Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 9/1 kur. 4-6
  • Je! Nafsi Huendelea Kuishi Baada ya Kifo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Nafsi Huendelea Kuishi Baada ya Kifo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Si Fundisho la Biblia
  • Ni Nini Hutukia Baada ya Kifo?
  • Kutoka Fundisho la Kipagani
  • Tumaini kwa Wafu
  • Nafsi Kulingana na Biblia
    Ni Nini Hutupata Tunapokufa?
  • Je, Una Nafsi Isiyoweza Kufa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Maoni Yako Juu ya Nafsi Huathiri Uhai Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Nafsi Yako Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 9/1 kur. 4-6

Je! Nafsi Huendelea Kuishi Baada ya Kifo?

“NAFSI: Sehemu ya kiroho ya binadamu ambayo huchukuliwa kwamba huendelea kuwa hai baada ya kifo na kuwa yaweza kupata furaha au mateso katika hali ya wakati ujao.” (The Compact Edition of the Oxford English Dictionary) Dini zilizo nyingi huafikiana na fasili hiyo kwa kadiri fulani. New Catholic Encyclopedia husema: “Fundisho la kwamba nafsi ya kibinadamu haifi na huendelea kuwa hai baada ya kifo cha binadamu . . . ni moja la mawe ya pembeni ya falsafa na theolojia ya Kikristo.”

Basi, labda ingekushangaza kujua kwamba imani hiyo iliyo jiwe la pembeni imetolewa katika falsafa ya kipagani. Muda mrefu kabla ya uzaliwa wa Yesu, iliaminiwa kwamba nafsi ilikuwa kitu kisichogusika ambacho kingeweza kuwako kando na mwili. Hivyo kingeweza kuendelea kuwa hai baada ya kifo cha mwili, kiendelee kuishi kwa namna ya mzuka, au roho.

Wagiriki walipambanua imani hii kwa maneno ya kifalsafa. Socrates, mwanafalsafa maarufu Mgiriki, amenukuliwa kuwa akisema: “Nafsi, . . . ikiondoka pweke-pweke, bila kwenda ikikokota sehemu yoyote ya mwili, . . . huenda kuingia ndani ya kile ambacho chafanana nayo yenyewe, ndani ya kile kisichoonekana, cha kimungu, kisichokufa, na chenye hekima, nayo iwasilipo huko huwa yenye furaha, kuwekwa huru kutoka kwenye makosa na upumbavu na hofu . . . na kasoro nyingine zote za kibinadamu, na . . . huishi katika ukweli wakati wote baada ya hapo ikiwa pamoja na miungu.”—Phaedo, 80, D, E; 81, A.

Si Fundisho la Biblia

Basi, je! hii imani ya kipagani katika kutokufa kwa nafsi ilikujaje kufundishwa katika Jumuiya ya Wakristo na Dini ya Kiyahudi?

New Catholic Encyclopedia huwa haitii mkazo wa kutosha isemapo: “Wazo la nafsi ikiendelea kuwa hai baada ya kifo halifahamiki kwa utayari katika Biblia.” Ingekuwa sahihi zaidi kusema kwamba fundisho la kutokufa kwa nafsi halipatikani hata kidogo katika Biblia! Ensaiklopedia hiyo yakiri hivi: “Katika A[gano] la K[ale] dhana inayohusu nafsi ya kibinadamu haiko kama vile ilivyo katika falsafa ya Kigiriki na ya ki-siku-hizi.”

Katika hilo liitwalo Agano la Kale, neno la Kiebrania neʹphesh, ambalo kwa kawaida hutafsiriwa “nafsi,” hutukia mara 754. Katika lile liitwalo Agano Jipya, neno la Kigiriki psy·kheʹ, ambalo kwa kawaida pia hutafsiriwa “nafsi,” huonekana mara 102. Tuchunguzapo jinsi maneno hayo yatumiwavyo katika Biblia, maoni ya kushangaza huibuka.

Kwenye Mwanzo 2:7 twasoma kwamba Mungu alipuliza pumzi ya uhai ndani ya mianzi ya pua ya Adamu, na Adamu “akawa nafsi hai [Kiebrania, neʹphesh].” Angalia: Adamu hakupewa nafsi hai; yeye alipata kuwa moja. Ndiyo kusema, Adamu aliyekuwa ameumbwa hivi karibuni alikuwa nafsi! Si ajabu sana kwamba New Catholic Encyclopedia hukata shauri hivi: “Nafsi katika A[gano] la K[ale] haimaanishi sehemu fulani ya binadamu, bali binadamu mzima—binadamu akiwa mtu hai.”

