Maoni Yako Juu ya Nafsi Huathiri Uhai Wako
“Mtu akawa nafsi hai.”—MWANZO 2:7.
1, 2. Dini zilizo nyingi huamini nini kuhusu mwanadamu na nafsi?
KARIBU dini zote hufundisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyokufa. New Catholic Encyclopedia husema kwamba nafsi “huumbwa na Mungu na kuingizwa ndani ya mwili wakati wa kuchukua mimba.” Husema pia kwamba fundisho la nafsi isiyokufa “ni moja la mawe ya pembeni” (ya msingi) ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Vivyo hivyo, The New Encyclopædia Britannica hutaarifu kwamba “wazo la Kiislamu hushikilia kwamba nafsi hutokea wakati mmoja na mwili; baada ya hapo, huwa na uhai wayo yenyewe, huku muungano wayo na mwili ukiwa ni hali ya muda tu.”
2 Dini hizo huamini kwamba nafsi huacha mwili mara tu kifo kitokeapo na huendelea kuishi milele, mwishowe ikikaa mbinguni kwa raha mustarehe, kukaa kwa muda katika purgatori, au kuteseka milele katika helo yenye moto. Kifo huonwa kuwa mlango uongozao kwenye uhai wa milele katika makao ya roho. Kama vile mwandikaji mmoja alivyosema katika kitabu We Believe in Immortality (Sisi Twaamini Katika Kutokufa): “Mimi huona Kifo kuwa ni kitendo kizuri sana cha ujasiri na chenye kuheshimika sana. Mimi huona Kifo kuwa ni kupandishwa cheo na Mungu.”
3. Ni nini imani ya dini mbalimbali za Mashariki?
3 Wahindu, Wabuddha, na wengine huamini kwamba nafsi huhamia makao mengine. Hiyo yatia ndani imani ya kwamba wakati wa kifo nafsi huingia upya katika umbo jingine, huzaliwa upya ikiwa mwanadamu mwingine au kitu kingine kilicho hai. Ikiwa mtu alikuwa amekuwa mwema, husemwa kwamba nafsi yake ingezaliwa upya ikiwa mtu wa cheo cha juu zaidi. Lakini ikiwa alikuwa amekuwa mbaya, angezaliwa upya akiwa mtu wa cheo cha chini zaidi au hata akiwa mnyama au mdudu.
4, 5. Kwa nini ni jambo la maana kujua ukweli juu ya nafsi?
4 Hata hivyo, namna gani ikiwa wanadamu hawana nafsi isiyokufa? Namna gani ikiwa kifo si “kupandishwa cheo na Mungu,” si mlango ambao huwaongoza wote waliokufa kwenye uhai-roho wa milele au kuingia upya katika umbo tofauti mara iyo hiyo? Hapo ile imani ya nafsi isiyokufa ingeongoza mtu upande usiofaa. Kitabu Official Catholic Teachings husema kwamba kanisa husisitiza juu ya imani ya nafsi isiyokufa kwa sababu kutoiamini “kungefanya sala zalo, desturi zalo za maziko na vitendo vya kidini ambavyo wafu hufanyiwa viwe havina umaana wowote au visivyo vya akili nzuri.” Kwa hiyo mwendo wa mtu wa maisha, ibada, na wakati ujao wa milele wahusika.—Mithali 14:12; Mathayo 15:9.
5 Ni jambo la maana kuujua ukweli juu ya imani hii. Yesu alisema: “Wamwabuduo [Mungu] imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yohana 4:24) Ukweli juu ya nafsi ya kibinadamu hupatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Maandiko yaliyovuviwa yana ufunuo wa Mungu juu ya makusudi yake, kwa hiyo twaweza kuwa na uhakika kwamba hayo hutueleza ukweli. (1 Wathesalonike 2:13; 2 Timotheo 3:16, 17) Katika sala Yesu alisema hivi kwa Mungu: “Neno lako ndiyo kweli.”—Yohana 17:17.
Je! Kaumbwa na Nafsi Isiyokufa?
