhai, kusababisha mtu arudi tena kwenye uhai. (Zaburi 104:30) Lakini, je! Mungu ana kusudi la kufanya hivyo?
[Maelezo ya Chini]
a Kulingana na New Catholic Encyclopedia, “Kwa ujumla Mababa wa [Kanisa] huwa wazi katika uthibitisho wao wa kuwako kwa pirigatori.” Lakini, kitabu hiki cha marejezo pia chakubali kwamba “fundisho la Kikatoliki kuhusu pirigatori lategemea juu ya pokeo, na si juu ya Andiko Takatifu.”
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
KUMBUKUMBU ZA UHAI ULIOTANGULIA
IKIWA hakuna kitu kinachoendelea kuishi kisha kufa kwa mwili, basi namna gani kuhusu kumbukumbu za uhai uliotangulia ambazo wengine hudai kuwa nazo?
Msomi mhindu Nikhilananda asema kwamba ‘mambo yanayoonwa baada ya kifo hayawezi kuonyeshwa kwa kutoa sababu.’ Katika hotuba “Vielelezo vya Imani katika Umilele katika Dini,” mwanateolojia Hans Küng aonyesha wazi: “Hakuna hata moja ya habari—zinazotoka kwa kawaida kwa watoto au kutoka nchi ambako watu huamini katika kuzaliwa upya katika mwili mwingine—za kumbukumbu la uhai uliotangulia zinazoweza kuthibitishwa.” Yeye aongeza: “Wengi wa [watafiti wanaotumika kwa bidii na kisayansi kuhusu jambo hilo hukubali kwamba uchunguzi uliofanywa nao hautoi msingi wa uthibitisho wa kweli wenye kusadikisha kweli kweli wa kurudia-rudia kwa uhai wa kidunia.”
Lakini namna gani ikiwa unahisi kwamba wewe unazo kumbukumbuku za kipekee za uhai uliotangulia? Kuhisi huko kwaweza kutokana na mambo mengi. Nyingi za habari tunazopokea zinalindwa akiba mbali katika ncha zenye kufichama za ufahamu wa akili zetu kwa sababu matumizi yazo si ya moja kwa moja au ya papo hapo. Wakati kumbukumbu zilizosahauliwa zinaporudi tena, watu wengine hueleza hayo kuwa uhakika wa uhai wa zamani. Hata hivyo, jambo hakika ni kwamba hatuna uchunguzi wenye kuthibitishwa wa uhai kuliko huu ambao tunaishi sasa. Watu walio wengi wanaoishi duniani hawana kumbukumbu juu ya jambo la kwamba waliishi mapema, wala hawafikiri kwamba huenda walikuwa na uhai uliotangulia.