Maandiko mengine huhakikisha hilo. Kwa kielelezo, Walawi 7:20, NW, hurejezea “nafsi ilayo mnofu wa dhabihu ya ushirika.” Walawi 23:30, NW, husema: “Kwa habari ya nafsi yoyote ambayo itafanya namna yoyote ya kazi.” Mithali 25:25, NW, husema: “Kama maji baridi juu ya nafsi iliyochoka, ndivyo ilivyo ripoti njema kutoka bara la mbali.” Na Zaburi 105:18, The Old Testament in Swahili (Mombasa), hutuambia hivi: “Walimuudhi maguu yakwe kwa pingu; nafusi yakwe iliingia vyumani.” Sasa, ni nini kiwezacho kula nyama, kufanya kazi, kuburudishwa kwa maji, na kutiwa katika vyuma? Je! ni sehemu fulani ya kiroho ya binadamu iliyo tofauti na yeye, au ni binadamu mwenyewe? Jibu liko wazi.

Kwa kupendeza, si binadamu peke yake aliye nafsi. Mwanzo 1:20 hutuambia kwamba katika muhula mmoja wa uumbaji, Mungu alisema: “Maji na yajawe kwa wingi na kitu kiendacho chenye uhai [nafsi, NW].” Ndiyo, hata samaki ni nafsi! Katika muhula mwingine wa uumbaji, Mungu alionyesha kwamba “mnyama wa kufugwa, nacho kitambaacho, na wanyama wa mwitu” ni nafsi!—Mwanzo 1:24; linganisha Walawi 11:10, 46; 24:18; Hesabu 31:28; Ayubu 41:21; Ezekieli 47:9.

Kwa hiyo, katika Biblia, “nafsi” hairejezei roho fulani iliyo kivuli ambayo huuacha mwili baada ya kifo. Humaanisha mtu au mnyama, au maisha ambayo mtu au mnyama huuonea shangwe.

Ni Nini Hutukia Baada ya Kifo?

Basi, kwa wazi Biblia yapingana na wazo la kipagani kwamba binadamu ana nafsi isiyokufa. Wewe wafikiri ni nani aliyefundisha ukweli katika habari hii? Ni wanafalsafa Wagiriki wa kipagani au ni watu wa agano la Mungu mwenyewe? Kwa uhakika, ni watu wa Mungu, ambao yeye aliwapa Neno lake lililovuviwa.

Na bado swali labaki, Ni nini hupata nafsi baada ya kifo? Kwa kuwa nafsi ndiyo mtu, kwa wazi nafsi hufa mtu afapo. Ndiyo kusema, mtu mfu ni nafsi iliyokufa. “Hiyo nafusi ya mtu ifanyayo dhambi ndiyo itakayokufa,” yasema Ezekieli 18:4, OTSW (Mombasa). Kwenye Waamuzi 16:30, twasoma: “Samsoni akasema; Na nife [acha nafsi yangu ife, NW] pamoja na hawa Wafilisti.” Maandiko mengine huonyesha kwamba nafsi zaweza kukatiliwa mbali (Mwanzo 17:14), kuchinjwa na upanga (Yoshua 10:37, NW), kusongwa pumzi (Ayubu 7:15), na kufa maji (Yona 2:5). Nafsi iliyoacha kuishi, au nafsi iliyokufa, ni mtu mfu.—Walawi 19:28; 21:1, 11, NW.

Basi, ni nini hali ya nafsi iliyokufa? Kwa kutaarifu kisahili, kifo ni kinyume cha uhai. Hisi zetu zote zimeungana na miili yetu halisi. Uwezo wetu wa kuona, kusikia, na kufikiri hutegemea utendaji ufaao wa macho, masikio, na ubongo wetu. Bila macho hatuwezi kuona. Bila masikio hatuwezi kusikia. Bila ubongo hatuwezi kufanya lolote. Mtu afapo, viungo vyote hivi vya kimwili hukoma kufanya kazi. Sisi hukoma kuwako.

Kwa kupatana na hilo, Mhubiri 9:5, 10, OTSW (Mombasa), husema: “Hao waliokufa hawajui neno lolote . . . Hapana kazi, wala hisabu, wala ujuzi, wala akili ndani ya kaburi wendeako.” Vivyo hivyo, Zaburi 146:3, 4, HNWW, hutaarifu: “Msiwategemee wakuu wa dunia; hao ni binadamu tu, hawawezi kuokoa. Binadamu akitoa pumzi yake ya mwisho, anarudi mavumbini alimotoka; na hapo mipango yake yote hutoweka.” Kwa hiyo watu (nafsi) wafapo, wao hukoma kuwako.

Kutoka Fundisho la Kipagani

Hadi Fundisho la Kanisa

‘Lakini je! Agano Jipya halifundishi kutokufa kwa nafsi?’ huenda watu fulani wakauliza. Sivyo hata kidogo. New Catholic Encyclopedia hukiri hivi: “A[gano] J[ipya] hubaki na uaminifu kwa uelewevu huu wa A[gano] la K[ale] juu ya kifo.” Ndiyo kusema, “Agano Jipya” hufundisha kwamba nafsi hufa. Yesu Kristo alionyesha kwamba yeye hakuamini kuwa nafsi haifi. Aliuliza: “Ni halali siku ya sabato kutenda mema, au kutenda mabaya? kuponya roho [nafsi, NW] au kuiua?” (Marko 3:4) Vilevile mtume Mkristo Paulo aliunga mkono maoni ya “Agano la Kale” juu ya nafsi kwa kunukuu Mwanzo 2:7: “Ndivyo ilivyoandikwa, Mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyo hai.”—1 Wakorintho 15:45.