6. Usimulizi wa Mwanzo watuambia nini wazi juu ya kuumbwa kwa mwanadamu?
6 Mwanzo 2:7 hutuambia hivi: “BWANA [Yehova, NW] Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Usimulizi hausemi kwamba Mungu aliingiza nafsi isiyokufa katika mwanadamu. Husema kwamba nguvu ya Mungu ilipotia nishati katika mwili wa Adamu, yeye “akawa nafsi hai.” Kwa hiyo mwanadamu ni nafsi. Si kwamba yeye anayo nafsi.
7. Kwa nini wanadamu waliwekwa duniani?
7 Mungu aliumba Adamu aishi duniani, si mbinguni. Dunia haikupasa kuwa mahali pa mtihani tu ili kuona kama Adamu alistahili kuwa mbinguni. Mungu alifanyiza dunia “ikaliwe,” na Adamu alikuwa mkaaji wayo wa kwanza wa kibinadamu. (Isaya 45:18; 1 Wakorintho 15:45) Baadaye, Mungu alipoumba Hawa awe mke wa Adamu, kusudi la Mungu kwao lilikuwa kwamba wafanye dunia iwe na watu na kuigeuza iwe paradiso iliyo kao la milele kwa aina ya kibinadamu.—Mwanzo 1:26-31; Zaburi 37:29.
8. (a) Kuwako kwa Adamu kulitegemea masharti gani? (b) Kama Adamu asingalitenda dhambi, angaliendelea kuishi wapi?
8 Hakuna popote ambapo Biblia husema kwamba sehemu fulani ya Adamu ilikuwa isiyokufa. Bali, kuwako kwake kulikuwa kwa masharti, kukitegemea utii kwa sheria ya Mungu. Akivunja sheria hiyo, angepata nini halafu? Je! ni uhai wa milele katika makao ya roho? Hata kidogo. Badala ya hivyo, ‘angekufa hakika.’ (Mwanzo 2:17) Angerudi alikotoka: “U mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 2:7; 3:19) Adamu hakuwa na maisha kabla hajaumbwa, na hangekuwa na yoyote baada ya kufa. Kwa hiyo alikuwa na machaguo mawili tu: (1) utii na uhai au (2) kutotii na kufa. Kama Adamu asingalitenda dhambi, angaliishi duniani milele. Asingalienda mbinguni kamwe.
9. Biblia huita kifo nini kwa usahihi, na kwa sababu gani?
9 Adamu alikosa kutii, naye akafa. (Mwanzo 5:5) Kifo kilikuwa adhabu yake. Hakikuwa mlango wa kwenda kwenye ‘kitendo jasiri chenye kuheshimika sana’ bali mlango wa kwenda kwenye kutokuwako. Hivyo, kifo si rafiki bali ni kama vile Biblia ikiitavyo, “adui.” (1 Wakorintho 15:26) Kama Adamu angalikuwa na nafsi isiyokufa ambayo ingeenda mbinguni akiwa mtii, basi kifo kingalikuwa ni baraka. Lakini hakikuwa baraka. Kilikuwa laana. Na kwa dhambi ya Adamu, laana ya kifo ilienea kwa wanadamu wote kwa sababu wote ni wazao wake.—Warumi 5:12.
10. Ni tatizo gani zito ambalo latokea katika kuamini kwamba Adamu alikuwa na nafsi isiyokufa?
10 Zaidi ya hilo, kama Adamu angaliumbwa akiwa na nafsi isiyokufa ambayo ingeteswa milele katika helo yenye moto akitenda dhambi, mbona hakuonywa juu ya hilo? Mbona aliambiwa angekufa na kurudia mavumbi tu? Ungalikuwa ukosefu wa haki kama nini kumlaani vikali Adamu kwenye umilele wa kuteswa kwa ajili ya kutotii, lakini asionywe juu ya hilo! Hata hivyo, “hakuna ukosefu wa haki” kwa Mungu. (Kumbukumbu 32:4, NW) Hakukuwa na uhitaji wa kuonya Adamu juu ya helo yenye moto kwa nafsi zisizokufa za waovu. Helo ya jinsi hiyo haikuwako, wala hakukuwa na nafsi zisizokufa. (Yeremia 19:5; 32:35) Hakuna mateso ya milele katika mavumbi ya ardhi.
Utumizi wa Biblia wa “Nafsi”
11. (a) Katika Biblia neno la Kiingereza “nafsi” hutokana na maneno gani ya Kiebrania na Kigiriki? (b) King James Version hufasirije maneno ya Kiebrania na Kigiriki kwa “nafsi”?
11 Katika Maandiko ya Kiebrania, neno la Kiingereza “nafsi” hutokana na neno la Kiebrania neʹphesh, ambalo huonekana mara zaidi ya 750. Mlingano walo katika Maandiko ya Kigiriki ni psy·kheʹ, ambalo huonekana mara zaidi ya 100. New World Translation of the Holy Scriptures hufasiri maneno hayo kwa upatani kuwa “nafsi.” Biblia nyinginezo huenda zitumie unamna-namna wa maneno. Baadhi ya njia ambazo King James Version hutafsiri neʹphesh ni hizi: hamu, hayawani, mwili, pumzi, kiumbe, -enye kufa (mwili), tamaa, moyo, uhai, mwanadamu, akili, mtu, binafsi, nafsi, kitu. Na hutafsiri psy·kheʹ hivi: moyo, uhai, akili, nafsi.
12. Biblia hutumiaje maneno ya Kiebrania na Kigiriki kwa “nafsi”?
12 Biblia huita viumbe wa baharini neʹphesh: “Kila nafsi hai ambayo imo katika maji.” (Walawi 11:10, NW) Neno hilo laweza kurejezea wanyama wa bara: “Acha ardhi itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zazo, mnyama wa kufugwa na mnyama anayejongea na hayawani mwitu.” (Mwanzo 1:24, NW) Mamia ya nyakati neʹphesh humaanisha watu. “Nafsi zote zilizotoka viunoni mwa Yakobo zilikuwa ni nafsi sabini.” (Kutoka 1:5) Kielelezo cha kutumiwa kwa psy·kheʹ katika njia hii ni 1 Petro 3:20, NW. Hiyo husimulia safina ya Noa, “ambamo watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupita katika maji.”
13. Biblia hutumia neno “nafsi” kwa njia zipi?
13 Biblia hutumia neno “nafsi” katika njia nyingine nyingi. Mwanzo 9:5, NW, husema hivi: “Nitaomba nirudishiwe damu yenu ya nafsi zenu.” Hapa nafsi yasemwa kuwa na damu. Kutoka 12:16, NW, husema: “Kile tu ambacho kila nafsi yahitaji kula, hicho tu ndicho nyinyi mwaweza kufanyiwa.” Katika kisa hiki nafsi yasemwa kuwa ikila. Kumbukumbu 24:7, NW, hunena juu ya mtu ‘akitorosha nafsi ya ndugu zake.’ Kwa uhakika iliyotoroshwa si nafsi isiyokufa. Zaburi 119:28 husema: “Nafsi yangu imeyeyuka kwa uzito [imekuwa bila usingizi kutokana na kihoro, NW].” Kwa hiyo nafsi yaweza hata kupoteza usingizi. Pia Biblia huonyesha kwamba nafsi yaweza kufa. Nayo hufa. “Nafsi hiyo ni lazima ikatiliwe mbali kutoka kwenye watu wake.” (Walawi 7:20, NW) “Asije akielekea kwenye nafsi yoyote iliyokufa.” (Hesa-bu 6:6, NW) “Nafsi zetu zitakufa.” (Yoshua 2:14, NW) “Nafsi yoyote isiyosikiliza Nabii huyo itaharibiwa kabisa.” (Matendo 3:23, NW) “Kila nafsi hai ikafa.”—Ufunuo 16:3, NW.
14. Biblia huonyesha wazi nafsi ni nini?
14 Kwa wazi, utumizi wa Biblia wa neʹphesh na psy·kheʹ huonyesha kwamba nafsi ndiye mtu au, katika kisa cha wanyama, ndicho kiumbe. Si sehemu fulani isiyokufa ya mtu. Kwa kweli, neʹphesh hata hutumiwa juu ya Mungu mwenyewe: “Nafsi yake humchukia asiye haki, na mwenye kupenda udhalimu [jeuri, NW].”—Zaburi 11:5.
Wanachuo Wengi Hukubaliana na Hilo
15. Kazi kadhaa za wanachuo hutoa maoni gani juu ya fundisho la nafsi isiyokufa?
15 Wanachuo wengi hukubali kwamba Biblia haineni juu ya nafsi isiyokufa. The Concise Jewish Encyclopedia hutaarifu hivi: “Biblia haitaarifu fundisho la kutokufa kwa nafsi, wala jambo hilo haliibuki waziwazi katika fasihi za mapema za kirabi.” The Jewish Encyclopedia husema hivi: “Imani ya kwamba nafsi huendeleza maisha yayo baada ya kufa kwa mwili ni jambo la kukisiwa-kisiwa kifalsafa tu au kinadharia wala si la imani yenye kuthibitika wazi, na kwa hiyo haifundishwi moja kwa moja mahali popote katika Andiko Takatifu.” The Interpreter’s Dictionary of the Bible husema hivi: “Nephesh . . . haiendelei kuwako bila kutegemea mwili, bali hufa pamoja nao. . . . Hakuna andiko la kibiblia la kuipa mamlaka taarifa ya kwamba ‘nafsi’ hutengwa kutoka kwenye mwili wakati wa kifo.”
16. Vitabu fulani vyenye mamlaka hutoa maoni gani juu ya nafsi?
16 Pia, Expository Dictionary of Bible Words husema: “‘Nafsi’ katika A[gano la] K[ale] haionyeshi sehemu fulani isiyo ya kimwili ya wanadamu ambayo huendelea baada ya kifo. [Neʹphesh] kwa msingi humaanisha uhai ulio maisha ya vitu vyenye utu peke yavyo. . . . Maana ya msingi ya [psy·kheʹ] huthibitishwa na neno ambalo lafanana nalo katika A[gano la] K[ale], wala haithibitishwi na utamaduni wayo wa Kigiriki.” Na The Eerdmans Bible Dictionary hutaarifu kwamba katika Biblia, neno nafsi “halionyeshi sehemu fulani ya mwanadamu, bali mtu mzima. . . . Katika maana hii wanadamu hawana nafsi—wao ni nafsi.”—Italiki ni zetu.
17. Vyanzo viwili vya Kikatoliki vyakiri nini juu ya “nafsi”?
17 Hata New Catholic Encyclopedia hukiri hivi: “Kwa kawaida maneno ya Kibiblia kwa nafsi humaanisha mtu kwa ujumla.” Huongezea hivi: “Katika A[gano la] K[ale] hakuna mgawanyo wa mwili na nafsi. . . . Neno hilo [neʹphesh], ingawa limetafsiriwa na neno letu nafsi, halimaanishi kamwe nafsi kwa kutofautiana na mwili au mtu mwenyewe. . . . Neno hilo [psy·khe’] ndilo neno la A[gano] J[ipya] linalolingana na [neʹphesh]. . . . Wazo la nafsi ikiendelea kuwa hai baada ya kifo halionekani vyepesi katika Biblia.” Na Georges Auzou, Profesa Mfaransa Mkatoliki wa Andiko Takatifu, aandika hivi katika kitabu chake La Parole de Dieu (Neno la Mungu): “Lile wazo la ‘nafsi,’ yenye kumaanisha kitu cha kiroho tu kisicho cha kimwili, kilicho kando na ‘mwili,’ . . . halimo katika Biblia.”
18. (a) Ensaiklopedia moja hutoaje maelezo juu ya utumizi wa Biblia wa neno “nafsi”? (b) Wanatheolojia walipata wapi wazo la kitu chenye kuendelea kuishi baada ya kifo cha mwili?
18 Hivyo, The Encyclopedia Americana hutoa maoni haya: “Wazo la Agano la Kale juu ya mwanadamu ni lile la muungamano mmoja, wala si muungano wa nafsi na mwili. Ingawa neno la Kiebrania [neʹphesh] hutafsiriwa mara nyingi kuwa ‘nafsi,’ ingekuwa si sahihi kulisoma kwa kuliingiza maana ya Kigiriki. . . . [Neʹphesh] haiwaziwi kamwe kuwa ikitenda kazi kando na mwili. Katika Agano Jipya neno la Kigiriki [psy·kheʹ] hutafsiriwa mara nyingi kuwa ‘nafsi’ lakini tena halipasi kueleweka kwa utayari kumaanisha vile neno hilo lilivyomaanisha kwa wanafalsafa Wagiriki. . . . Biblia haiandai maelezo ya wazi juu ya jinsi mtu huendelea kuwa hai baada ya kifo.” Yaongezea hivi: “Wanatheolojia wamelazimika kutegemea mazungumzo ya wanafa-lsafa ili wapate njia ya kutosha ya kueleza kuendelea kuishi kwa mtu baada ya kufa.”
Si Biblia Bali Ni Falsafa
19. Falsafa ya Kigiriki yakamatanaje na imani ya nafsi isiyokufa?
19 Ni kweli kwamba wanatheolojia walichagua kufuata mawazo ya wanafalsafa wapagani ili waeleze wazi fundisho la nafsi isiyokufa. Kamusi ya Kifaransa Dictionnaire Encyclopédique de la Bible (Kamusi Iliyo Ensaiklopedia ya Biblia) husema hivi: “Wazo la kutokufa limetokana na kufikiri kwa Kigiriki.” The Jewish Encyclopedia huhakikishia hivi: “Imani ya kutokufa kwa nafsi iliwajia Wayahudi kwa kugusana na fikira ya Kigiriki na hasa kupitia falsafa ya Plato, mwelezaji walo mkuu,” aliyeishi katika karne ya nne kabla ya Kristo. Plato aliamini hivi: “Nafsi haifi na haiwezi kuangamia, na nafsi zetu zitaishi kikweli katika ulimwengu mwingine!”—The Dialogues of Plato.
20. Ni wakati gani na jinsi gani falsafa ya kipagani ilipenya ndani ya Ukristo?
20 Ni wakati gani falsafa hii ya kipagani ilipopenya katika Ukristo? The New Encyclopædia Britannica husema hivi: “Kuanzia katikati ya karne ya 2 AD Wakristo waliokuwa na mazoezi fulani katika falsafa ya Kigiriki walianza kuhisi uhitaji wa kueleza imani yao kwa kutumia maneno yayo, ili waridhishe uelewevu wa akili yao wenyewe na pia ili wageuze wapagani wenye elimu. Falsafa waliyoona ikiwafaa kabisa ilikuwa mawazo ya Plato.” Kwa hiyo, kama vile Britannica isemavyo, “wanafalsafa Wakristo wa mapema walichagua kufuata wazo la Kigiriki la kutokufa kwa nafsi.” Hata Papa John Paul 2 alikiri kwamba fundisho la nafsi isiyokufa huingiza humo “nadharia za shule fulani za falsafa ya Kigiriki.” Lakini kukubali nadharia za falsafa ya Kigiriki kulimaanisha kwamba Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imeachilia mbali ukweli sahili ambao hutajwa kwenye Mwanzo 2:7: “Mtu akawa nafsi hai.”
21. Imani katika nafsi isiyokufa inarudi nyuma umbali gani?
21 Hata hivyo, fundisho la nafsi isiyokufa hurudi nyuma mbali zaidi ya Plato. Katika kitabu The Religion of Babylonia and Assyria, kilichotungwa na Morris Jastrow, twasoma hivi: “Tatizo la kutokufa . . . lilishughulisha sana fikira za wanatheolojia Wababuloni. . . . Kifo kilikuwa kipito cha kwenda kwenye uhai wa aina nyingine.” Pia, kitabu Egyptian Religion, kilichotungwa na Siegfried Morenz, hutaarifu hivi: “Wamisri wa kale walichukua maisha baada ya kifo kuwa mwendeleo tu wa maisha duniani.” The Jewish Encyclopedia huarifu ukamatano wa dini hizi za kale na Plato wakati isemapo kwamba Plato aliongozwa kwenye wazo la nafsi isiyokufa “kupitia mafumbo ya Kiorfi na Kieleusini ambamo maoni ya Kibabuloni na Kimisri yalichanganywa kiajabu.”
22. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba mbegu za fundisho la nafsi isiyokufa zilipandwa hasa kwenye pambazuko la historia ya kibinadamu?
22 Hivyo, wazo la nafsi isiyokufa ni la kale. Kwa uhakika, mizizi yalo hurudi nyuma kwenye pambazuko la historia ya kibinadamu! Baada ya Adamu kuambiwa kwamba angekufa asipotii Mungu, mke wa Adamu, Hawa, alitajiwa maoni ya kinyume. Aliambiwa hivi: “Hakika hamtakufa.” Hapa mbegu za fundisho la nafsi isiyokufa zilipandwa. Na muda wote tangu hapo, utamaduni mmoja baada ya mwingine umechagua kufuata maoni ya kipagani kwamba ‘hutakufa hakika bali utaende-lea kuishi.’ Hiyo ni kutia na Jumuiya ya Wakristo, ambayo iliingiza wafuasi wayo ndani ya uasi-imani wenye kupinga makusudi na mapenzi ya Mungu.—Mwanzo 3:1-5; Mathayo 7:15-23; 13:36-43; Matendo 20:29, 30; 2 Wathesalonike 2:3, 7.
23. Ni nani aliyesitawisha fundisho la nafsi isiyokufa, na kwa nini?
23 Ni nani aliyeongoza wanadamu kuamini uwongo huo? Yesu alimtambulisha aliposema hivi kwa viongozi wa kidini wa siku yake: “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. . . . Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yeye ni mwongo, na baba wa huo [uongo].” (Yohana 8:44) Ndiyo, ni Shetani aliyesitawisha wazo la nafsi isiyokufa ili ageuze watu mbali na ibada ya kweli. Kwa hiyo mwendo wa maisha ya mtu na tumaini la wakati ujao huwekwa kwenye kijia kisichofaa kwa kuamini mafundisho yaliyokua kutokana na uwongo ulio wa kwanza kurekodiwa katika Biblia, ingawa bila shaka kile tu ambacho Hawa alielewa wakati huo ni kwamba nyoka alimaanisha hangekufa kamwe kimnofu.
24. Ni maswali gani ambayo kwa kufaa yaweza kuulizwa kuhusu uhai wa milele na kutokufa?
24 Biblia haifundishi kwamba wanadamu wana nafsi isiyokufa. Basi, kwa nini hiyo hunena juu ya tumaini la uhai wa milele? Zaidi ya hilo, kwani Biblia haisemi hivi kwenye 1 Wakorintho 15:53, NW: “Huu ambao ni wenye kufa ni lazima uvae kutokufa”? Na je! Yesu hakwenda mbinguni baada ya ufufuo wake, na je! hakufundisha kwamba wengine pia wangeweza kwenda mbinguni? Maswali haya na mengine yatachunguzwa katika makala yetu inayokuja.
Maswali kwa Kupitia
◻ Dini zilizo nyingi huamini nini kuhusu nafsi?
◻ Biblia huonyeshaje kwamba mwanadamu hakuumbwa akiwa na nafsi isiyokufa?
◻ Ni jambo gani lililo wazi kutokana na utumizi wa Biblia wa maneno ya Kiebrania na Kigiriki kwa “nafsi”?
◻ Wanachuo wengi husema nini juu ya maoni ya Biblia juu ya nafsi?
◻ Fundisho la nafsi isiyokufa hurudi nyuma umbali gani katika historia?
[Picha katika ukurasa wa 20]
Wote ni nafsi