Nafsi Yako Ni Nini?
WATU wengi wanaamini kwamba mwanadamu anayo nafsi iliyo kando na tofauti na mwili. Nafsi hii yadhaniwa kuwa inauacha mwili wakati wa kufa. Ikitegemea kama mtu ameishi maisha mema au sivyo, yasemekana nafsi yake inakwenda ama hell ikapate mateso ama mbinguni ikapate furaha ya milele pamoja na Mungu.
Imani katika hell yenye mateso kwa njia hiyo yaonekana kulitegemea fundisho la kwamba mwanadamu anayo nafsi inayookoka mwili unapokufa. Lakini je! fundisho hili linapatana na Biblia?
Kitabu cha kwanza cha Maandiko Matakatifu, Mwanzo, kinaonyesha wazi namna nafsi ya kibinadamu ilivyo. Ukisimulia kuumbwa kwa mtu wa kwanza, Mwanzo 2:7, NW, unasema: “Yehova Mungu akaendelea kumfanyiza mtu katika mavumbi ya ardhi na kupuliza katika matundu ya pua yake pumzi ya uhai, naye mtu akawa nafsi yenye uhai [neʹphesh, Kiebrania].” Angalia kwamba Biblia haisemi ‘mtu alipokea nafsi,’ bali kwamba “mtu akawa nafsi yenye uhai.”
Katika barua yake iliyoongozwa na roho ya Mungu kwa Wakorintho, mtume Paulo anaonyesha kwamba fundisho la Kikristo juu ya nafsi halikutofautiana na linaloonyeshwa katika Mwanzo. Yeye alitaja Mwanzo 2:7 kwa kusema: “Imeandikwa hata hivyo: ‘Mtu wa kwanza Adamu akawa nafsi iliyo hai.’” (1 Kor. 15:45, NW) Kwa maana Paulo alilitumia neno la Kigiriki kwa nafsi, psy·kheʹ, hii yahakikisha kwamba, kama vile neno la Kiebrania neʹphesh, psy·kheʹ laweza kumaanisha mwanadamu mwenyewe.
Yastahili kuangaliwa kwamba wanafunzi wengi wa Biblia wa karne ya 20, wa Katoliki, wa Kiprotestanti na wa Kiyahudi, wamekubali waziwazi kwamba mwanadamu mwenyewe ni nafsi. Twasoma:
“Mstari ujulikanao sana katika Mwanzo [2:7] hausemi, kama inavyodhaniwa mara nyingi, kwamba mwanadamu amefanyizwa na mwili na nafsi; wasema kwamba Yahweh alimfanya mwanadamu, kutoka ardhini, kisha akaendelea kutia uzima katika mfano usioishi kwa njia ya pumzi ya uhai iliyopulizwa katika matundu yake ya pua, hivyo kwamba mwanadamu akawa kiumbe chenye uhai, ambacho ndicho kinachomaanishwa hapa na nephesh [nafsi].”—Zeitschrift fiir die alttestamentliche Wissenschaft, Kitabu cha 41.
“Haimpasi mwanadamu kufikiriwa kana kwamba anayo nafsi; yeye ndiye nafsi.”—The New Bible Commentary.
“Nafsi katika Agano la Kale haimaanishi sehemu ya mwanadamu, bali mwanadamu mzima—mwanadamu kama kiumbe chenye uhai. Vivyo hivyo, katika Agano Jipya yamaanisha uhai wa kibinadamu: uhai wa mtu mwenyewe, mtu mwenye fahamu.”—New Catholic Encyclopedia.
“Katika Agano Jipya, ‘kuokoa nafsi ya mtu’ (Mk 8:35) hakumaanishi kuokoa sehemu fulani ‘ya kiroho’ ya mwanadamu, iliyo tofauti na ‘mwili’ (katika maana ya akili) bali mtu mzima pamoja na mkazo wa kwamba mtu huyo anaishi, anatamani, anapenda na kunuia, n.k., zaidi ya kuwa awezaye kuguswa na kuonekana.”—The New American Bible, “Glossary of Biblical Theology Terms.”
“Biblia haisemi sisi tunayo nafsi. ‘Nefesh’ ndiye mtu mwenyewe, haja yake ya chakula, damu yenyewe katika mishipa yake, kuwako kwake.”—Dr. H. M. Orlinsky wa Hebrew Union College, aliyetajwa katika Times la New York, Oktoba 12, 1962.
Kwa kuwa maneno ya lugha za kwanza kwa “nafsi” (ne’phesh na psy·kheʹ) yanaweza kumaanisha mwanadamu mwenyewe, imetupasa tutazamie kuona ikihesabiwa kazi za kimwili za kawaida au tabia za wanadamu. Je! ndivyo ilivyo? Je! nafsi yako ndiyo wewe kweli kweli? Angalia:
Uchunguzi wa matumizi ya Biblia ya maneno haya ya Kiebrania na Kigiriki wafunua kwamba nafsi ya kibinadamu inazaliwa. (Mwa. 46:18) Yaweza kula au kufunga kula. (Law. 7:20, NW; Zab. 35:13) Yaweza kuwa yenye shangwe au yenye huzuni. (Zab. 35:9; Mt. 26:38, NW) Yaweza kupendana na nyingine. (Mwa. 34:3, NW) Yaweza kubariki wengine. (Mwa. 27:4, NW) Yaweza kusikiliza. (Matendo 3:23, NW) Nafsi yaweza kutenda dhambi, kuapa, kutamani vitu na kushindwa na woga. (Law. 4:2; 5:4; Kum. 12:20; Matendo 2:43, NW) Yaweza kutoroshwa na kufungwa pingu. (Kum. 24:7; Zab. 105:18, NW) Je! mambo haya yote wewe huwezi kuyafanya au huwezi kufanyiwa wewe? Ndiyo, nafsi yako ndiyo wewe.
Kwa hiyo nafsi yako inapokufa, wewe unakufa, unakoma kuwako ukiwa mwenye fahamu. Kwa kurudia-rudia Biblia inaizungumza nafsi kama ikifa. Kupitia kwa nabii wake Ezekieli, Yehova alitangaza: “Tazama! Nafsi zote—ni mali yangu. Kama vile nafsi ya baba vivyo hivyo na nafsi ya mwana—ni mali yangu. Nafsi itendayo dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (Eze. 18:4, 20, NW) Kwa habari ya Masihi au Kristo, unabii wa Isaya ulitangulia kusema: “Yeye aliimwaga nafsi yake hata kufa kwenyewe.” (Isa. 53:12, NW) Naye Yesu Kristo alisema: “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza.”—Yohana 12:25.
Lakini je! hakuna walau maandiko fulani yanayoweza kufahamiwa kama yanayoutegemeza uwezekano wa kuwa kwa mwanadamu na nafsi isiyokufa? Sivyo. Kwa kupendeza, hata wanafunzi wa Biblia wasio mashahidi wa Yehova wamefikia azimio hili kwa msingi wa uchunguzi wao. Akiandika katika Presbyterian Life (Mei 1970), David G. Buttrick, Mtaalamu Mshirika katika Church and Ministry, Pittsburgh Theological Seminary, anasema: “Mimi sioni lo lote katika Andiko la kuyategemeza maoni ya kwamba nafsi zinayo ‘asili ya kutokufa.’” Juu ya maana ya neno “nafsi,” mwanafunzi huyu anasema: “Wakati Biblia inapotumia neno hilo nafsi, kwa kawaida inamaanisha ‘uhai’ au ‘hali ya kuishi,’ wala siyo sehemu yetu iliyo kando. Kwa hiyo fikiri: Wakati Biblia inapotuambia sisi twaweza kufa, inasema kwamba sisi tunakufa—tunakufa kweli kweli.” Akiendelea na kuonyesha sababu yake, anasema: “Kama tungalikuwa na nafsi zisizokufa, tusingemhitaji Mungu—kutokufa kwetu kungefaa. Lakini Biblia inalipinga tumaini hilo lisilofaa kitu: sisi twaweza kufa na kwa hiyo lazima tuushikilie upendo wa Mungu peke yake. Wakristo hawaamini katika kuendelea kuwapo, bali katika ufufuo.”
Biblia yaonyesha wazi kwamba mtu hawi mwenye fahamu katika hali ya kufa. Mhubiri 9:10 anasema hivi, kulingana na tafsiri ya Douay Version ya Katoliki: “Jambo liwalo lote mkono wako uwezalo kulifanya, lifanye kwa bidii: kwa maana wala kazi, wala kuwaza, wala hekima, wala maarifa, hayatakuwamo katika hell, ambako wewe unaelekea kwa kasi.” Kwa kuwa hakuna nafsi isiyokufa ya kuokoka mwili unapokufa, hakuna cho chote kiwezacho kuteswa katika hell yenye moto nyuma ya kifo.
Ahadi ya Mungu ya ufufuo, hata hivyo, yatoa uhakikisho kwamba wafu waliomo katika hell watafufuliwa. Lakini hell hii yenyewe ni nini nao wafu wawezaje kukombolewa katika uwezo wake? Tafadhali uiangalie makala ifuatayo.