Basi, je! fikira ya Kiplato ilikujaje kuwa fundisho la kanisa? Encyclopædia of Religion and Ethics, ya James Hastings, hueleza hivi: “Wakati gospeli ya Kikristo ilipotoka nje kwa kupitia lango la sinagogi la Kiyahudi na kuingia uwanja wa mapambano wa Milki ya Kiroma, wazo la nafsi lililokuwa la Kiebrania kabisa lilihamishwa likaingizwa katika mazingira ya wazo la Kigiriki, na wakati wa kufanya mrekebisho huo kukawa na matokeo mazito.” Walimu wa makanisa walijaribu kufanya ujumbe wao “[usikike] kuwa wa kiakili kwa ulimwengu wenye fikira za Kigiriki” kwa kutumia “maneno na dhana zilizoimarika za saikolojia ya Kigiriki.” Vilevile wanatheolojia Wagiriki walianza kuonyesha “mavutano imara ya kufuata mawazo ya Plato” katika miandiko yao.—Encyclopedia Judaica.

Hivyo fundisho la Kibiblia juu ya nafsi lilitupiliwa mbali na mahali palo pakachukuliwa na fundisho ambalo pasipo shaka lilikuwa la kipagani. Jambo hilo haliwezi kamwe kutetewa kwamba lilikuwa la haki eti kwa sababu kufanya hivyo kulifanya Ukristo uvutie halaiki za watu. Alipokuwa akihubiri katika Athene, ambapo hasa palikuwa ndipo moyo wa utamaduni wa Kigiriki, mtume Paulo hakufundisha fundisho la Kiplato juu ya nafsi. Kwa kinyume, alihubiri fundisho la Kikristo juu ya ufufuo hata ingawa wengi wa wasikilizaji wake waliona ikiwa vigumu kukubali aliyosema.—Matendo 17:22-32.

Kwa kweli, mtume Paulo alionya dhidi ya mwunganisho wowote wa ukweli wenye msingi wa Biblia na upagani aliposema: “Pana shirika gani kati ya nuru na giza? Tena pana ulinganifu gani kati ya Kristo na Beliari?” (2 Wakorintho 6:14, 15) Hakuwezi kuwa na shaka lolote kwamba katika kuruhusu fundisho la kipagani liwe moja la mawe ya pembeni ya falsafa na theolojia yayo, Jumuiya ya Wakristo imemvunjia heshima Mungu mwenyewe!

Tumaini kwa Wafu

Watu wako huru kuamini wachagualo. Hata hivyo, haiwezi kukanwa kwamba fundisho la kutokufa kwa nafsi si la Kimaandiko. Basi, je! wanadamu hawana tumaini la kuwa na uhai baada ya kifo?

Baada ya Ayubu kuuliza lile swali, “Je! [binadamu] atakuwa hai tena?” aliendelea kutoa jibu lililovuviwa. Alisema: “Wewe [Yehova] ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15) Ndiyo, Biblia yatoa tumaini la ufufuo kwa ajili ya wale walio katika kumbukumbu la Mungu. Yeye ana hamu nyingi ya kurudisha watumishi wake waaminifu, kama Ayubu, kwenye uhai! Kristo Yesu alithibitisha uhalisi wa tumaini hilo, akisema: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini [maziara ya ukumbusho, NW] wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu.”—Yohana 5:28, 29.

Wakati ujapo ili unabii huo utimizwe, Isaya 25:8 yaahidi, Mungu ‘atameza mauti hata milele.’ Hiyo yamaanisha ulimwengu ambamo, kama vile Ufunuo 21:4 uwekavyo wazo hilo, “mauti haitakuwapo tena.” Je! wewe ungependa kuishi katika ulimwengu usio na maziko au masebule ya maziko, usio na mawe ya makaburi au nyanja za makaburi, usio tena na machozi ya kihoro bali machozi ya shangwe?

Ni kweli, huenda ikawa wewe ulilelewa kuamini fundisho la nafsi isiyokufa. Lakini kwa kujifunza Biblia, waweza kusitawisha imani katika ahadi zenye kukomboa za Biblia.a Waweza pia kujifunza mambo ambayo ni lazima ufanye ili uirithi ahadi ya Biblia, si ya kuendelea kuwa hai ukiwa nafsi isiyokufa, bali ya kupokea “uhai wa milele” katika Paradiso duniani!—Yohana 17:3; Luka 23:43, NW.

[Maelezo ya Chini]

a Ikiwa ungependa kufanya hivyo, tafadhali uwe huru kuandikia wachapishaji wa gazeti hili au pasha habari Jumba la Ufalme la kwenu la Mashahidi wa Yehova.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki